January 24, 2013

HAPPY BIRTHDAY CHADEMA


Ben Saaanane

Na Ben Saanane, Dar es Salaam
Hebu tuone:Chama cha Patriotic Front cha Zambia(Ninakifananisha na CHADEMA katika Historia na Harakati zake Kuchukua Dola) kilichoanzishwa Mwaka 2001 kimeweza kuwa chama imara kwa kuwachukulia hatua wasaliti bila kujali cheo au nafasi ya mtu.
Leo hii tunapoandika hapa waziri wa mambo ya nje Given Lubinda anajiandaa kukutana na kamati ya Nidhamu ya chama hicho kwa tuhuma za kukisaliti chama hicho na kushirikiana na vyama hasimu.
Akipatikana na hatia kwenye kamati kuu ya PF atafukuzwa uanachama moja kwa moja.
Pia wakati huo huo kiongozi wa upinzani Hakainde Hichilema wa chama cha UPND(nilishawahi kukifananisha na chama cha CUF) anakabiliwa na mashtaka ya defamation huku chama Tawala cha Zamani cha MMD(CCM ya Zambia iliyounda aliiance na UPND kuihujumu PF) kikipambana kujinusuru kisifutwe kwa kukiuka sheria na kuhodhi mali za umma.Huu ni mfano mzuri wa kufuata misingi na sio kufuata watu.
Hakuna aliyewahi kuwa juu ya chama.Chama cha ODM nchini Kenya kilichoanzishwa mwaka 2005 kilionyesha njia kuwaondoa akina Ruto,Chama cha MDC nchini Zimbabwe kilichoanzishwa mwaka 1999 kilionyesha njia kwa kuwaacha akina prof.Arthur Mutambara,CCM Chini ya uenyekiti wa Mwl.Nyerere kilifuata Misingi kwa kumfukuza Maalimu Seif akiwa waziri kiongozi(NASIZITIZA CCM ya NYERERE)....CHADEMA leo kimefikisha miaka 20 Rasmi tangu kisajiliwe.
Tuendelee kufuata misingi kwa mifano hii.Happy Birthday CHADEMA,Viva M4C

JOHN STEVEN AKHWARI ANASTAHILI HESHIMA


Na Hance Forogo, Dar es salaam
Mzee wetu tunayempa Heshima leo alizaliwa mwaka 1938 katika wilaya ya Mbulu iliyoko mkoa wa Arusha....hapa namzungumzia mzee John Steven Akhwari!....akiwa kijana mdogo kabisa alianza kujiingiza katika mchezo wa riadha na haikumchukua muda mrefu kuwa mwanariadha wa mbio ndefu wa kutegemewa na Taifa la Tanzania akishiriki mashindano mengi ndani na nje ya Tanzania na amewahi kuwa bingwa wa mbio ndefu wa bara la Afrika,pia mwaka 1970 alimaliza mbio akiwa na 05 katika mashindano ya mbio ndefu kwa nchi za jumuia ya madola!....
Akitumia muda wa 2:15:05 wakati mshindi alitumia muda wa 2:09:28,inaaminika kuwa alikuwa ni mkimbiaji "World Class" mwenye hadhi ya dunia kati ya miaka ya 1960 na 1980!....
Katika tukio la kihistoria,mzee Akhwari katika mashindano ya Olimpiki mwaka 1938 nchini Mexico,katika mji wa Mexico akiwa wanafanya utani na wakimbiaji wa kuviziana na wakimbiaji wengine ili kupitana na kuwania ushindi alianguka ghafla akiwa amemaliza 19km kati ya 42km.
Baada ya kubanwa na misuli tatizo lililotokana na hali ya hewa kwani kabla hakuwa amefanya mazoezi katika mazingira yenye hali ya miinuko na hali ya nchi kama ya Mexico.
Kutokana na tukio hilo aliteguka goti na kupata jeraha kubwa pia alipata maumivu makali kwenye bega lake!.....hata hivyo aliendelea na mashindano na kumaliza wa mwisho akitumia muda wa 3:25:27 kati ya 57 waliomaliza mbio wakati wanariadha 18 hawakuweza kumaliza mbio huku mshindi Mamo Wolde toka Ethiopia akitumia muda wa 2:20:26!....baada ya muda mfupi kumaliza mbio zake,waandishi walimfuata na kumuuliza kwa nini aliendelea na mbio wakati alikuwa ameumia sana!?....
akajibu kuwa "Nchi yangu(Tanzania) haikunituma kushiriki maili 5000,imenituma nije kumaliza mbio za maili 5000" Jina lake linatumiwa na taasisi ya John Steven Akhwari Athletic Foundation ambayo inatumika kuandaa wanamichezo wanaojiandaa kwa mashindano ya Olimpiki,mwaka 2000 alialikwa kwenye mashindano ya Olimpiki yaliyofanyika Sydney nchini Australia na baada ya hapo alichaguliwa kuwa balozi wa heshima katika maandalizi ya mashindano ya Olimpiki jijini Beijing,China,pia 13/04/2008 alihusika na ubebaji wa Mwenge wa Olimpiki ulipokuja Tanzania katika maandalizi ya Olimpiki!....
Licha ya kwamba mwaka 1983 mzee wetu alitunukiwa medal ya heshima kama shujaa wa Taifa "National Hero Medal of Honor" hatuna budi nasi pande hizi KUMPA HESHIMA ZAKE kwa juhudi kubwa na uzalendo alioufanya kwa ajili ya nchi yake!....ameitangaza nchi kupitia mchezo wa riadha!.....
Huyo ndiye mzee John Steven Akhwari ambaye kwa sasa ni mkulima stadi,hakika anastahili HESHIMA!....Thanx!...

January 23, 2013

SAKATA LA GESI LIMEZUA JIPYA MKOANI MTWARA-Mgodi Unaotembea


Kambi Mbwana

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

HALI ya mkoani Mtwara ni dhahiri inatishia amani, hivyo kuna kila sababu ya serikali na wadau wote kukaa na kuliangalia suala hilo kwa marefu. Nikiwa kama Mtanzania, nimekuwa nikifuatilia kwa karibu mno sakata hilo la gesi inayopingwa na wadau kuletwa jijini Dar es Salaam, badala yake wanataka ibaki mkoani Mtwara, ingawa wenye akili ndogo wanapinga au kutukashifu kadri ya uwezo wao, wakijidanganya kuwa sipaswi kufuatilia mambo ya Mtwara na Lindi.
Huu ni udhaifu na hauwezi kuchekewa, maana ni dhahiri Mtwara, Lindi ni sehemu ya Tanzania kama ilivyokuwa Tanga, Arusha, Kilimanjaro na kwingineko. Wananchi hao waliojikusanya kwa ajili ya kupigania sakata hilo, wamefikia kubadilisha kabisa hisia zao, bila woga wowote katika kulizungumzia suala la gesi.
Kama nilivyowahi kuhoji hapo nyuma, kuwa tatizo ni gesi, choyo, siasa au ubaguzi? Makala haya yalitoka katika blog hii ya Handeni Kwetu na kupokea maoni mbalimbali. Na haya ndio maoni ya Watanzania hao wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Mwanzo wa ugaidi Tanzania ni mwisho wa amani. Kusini hawaogopi jeshi. Kauli ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete ipo kwenye mioyo yao. Leo nasema, ila wana Mtwara watasema kwa sauti zao, maana vitisho kwao ni kama kuitukana maiti.
Chochote kitatokea iwe ni vita vyovyote vile 2015 hatutaki uchaguzi na hatutaki pia tuletewe kiongozi na ole wenu, +255712897794
Maandamano Mtwara
Kaka nimefurahishwa na makala yako isemayo Tatizo ni ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Inaonekana na wewe pia umeandika makala hii kwa lengo lako binafsi. Umeshindwa kutoa uhalisia wa jambo lenyewe, badala yake umeandika kwa lengo la kutaka kumfurahisha ama kuwafurahisha watu fulani. Rudi nyuma angalia wanachofanyiwa wakulima wa korosho wa Mtwara je ni sahihi? Lile zao halisaidii kuinua pato la Taifa? Angalia hali ya maisha ya wakazi wa Mtwara. Nadhani umekurupuka na si mawazo yako kuna mkono wa mtu nyuma yako.
Nenda kazunguuke na kufanya utafiti wa kina utapata majibu sahihi kwa wenyeji. +255657614354.
 Tatizo la mikoa ya Kusini sio gesi bali ni kusahauliwa kwa miaka 51 ya Uhuru. Korosho, reli, Bandari, miundo mbinu, tatizo la elimu na kuwa waanga wa ukombozi wa nchi zilizopo kusini mwa Afrika.
Wanasiasa kujiingiza katika hoja si ajabu kwasababu duniani kote wanasiasa ndio huibua matatizo ya wananchi , maana wasomi wetu wengi hawana meno ya na ndio wanaopitisha  mikataba mibovu .
Sio choyo, lakini tunafikia wakati tunajuta kwa nini sisi Mtwara Lindi tumekuwa sehemu ya Tanzania. Tuna rasilimali tosha za kuweza kuitwa, kama vile Bandari, Bahari, Ardhi yenye rutuba, watu, mito, madini, korosho, ufuta, mhogo na nyinginezo. Kusini tuna haki ya kumdai mume wetu Tanzania haki zetu za msingi, maana tumevumilia mno hadi kilio cha kwi kwi. Ni mimi mwanaharakati,  Amoni, wa Kata Msangamkuu, Mtwara Vijijini. +255652221100.
Ninaomba uelewe lengo la wananchi wa Mtwara na Lindi sio kwamba hawataki gesi isitumiwe na wengine hapana, wao wanataka kiwanda kitengenezwe Mtwara. Kule itoke gesi safi, maana wanakataa mambo yasijekuwa kama ya madini ya Geita ambayo mwekezaji anachimba anaenda kuhakiki Mwanza na kulipa kodi ya uwongo na kuiibia nchi na kuwa masikini, huku wakifaidi watu kutoka nje.
Nimesoma makala yako, inayosema tatizo ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Mimi nimeisoma na kwa utafiti wangu, nimegundua kwamba wewe ni CCM na ndio maana ukaona eti ni siasa. Hapana, ni kwasababu vyama vya upinzani vinapenda maendeleo ya Watanzania.
Mbona hawakuhamisha miwa kutoka Kagera na kuileta Dar es Salaam ili itengenezwe hapa? Pili, hebu fikiria gharama za kuweka bomba ni kiasi gani? Tatu, kumbuka msongamano mkubwa wa watu, ina maana wakiongeza viwanda wanazidisha msongamano. Nne, kwanini wasiwaachie watu wa Mtwara na Lindi na wao wapate ajira? Tano, kila kilichokuwapo Dar es Salaam, Mtwara kipo kama vile Bandari na mengineyo. +255713221244.
Ingawa hujaonyesha wazi ujumbe unaopeleka kwa wana Mtwara, lakini ninachofahamu, Taifa halina rasilimali. Mikoa, wilaya, vijiji, ndivyo vyenye rasilimali, kama vile mbuga za wanyama, madini, mazao na mengineyo ambayo mapato yake hukusanywa na kuwa pato la Taifa. Gesi ni kama rasilimali nyingine tu. Ikiwa Mtwara, Lindi, Kigoma, Mbeya au popote nchini, tueleze ni vipi italinyima Taifa letu pato? Au italigawa vipi Taifa? +255717757797.
Hongera bwana Kambi Mbwana kwa makala yako. Endelea kuwapa elimu Watanzania wenzetu wasioelewa. Naitwa Moi, +255757295249.
Unajua sisi tunaotoka Mtwara tunafananishwa na nyani katika Taifa hili. Hatuna thamani mbele ya makabila mengine toka Uhuru. Barabara haijaisha, mazao yetu hayana usimamizi na hatuna huduma za jamii zilizo bora. Tukipata wakarimu, sio bora pamoja na watumishi wote. Sisi ni jamii ya mwisho katika Taifa hili, hujiulizi gesi na mafuta aliyotupatia Mwenyezimungu ingekuwa sehemu nyingine ingehamishwa? Kwakuwa sisi nyani, hatuna thamani, gesi itaondoka na mafuta pia yataondoka, maana hawa hawatatuthamini milele. +255712848839.
Asante kwa makala yako, lakini usiwe mwandishi mwoga anayeogopa watawala walioshindwa kuwaondolea wananchi umasikini na kuligawa Taifa, kati ya wenye nacho na wasiokuwa nacho. Jitahidi kuwa mkweli ili upate mafanikio maishani mwako. +255755045295. Kijana mbona unakuwa kama popo asiyejulikana kama ni mnyama au ndege. Ya Handeni Kwenu yamekushinda sasa umehamia kwenye gesi.
Nasikitika ujumbe huu uliotumwa kwa namba +255757602075. nimeufipisha kwa sababu za kimaadili, maana ulijaa matusi na kashfa kutoka kwa mtumaji, ambaye pia hakujitambulisha jina lake. Kaka nimesoma makala zako nyingi, nimegundua wewe ni kada wa CCM na usiyejua nini wanachokitaka Watanzania.  Hata hujui huko vijijini watu wanaishi vipi. Unaogopa ya Daudi Mwangosi na Amina Chifupa na huo sio uzalendo, hivyo hupaswi kuwa mwandishi.
Hivi unajua CCM wanaiendashaje nchi hii? Umeshahoji wananchi wangapi kuhusu maisha yao badala yake unamfuata Nape Nnauye, unataka CCM ndio waiongoze nchi milele na milele kwakuwa wewe si mzalendo. Ujumbe huu ulitoka kwa namba +255652273836. Nashukuru brother kwa kuweza kupata fursa ya kuweza kusoma makala yako.
Ni kweli hoja zako ulizozisema zinaweza kushabihiana na ukweli,  ila kutokana na vile hali ilivyo naweza (kudetermine ya words) nazo yanatokana na siasa pia. Hebu nambie kaka angu, umaskini uliopo katika mikoa ya kusini, moja kwa moja tumekuwa maskini na hii ilikua nafasi pekee ya kuweza kupata ahueni.
Hebu jamani isifike wakati tukawa tunaangalia swala hili kijuu juu, hali ni mbya kusini hatuna pa kushikia, serikali ilibidi iangalie gesi hii pia katika kutafuta namna ya kuikomboa miji hii ya kusini.
Ni wazi kuwa serikali imekua ikifurahia tu kupata neema hiyo kuendesha mambo yao na si kusaidia kuondosha umaskini.
Nyinyi waandishi tunawategemea kutoa hoja za kusaidia kuondokana na majanga ya kimaskini. Ujumbe huu ulitumwa kwa njia ya barua pepe kutoka kwa Raya Juma, Nashkuru Haya ni baadhi ya maoni yaliyoingia mara baada ya kuandika makala ile, huku watu wakiingia moia kwa moja katika hoja yangu ya siasa, ubaguzi na choyo nilizokemea. Kwanini nasema siasa? Ukiangalia hapo, wapo waliotuma ujumbe huo wakiwa na chukia serikali ya CCM. Hata hivyo, kuyaanika maoni yao si kuwaletea matatizo, bali kusoma mawazo ya watu wa Mtwara.
Wao ndio wahusika. Ndio wenye kupigania suala la gesi, hivyo inaweza kuwa njia muafaka ya kuepusha shari inayozidi kujengeka mioyoni mwa Watanzania, hususan wale wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Watu wamekuwa na mawazo tofauti juu ya sakata hilo. Wapo wale wanaofikia kutamani Mtwara iwe na utawala wake, jambo ambalo hakika si la kuchekea.
Rasilimali za Tanzania zinaanza kutugawa kadri siku zinavyozidi kwenda mbele, ndio maana nikaamua kuyaanika mawazo ya ndugu zetu hao. Kwa kumalizia tu, sakata la gesi linaweza kujadiliwa upya kwa kuwashirikisha wadau na wananchi wa Mtwara, hasa kwa kupewa mikakati ya namna ya serikali kuwapelekea maendeleo maana ni wajibu wao.
Masuala ya chokochoko ya gesi yasiachwe tu kwa wanasiasa ambao wamekuwa wabunifu kuingia kwenye hoja zinazoshirikisha watu kwa ajili ya kujijenga kisiasa, jambo ambalo si zuri.
Na sisi tunaofikia kujadili suala la gesi, wakiwamo wana harakati, wasitumie maneno makali, maana siku zote jazba inaondosha maana husika. Maoni mengi ya Watanzania nimeshindwa kuyaandika kwa kwasababu hayajatolewa kiungwana, huku niliyoaandika nikiyafanyia marekebisho mengi mno.
Katika hili, serikali kwa kupitia Waziri wake wa Nishati na Madini, Professa Sospeter Muhongo, anapaswa kukaa na kulijadili jambo hili kwa mapana yake.

kambimbwana@yahoo.com
www.handenikwetu.blogspot.com
+255712053949
+255753806087

January 22, 2013

EMMANUEL NDEMBEKA, WAKILI MWENYE MAJUKUMU MENGI KWA WAKAZI WA WILAYA YA NYASA


Na Mwandishi Wetu, Mbamba Bay
Mwaka 2012 utakuwa wa kukumbukwa sana kwa wakazi wa Mbamba Baya na vitongoji vyake vinavyounda pia wilaya ya Nyasa. Moja ya tukio la kuelekea mwisho wa mwaka wa 2012 ni baadhi ya vijana kutoka wilaya ya Nyasa kutunukiwa nishani za uwakili kutokana na taaluma zao za sheria. Miongoni mwa vijana hao ni dada yetu mpendwa Beatrice Mpangala. Yeye ni wakili kwa sasa na analo jukumu kubwa la kusimamia haki ya wananchi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania. 
Emanuel Ndembeka alipoapishwa kuwa wakili
Mbali ya huyo, kijana mwingine Emmanuel G. Ndembeka alitunukiwa uwakili kama ilivyo kwa dada Beatrice Mpangala. Emmanuel G. Ndembeka kijana mzaliwa wa Mbamba Bay, alianza elimu yake ya sekondari akiwa Lundo Sekondari kabla ya kuhamia Kigonsera sekondari maarufu kama Caigo Boys. 
Kigonsera sekondari ndio aliyosoma aliyekuwa rais wa awamu ya tatu katika jamhuri ya muungano wa Tanzania, Benjamin William Mkapa, mzaliwa wa Lupaso mkoani Mtwara. Emmanuel G. Ndembeka anakuwa mtetezi wa jamii yetu kutokana na taaluma yake. 
Umuhimu wake katika jamii ya watanzania ni mkubwa. Mosi, wana jamii wa wilaya ya Nyasa wanajivunia kuzalisha kijana mwenye taaluma ambayo itawasaidia kwa kiwango kikubwa katika kuelewa haki za kumiliki ardhi. 
Kama tujuavyo kwa wakazi wa wilaya ya Nyasa wengi wao wanamiliki ardhi kwa mtindo wa kiutamaduni yaani kurithi ardhi kutoka kwa wazazi hadi kizazi kingine. Matokeo ya jambo hili ni baadhi ya wakazi wasiokuwa na uelewa juu ya haki za kuhifadhi ardhi zao wanaziuza kwa bei ya chini sana kiasi ambacho husababisha matatizo kifamilia. Emmanuel G. Ndembeka anafahamu hili, na kutokana na uelewa wake na namna ya kuelimisha jamii ya wanyasa juu ya kuhifadhi ardhi bila shaka atakuwa mstari wa mbele kuwalinda na kutoa elimu mbadala ili kuzuia uuzaji radhi holela. 
Wakazi wa nyasa wanajivunia kijana ambaye amekulia mazingira yao na anayaelewa kwa kina zaidi. Kwa niaba ya wasomaji wote na wenyeji wa Nyasa, mtandao huu wa Lundunyasa(Lundunyasa Network) unamtakia kila la heri katika mafanikio zaidi. Pia tumkumbushe anauanza mwaka 2013 akiwa na nishani ya wakili mwenye elimu inayotosha kabisa. Mwenyezi Mungu amjaze hekima, upendo na amani zaidi. WAKILI EMANUEL NDEMBEKA, TUNAKUTEGEMEA SANA.

TEKNOLOJIA YA GOLI ITAMALIZA UTATA WA MAGOLI?


Na Markus Mpangala

Mwaka 1986 Diego Maradona alifunga bao la mkono, lakini mwamuzi hakuona akakubali kuwa ni bao halali. Waingereza walilalamikia hilo, lakini mwamuzi alishapitisha uamuzi wake ni bao halali. Tangu hapo Maradona amekuwa akisema bao lake hilo ni la ‘mkono wa mungu’. Mwaka 1966, kiungo wa England, Geoff Hurst apiga shuti kali likagonga mtambaa panya na kugonga chini kisha kurudi uwanjani. 
Diego Maradona

Lakini wakati mwamuzi wa mchezo hajaamuru chochote wachezaji wa England wakaungana na kiungo huyo kushangilia na mwamuzi akakubali ni bao halali. Lakini mpira ule ulipogonga mtambaa panya kisha kugonga chini wala haukugusa mstari. Geoff Hurst akaingia kwenye rekodi ya dunia kwa
kufunga mabao matatu katika mechi ya fainali. Rekodi hiyo imefikiwa na kinda wa Brazil, Oscar Dos Santos ambaye alifunga mabao matatu wakati wa mechi ya fainali ya kombe la dunia kwa vijana chini ya miaka 20 dhidi ya Ureno. 
Lakini miaka 44 baadaye yaani mwaka 2010 katika michuano ya kombe la dunia nchini Afrika Kusini, ni England iliyonyimwa bao.
Frank Lampard alifumua shuti kali likagonga mtambaa panya kisha litua ndani ya lango huku kwa kasi ya ajabu golikipa wa Ujerumani, Manuel Neuer alidaka kiustadi mkubwa.
Mbwana Samatta, akikabiliana na beki wa Zamaleki ya Misri
Mwamuzi wa pambano hilo alikataa kuwapa bao England. Waingereza walichachamaa baada ya michuano hiyo huku wakikumbuka kipigo cha mabao 4-1 walichopata kutoka kwa Ujerumani. 
Waingereza wakasahau kuwa wao walitwaa kombe la dunia kupitia bao lenye utata, kwani walifanikiwa kuifunga Ujerumani ya akina Franz Backenbauer na  Gerd Muller. Lakini ilipotokea kwao kunyimwa bao wakapayuka dunia nzima. Na sasa majadiliano ya kutumia Teknolojia ya goli yakachukua mkondo wake.Teknolojia hiyo maarufu kwa jina ka Jicho la Kipanga (Hawk Eye) ilipenyezwa katika korido la FIFA ili ipate uungwaji mkono. 
Nadhani teknolojia hiyo ilipaswa pia kutumika kutambua mpira wa kichwa uliopigwa na mshambuliaji wa Kilimanjaro Stars, John Bocco dhidi ya Burundi kwenye michuano ya CECAFA inayoendelea nchini Uganda. Tukiacha hilo, ni wazi sasa teknolojia ya goli (Hawk Eye) itakuwa njia mbadala huku tukikumbuka shirikisho la soka la Ulaya linatumia waamuzi watano katika pambano moja. 
Waamuzi wawili wanakaa nyuma ya goli, yaani mmoja mmoja kila upande. Hivyo ukiongeza na mwamuzi wa akiba wanakuwa watano. Naam, Jicho la Kipanga(Hawk Eye) imeshakubalika na kuthibitishwa na FIFA. Kwahiyo, FIFA imesaini  Mkataba Matumizi ya Teknolojia ya kutambua goli (Hawk Eye). Teknolojia hiyo itafanyiwa majaribio nchini Japan, ambapo baadaye itajaribiwa kwenye michuano ya klabu bingwa dunia itakayofanyika nchini humo. 
Dhumuni la teknolojia hii ni kutoa msaada kwa waamuzi ili kuamua kama Mpira umevuka mstari wa Goli na hivyo kuwa Goli halali. FIFA imepiga hatua mbele baada ya kusaini Mikataba na Kampuni mbili za Waundaji wa Mitambo itakayotumika ya kutambua goli. Mitambo hiyo inajulikana kwa jina la GLT (Goal Line Technology).
Kampuni za zilizoshinda tenda hiyo ni Hawk-Eye Innovations na Fraunhofer ISS (GoalRef), ambapo mitambo yake itatumika kwenye Mashindano ya FIFA ya Klabu Bingwa Duniani huko Japan kuanzia Desemba 6 hadi 16 mwaka jana. 
Franz Beckenbauer
Katika hali hiyo wengi wanaweza kusema ni suala zuri kwa maendeleo ya mpira wa miguu. Lakini vilevile tunapaswa kuwaangalia waamuzi na mamlaka yao katika mechi na soka kwa ujumla. Kwa hali halisi kwanza teknolojia hiyo itaondoa kabisa malalamiko ya mabao ambayo yanakataliwa na waamuzi. Lakini vilevile itasaidia waamuzi kuwa na nafasi bora kuondoa malalamiko yoyote ambayo yatachangiwa na uamuzi wao. 
Tekonoliia hiyo inatumika pia katika mchezo wa Tennis ambapo humsaidia mwamuzi kuangalia mpira kama umegusa mstari au umeangukia nje ya mstari au ndani ya uwanja. Teknolojia hiyo inasaidia sana waamuzi wa Tennis kuamua pointi halali kwenye kutafuta Seti. Tumeona hayo kwenye michuano mingi kama US Open, Wimbledon, Ausralia Open, Beijing Open, Olimpiki, na michuano kemkem
inayosimamiwa na shirikisho la Tennis. Hata hivyo kwa suala hili bado naona tunawahitaji sana waamuzi ambao wanaweza kutuletea matokeo mazuri dimbani. Licha ya kuletewa teknolojia hii bado tunahitaji kuwaamini waamuzi ingawaje kuna nyakati wanakera. Pia teknoloajia hii inaamua magoli tu, lakini haitoi nafasi kwa rafu mbaya au mchezo mbaya wa mchezaji fulani ambao mwamuzi anashindwa kuona. 
Mathalani Mwinyi Kazimoto, David Beckham, Dickson Daudi, na wengineo wamekuwa waathirika wa ukosefu wa teknolojia ambayo ingeweza kusaidia namna bora ya kubaini uchezaji mbaya kwa baadhi ya wachezaji.
Madhara ya teknolojia hii ni kuongezeka kwa malalamiko mengine ya uamuzi wa waamuzi. Hali ambayo itawapotezea uwezo wao wawapo dimbani. Ni hatua nzuri kwa Hawk Eye lakini ni wakati mzuri pia kuchambua makosa mengine dimbani yanayostahili kutegemea kamera ili kuepusha madhara kwa wachezaji.

January 21, 2013

SETH DE JESUS GIOVANNI NA HUDUMA MPYA YA USHAURI WA KIMAPENZI


STRAIGHT TO YOUR PHONE ndio Service nimeizindua rasmi leo.Do you believe kuna True Love dunia ya leo???Je,unaamini you can fall inlove again baada ya kuumizwa sana???Unataka kujua jinsi ya kum-handle Mwanaume/Mwanamke unayempenda??Unataka kujua jinsi ya ku-deal na Mpenzi wako mkorofi na asiyekujali??
Yote haya utayapata Ukijiunga na Huduma hii ya SETH...Tutajadili kama tunavyojadili kwenye Wall hii lakini this time popote ulipo,huna haja ya ku-Log in Facebook kujua. Ukiwa mteja wa Mtandao wowote ule,iwe TIGO,AIRTEL,VODACOM au ZANTEL ukituma neno SETH kwenda 15678 utakuwa umejiunga na Huduma hii BURE!Hukatwi chochote kwa kutuma SMS hiyo!
Kuanzia sasa nitakuwa natuma Status ya Siku kwenye Simu yako ya Mkononi na utapokea ujumbe huo kama SMS...Najaribu kuyafanyia kazi Maoni yenu,kila mmoja kwa kadri Mungu anavyonijalia...
...SMS utaipata popote ulipo kwenye Simu yako na kama una tatizo au swali lolote,NITAKUJIBU!
SETH kwenda 15678,Please Support me on this one,NAWAPENDA! 

MRADI WA MAJI SAFI NA SALAMA KIGONSERA-MBINGA

Na Mwandishi Wetu, Kigonsera

Kigonsera ni miongoni mwa miji muhimu sana wilaya ya Mbinga. lkaini kwa kipindi kirefu baadhi ya wakazi wa mji huo walikuwa wakikabiliwa na uhaba wa maji safi na salama. kwa sasa mradi mkubwa wa kusambaza maji safi na salama katika wilaya ya Mbinga umeshika kasi huku mji wa Kigonsera ukiwa miongoni mwa miji muhimu sana kiuchumi na biashara.
 Ni mji ambao upo pembezoni mwa barabara kuu iendayo Songea mjini kutokea Mbinga. Kutokana na shughuli nyingi za kiuchumi, watu wengi hutumia mji huu kufanya biashara na zingine za ujenzi wa taifa, hivyo wanahitaji huduma muhimu sana ili kusogeza mbele maendeleo ya mji wao na taifa kwa ujumla.
       
Pichani msimami wa Mradi ndugu Egbart Jeremy akiwa katika intake ya maji safi na salama mjini Kigonsera, ikiwa ni moja ya miji ambayo inatakiwa kufanyiwa marekebisho ya kuleta uhuduma ya maji kwa wakazi wake.


     
Wahandisi wa maji wa wizara ya maji, mkoa wa Ruvuma na wilaya ya Mbinga wakikagua ujenzi wa tanki la maji lenye uwezo wa kubeba ujazo wa mita za ujazo mia mbili(200) katika mji wa Kigonsera. Tanki hilo lipo katika ujenzi na kampuni ya ujenzi ya Mwalongo Cont ya mkoani Njombe.

UHARIBIFU WA MAZINGIRA MDUNDUALO-MBINGA


Egbart Jeremy
Na Egbart Jeremy, Mbinga

Utunzaji wa mazingira umekuwa jambo muhimu sana. Kwa muda mrefu ripoti mbalimbali zimekuwa zikielezea juu ya umuhimu wa kutunza mazingira. Kuna wataalamu wa mazingira wamekuwa wakishughulikia ukaguzi wa mazingira katika maeneo mbalimbali kwenye wilaya ya Mbinga. Miongoni mwao ni hapa pichani wataalamu wa mazingira wakikagua uharibu wa mazingira uliojitokeza kwenye maeneo mbalimbali.
Mathalani ni kijiji cha Mtundualo, kilichopo kwenye wilaya ya Mbinga ambako kunaendeshwa uchimbaji wa makaa ya mawe (TANCOAL). mtundualo ni miongi mwa maeneo yanayokaguliwa mara kwa mara kutokana na hali iliyowahi kujitokeza pia katika kijiji cha Ndumbi, kilichopo wilaya ya Nyasa.

Mtaalamu wa mazingira kutoka ofisi ya mkurugenzi mtendaji wa wilaya, Egbart Jeremy akijadiliana jambo na ofisa usalama na mazingira kutoka mgodi wa makaa ya mawe(TANCOAL) kuhusu uchafuzi uliofanywa na 




Timu ya wataalamu wa mazingira wakikagua uharibu wa mazingira kijiji cha Mdundualo
                            
Mtaalamu Egbart Jeremy akikagua maji yanayodaiwa kuathiriwa na uchafuzi wa mazingira kutokana na uchimbaji wa makaa ya mawe(TANCOAL)

NINI SABABU YA UMASIKINI AU UTAJIRI WA NCHI?



Na Dkt. Hamisi Kigwangalla
Mnamo mwaka 1945 wakati vita kuu ya pili ya dunia ilipokuwa inaelekea kuisha, Korea ambayo ilikuwa iko chini ya utawala wa kikoloni wa Japan toka mwaka 1910 ilipata uhuru wake. Kabla ya hapo majeshi ya ukombozi ya Korea (Korean liberation army) yalikuwa na mpango wa kupigana na japan ili kudai uhuru wao. Kama bahati haikufikia kwenye kudai uhuru kwa vita lakini anguko la Japan kwenye vita kuu ya pili ya dunia ilifanya Korea ipewe uhuru wake bila mtutu wa bunduki. 
Ndani ya mwezi mmoja tu baada ya Japan kunyoosha mikono juu, Korea ilijikuta ikigawanywa mara mbili kwenye mstari unaojulikana kama ‘the 38th parallel north’ (nyuzi 38 kaskazini na sambamba na ikweta) na kuwa mamlaka mbili tofauti zenye ushawishi tofauti. Kusini ikiwa chini ya usimamizi wa Marekani na Kaskazini chini ya Urusi.
Amani ya kipindi cha vita baridi kati ya mamlaka hizi mbili iliisha katikati ya mwaka 1950 pale Korea ya Kaskazini ilipoamua kuivamia Korea ya Kusini na kufikia hadi kuuteka mji mkuu wa Korea ya Kusini, Seoul.
Leo hii nchi hizi zimekuwa dunia mbili tofauti kabisa. Korea ya Kaskazini ikiwa na mfumo tofauti kabisa wa kiuchumi na ile ya kusini. Pengine sababu pekee inayozitofautisha hizi Korea mbili, ambazo zamani zilikuwa moja na sawia kabisa katika kila Nyanja. Leo hii Korea ya Kaskazini hakuna ruhusa kuwa na simu ya mkononi inayotoa mawasiliano nje ya mipaka ya nchi, kuna watu wanaishi chini ya dola moja, kuna ugumu wa namna ya kusafiri kutoka sehemu moja mpaka nyingine, wakati ndugu zao wa Korea ya Kusini wanaishi maisha ya utajiri, ya uhuru wa kuwasiliana kwa simu za kiganjani, kwa mitandao na uhuru hata wa kusafiri na kufanya biashara na yeyote yule wa popote pale duniani – tunu ambazo zimewafanya leo hii wawe kwenye nchi ambazo zinahesabika kama ni za dunia ya kwanza.

Wakati Korea ya Kaskazini ikiishi kwa kutegemea misaada ya chakula na fedha kutoka nchi nyingine, Korea ya Kusini imejenga uchumi imara unaotokana na matumizi ya teknolojia na sayansi ya zama za sasa na imekuwa ni mfadhili wa nchi zinazoendelea kama Tanzania na hata Korea ya Kaskazini.

Ukiangalia kwa undani sana utabaini kuwa kinachotofautisha nchi hizi, zenye historia ya kufanana, zenye jiografia ya kunana, zenye watu wenye kuongea lugha moja, zenye dini, utamaduni na mila na desturi za kufanana, mienendo ya kufanana, kila kitu kinafanana, leo hii kinachowatofautisha si kingine zaidi ya ule mpaka uliowekwa kati yao (the 38th parallel north). Ni nini haswa kinachowafanya wa Kusini wawe matajiri na wa Kaskazini wawe maskini? Maisha ya watu wa Korea ya Kaskazini na yale ya watanzania hayana tofauti sana leo hii wakati yale ya ndugu zao wa Korea ya Kusini yanafanana kabisa na ya wazungu wa Ureno ama wa Hispania. Miaka ya kuishi ya mtu wa Korea ya Kaskazini ni kumi nyuma ya ile ya ndugu zao wa Korea ya Kusini, upande wa pili tu wa ule mstari.

Hizi tofauti zinazoonekana leo siyo za kihistoria. Na kwa hakika hazikuwepo kabla ya ile vita kuu ya pili ya dunia. Kilichotokea baada ya mwaka 1945 ni kwamba hizi serikali mbili, ya Kusini na ile ya Kaskazini zilifuata mifumo miwili tofauti ya kiuchumi, moja ilijenga mfumo wake kufuatia mfano wa kiliberali wa soko huria lililoruhusu uhuru wa masoko na mitaji kama ule unaofuatwa na nchi za magharibi na marekani, na nyingine, Korea ya Kaskazini, ilifuata mfumo wa kikomunisti.

Japokuwa marais wa kwanza wa Korea ya Kusini hawakuweka mfumo wa kisiasa wa kidemokrasia, wengine wanasema kwa kuhofia kuvamiwa na mfumo wa kitawala wa kikomunisti uliokuwa unasambaa kwa kasi sana maeneo ya Asia wakati huo, walisimamia mfumo wa soko huria. Marais hao, Syngman Rhee, ambaye alisomea vyuo mashuhuri duniani vya Harvard na Princeton, na mwenzake Jenerali Park Chung-Hee, ambaye ni baba mzazi wa Rais wa kwanza wa kike wa nchi hiyo aliyeshinda uchaguzi mkuu juzi tu hapa, wameingia kwenye historia za marais waliotumia nguvu kuongoza nchi yao na ikafanikiwa.
Rais wa pili wa Korea ya Kusini atakumbukwa daima na watu wa Korea ya Kusini kwa kusukuma ruzuku na mikopo kwenye makampuni yaliyoonesha mwelekeo wa kufanikiwa. Kwa upande wa Korea ya Kaskazini, Kim Il-Sung, ambaye alikuwa kiongozi aliyeendesha harakati za kikomunisti za kupinga utawala wa kijapan alitawazwa kuwa Rais wa Korea ya Kaskazini mwaka 1947, na moja kwa moja aliwekeza nguvu zake katika kujenga mfumo wa kiuchumi ambao uliweka chini ya serikali kuu mamlaka yote ya kuandaa mipango ya kukuza na kuendesha uchumi wa nchi chini ya mfumo wa kikomunisti wa ‘Juche’. Rais Kim Il-Sung alizuia mfumo wa soko huria na hakukuwa na ruhusa ya kumiliki mali binafsi.

Hakuna jiografia, wala utamaduni, wala historia ya nchi inayoweza kuelezea tofauti ya kiuchumi kati ya nchi hizi mbili, ambazo si zaidi ya miaka 60 iliyopita zilikuwa nchi moja. Tukichukulia haya ‘maajabu ya Korea ya Kusini’ (the south Korean miracle) kama somo, tunapaswa tujifunze kitu, kwanza tuangalie ni nini chanzo cha kuendelea kwa Korea hii moja na kushidwa kwa nyingine? Majibu yake yanapatikana, kwa vyovyote vile kwenye mfumo wa kisiasa na kiuchumi uliofuatwa baada ya uhuru wa Korea kutoka chini ya utawala wa kikoloni wa Japan. 
Moja ilifuata mfumo wa soko huria na nyingine mfumo wa kikomunisti, je tofauti hizi za kimfumo zinaweza kutumika pia kuelezea utofauti wa kiuchumi kati ya Tanzania na Kenya? Na je sababu hizi zinaweza kutumika kuelezea spidi ya ukuaji wa Uchumi wa nchi ya Rwanda? Sina jibu sahihi la maswali haya. Watanzania tuendelee kujipanga, pengine tusijidai sana na nafasi yetu kijiografia, kihistoria na hata kiutamaduni, maana jibu la umaskini wetu halipo huko, lipo kwenye mfumo wa kisiasa na kiuchumi tunaoufuata.
Mafanikio baina ya nchi kiuchumi yanatofautiana kwa sababu za tofauti ya aina za taasisi walizoweka kwenye nchi husika, sheria, kanuni na taratibu zinazoathiri uchumi walizotunga na namna ya motisha walizoweka kwa ajili ya watu wao. Angalia tofauti ya mtoto wa Korea ya Kaskazini na yule wa Korea ya Kusini, mmoja anakua huku akipata elimu ya uhakika na itakayomwezesha kushindana, anapata motisha ya kushindana kuingia kwenye ujasiriamali na anakuta kuna mazingira ya kumwezesha kufikia ndoto yake wakati mwingine hapati elimu stahiki na hana fursa ya kuanzisha, kumiliki mali na kuendesha biashara; ni yupi kati yao atakuwa na motisha ya kufanya ubunifu na kutafuta pesa?

Dkt. Hamisi Kigwangalla ni Mbunge wa Jimbo la Nzega, Mkoani Tabora. Amesoma shahada ya kwanza ya udaktari wa tiba, na ana shahada mbili za uzamili, moja kwenye afya ya jamii na nyingine kwenye uongozi. Na sasa anaandika tasnifu ya shahada yake ya uzamivu (Ph.D.) kwenye usawa, haki na uchumi, pia anamalizia kuandika kitabu chake kwenye sera za maendeleo.

WAPIGAKURA HABA, WALALAMIKAJI WAMEJAA POMONI


Na Markus Mpangala, Dar es salaam

Markus Mpangala
Wenyeji wa Latini Amerika ndio wavumbuzi wa neno “Suffragium”, ambalo walilitumia kuanzia karne ya 14. Maana ya neno hilo ni “haki ya kuchagua” au “Haki ya kuunga mkono”.

Ni ile hali ya mwananchi kuchagua viongozi, au masuala muhimu kitaifa. Tangu kuvumbuliwa kwa neno hilo ndipo dunia ilishuhudia taasisi za kisiasa zenye kujikita katika haki ya kuchagua au kuunga mkono wagombea mbalimbali katika chaguzi.

Kimsingi mkondo mkubwa wa siasa hizo ulijikita zaidi barani ulaya hususani jamii ya Warumi na Wagiriki hasa katika karne ya 17 na 18. Katika kipindi hicho wanafalsafa mbalimbali walikubali kuwa huo ulikuwa mtindo wa serikali binafsi ambapo mwananchi alikuwa na mamlaka ya kuwachagua viongozi anaowataka. 
Rais Nyerere
Wanafalsafa waliamini kuwa uchaguzi wowote unaofanywa na mwananchi (mpigakura) una lengo la kuunda serikali yake kwa mtazamo wake (Self government). Licha ya mabaidliko ya Kiliberali kuleta mfumo wa uchaguzi wa viongozi kupitia vyama vya siasa, bado muundo wa “self government’ umesalia katika serikali za kisasa duniani kote kupitia chaguzi zinazofanyikwa mara kwa mara kulingana na utaratibu wa nchi husika.
Mathalani Tanzania inafanya uchaguzi mkuu kila baada ya miaka mitano, Malawi kila  baada ya miaka minne sawa na Marekani. uchaguzi wa Rais, Wabunge wa Kongresi, Seneti, Madiwani na kadhalika wote hupitia kapu la mwananchi ambaye analazimika kuwapigia kura ili kuhalalisha mamlaka yao.

Kwahiyo, mamlaka ya mwananchi ya kupiga kura ni makubwa na ndiyo anayeamua kuwa mgombea fulani amepata kura nyingi kuliko mwenzake au wenzake(kama wanakuwa wengi). Baadhi ya nchi hurudia uchaguzi kama hakuna mgombea anayefikisha wastani wa kura zilizopangwa.
Liberia walirudia uchaguzi baada ya aliyeongoza Bi. Hellen Sirleaf kutofikisha asilimia 50, lakini duru la pili alifanikiwa kumshinda mshindani wake George Weah. Senegal pia Mack Sall alishinda uchaguzi baada ya Abdoulaye Wade kukiri kushindwa.
Kwa baadhi ya wanasiasa wapigakura ni nyenzo tu, lakini kimsingi wapigakura ni muhimu sana katika mfumo wa kidemokrasia. Hii inatokana na jinsi ushiriki wao unavyoweza kumfanya mgombea fulani kujivunia kura anazopata.

Hapa nchini Katiba yetu haizuii mgombea asiyefikisha asilimia 50 kuchukua madaraka. Kwa mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2000 haionyeshi kuwa mgombea urais wan chi yetu asipofikisha asilimia 50 basi anyimwe kutangazwa mshindi.

Bali Katiba yetu inampa nguvu yule aliyeongoza kupata kura nyingi bila kujali zimefika asilimia 50 au kidogo. Nadhani Katiba mpya inatakiwa kubainisha kwamba mshindi wa kiti cha urais anatakiwa kutangazwa tu akifikisha siyo chini ya asilimia 50.

Rais Mkapa
Tukisogea mbele kidogo tunaona kuwa katika uchaguzi wamwaka 2015 umekuwa gumzo mno kwa wananchi na mashabiki wa vyama vya siasa. Gumzo hili linatokana na hamasa mpya ambayo wananchi wameipata, na ndio maana ya haki ya kuchagua serikali waitakayo. 


Mwananchi amekuwa akiwapigia kura wagombea mbalimbali katika kiti cha urais, wabunge, madiwani na viongozi wa serikali za mitaa. Inaonekana kutoka utawala wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere tumekuwa na udhaifu mkubwa katika suala la upigaji kura.

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1965, rekodi zinaonyesha kuwa waliojiandikisha kupigakura walikuwa watu 3,373,089. Katika uchaguzi huo waliopiga kura walikuwa watu 2,600,040 sawa na asilimia 77.1.

Mwalimu Nyerere alipata kura 2,410,903 sawa na asilimia 96.46, ambapo wapikura 88,600 sawa na asilimia 03.54 walimkataa, huku kura 100,537 zikiharaibika. Katika uchaguzi wa mwaka 1970, jumla wananchi waliojiandikisha kupiga kura ni 5,051,938.

Wapigakura waliompigia kura za ushindi Mwalimu Nyerere walikuwa 3,465,537 sawa na asilimia 72.2, huku kura 109,828 sawa na asilimia 03.07 zilimkataa, ambapo kura 74,388 ziliharibika.

Aidha, uchaguzi wa mwaka 1975 jumla watu waliojiandikisha kupigakura walikuwa 5,577,566, ambapo wapigakura 4,172,267 sawa na asilimia 93.25 walimpa ushindi Mwalimu Nyerere. Wapigakura 302,005 ambao sawa na asilimia 06.75 walimkataa Mwalimu Nyerere, huku kura 83,322 ziliharibika.

Katika uchaguzi wa mwaka 1980 jumla ya wananchi waliojiandikisha kupigakura walikuwa 6,696,803. Waliompigia kura Mwalimu Nyerere walikuwa 5,570, 883 sawa na asilimia 95.56, ambapo kura 295, 040 sawa na asilimia 04.44 zilimkataa, huku kura 157,019 ziliharibika.

Ukiangalia wastani wake utaona kuwa kuna kura zilikuwa zinaongezeka kwa kila uchaguzi. Mwaka 1965 waliomkataa Mwalimu Nyerere walikuwa  88,600, halafu kura 100,537 ziliharibika, kisha mwaka 1970 kura zilizomkataa zilikuwa 109,828 sawa na asilimia 03.07.

Kwa maana hiyo katika chaguzi hizo mbili Nyerere alishindwa kuwavutia wapigakura, kwani kutoka wapigakura 88,600 sawa na asilimia 03.54 waliomkataa  mwaka 1965 hadi wapigakura 109,828 ambao waliomkataa mwaka 1970 inaonyesha bado wananchi wetu hawakuwahi kuchukua uamuzi mgumu kupitia sanduku la kura.

Katika uchaguzi wa mwaka 1975 wapigakura waliomkataa Nyerere waliongezeka ambapo walikuwa 302, 005 sawa na asilimia 06.75. Lakini mwaka 1980 idadi ya waliomkataa Mwalimu Nyerere ilikuwa ndogo kuliko kwani wapigakura 259,040 walimkataa ingawaje alifanikiwa kushinda kwa wastani wa 95% ya uchaguzi huo.

Ali Hassan Mwinyi aligombea urais mwaka 1985 baada ya Mwalimu Nyerere kujiuzulu. Mwinyi alishinda kwa kura 4,778,114 sawa na asilimia 95.68 kati ya wapigakura 6,910,555 waliojiandikisha mwaka huo.

Kura zilizomkataa zilikuwa zilikuwa 215,626 sawa na asilimia 04.32, huku kura 188,259 ziliharibika. Uchaguzi wa mwaka 1990 wananchi waliojiandikisha walikuwa 7,296,553, lakini waliopiga kura walikuwa 5,198.120 sawa na asilimia 97.79%. Wapigakura 117,366 sawa na asilimia 02.21 walimkataa Ali Hassan Mwinyi.

Uchaguzi wa mwaka 1995 ulikuwa wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi. Mgombea wa CCM, Benjamin Mkapa alishinda uchaguzi huo kwa jumla ya kura 4,026,422 sawa na asilimia 61.82 kati ya wapigakura 8,929,969 waliojiandikisha.

Wagombea wa vyama vya upinzani, Agustine Mrema (NCCR-Mageuzi) alipata kura 1,808,516 sawa na asilimia 27.77. Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) alipata kura 418,973 sawa na asilimia 6.43. John Cheyo alipata kura 258,734 sawa na asilimia 3.97. kura zilizoharibika katika uchaguzi huo zilikuwa 333,936.

Kwenye uchaguzi wa mwaka 2000 waliojiandikisha kupigakura walikuwa 10,088,484, ambapo kulikuwa na ongezeko la karibu milioni 1.2 ikilinganishwa na mwaka 1995. Benjamini Mkapa (CCM) alipata kura 5,863,201 sawa na asilimia 71.74. Profesa Lipumba (CUF) alipata kura  1,329,077 sawa na asilimia 16.26. Agustine Mrema alipata kura 637,115 sawa na asilimia 7.80. John Cheyo alipata kura 342,891 sawa na asilimia 4.20. wakati kura zilizoharibika zilikuwa 345,214.

Uchaguzi wa mwaka 2005 waliojiandikisha kupiga kura ni 16,401,694 yaani wapigakura walioongezeka ni milioni 6. Wapigakura 9,123,952 sawa na asilimia 80.28 ndio waliomchagua Jakaya Kikwete (CCM). Profesa Lipumba (CUF) alipata kura 1,327,125 sawa na asilimia 11.687. Freeman Mbowe (Chadema) alipata kura 663,756 sawa na asilimia 5.88. Augustine Mrema alipata kura 84,901 sawa na asilimia 0.75. katika uchaguzi huo, waliopiga kura walikuwa 11,875, 927 sawa na asilimia 72.4, huku kura zilizoharibika zilikuwa 310,460, kisha watu milioni 5 wakakosa kupiga kura.
Rais Mwinyi
Kwenye uchaguzi wa mwaka 2010 jumla ya wapigakura walikuwa 8,626,283 sawa na asilimia 42.8, wakati waliojiandikisha walikuwa 11,511,020 sawa na asilimia 57.2. ukiangalia hesabu za kura kwa miaka yote utagundua kuwa hakuna wakati ambao wapigakura wetu walichukua uamuzi mgumu kubadilisha uongozi wa nchi hii.

Vilevile hakuna wakati ambao hakukuwepo na kura zilizoharibika. Hii ina maana kuna wapigakura haba, lakini walalamikaji katika nchi yetu hii wamejaa pomoni. Mathalani kama tunafika mahali tunasababisha kuharibika kwa kura, mfano mwaka 1965 (kura 100,537), mwaka 1970 (kura 74,388), mwaka 1975 (83,322), mwaka 1980 (kura 157,019), mwaka 1985(kura 188,259), mwaka 1990 (kura 109,796), mwaka 1995 (kura 333,936) mwaka 2000 (kura 345,314), mwaka 2005 (kura 310,460) na mwaka 2010 zipo kura zilizoharibika.

Katika hali kama hiyo bado wapo watu wamejaa kila kona ya nchi kazi yao kubwa ni kulalamikia hali fulani ndani ya taifa hili. Mlolongo wa kura zinazoonyesha hapo inaelekea CCM imekuwa chama kinachopata kura nyingi kila chaguzi.

Na wapigakura hao ni walewale ambao miongoni mwao wanaruhusu kura 333,936 kuharibika halafu wanalalamika hali duni au hali mbovu juu ya jambo fulani ndani ya nchi yetu au wengine hawapigi kura kabisa. Sijawahi kuona wananchi wa nchi hii wakichukua uamuzi mgumu kupitia sanduku la kura tangu mwaka 1965. Hivyo tunao wapigakura haba, ila walalamikaji wamejaa pomoni.

January 18, 2013

NIMEBOBEA KATIKA UFUGAJI WA NYUKI KWA NJIA ZA KISASA-ERNEST NDONDE

Na Mwandishi Wetu, Mbinga

Miongoni mwa mabadiliko makubwa ya ufugaji wa nyuki ni ile hatua ya watu kuamua kujitoa kwa dhati kabisa kupata mafunzo ya ufugaji wa nyuki. Wengi tumezoea kuona njia za zamani ambazo zinawafanya baadhi ya watu wasio watalaamu kuelezea kuwa wanasumbuliwa na ufugaji wa nyuki pamoja na ulinaji asali kwa ujumla. 
Lakini kijana Ernest Ndonde kutoka Lundu alifanya mazungumzo na Lundunyasa Network, kuelezea juu ya utaalamu wake aliopata huko Mpanda wa kufuga nyuki. 
Yeye anasema wka sasa anakaribia kuanzisha mradi wa ufugaji nyuki katika kijiji cha Mbaha ambacho ni kipo jirani kabisa na kijiji cha Lundu, katika tarafa ya Ruhuhu wilayani Nyasa. Ernest Ndonde aliamua kuchukua ujuzi wa kufuga nyuki wka njia za kisasa kutokana na mahitaji na mabadiliko ya namna ya kulina asali na wateja wake. 
Pia alichukua njia hiyo kuwa moja ya utaalamu ambao anaufanyia kazi katika maeneo mbalimbali ambayo wateja huhitaji mafunzo ya ufugaji nyuki kwa njia za kisasa. Akiwa mjini Mbinga alisema, "Niliamua kuchukua mafunzo hayo ili kufanya kazi hiyo kwa njia za kuboresha maisha ya watu na binafsi. Naelewa ufugaji wa nyuki haufanywi kwa njia za kisasa lakini sasa nina utaalau huo nitafanya na kila mmoja kulingana na mahitaji yake na popote nchini". 
Kwa mujibu wa bwana Ndonde ni kwamba ameona kuna haja ya kuwekeza kupitia ufugaji wa nyuki kuliko wote kutegemea upande mmoja ambao kwa kiasi fulani unazorotesha mahitaji na kuinuka kiuchumi kwa baadhi ya vijana. 
Lundunyasa Network ilimuuliza kama yuko tayari kufanya kazi za watu wengine ambao watahitaji utaalamu wake, yeye alisema haya, "Utaalamu wangu ninaufanya kwa yeyote anayehitaji. Jambo muhimu ni makubaliano ambayo yanaleta faida kwa pande zote, hivyo sote tutaweza kuinuka kiuchumi kwa kuifanya kazi kwa ufasaha zaidi. 
Alisema pia kwa wale wanaohitaji huduma zake za kutoa mafunzo ya ufugaji wa nyuki kwa njia za kisasa wanaweza kuwasiliana naye kwa simu;  0759 965843, 0777665843, 0684965843 au 0655965843 au wka barua pepe; ernestndonde@ymail.com. Naam na Lundunyasa Network inamtakia kila la heri katika utaalamu wake huu mpya ili aweze kusaidia watanzania wanaopendelea kufugaji nyuki na wale wanaotarajiwa kufuga nyuki hapo baadaye.