January 28, 2013

CHOMBEZO: AMUA SASA NI MAISHA YAKO


Markus Mpangala

Na Markus Mpangala
Usinitazame kwa huzuni. Nitazame kwa furaha kwakuwa sijui namna ya kufirikia matatizo. Sijui namna ya kuwaza kwamba vikwazo vitaniandama. Bali nawaza namna bora na namna ninavyoweza kuishi kwa njia bora. Huwa siwezi kufikiria vikwazo kwakuwa najua vitanirejesha nyuma ili nitaabike. Ninasonga mbele. Usikae ukajuta. Fikiria njia zako. Tafakari kile unachokifanya ili kufanye jambo moja tu la kuamua maisha yako. 
Amua leo usisubirie kesho. Amua kitu kimoja tu ili uweke misingi maishani au kutoweka misingi. Amua moja kama unadhani kkimbia matatizo ni suluhisho. Amua tu kama unadhani mapenzi bora  anapatikana nyumba ndogo kuliko kwa njiwa wako ulimwahidi kuimba naye nyimbo zenye marashi ya huba milele. 
Iko wapi ile ahadi ulimwahidi mwenzio kuwa mtaimba nyote nyimbo tamu za mapenzi yaliyojaa huba. Iko wapi ahadi ulimwahidi binti wa wenzio kwamba utamvika pete ya ndoa. Kwani umgeuze mtoto wa wenzio kuwa kitoweo kisha ukishiba unatanga na njia?
Kwanini iwe hivi kwake na si wewe kutendewa. Ni vizuri kufanya uamuzi mapema kuliko kumwingiza kwenye matatizo huku ukijua unaweza kuyakwepa. Amua sasa maana siku utakayoamua utakuwa umechelewa, basi nakuhimiza sasa. 
Endapo njia zako hazina misingi basi unakaribisha tatizo kubwa. Endapo huna falsafa basi  nakaribisha kasoro maishani mwako. Acha kuwarubuni watoto wa wenzio, acha kuwafanya wao ni kitoweo chako pale udhaniapo unahitaji kula daima. Nakutaka uamue leo na si kesho ambayo hujui itakuwa na sura gani siku hiyo. 
Amua sasa kama unaona hakuna haja ya kusoma au kufanya kazi. Maana wapo watu wanadhani wanaakili kuliko akili zao zilivyo. 
Amua sasa kwamba hutawasumbua watoto wa wenzio. 
Amua sasa kwamba unahitaji kufanya kazi kwa bidii. 
Amua sasa kwamba ofisi yako inahitaji uwajibikaji wa pamoja. 
Taswira ya Mungu
Amua sasa kama unaona mkataba wako haukunufaishi, basi achana nao kwa nia njema kabisa kuliko kuwaghilibu wenye kampuni kuwa u mfanyakazi mwenye hamu ya kuendelea kufanya nao kazi. 
Kuna mambo maishani ni lazima yafanyiwe uamuzi. 
Ni muhimu kuyaangalia kila leo maana ya kesho huwezi kuyaona kwakuwa mshale wa saa unakuwa na mambo mengine zaidi ya hayo. Najua wapo wengine wenye matatizo ya kiafya,mali na mengineyo. Lakini hakuna jambo zuri kwenye maisha kama kufanya uamuzi juu ya hali uliyonayo.
Endapo wewe huna kazi, amua kuwa unahitaji kazi inayoweza kukufanya ukafanya mambo mazuri zaidi. Au unaweza kuamua kwa kuwa mchuuzi maana kushindwa yule si kushindwa kwa wewe. 
Jukumu lako ni kuamua namna ya kuishi kwenye hii sayari yetu ya dunia. Ni muhimu kuyafanya maisha yako kuwa bora kwakuwa hakuna kizuizi chochote. 
Hakuna awezaye kukuzuia ikiwa unafuata taratibu halali za maisha yako. Ni mwenyezi Mungu pekee anaweza kukuzuia lakini mafanikio yako yapo mikononi mwako. Juhudi zako ndizo zitakufanya uwe bora kila siku. 
Amua moja kusuka ama kunyoa, kufunga pingu za maisha au kukaa kuoa. Kuishi vizuri au kuishi kipuuzi. Ni wewe unaweza kuamua namna ya kuishi kwenye hii dunia. Amua moja tu ndugu yangu. Amua ukijua kuwa uamuzi wako unastahili kuheshimiwa na watu wote. 
Usifanye jambo ambalo linaumiza nafsi yako. Amini uamuzi wako unastahili kukufanya uishi vizuri zaidi ya leo. Ni wakati wako wa kufanya uamuzi ili uweze kujua unakokwenda na namna gani unaweza kuishi kwa amani. Amua sasa. 
Misingi ambayo itakufanya uwe na nyumba bora, familia bora na yenye amani ila siku. Familia yenye heshima na wingi wa upendo. Lakini muhimu ni kuamua namna ya kuwa familia hiyo.  Huwezi kupanga kuwa na familia yenye upendo ikiwa hujawa sehemu ya upendo huo. 
Huwezi kuota kuwa na mke mwema/mume ikiwa matendo yako hayaambatani na wema/upendo. Unatakiwa kujiuliza sana kila unavyoishi. Jaribu kujenga picha ambayo mbele yako unajiona na kujisemea kuwa unajipenda. 
Basi vivyo hivyo unatakiwa kuwapenda wengine ama famili yako. Yote haya yanakujia ikiwa tu umeamua kupenda na kutazama njia zenye mustakabali mwema maishani. Hebu  jiulize kwanini wewe huwi mfano wa kuigwa bali unabaki kusema kwamba unataka kumuiga fulani? Kwanini usiamue kuwa wewe unayeigwa badala ya kuwatazama wengine? 
Amua sasa kuwa maisha yako yatakuwa mfano wa kuigwa zaidi kadiri unavyokwenda maana ni wewe tu uwezaye kusuka taswira ya maisha yako. Uwe mfano zaidi kila siku ili utambue thamani ya kuigwa. Sasa ili kuweza kuamua maisha yako basi ni lazima utambue kuna kanuni zinazoongoza maisha ya wale unaowaiga kwa maisha yao mazuri na mema. 
Ni misingi 6 tu ya kuamua namna ya kuishi kutenda mema ama mabaya. Bila shaka utanielewa vema. Na uichunge misingi 6 hii iwe dira yako maishani mwako ili ufanikiwe.
1.Usimchukie yeyote hata kama atakukosea vipi.
2.Ishi maisha ya kawaiada hata kama upo juu kwa kiasi kikubwa.
3. Tarajia heri hata kama mitihani inakusakama.
4. Toa kwa wingi hata kama wewe umenyimwa.
5. Onesha tabasamu hata kama moyo  unavuja damu
6. Usiache kumuabudu mungu.
Nakutakia siku njema na afya nje. Usisahau kuwa yaliyotokea jana yanakufahamisha kwamba aidha ujirekebishe au unapaswa kusonga mbele kutokana na hali ilivyo sasa. Ichunge misingi hiyo muhimu maishani. AMUA SASA.

HAKUNA AJUAYE SIKU YA MWISHO WA DUNIA


Na Markus Mpangala, Nyasa
Mchungaji Harold Camping wa Family Radio alisema kuwa mwisho wa dunia ungelikuwa ni Mei 21/2011. Akaongeza kwa kusema siku hiyo Watakatifu watakwenda mbinguni na hapo ndipo mwisho wa dunia utatokea. Katika mahubiri wa Mchungaji Harold Camping moja kwa moja yanashabihiana na yale ya Mchungaji Benny Hinn, naye mwenyeji wa Marekani.

Mchungaji Benn Hinn naye akafuata mkondo wa Harold Camping kwa kubashiri mambo mbalimbali, kwamba yatatokea, lakini hakuna lililojiri hata moja. Ubashiri wa Mchungaji Harold Camping ameweka kwenye kitabu chake cha  Time has an end. Na amehubiri kuwa Mei 21, 2011 ndiyo mwisho wa dunia.

Lakini naomba niwaambie neno hili; “Watu huniheshimu kwa midomo yao, ila mioyo yao iko mbali nami. Nao huniabudu bure wakifurahisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu” (Mathayo 15;8). 

Tunaishi nyakati hizi lakini hatujui tushike kitu gani kumuabudu Mwenyezi Mungu. Tumekuwa watu wa kutangatanga kwa kila aina ya mahubiri. Lakini haigombi kuyasikiliza ila mwana mwema husikiliza na kufanya tafakuri juu ya yale maagizo ya Baba wa Mbinguni. Pia niharakishe kusema sikupendelea kujikita katika dini hivi kwani wasomaji wetu wengine ni waumini wa dini zingine. Kwakuwa tunavunja mlango ili tujenge nyumba basi leo waniwie radhi nitasema machache.
Je, Biblia anayosoma Mchungaji Harold Camping ni ile ambayo sote tuisomayo? Hilo la kwanza, na kama jawabu ni ndiyo ni kwanini anataka kupingana na Biblia anayohubiri na kuwafundisha watu wake?
Je, tujiulize alifanya hivyo kwa Nasibu kwamba Mei 21, 2011 kuwa mwisho wa dunia? Ni muujiza ama neema gani aliyoshushiwa hata akasema kuwa siku hiyo ndiyo ile ambayo Mwana wa Adamu alisema kuwa ni Baba wa Mbinguni pekee aijuaye siku hiyo?

Iliandikwa hivi; “Walakini habari ya siku ile hakuna aijuaye, hata Malaika walio Mbinguni wala Mwana, ila Baba peke yake” (Mathayo 24:36). Kwa vyovyote itakavyokuwa na kwa namna yoyote yanavyokujia mahubiri ya namna hii, kitu cha kwanza yanakupa hofu. Kwahiyo matokeo yake ni kuchanganyikiwa kwamba unabii unakuja tarehe hiyo ya Harold Camping?
Lakini tutumia Biblia hiyo kuangalia unabii unaohubiriwa, kama ambavyo tulivyoona Injili ya Mathayo kwamba ‘WALAKINI’ hakuna aijuaye siku ile, bali Baba peke yake. Hivyo angalia neno la Mungu linasema; “Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni, mmoja atwaliwa, mmoja aachwa, wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa”, (Mathayo 24; 40-41).
Kuna mambo mengi ynasemwa kuwa ni mwisho wa dunia, lakini mara zote hakuna ukweli wowote kwani hakuna ajuaye siku ile. Mwaka 1999 lilitokea shirika fulani la Bima huko Marekani, ambalo likuwa linachukua mali za watu waliosadiki kuwa mwisho wa dunia ni mwaka 2000.
Sijui ni kitu gani kilichowafanya waamini hivyo lakini ukweli haikutokea, ni Mungu pekee ajuaye. Wakaishia kuendelea kuishi kwa kubashiriwa, hata hivyo ilisemwa na mwana wa Adamu kuwa angalieni mtu asiwadanganye. Kwasababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi.

Kwa mambo yanavyotokea na kwa jinsi tunavyojipa hangaiko ndivyo tunavyozidi kuona akina Harold Camping ndiyo tumaini letu. Waandishi wa Biblia hawakuwa magwiji wa Theolojia, hawakuwa Maprofesa wala madaktari walau wasanifu wa habari bali walielewa mafunzo ya Kristo wakayaandika na kuyafundisha kwa uhuru ili watu wajue na kurudisha waliopotea.
Na wakasisitiza kuwa  mkisikia yuko Jangwani asilani msitoke, wala mkisikia yumo ndani ya nyumba fulani, msihangaike kutoka. Sikiliza ndugu msomaji; ilisemwa kwamba desemba 31, 1999 utakuwa mwisho wa dunia, lakini haukutokea hivyo.

Ikasemwa Desemba 31, 2000 utakuwa mwisho wa dunia, lakini haikutokea hivyo. Sisiti kusema haya ni mafunzo ya akina Kibwetere wa Uganda na miungu bubu ya wahuni inayopigiwa kelele.

Mfano wa pili ni waumini wa UFO, ambao walikufa kwenye mji wa San Diego, Marekani mnamo Mei 26, 1997 kwa madai kuwa walikuwa wakisubiri kwenda mbinguni kwa dhehebu lao la ‘Lango la Mbinguni’.

UFO ni itikadi juu ya vitu vya anga visivyotambuliwa, wanaamini kuliko imani yenyewe, inatisha kweli kweli! Neno hili UFO ni kirefu cha Unidentified Flying Objects. Mwisho wa waumini hawa wa UFO wakawa ni kama akina Harold Camping wanaohubiri mwisho wa dunia ungelikuwa ni Mei 21, 2011.

Mfano wa tatu; Mchungaji Jim Jones wa nchini Marekani katika dhehebu lake walikufa watu 914 mwaka 1978 kutokana na imani hizo za mwisho wa dunia kuwa ni siku fulani. Dhehebu jingine lilijiita ‘Tawi la Daudi’, ambalo ilikuwa mjini Waco jijini Texas, yapata April 19, 1993 nchini Marekani lilikuwa katika mashambuliano ya risasi dhidi ya jeshi la Polisi na wengi wakauawa.
Sababu kubwa ilikuwa kuamini siku ya mwisho ni hii hapa, au ile kule na zaidi ipo pale. Hivyo hata kutii sheria za nchi tabu! Mahubiri ya Harold Camping siyo mageni, kwani Yuda alikwisha kuwavuta watu siku ile wakamsadiki kisha akawahadaa.

“Hata kabla ya hapo alipoondoka Theudia, akajidai kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu” (Matendo 5; 36-37).

Hivyo ukitazama wafuasi wa wachungaji hao waliangamizwa kabisa hawakusalia hata chembe. Na imeandikwa “Msimwamini rafiki, msimwekee kiongozi tumaini” (Mika 7:5). Ni upendo wa mwenyezi Mungu.
Lakini wafuasi wanaoamini kwamba siku hiyo ni ile aliyoitaja mhubiri Harold Camping, angalieni kwamba watambaratika hakuna akayesalia. Wengi hawajui kwamba wanadanganywa, wameweka kila kitu mikononi mwa Harold Camping wala hawajisumbui kujua ukweli. Na hao wengi ‘watakuwa siyo kitu.’

Ni dhahiri kwamba siku ya mwisho itawadia katika ulimwengu huu na hakuna atakayesalia. Bibilia inasema hivi; ‘Halitasalia jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa’. Na hakuna kiumbe hai atakayesalia kati yetu tuliomo.

Imeandikwa “Basi alikaribia mahali niliposimama; nami niliogopa alipokaribia nikaanguka kifudifudi; lakini aliniambia fahamu, Ee mwanadamu, kwa maana maono haya ni ya wakati wa mwisho” (Daniel 8:17).
Wakati watu wakiwa katika mshangao huo wa siku ile (nasema ile maana haikutajwa siku rasmi katika Biblia) viumbe wote wataondolewa katika ulimwengu huu na kupotezwa kabisa. “Basi yoyote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi” (Mathayo 24:3).

Vilevile imesemwa “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,”(2 Timotheo 3:1-2).

“Lakini siku ya bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea. Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuhimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? (2 Petro 3:10-12).

Na imeandikwa kwamba; “Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na  kusema iko wapi ahadi ya kuja kwake? Kwa maana tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali hiyo tangu mwanzo wa kuumbwa” (2 Petro 3:3-4).

Sasa kwakuwa mahubiri ya Harold Camping yalida kuwa siku ya mwisho kuwa ni Mei 21, 2011 basi tutafakari mwenendo hu unaashiria nini. Kwa imani ya mwenyezi mungu na kwa mwongozo wa Biblia tumwachie Mungu aamue. Imeandikwa “Mbingu na nchi zitapita Kamwe; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” (Mathayo 24:35).

“Mungu si mtu, aseme uwongo; wala si mwanadamu, ajute; iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? (Hesabu 23:19).

Je, ni Yesu yupi na Mungu yupi aliyetaja siku hiyo hata Harold Camping akatubashiria kuwa ilikuwa ni Mei 21, 2011 na kwanini haijatokea? Na hata kama tutajiuliza siku hiyo ni lini, hakuna anayejua. Tumeonywa kwamba dai la kujua siku ile lipo tangu zamani za wanafunzi wa Yesu, lakini hawakupata kuijua, na hakuna aliyeijua baadaye hata ufufuko wa Yesu.

“Si juu yenu kupata ujuzi wa nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe” (Matendo 1:7). “Nani ni mshauri wa Bwana? “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! Hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani,” (Warumi 11:33-34). 

“shauri la Bwana lasimama milele, makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi” (Zaburi 33:11). Imesemwa kwamba mawazo ya bwana siyo mawazo yetu, na kamwe siyo mawazo ya Harold Camping yatafikisha ulimwengu mwisho. Soma Isaya 55:8-11.

Na tumefundishwa katika; 2 Timotheo 3:1-5).  Watu wamepoteza maisha yao, kwakuwa wanasadiki kuwa siku hiyo ni ile aliyotaja Mchungaji Harold Camping.
Amri ya Bwana haina mshauri, yeye hutenda awezavyo na apendavyo ndiyo maana hakuna binadamu aliyetajiwa siku ile. Na ‘WALAKINI’ hakuna aijuaye wala Malaika wa Mbinguni, wala Mwana wa Adamu, bali ni Baba peke yake.

JE WAJUA ZANZIBAR ILIFANIKIWA KUWA MWANACHAMA WA UMOJA WA MATAIFA?


Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Siku kama ya Jana (Tarehe 16 Mwezi wa 12) miaka 49 iliyopita (mwaka 1963) Bendera ya lililokuwa Taifa la Zanzibar (sasa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania) na Bendera ya Jamhuri ya Kenya zilipandishwa Hewani katika Viwanja vya Umoja wa Mataifa huko New York, Marekani ikiwa ni ishara ya kutambulika Rasmi kwa Mataifa hayo kama Wanachama wapya wa Umoja wa Mataifa.

Zanzibar ilipata Uhuru wake Disemba 10, mwaka 1963 chini ya Utawala wa Sultan kama Mkuu wa Nchi na Uongozi wa Shughuli za Serikali wa Waziri Mkuu Sheikh Mohammed Hamad Shamte wa Ushirikiano wa Vyama vya Zanzibar & Pemba Peoples Party (ZPPP) na Zanzibar Natiolist Party (ZNP) au "Hizbu" cha aliyekuwa Waziri wa Kwanza Mambo ya Nje wa Zanzibar Sheikh Ali Muhsin Barwany.
Balozi Hilal Mohammed Hilal Al-barwan aliteuliwa kuwa Balozi wa Kwanza wa Zanzibar katika Umoja wa Mataifa ambapo Disemba 16, 1993 Waziri Mkuu Mohammed Hamad Shamte alilihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika Hotuba yake ya kuitambulisha Zanzibar kama Mwanachama Mpya wa Umoja wa Mataifa.

Tarehe 17 Disemba, 1963 Balozi Hilal Mohammed Hilal Al-Barwan aliwasilisha Hati zake za Utambulisho kama Balozi wa Kudumu wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana U Thant.

Serikali husika (iliyokabidhiwa Uhuru) ilidumu kukaa Madarakani kwa muda Mchache tu kabla ya kufanyika Mapinduzi yaliyoongozwa na Makomredi wa ASP na wale wa Chama cha Ummah Party kwa Msaada Mkubwa wa Serikali ya Chama cha Tanu ya iliyokuwa Nchi ya Tanganyika (sasa Tanzania Bara, ikiwa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania).

Mapinduzi hayo yalimleta Madarakani Sheikh Abedi Amani Karume kama Rais Mpya wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika Serikali iliyoundwa kwa ubia wa Wanachama wa Chama cha ASP na wale wa Ummah Party cha Komredi Abdulrahman Mohammed Babu.

MCHAKATO ULIPOANZIA.

Mchakato wa Zanzibar kuwa Mwanachama wa Umoja wa Mataifa ulianza Mwaka 1960 ambapo aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Dag Hamaskold aliitembelea Zanzibar Tarehe 6, Januari, mwaka 1960 wakati akielekea katika Ziara yake Maalum ya Kikazi Nchini Zaire (Sasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo).

Pichani ni Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Dag Hamaskold akiwa pamoja na Viongozi Mbalimbali pamoja na Wajumbe wa Baraza la kutunga Sheria la Zanzibar (Legco) katika Viwanja vya Bustani ya Victoria huko Zanzibar wakati wa Ziara yake hiyo, ambapo Picha hii hutajwa kama Picha ya Mwisho ya Bwana Darg na jopo lake kabla ya Ndege yake kuanguka huko Rhodesia ya Kusini (sasa Zambia) wakati akielekea Zaire.

Wengine kwenye Picha waliosimama kutoka kushoto kwenda kulia ni Sheikh Dahman (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia chama cha ZNP), Sheikh Ali Sharif (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia Chama cha ASP), Bwana N.V.Patel (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia ASP), Bwana Master (Mjumbe katika Msafara wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Sheikh Rashid Al-Ghaithy (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia ZNP) na Sheikh Juma S. Al-Mugheiry (Karani wa Baraza la kutunga sheria, LEGCO).

Waliokaa kutoka Kushoto kwenda kulia ni Sheikh Juma Aley (Waziri kupitia Chama cha ZNP), Sheikh Abeid Amani Karume (Waziri kupitia ASP) Bwana Dag Hamaskold (Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Bwana Smithson (Waziri katika Serikali ya Uingereza), Bwana Kirk Madan (Katibu Mkuu Kiongozi), Bwana Hilal Mohammed Hilal Al-Barwani (Waziri, ZNP na Pia Balozi wa Kwanza wa Zanzibar Umoja wa Mataifa) na Sheikh Ameir Tajo (Waziri, ASP).

ZANZIBAR NA TANGANYIKA ZAPOTEZA UANACHAMA WAKE KATIKA UMOJA WA MATAIFA.

Tanganyika imekuwa Mwanachama wa Umoja wa Mataifa tokea Disemba 14, mwaka 1961 mara baada ya kupata Uhuru wake tarehe 9 Disemba, mwaka 1961 kutoka kwa Wakoloni wa Kiingereza ambapo Dr. Vedastus Kyaruzi alikuwa Balozi wa Kwanza wa Tanganyika katika Umoja wa Mataifa akifuatiwa na Balozi A. Z. Nsilo Swai na kisha Chifu Erasto A. M. Mang'enya kuwa Balozi wa Mwisho wa Tanganyika katika Umoja wa Mataifa. 
Mara baada ya Muungano wa Nchi za Tanganyika na Zanzibar Mwaka 1964 na kuundwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Nchi ya Zanzibar pamoja na Nchi ya Tanganyika zilipoteza Viti vyake katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambapo kilitengwa kiti kipya kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kiti ambacho kimeendelea kuwepo mpaka leo kikiiwakilisha Tanzania huko Umoja wa Mataifa. 
Tarehe 19 Mwezi Novemba Mwaka 1964 Bwana John Samuel Cigwensisi Malecela aliteuliwa Kuwa Balozi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Tanzania. Mabalozi wengine waliowahi kuiwakilisha Tanzania katika Umoja wa Mataifa ni Balozi Akil B.C. Daniel, Balozi Salim Ahmed Salim, Balozi Paul M. Rupia, Balozi Mohamed Ali Foum, Balozi Dr.Wilbert K. Chagula, Balozi Anthony B. Nyaki, Balozi Daudi N. Mwakawago, Balozi Dr.Augustine P. Mahiga, Balozi Ombeni Y. Sefue na huyu Mpya Balozi Tuvako Manongi.

CHANGAMOTO ZA MUUNGANO.

Miongoni mwa mambo ambaye yamekuwa yakiibuliwa kama moja ya malalamiko ya baadhi ya Wazanibari juu ya kero za Muungano ni ukweli kuwa Ushirikiano wa Kimataifa halikuwa katika moja ya Mambo yaliyokubalianwa katika Mkataba wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar (Kimsingi Mambo ya Nje ndio moja ya yaliyokubalianwa katika Mkataba wa Muungano).
Hivyo basi kuingizwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa katika Mambo ya Muungano kinyume na Makubaliano ya Muungano huonekana kama ni batili na sehemu ya kuiminya Zanzibar katika Muundo wa Muungano (ukitolewa Mfano kuwa katika Mabalozi wote waliowahi kuiwakilisha Tanzania katika Umoja wa Mataifa tokea Muungano Wawili tu ndo Wazanzibari na waliobaki wote ni Watanganyika).
Kwa kiasi flani hali hii (ya kuingizwa kinyemela kwa Ushirikiano wa Kimataifa kwenye Mambo ya Muungano na kutokuwepo kwa uwiano wa kuridhisha wa Uteuzi wa Mabalozi wa Kudumu katika Chombo hiki kikuu cha Ushirikiano wa Kimataifa Duniani) inatumika kama moja ya sababu kuu za Msingi za wanaodai Zanzibar huru na kuvunja Muungano, lakini pia imekuwa Moja ya madai makuu ya wanaotaka kuendelea kwa Mashirikiano na Muungano wenye Utu na Heshima kati ya Tanganyika na Zanzibar kwa Kuboresha Muundo na kuondoa zile ambazo zinaonekana kuwa ni kero za Muungano. 
Jambo hili ni zito na lina Mantiki makubwa katika mustakabali wetu kama Nchi, Kwa nafasi yetu kila mmoja ana wajibu wa kulitafakari hili na kuja na majibu ya msingi kulingana na uelewa wake, mifano kuntu na uzoefu juu ya hali hii kutoka katika Mataifa mbalimbali yenye Mashirikiano kama yetu.

Naamini Tutafanikiwa, Mungu Ibariki Tanzania.

Picha ni kwa Hisani kubwa ya Bwana Shafiq Sanya na Maelezo ni Kwa Hisani Kubwa ya Seif Abalhassan wa Watanzania Mashuhuri.

MHADHIRI WA MAPENZI DUNIANI


''Unapoongelea Utaalamu wa Mapenzi,Unapoongelea Uponywaji wa Hisia zako,Unapowaza upate wapi mbinu kuendesha Mapenzi yako ili yawe Matamu...Meseji yake moja tu ni dawa tosha kwa Kwa Machozi yako,Ni dawa tosha ya relationship yako isiyoeleweka...Dawa tosha ya Kurudisha Smile yako iliyopotea...Muite Seth aka Doctor Love
JIUNGE LEO,Your Love Life will never be the same

January 24, 2013

HAPPY BIRTHDAY CHADEMA


Ben Saaanane

Na Ben Saanane, Dar es Salaam
Hebu tuone:Chama cha Patriotic Front cha Zambia(Ninakifananisha na CHADEMA katika Historia na Harakati zake Kuchukua Dola) kilichoanzishwa Mwaka 2001 kimeweza kuwa chama imara kwa kuwachukulia hatua wasaliti bila kujali cheo au nafasi ya mtu.
Leo hii tunapoandika hapa waziri wa mambo ya nje Given Lubinda anajiandaa kukutana na kamati ya Nidhamu ya chama hicho kwa tuhuma za kukisaliti chama hicho na kushirikiana na vyama hasimu.
Akipatikana na hatia kwenye kamati kuu ya PF atafukuzwa uanachama moja kwa moja.
Pia wakati huo huo kiongozi wa upinzani Hakainde Hichilema wa chama cha UPND(nilishawahi kukifananisha na chama cha CUF) anakabiliwa na mashtaka ya defamation huku chama Tawala cha Zamani cha MMD(CCM ya Zambia iliyounda aliiance na UPND kuihujumu PF) kikipambana kujinusuru kisifutwe kwa kukiuka sheria na kuhodhi mali za umma.Huu ni mfano mzuri wa kufuata misingi na sio kufuata watu.
Hakuna aliyewahi kuwa juu ya chama.Chama cha ODM nchini Kenya kilichoanzishwa mwaka 2005 kilionyesha njia kuwaondoa akina Ruto,Chama cha MDC nchini Zimbabwe kilichoanzishwa mwaka 1999 kilionyesha njia kwa kuwaacha akina prof.Arthur Mutambara,CCM Chini ya uenyekiti wa Mwl.Nyerere kilifuata Misingi kwa kumfukuza Maalimu Seif akiwa waziri kiongozi(NASIZITIZA CCM ya NYERERE)....CHADEMA leo kimefikisha miaka 20 Rasmi tangu kisajiliwe.
Tuendelee kufuata misingi kwa mifano hii.Happy Birthday CHADEMA,Viva M4C

JOHN STEVEN AKHWARI ANASTAHILI HESHIMA


Na Hance Forogo, Dar es salaam
Mzee wetu tunayempa Heshima leo alizaliwa mwaka 1938 katika wilaya ya Mbulu iliyoko mkoa wa Arusha....hapa namzungumzia mzee John Steven Akhwari!....akiwa kijana mdogo kabisa alianza kujiingiza katika mchezo wa riadha na haikumchukua muda mrefu kuwa mwanariadha wa mbio ndefu wa kutegemewa na Taifa la Tanzania akishiriki mashindano mengi ndani na nje ya Tanzania na amewahi kuwa bingwa wa mbio ndefu wa bara la Afrika,pia mwaka 1970 alimaliza mbio akiwa na 05 katika mashindano ya mbio ndefu kwa nchi za jumuia ya madola!....
Akitumia muda wa 2:15:05 wakati mshindi alitumia muda wa 2:09:28,inaaminika kuwa alikuwa ni mkimbiaji "World Class" mwenye hadhi ya dunia kati ya miaka ya 1960 na 1980!....
Katika tukio la kihistoria,mzee Akhwari katika mashindano ya Olimpiki mwaka 1938 nchini Mexico,katika mji wa Mexico akiwa wanafanya utani na wakimbiaji wa kuviziana na wakimbiaji wengine ili kupitana na kuwania ushindi alianguka ghafla akiwa amemaliza 19km kati ya 42km.
Baada ya kubanwa na misuli tatizo lililotokana na hali ya hewa kwani kabla hakuwa amefanya mazoezi katika mazingira yenye hali ya miinuko na hali ya nchi kama ya Mexico.
Kutokana na tukio hilo aliteguka goti na kupata jeraha kubwa pia alipata maumivu makali kwenye bega lake!.....hata hivyo aliendelea na mashindano na kumaliza wa mwisho akitumia muda wa 3:25:27 kati ya 57 waliomaliza mbio wakati wanariadha 18 hawakuweza kumaliza mbio huku mshindi Mamo Wolde toka Ethiopia akitumia muda wa 2:20:26!....baada ya muda mfupi kumaliza mbio zake,waandishi walimfuata na kumuuliza kwa nini aliendelea na mbio wakati alikuwa ameumia sana!?....
akajibu kuwa "Nchi yangu(Tanzania) haikunituma kushiriki maili 5000,imenituma nije kumaliza mbio za maili 5000" Jina lake linatumiwa na taasisi ya John Steven Akhwari Athletic Foundation ambayo inatumika kuandaa wanamichezo wanaojiandaa kwa mashindano ya Olimpiki,mwaka 2000 alialikwa kwenye mashindano ya Olimpiki yaliyofanyika Sydney nchini Australia na baada ya hapo alichaguliwa kuwa balozi wa heshima katika maandalizi ya mashindano ya Olimpiki jijini Beijing,China,pia 13/04/2008 alihusika na ubebaji wa Mwenge wa Olimpiki ulipokuja Tanzania katika maandalizi ya Olimpiki!....
Licha ya kwamba mwaka 1983 mzee wetu alitunukiwa medal ya heshima kama shujaa wa Taifa "National Hero Medal of Honor" hatuna budi nasi pande hizi KUMPA HESHIMA ZAKE kwa juhudi kubwa na uzalendo alioufanya kwa ajili ya nchi yake!....ameitangaza nchi kupitia mchezo wa riadha!.....
Huyo ndiye mzee John Steven Akhwari ambaye kwa sasa ni mkulima stadi,hakika anastahili HESHIMA!....Thanx!...

January 23, 2013

SAKATA LA GESI LIMEZUA JIPYA MKOANI MTWARA-Mgodi Unaotembea


Kambi Mbwana

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

HALI ya mkoani Mtwara ni dhahiri inatishia amani, hivyo kuna kila sababu ya serikali na wadau wote kukaa na kuliangalia suala hilo kwa marefu. Nikiwa kama Mtanzania, nimekuwa nikifuatilia kwa karibu mno sakata hilo la gesi inayopingwa na wadau kuletwa jijini Dar es Salaam, badala yake wanataka ibaki mkoani Mtwara, ingawa wenye akili ndogo wanapinga au kutukashifu kadri ya uwezo wao, wakijidanganya kuwa sipaswi kufuatilia mambo ya Mtwara na Lindi.
Huu ni udhaifu na hauwezi kuchekewa, maana ni dhahiri Mtwara, Lindi ni sehemu ya Tanzania kama ilivyokuwa Tanga, Arusha, Kilimanjaro na kwingineko. Wananchi hao waliojikusanya kwa ajili ya kupigania sakata hilo, wamefikia kubadilisha kabisa hisia zao, bila woga wowote katika kulizungumzia suala la gesi.
Kama nilivyowahi kuhoji hapo nyuma, kuwa tatizo ni gesi, choyo, siasa au ubaguzi? Makala haya yalitoka katika blog hii ya Handeni Kwetu na kupokea maoni mbalimbali. Na haya ndio maoni ya Watanzania hao wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Mwanzo wa ugaidi Tanzania ni mwisho wa amani. Kusini hawaogopi jeshi. Kauli ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete ipo kwenye mioyo yao. Leo nasema, ila wana Mtwara watasema kwa sauti zao, maana vitisho kwao ni kama kuitukana maiti.
Chochote kitatokea iwe ni vita vyovyote vile 2015 hatutaki uchaguzi na hatutaki pia tuletewe kiongozi na ole wenu, +255712897794
Maandamano Mtwara
Kaka nimefurahishwa na makala yako isemayo Tatizo ni ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Inaonekana na wewe pia umeandika makala hii kwa lengo lako binafsi. Umeshindwa kutoa uhalisia wa jambo lenyewe, badala yake umeandika kwa lengo la kutaka kumfurahisha ama kuwafurahisha watu fulani. Rudi nyuma angalia wanachofanyiwa wakulima wa korosho wa Mtwara je ni sahihi? Lile zao halisaidii kuinua pato la Taifa? Angalia hali ya maisha ya wakazi wa Mtwara. Nadhani umekurupuka na si mawazo yako kuna mkono wa mtu nyuma yako.
Nenda kazunguuke na kufanya utafiti wa kina utapata majibu sahihi kwa wenyeji. +255657614354.
 Tatizo la mikoa ya Kusini sio gesi bali ni kusahauliwa kwa miaka 51 ya Uhuru. Korosho, reli, Bandari, miundo mbinu, tatizo la elimu na kuwa waanga wa ukombozi wa nchi zilizopo kusini mwa Afrika.
Wanasiasa kujiingiza katika hoja si ajabu kwasababu duniani kote wanasiasa ndio huibua matatizo ya wananchi , maana wasomi wetu wengi hawana meno ya na ndio wanaopitisha  mikataba mibovu .
Sio choyo, lakini tunafikia wakati tunajuta kwa nini sisi Mtwara Lindi tumekuwa sehemu ya Tanzania. Tuna rasilimali tosha za kuweza kuitwa, kama vile Bandari, Bahari, Ardhi yenye rutuba, watu, mito, madini, korosho, ufuta, mhogo na nyinginezo. Kusini tuna haki ya kumdai mume wetu Tanzania haki zetu za msingi, maana tumevumilia mno hadi kilio cha kwi kwi. Ni mimi mwanaharakati,  Amoni, wa Kata Msangamkuu, Mtwara Vijijini. +255652221100.
Ninaomba uelewe lengo la wananchi wa Mtwara na Lindi sio kwamba hawataki gesi isitumiwe na wengine hapana, wao wanataka kiwanda kitengenezwe Mtwara. Kule itoke gesi safi, maana wanakataa mambo yasijekuwa kama ya madini ya Geita ambayo mwekezaji anachimba anaenda kuhakiki Mwanza na kulipa kodi ya uwongo na kuiibia nchi na kuwa masikini, huku wakifaidi watu kutoka nje.
Nimesoma makala yako, inayosema tatizo ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Mimi nimeisoma na kwa utafiti wangu, nimegundua kwamba wewe ni CCM na ndio maana ukaona eti ni siasa. Hapana, ni kwasababu vyama vya upinzani vinapenda maendeleo ya Watanzania.
Mbona hawakuhamisha miwa kutoka Kagera na kuileta Dar es Salaam ili itengenezwe hapa? Pili, hebu fikiria gharama za kuweka bomba ni kiasi gani? Tatu, kumbuka msongamano mkubwa wa watu, ina maana wakiongeza viwanda wanazidisha msongamano. Nne, kwanini wasiwaachie watu wa Mtwara na Lindi na wao wapate ajira? Tano, kila kilichokuwapo Dar es Salaam, Mtwara kipo kama vile Bandari na mengineyo. +255713221244.
Ingawa hujaonyesha wazi ujumbe unaopeleka kwa wana Mtwara, lakini ninachofahamu, Taifa halina rasilimali. Mikoa, wilaya, vijiji, ndivyo vyenye rasilimali, kama vile mbuga za wanyama, madini, mazao na mengineyo ambayo mapato yake hukusanywa na kuwa pato la Taifa. Gesi ni kama rasilimali nyingine tu. Ikiwa Mtwara, Lindi, Kigoma, Mbeya au popote nchini, tueleze ni vipi italinyima Taifa letu pato? Au italigawa vipi Taifa? +255717757797.
Hongera bwana Kambi Mbwana kwa makala yako. Endelea kuwapa elimu Watanzania wenzetu wasioelewa. Naitwa Moi, +255757295249.
Unajua sisi tunaotoka Mtwara tunafananishwa na nyani katika Taifa hili. Hatuna thamani mbele ya makabila mengine toka Uhuru. Barabara haijaisha, mazao yetu hayana usimamizi na hatuna huduma za jamii zilizo bora. Tukipata wakarimu, sio bora pamoja na watumishi wote. Sisi ni jamii ya mwisho katika Taifa hili, hujiulizi gesi na mafuta aliyotupatia Mwenyezimungu ingekuwa sehemu nyingine ingehamishwa? Kwakuwa sisi nyani, hatuna thamani, gesi itaondoka na mafuta pia yataondoka, maana hawa hawatatuthamini milele. +255712848839.
Asante kwa makala yako, lakini usiwe mwandishi mwoga anayeogopa watawala walioshindwa kuwaondolea wananchi umasikini na kuligawa Taifa, kati ya wenye nacho na wasiokuwa nacho. Jitahidi kuwa mkweli ili upate mafanikio maishani mwako. +255755045295. Kijana mbona unakuwa kama popo asiyejulikana kama ni mnyama au ndege. Ya Handeni Kwenu yamekushinda sasa umehamia kwenye gesi.
Nasikitika ujumbe huu uliotumwa kwa namba +255757602075. nimeufipisha kwa sababu za kimaadili, maana ulijaa matusi na kashfa kutoka kwa mtumaji, ambaye pia hakujitambulisha jina lake. Kaka nimesoma makala zako nyingi, nimegundua wewe ni kada wa CCM na usiyejua nini wanachokitaka Watanzania.  Hata hujui huko vijijini watu wanaishi vipi. Unaogopa ya Daudi Mwangosi na Amina Chifupa na huo sio uzalendo, hivyo hupaswi kuwa mwandishi.
Hivi unajua CCM wanaiendashaje nchi hii? Umeshahoji wananchi wangapi kuhusu maisha yao badala yake unamfuata Nape Nnauye, unataka CCM ndio waiongoze nchi milele na milele kwakuwa wewe si mzalendo. Ujumbe huu ulitoka kwa namba +255652273836. Nashukuru brother kwa kuweza kupata fursa ya kuweza kusoma makala yako.
Ni kweli hoja zako ulizozisema zinaweza kushabihiana na ukweli,  ila kutokana na vile hali ilivyo naweza (kudetermine ya words) nazo yanatokana na siasa pia. Hebu nambie kaka angu, umaskini uliopo katika mikoa ya kusini, moja kwa moja tumekuwa maskini na hii ilikua nafasi pekee ya kuweza kupata ahueni.
Hebu jamani isifike wakati tukawa tunaangalia swala hili kijuu juu, hali ni mbya kusini hatuna pa kushikia, serikali ilibidi iangalie gesi hii pia katika kutafuta namna ya kuikomboa miji hii ya kusini.
Ni wazi kuwa serikali imekua ikifurahia tu kupata neema hiyo kuendesha mambo yao na si kusaidia kuondosha umaskini.
Nyinyi waandishi tunawategemea kutoa hoja za kusaidia kuondokana na majanga ya kimaskini. Ujumbe huu ulitumwa kwa njia ya barua pepe kutoka kwa Raya Juma, Nashkuru Haya ni baadhi ya maoni yaliyoingia mara baada ya kuandika makala ile, huku watu wakiingia moia kwa moja katika hoja yangu ya siasa, ubaguzi na choyo nilizokemea. Kwanini nasema siasa? Ukiangalia hapo, wapo waliotuma ujumbe huo wakiwa na chukia serikali ya CCM. Hata hivyo, kuyaanika maoni yao si kuwaletea matatizo, bali kusoma mawazo ya watu wa Mtwara.
Wao ndio wahusika. Ndio wenye kupigania suala la gesi, hivyo inaweza kuwa njia muafaka ya kuepusha shari inayozidi kujengeka mioyoni mwa Watanzania, hususan wale wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Watu wamekuwa na mawazo tofauti juu ya sakata hilo. Wapo wale wanaofikia kutamani Mtwara iwe na utawala wake, jambo ambalo hakika si la kuchekea.
Rasilimali za Tanzania zinaanza kutugawa kadri siku zinavyozidi kwenda mbele, ndio maana nikaamua kuyaanika mawazo ya ndugu zetu hao. Kwa kumalizia tu, sakata la gesi linaweza kujadiliwa upya kwa kuwashirikisha wadau na wananchi wa Mtwara, hasa kwa kupewa mikakati ya namna ya serikali kuwapelekea maendeleo maana ni wajibu wao.
Masuala ya chokochoko ya gesi yasiachwe tu kwa wanasiasa ambao wamekuwa wabunifu kuingia kwenye hoja zinazoshirikisha watu kwa ajili ya kujijenga kisiasa, jambo ambalo si zuri.
Na sisi tunaofikia kujadili suala la gesi, wakiwamo wana harakati, wasitumie maneno makali, maana siku zote jazba inaondosha maana husika. Maoni mengi ya Watanzania nimeshindwa kuyaandika kwa kwasababu hayajatolewa kiungwana, huku niliyoaandika nikiyafanyia marekebisho mengi mno.
Katika hili, serikali kwa kupitia Waziri wake wa Nishati na Madini, Professa Sospeter Muhongo, anapaswa kukaa na kulijadili jambo hili kwa mapana yake.

kambimbwana@yahoo.com
www.handenikwetu.blogspot.com
+255712053949
+255753806087

January 22, 2013

EMMANUEL NDEMBEKA, WAKILI MWENYE MAJUKUMU MENGI KWA WAKAZI WA WILAYA YA NYASA


Na Mwandishi Wetu, Mbamba Bay
Mwaka 2012 utakuwa wa kukumbukwa sana kwa wakazi wa Mbamba Baya na vitongoji vyake vinavyounda pia wilaya ya Nyasa. Moja ya tukio la kuelekea mwisho wa mwaka wa 2012 ni baadhi ya vijana kutoka wilaya ya Nyasa kutunukiwa nishani za uwakili kutokana na taaluma zao za sheria. Miongoni mwa vijana hao ni dada yetu mpendwa Beatrice Mpangala. Yeye ni wakili kwa sasa na analo jukumu kubwa la kusimamia haki ya wananchi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania. 
Emanuel Ndembeka alipoapishwa kuwa wakili
Mbali ya huyo, kijana mwingine Emmanuel G. Ndembeka alitunukiwa uwakili kama ilivyo kwa dada Beatrice Mpangala. Emmanuel G. Ndembeka kijana mzaliwa wa Mbamba Bay, alianza elimu yake ya sekondari akiwa Lundo Sekondari kabla ya kuhamia Kigonsera sekondari maarufu kama Caigo Boys. 
Kigonsera sekondari ndio aliyosoma aliyekuwa rais wa awamu ya tatu katika jamhuri ya muungano wa Tanzania, Benjamin William Mkapa, mzaliwa wa Lupaso mkoani Mtwara. Emmanuel G. Ndembeka anakuwa mtetezi wa jamii yetu kutokana na taaluma yake. 
Umuhimu wake katika jamii ya watanzania ni mkubwa. Mosi, wana jamii wa wilaya ya Nyasa wanajivunia kuzalisha kijana mwenye taaluma ambayo itawasaidia kwa kiwango kikubwa katika kuelewa haki za kumiliki ardhi. 
Kama tujuavyo kwa wakazi wa wilaya ya Nyasa wengi wao wanamiliki ardhi kwa mtindo wa kiutamaduni yaani kurithi ardhi kutoka kwa wazazi hadi kizazi kingine. Matokeo ya jambo hili ni baadhi ya wakazi wasiokuwa na uelewa juu ya haki za kuhifadhi ardhi zao wanaziuza kwa bei ya chini sana kiasi ambacho husababisha matatizo kifamilia. Emmanuel G. Ndembeka anafahamu hili, na kutokana na uelewa wake na namna ya kuelimisha jamii ya wanyasa juu ya kuhifadhi ardhi bila shaka atakuwa mstari wa mbele kuwalinda na kutoa elimu mbadala ili kuzuia uuzaji radhi holela. 
Wakazi wa nyasa wanajivunia kijana ambaye amekulia mazingira yao na anayaelewa kwa kina zaidi. Kwa niaba ya wasomaji wote na wenyeji wa Nyasa, mtandao huu wa Lundunyasa(Lundunyasa Network) unamtakia kila la heri katika mafanikio zaidi. Pia tumkumbushe anauanza mwaka 2013 akiwa na nishani ya wakili mwenye elimu inayotosha kabisa. Mwenyezi Mungu amjaze hekima, upendo na amani zaidi. WAKILI EMANUEL NDEMBEKA, TUNAKUTEGEMEA SANA.

TEKNOLOJIA YA GOLI ITAMALIZA UTATA WA MAGOLI?


Na Markus Mpangala

Mwaka 1986 Diego Maradona alifunga bao la mkono, lakini mwamuzi hakuona akakubali kuwa ni bao halali. Waingereza walilalamikia hilo, lakini mwamuzi alishapitisha uamuzi wake ni bao halali. Tangu hapo Maradona amekuwa akisema bao lake hilo ni la ‘mkono wa mungu’. Mwaka 1966, kiungo wa England, Geoff Hurst apiga shuti kali likagonga mtambaa panya na kugonga chini kisha kurudi uwanjani. 
Diego Maradona

Lakini wakati mwamuzi wa mchezo hajaamuru chochote wachezaji wa England wakaungana na kiungo huyo kushangilia na mwamuzi akakubali ni bao halali. Lakini mpira ule ulipogonga mtambaa panya kisha kugonga chini wala haukugusa mstari. Geoff Hurst akaingia kwenye rekodi ya dunia kwa
kufunga mabao matatu katika mechi ya fainali. Rekodi hiyo imefikiwa na kinda wa Brazil, Oscar Dos Santos ambaye alifunga mabao matatu wakati wa mechi ya fainali ya kombe la dunia kwa vijana chini ya miaka 20 dhidi ya Ureno. 
Lakini miaka 44 baadaye yaani mwaka 2010 katika michuano ya kombe la dunia nchini Afrika Kusini, ni England iliyonyimwa bao.
Frank Lampard alifumua shuti kali likagonga mtambaa panya kisha litua ndani ya lango huku kwa kasi ya ajabu golikipa wa Ujerumani, Manuel Neuer alidaka kiustadi mkubwa.
Mbwana Samatta, akikabiliana na beki wa Zamaleki ya Misri
Mwamuzi wa pambano hilo alikataa kuwapa bao England. Waingereza walichachamaa baada ya michuano hiyo huku wakikumbuka kipigo cha mabao 4-1 walichopata kutoka kwa Ujerumani. 
Waingereza wakasahau kuwa wao walitwaa kombe la dunia kupitia bao lenye utata, kwani walifanikiwa kuifunga Ujerumani ya akina Franz Backenbauer na  Gerd Muller. Lakini ilipotokea kwao kunyimwa bao wakapayuka dunia nzima. Na sasa majadiliano ya kutumia Teknolojia ya goli yakachukua mkondo wake.Teknolojia hiyo maarufu kwa jina ka Jicho la Kipanga (Hawk Eye) ilipenyezwa katika korido la FIFA ili ipate uungwaji mkono. 
Nadhani teknolojia hiyo ilipaswa pia kutumika kutambua mpira wa kichwa uliopigwa na mshambuliaji wa Kilimanjaro Stars, John Bocco dhidi ya Burundi kwenye michuano ya CECAFA inayoendelea nchini Uganda. Tukiacha hilo, ni wazi sasa teknolojia ya goli (Hawk Eye) itakuwa njia mbadala huku tukikumbuka shirikisho la soka la Ulaya linatumia waamuzi watano katika pambano moja. 
Waamuzi wawili wanakaa nyuma ya goli, yaani mmoja mmoja kila upande. Hivyo ukiongeza na mwamuzi wa akiba wanakuwa watano. Naam, Jicho la Kipanga(Hawk Eye) imeshakubalika na kuthibitishwa na FIFA. Kwahiyo, FIFA imesaini  Mkataba Matumizi ya Teknolojia ya kutambua goli (Hawk Eye). Teknolojia hiyo itafanyiwa majaribio nchini Japan, ambapo baadaye itajaribiwa kwenye michuano ya klabu bingwa dunia itakayofanyika nchini humo. 
Dhumuni la teknolojia hii ni kutoa msaada kwa waamuzi ili kuamua kama Mpira umevuka mstari wa Goli na hivyo kuwa Goli halali. FIFA imepiga hatua mbele baada ya kusaini Mikataba na Kampuni mbili za Waundaji wa Mitambo itakayotumika ya kutambua goli. Mitambo hiyo inajulikana kwa jina la GLT (Goal Line Technology).
Kampuni za zilizoshinda tenda hiyo ni Hawk-Eye Innovations na Fraunhofer ISS (GoalRef), ambapo mitambo yake itatumika kwenye Mashindano ya FIFA ya Klabu Bingwa Duniani huko Japan kuanzia Desemba 6 hadi 16 mwaka jana. 
Franz Beckenbauer
Katika hali hiyo wengi wanaweza kusema ni suala zuri kwa maendeleo ya mpira wa miguu. Lakini vilevile tunapaswa kuwaangalia waamuzi na mamlaka yao katika mechi na soka kwa ujumla. Kwa hali halisi kwanza teknolojia hiyo itaondoa kabisa malalamiko ya mabao ambayo yanakataliwa na waamuzi. Lakini vilevile itasaidia waamuzi kuwa na nafasi bora kuondoa malalamiko yoyote ambayo yatachangiwa na uamuzi wao. 
Tekonoliia hiyo inatumika pia katika mchezo wa Tennis ambapo humsaidia mwamuzi kuangalia mpira kama umegusa mstari au umeangukia nje ya mstari au ndani ya uwanja. Teknolojia hiyo inasaidia sana waamuzi wa Tennis kuamua pointi halali kwenye kutafuta Seti. Tumeona hayo kwenye michuano mingi kama US Open, Wimbledon, Ausralia Open, Beijing Open, Olimpiki, na michuano kemkem
inayosimamiwa na shirikisho la Tennis. Hata hivyo kwa suala hili bado naona tunawahitaji sana waamuzi ambao wanaweza kutuletea matokeo mazuri dimbani. Licha ya kuletewa teknolojia hii bado tunahitaji kuwaamini waamuzi ingawaje kuna nyakati wanakera. Pia teknoloajia hii inaamua magoli tu, lakini haitoi nafasi kwa rafu mbaya au mchezo mbaya wa mchezaji fulani ambao mwamuzi anashindwa kuona. 
Mathalani Mwinyi Kazimoto, David Beckham, Dickson Daudi, na wengineo wamekuwa waathirika wa ukosefu wa teknolojia ambayo ingeweza kusaidia namna bora ya kubaini uchezaji mbaya kwa baadhi ya wachezaji.
Madhara ya teknolojia hii ni kuongezeka kwa malalamiko mengine ya uamuzi wa waamuzi. Hali ambayo itawapotezea uwezo wao wawapo dimbani. Ni hatua nzuri kwa Hawk Eye lakini ni wakati mzuri pia kuchambua makosa mengine dimbani yanayostahili kutegemea kamera ili kuepusha madhara kwa wachezaji.