March 02, 2009

Nakumbuka Mengi sana

Nayakumbuka mengi niliyoyaona na kuishi. Nakumbuka enzi zile kuvaa kandambili tu bonge la utajiri. Nakumbuka mbali kwa kweli, nakumbuka bibi akiwa mfinyanga vyungu. Nakumbuka kwakuwa wazazi wangu walikuwa na ahueni ya maisha basi hali hii niliepuka kidogo sana. Na kwakuwa kila jambo lifanyikalo lilionekana basi kila mtu anajua kwanini nina uchungu pia na msimamo mkali. Weka mapenzi kando, nipe hoja msingi! Ni wangapi mtanipenda nikiwa sina SHILINGI?????

Nikumbuka sana maisha yale, kuvaa viatu tu tulichukiwa eti watoto wa matajiri, lakini nikiangalia hali nyumbani eti kwakuwa nilikuwa na viti vizuri kama vya ofisini. Nakumbuka niliwahi kupigwa kwa kuitwa :najivuna" kwa hali yetu nyumbani, lakini nakumbuka tulikuwa tunakunywa chai isiyo na sukari tena kwa mihogo jamani.
Nikikumbuka muundo ule ndiyo maana wazazi wangu walipiga sana kelele hoja yangu ya kutaka kucheza soka tu bila kusoma shule. Nakumbuka baba yangu anaposema 'huna kitu hapa nyumbani, tafuteni vyenu kwani hivi ni vyangu na mke wangu"

Nakumbuka sana, yaani unaona wengi wanakuchukia sababu wewe kwenu kuna wageni wanakuja toka mbali, au kwavile ndugu zako wanasoma mahali. Jamani, mazingira yangu yananikumbusha na kunitoa machozi, yananifanya nione hakuna ninayeweza kumwamini kama siyo mimi ingawa wakati mwingine simwamini hata mimi mwenyewe..
Lakini leo najua wapi nilipotoka, wapi nilipoanzia na wapi niliposimama kabla ya kutembea na vidole katika blogu tena kabla ya kugeuka mtundu wa teknolojia niliyojifunza kupitia maandishi kama hadithi ya sungura na fisi. Nisije nikalia zaidi, najua wenzangu hawa wanaweza wakasema mbona umepata nafuu, tuokoe na nasi. NAWAPENDA SANA, SIJAIONA KESHO!!!!