May 15, 2008

Kuzaliwa kwangu Na Teknolojia Mpya

Ndiyo leo ni siku yangu ya kuzaliwa.Nakumbuka miaka ile nilipozaliwa kijiji hiki cha Lundu hapa nyasa.Yaani naikumbuka siku maridadi.Sasa kuna kitu kimoja kinanishangaza sana,ni hiki kila ifikapo kumbukumbu ya siku yangu ya kuzaliwa nasahau kabisa shauri ya majukumu si unajua tena kuvua samaki,nyavu nazo zinahitaji tiba ikiwa zimeraruka.Lakini usiniulize wala usijiulize nimekumbukaje leo mpaka nikaadika.Tarehe hii ni muhimu sana Mama na Baba yangu ndiyo ilikuwa siku yao ya furaha kupata toto la kinyasa ambalo leo linapiga gumzo bloguni.Mmmh nakumbuka mwalimu wangu mmoja enzi zile alinifundisha eti kukumbuka siku hii ni sawa na kuomboleza msiba kwani mzazi wangu alipata uchungu sana...sawa ndiyo maana nawasifia kila dakika kwamba wazazi wangu ni zaidi ya upendo,kama unabisha soma pale bloguni pale ruhuwiko uone dada yetu alivyomthamini Mama lakini amemsahau Baba...sijui kwanini...ebu tuambie...Zawadi kubwa niliyojinunulia ni kitambaa cha mkononi(leso) chenye rangi ya bendera ya taifa ya Tanzania naipenda nchi yangu...Tuache hilo kwani tayari ni kumbukumbu inayonikuna.Kuna habari moja ya mambo ya teknolojia kwamba shirika la mradi wa Teknolojia la Tanzania(tzNiC0)limezindua mpango wa kubadili taarifa za mdalakilishi(intaneti)kwa lugha ya kiswahili.Mwenyekiti wa bodi hiyo Profesa Beda Mutagahywa amesema hiyo itakuwa kama Google/wikipedia ya kiswahili ambayo itakuwa inataarifa mbalimbali za duniani kwa lugha ya kiswahili.Kasema hayo katika maadhimisho ya wiki ya teknolojia TEKNOHAMA na kutoa mwaliko kwa vijana wenye uwezo wa kuandika taarifa waadnike humo zikiwa sahihi.Kwahiyo huu ni mwaliko kwa wanateknolojia....tunasubiri huku nyasa itatunufaisha hata kama hatuna umeme na mitandao

May 14, 2008

Ruvuma Yatolewa Kombe La Taifa,Huzuni...

Jana ilikuwa siku mbaya kwa Wanaruvuma shauri timu yetu ya soka katika michuano ya kombe la Taifa ilitolewa.Mechi ilikuwa kali bwana asikuambie mtu. kama hujashuhudia Wanaruvuma basi jinyonge kwa utandu wa buibui(natania).Nakwambia mechi zote za timu ya mkoa wa Ruvuma zinavutia sana,toka ile ya kwanza dhidi ya Kigoma.Basi jana mechi ikaanza mkoa wa Kagera kupata bao dakika ya pili kupitia kwa Musa Kaunda aliyemalizia pasi nzuri ya Shamte Ali.Lakini "wangoni" tukasawazisha katika dakika ya 34 kupitia kwa Abdalla Ausi ambaye alitumia makosa ya golikipa wa Kagera Odo Nombo aliyemrushia mpira huku akiwa ametoka golini.Katika kipindi hicho cha kwanza Pauli Ngwai aliipatia Kagera bao la pili baada ya kupata pasi ya Pauli Kabange.......mpira ukawa mapumziko.......Naam kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Ruvuma wakionekana kutafuta bao la kusawazisha.Kocha Pita Mhina wa Ruvuma alifanya mabadiliko yaliyosaidia kupatikana kwa bao la kusawazisha.Ruvuma walifanya shambulizi katika dakika ya 89 na beki mmoja wa Kagera aliutoa nje na kuwa kona ambayo ilipigwa vizuri lakini ikatolewa tena na kipa Odo Nombo,kisha mpira ukamkuta Omari Kapilima aliyeachia shuti kali lililokwenda kimiani.Lakini mnamo dakika ya 90 Kagera ilimwingiza golikipa Abdulrazak Jakisoni kuchukua nafasi ya Nombo, lengo lilikuwa kwa ajili ya penati.Mpaka Mwamuzi wa mchezo anapuliza kipenga(siyo kupenga kamasi) cha mwisho matokeo yalikuwa mabao 2-2.Sasa hatua za kupiga penati ziliwadia.Wafungaji wa Penati za kagera ni Daudi Chalesi,Martini Muganyizi,Juma Seifu na Ladislausi Mbodo.Zile za Ruvuma zilifungwa na Ramadhani Kudundwa na Patisoni Chiwanga ambaye alikuwa mchezaji bora wa mechi.Kiujumla Ruvuma walicheza vizuri na walipoteza penati mbili kupitia kwa Abdala Ausi na Daudi Ajilo....mchezo ulikuwa mzuri na kwa hakika licha ya kutolewa timu yetu ya mkoa wa Ruvuma ilicheza kandanda safi huku ikikusanya mashabiki wengi uwanjani hapo kuliko Kagera.Mchezo ulipendeza na dadangu pale bloguni ruhuwiko umeikosa mechi muhimu ya kuuona mkoa wako lakini najua ni majukumu tu.Tunahuzunika ....lakini tunafuraha timu yetu imecheza vizuri na ikitunzwa basi mwakani 2009 malengo yawe kufika nusu fainali kwani robo fainali ya mwaka huu inatosha Tuombe mungu kwa lugha yetu .....haya ewe mngoni na wengine anza.........mmh wavivu eeh..msijali mimi nimeiona mechi mnyasa mie yaani imenikuna sana....mmh nilisahau unajua huyu Odo Nombo kipa wa Kagera ni mtoto wetu wa Ruvuma?....unabisha?....Nimecheza naye Umiseta(michezo ya sekondari Tanzania) enzi zile na kina Masumbuko Hassani uwanja wa Majimaji pale,yaani kama siyo kuvua samaki hapa nyasa basi leo ningekuwa ughaibuni shauri ya kucheza soka tena kule Hispania shauri napenda sana soka lao maridadi halina fujo kama soka Uingereza wanaojisifu na........malizia wewe..