January 29, 2013

VURUGU ZA MTWARA HEBU TUKUMBUKE KAULI YA MWAKA 2011 KUHUSU MRADI WA UMEME MKOANI MTWARA. ........?


• Mradi kabambe wa umeme kujengwa
• Rais Kikwete apokea ripoti ya maandalizi
• Utagharimu mabilioni ya fedha
• Utaunganisha mikoa yote kwenye Gridi ya Taifa

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatano, Oktoba 12, 2011, amepokea ripoti kutoka makampuni mawili ya kimataifa kuhusu Mpango Kabambe ya mradi mkubwa wa umeme ambao utaunganisha kwenye Gridi ya Taifa mikoa yote sita ambayo kwa sasa haiko kwenye gridi hiyo.

Rais Kikwete amepokea ripoti hiyo kutoka makampuni ya China National Machinery & Equipment Import & Export Corporation (CMEC) ya China na Siemens ya Ujerumani ambayo kwa pamoja yanatarajia kujenga kituo kikubwa cha kuzalisha umeme kutokana na gesi katika eneo la Mnazi Bay, mjini Mtwara na pia kujenga njia ya kusafirisha umeme ya kilomita 1,100 kutoka Mtwara hadi Singida.

Mradi huo mkubwa wa umeme wa megawati 300 utakaogharimu karibu dola za Marekani milioni 684 na utakaozalisha umeme wa moja kwa moja na wenye nguvu kubwa ya 300 kV (300 kV High Voltage Direct Current – HVDC) utagharimiwa kwa pamoja na mkopo kutoka Benki ya Exim ya China na Serikali ya Tanzania.

Umeme kutokana na mradi huo utaunganishwa kwenye gridi ya taifa na kutoka Singida hatimaye utavutwa kupelekwa katika mikoa ya Kaskazini Magharibi mwa Tanzania ya Kagera, Kigoma na Rukwa ambako pia utaongeza upatikanaji wa umeme katika machimbo ya madini yaliyoko katika mikoa hiyo.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mbali na mikoa hiyo mitatu, pia mikoa ya Lindi na Mtwara ambayo nayo haiko katika Gridi ya Taifa nayo itaunganishwa katika Gridi hiyo kupitia umeme huo.

Kuunganishwa kwa mikoa hiyo sita katika Gridi ya Taifa kupitia umeme wa mradi huo pamoja na Mkoa wa Ruvuma ambao utaunganishwa katika Gridi hiyo kwa mradi unaogharimiwa na Serikali ya Sweden kutakamilisha mpango wa Serikali ya Awamu ya Nne kuunganisha mikoa yote ya Tanzania kwenye umeme wa Gridi ya Taifa.

Kwa sasa Mkoa wa Kagera unahudumiwa na umeme kutoka Uganda, wakati Mikoa ya Kigoma na Rukwa inahudumiwa na umeme wa mafuta ya dizeli. Mikoa ya Mtwara na Lindi inapata umeme wake kutoka kampuni ya Wentworth ambao haujaunganishwa kwenye gridi ya taifa.

Kuunganisha mikoa yote ya Tanzania kwenye Gridi ya Taifa ilikuwa moja ya ahadi kubwa zilizotolewa na Serikali ya Rais Kikwete wakati anaingia maradakani na kwa kuuunganisha mikoa hiyo sita kwenye Gridi hiyo, Serikali hiyo itakuwa imetimimiza ahadi hiyo.

Akipokea ripoti hiyo, Rais Kikwete ameishukuru Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati na Madini pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa juhudi zao zilizofanikisha makubaliano ya kujengwa kwa mradi huo mkubwa wa umeme ambao utachangia kuongeza wingi wa umeme nchini katika kipindi ambacho kwa miezi kadhaa Tanzania imekabiliwa na mgawo wa umeme kutokana na ukame uliokausha maji kwenye mabwawa makubwa ya uzalishaji umeme nchini.

Rais Kikwete pia ameitaka Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Benki ya EXIM ya China kuhakikisha kuwa fedha za kutekeleza mradi huo zinapatikana haraka iwezekanavyo na pia ameitaka TANESCO na makampuni ya CMEC na Siemens baada ya kupatikana kwa fedha kuanza ujenzi wa mradi huo kwa kasi na kuukamilisha katika muda na ubora unaotarajiwa.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu
DAR ES SALAAM.

12 Oktoba, 2011

IMECHUKULIWA KUTOKA WANABIDII FORUM hii leo jumanne.

WATOTO/VIJANA WASOMAO NJE YA NCHI



Haika Lawere
Na Haika Lawere, via Facebook

Huwa nawatazama wazazi wengi hapa Tz wanavyojinyima usiku na mchana ili kupata ada kuwalipia watoto wao school fees uko nje eg USA/UK,India,Malysia,SA nk nk,wengine huiba ktk ofisi zao ili tu mtoto asome,wengine watauza properties ili mtoto ailimike,wengine hukopa,wengine hata maendeleo binafis yana simama ili vijana wasome!!! 
ila sasa...huko waliko hawa watoto,baadhi yao hawasomi,wengine huishia kuzaa na foreigners ili kupata papers,wengine hu-cohabitate na strangers ili kupata unafuu wa kodi,wengine ni mwaka wa 10 na zaidi hata Certificat/Diploma hawana hata darasa hawajawahi kuingia!!wingine wameshajilipua hata wazazi wakiumwa/kufa hawaji kuwaona!!
Wengine huaribikiwa kabissaaa kitabia/ kiakili/ki-mtazamo na wanakuwa hawa-fit mazingira ya uku!!mi niwasihi tu wadogo zetu ambao wazazi wenu wana-sacrifice kuwasomesheni nje muwe apprecitive,waoneeni wazazi wenu huruma wanavyoteseka,bongo pagumu jamani!! someni na muelimike na mkimaliza shule, ni vizuri mkarudi kutumikia nchi yenu,jamii yenu na kuwatunza wazazi wenu hapo watakapozeeka!!!msizamie nchi za watu wakati kwenu kuna-oppoturnities chungu-mzima!!!simhukumu mtu,ni mtazamo tu anyone can challenge!!

SOKA AFCON; CAPE VERDE, WANAJIAMINI WANAJUA SOKA


Na Markus Mpangala, Dar es salaam

Angola imechapwa magoli 2-1 na Cape Verde, taifa ambalo taifa linalokadiriwa kuwa na idadi ya watu 500,000 tu kulingana na sense zao. Cape Verde imeingia robo fainali huku kocha wake, Lucio Antunes akiongeza sifa katika kazi yake ya ukocha. Ingawa nahodha wake Fernando Neves alijifunga bao la kwanza, lakini aliongoza vema kikosi chao kuishinda Angola kisha kutinga robo fainali. Ni mafanikio makubwa kwao.

Cape Verde inashiriki michuano ya mataifa ya afrika yanayoendelea nchini Afrika Kusini. Kama tujuavyo michuano hii ilitakiwa kufanyika nchini Libya, lakini kutokana na matatizo ya kisiasa yaliyotokea nchini humo yalisababisha majadiliano baina ya chama cha soka cha Afrika kusini na kile cha Libya hivyo kubadilisha michuano.
Kocha wa Cape Verde, Lucio Antunes
Kimsingi Afrika Kusini ilitakiwa kuwa mwenyeji wa michuano ya mwaka 2015, hivyo basi kwakuwa imekuwa mwenyeji mwaka huu basi michuano ijayo itafanyika nchini Libya. Tukiitazama Cape Verde inayoshiriki michuano hiyo ikiwa na wachezaji wengi vijana wameonyesha soka safi ambalo liliwafanya waweze kufuzu kwa michuano hiyo.

Cape Verde imetinga fainali hizo ikiwa na kumbukumbu ya kuisambaratisha Cameroon kwa mabao 4-0 wakati wa kuwania kufuzu kwa AFCON. Kwa sasa wengi wanaitazama Cape Verde kama somo la kuendeleza soka. Idadi ndogo ya watu, kujiamini, kujua soka, lakini imejikuta ikikosa jambo moja tu uzoefu wa mashindano ya kimataifa kama AFCON. Pambalo la kwanza la Cape Verde lilikuwa baina yao na wenyeji Bafana Bafana. Pambano hilo lilimalizika kwa suluhu ya kutofungana hali ambayo iliibua maswali kwa wadau wa soka wa kote afrika hususani wenyeji waafrika kusini.

Matokeo ya pambano hilo ilimlazimu kocha wa Afrika kusini, Gordon Ingesund kufanya mabadiliko katika kikosi chake. Awali alimweka benchi mshambuliaji hatari Katlego Mphela na kumwanzisha Majoro hali ambayo iliwakuta wakishindwa kufurukuta mbele ya ngome ya Cape Verde inayoongozwa na nahodha Neves na T. Varela.

Pambano la kwanza kwa Cape Verde lilionyesha ushahidi kuwa ilijiandaa kwa AFCON mwaka huu na ilipania kufanya vema. mpaka sasa Cape Verde wamejikusanyia pointi mbili, wakiwa nyuma kwa pointi mbili kutoka kwa vinara Afrika kusini. Cape Verde ilitoka sare ya mabao 1-1 dhidi ya Morocco, hivyo kushika nafasi ya pili. Huku Morocco ikishika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi mbili na bao moja baada ya kutoka suluhu na Angola.

Aidha, pambano la pili Afrika Kusini iliichapa Angola kwa mabao 2-0, huku mshambuliaji Siyabongwa Sangweni wa Afrika Kusini akiibuka shujaa kutokana na mchezo mzuri uliomfanya apachike bao la kwanza. Afrika kusini iliingia pambano la pili ikimwanizhs beki wake hodari Tsepo Masilela ambaye alikosekana kwenye pambano la kwanza. Hali hii ilimsaidia sana nahodha wao Khumalo kucheza kwa kujiamini na kuongoza jahazi la nchi hiyo kwa ufanisi.

Lakini kwa Cape Verde ni wazi imeingia kwenye michuano hii ikielewa kuwa ni sehemu ya kujifunza licha ya kushindana kwa dhati. Washambuliaji wake Platini, Ryan Mendes wamekuwa kivutio kwa mashabiki wa soka wanaoifuatilia timu hiyo. Ryan Mendes akicheza kama shambuliaji wa pili katika mfumo 4-3-3, ameng’ara sana kutokanana kujaliwa kipaji kikubwa cha soka. Platini licha ya kuwa mshambuliaji mwenye kipaji anakabiliwa na ukosefu wa stamina ambayo ingelimwezesha kufanya maajabu mbele ya lango la adui.

Kwa upande wa kushoto beki Nivaldo anaonekana kucheza kwa utulivu lakini anaoksa kasi ya mchezo. Yeye ni beki aina ya Timothee Atouba, wanaocheza soka la taratibu sio kasi kasi kama Essou Ekotto. Lakini moja ya mabeki wanavutia kuwatazama jinsi wanavyoshughulikia washambuliaji ni nahodha wa Cape Verde, Neves  na Gege ambaye ni beki wa kulia wa timu hiyo.
wachezaji wa Cape Verde wakishangilia
Wanacheza soka la nguvu na vipaji. Wanajua namna ya kukabiliana na washambuliaji hatari kama Belhanda wa Morocco, mawinga hatari kama Siphiwe Tshabalala  wa Afrika kusini. Kila unapoitazama Cape Verde ikitandaza soka, utaona kwua inao vijana wanaojiamini sana, na wanajua kucheza soka. Mpangalio wao wa mashambulizi mara nyingi hutegemea kasi ya Ryan Mendes, ambaye amekuwa mchezaji kivutio zaidi na mwenye kilifahamu lango la adui kwa ufasaha.
Pia Cape Vaerde inayo bahati moja kubwa, viungo Soares na Mendes wake wanajua kupiga mashuti makali wakiwa na lengo la kujaribu kufunga. Mashuti hayo yanaweza kulenga goli (on target) au kutoka nje ya goli(off target) lakini jambo la msingi wanajaribu kutuonyesha kile walichonacho katika soka. Kwenye safu ya ushambuliaji Platini na Tavares wamekuwa tishio kwa kiwango cha kuridhisha, lakini wanaosa uzeofu tu. 

Tavares anatumika kama mshambuliaji wa kupambana na mabeki, huku Platini akiwa mshambuliaji wa pili maalumu wa kupachika mabao. Ni sababu hii inaonekana timu pinzani zinamfanya rafu mbaya sana Platini kuliko mchezaji mwingine yeyote wa Cape Verde. Kila dakika wanayocheza dimbani wanavutia, wanaburudisha na kujenga taswira mpya ya soka baada ya vigogo kama Cameroon na Senegal kukosekana kwenye michuano hii. Kwa watanzania wanaikumbuka Cape Verde iliyotuchapa mabao 2-1 wakati Taifa Stars ilipokuwa ikinolewa na Marcio Maximo.

Ni wazi wakati ule Cape Verde nayo ilikuwa kwenye kipindi cha mpito cha kujitengenezea njia ya mafanikio kisoka. Hatimaye mwaka huu wanashiriki AFCON, na wametuonyesha kuwa vipaji, kujiamini na kupangilia mambo ni msingi mkubwa wa mafanikio. Jambo lililo wazi na kufurahisha ni kwamba mfumo wa Cape Verde wa 4-3-3 uko wazi sana na unaonekana kwa uwazi ambao timu pinzani zinaweza kuichapa mabao mengi. Lakini Cape Verde wana nidhamu sana katika mchezo. Wanajua soka, wanajiamini lakini safu ya ulinzi inahitaji uzoefu zaidi. Platini anahitaji stamina, Mendes atakuwa bonge la kiungo siku za mbele. Tujifunze, na ku-graduate.

January 28, 2013

CHOMBEZO: AMUA SASA NI MAISHA YAKO


Markus Mpangala

Na Markus Mpangala
Usinitazame kwa huzuni. Nitazame kwa furaha kwakuwa sijui namna ya kufirikia matatizo. Sijui namna ya kuwaza kwamba vikwazo vitaniandama. Bali nawaza namna bora na namna ninavyoweza kuishi kwa njia bora. Huwa siwezi kufikiria vikwazo kwakuwa najua vitanirejesha nyuma ili nitaabike. Ninasonga mbele. Usikae ukajuta. Fikiria njia zako. Tafakari kile unachokifanya ili kufanye jambo moja tu la kuamua maisha yako. 
Amua leo usisubirie kesho. Amua kitu kimoja tu ili uweke misingi maishani au kutoweka misingi. Amua moja kama unadhani kkimbia matatizo ni suluhisho. Amua tu kama unadhani mapenzi bora  anapatikana nyumba ndogo kuliko kwa njiwa wako ulimwahidi kuimba naye nyimbo zenye marashi ya huba milele. 
Iko wapi ile ahadi ulimwahidi mwenzio kuwa mtaimba nyote nyimbo tamu za mapenzi yaliyojaa huba. Iko wapi ahadi ulimwahidi binti wa wenzio kwamba utamvika pete ya ndoa. Kwani umgeuze mtoto wa wenzio kuwa kitoweo kisha ukishiba unatanga na njia?
Kwanini iwe hivi kwake na si wewe kutendewa. Ni vizuri kufanya uamuzi mapema kuliko kumwingiza kwenye matatizo huku ukijua unaweza kuyakwepa. Amua sasa maana siku utakayoamua utakuwa umechelewa, basi nakuhimiza sasa. 
Endapo njia zako hazina misingi basi unakaribisha tatizo kubwa. Endapo huna falsafa basi  nakaribisha kasoro maishani mwako. Acha kuwarubuni watoto wa wenzio, acha kuwafanya wao ni kitoweo chako pale udhaniapo unahitaji kula daima. Nakutaka uamue leo na si kesho ambayo hujui itakuwa na sura gani siku hiyo. 
Amua sasa kama unaona hakuna haja ya kusoma au kufanya kazi. Maana wapo watu wanadhani wanaakili kuliko akili zao zilivyo. 
Amua sasa kwamba hutawasumbua watoto wa wenzio. 
Amua sasa kwamba unahitaji kufanya kazi kwa bidii. 
Amua sasa kwamba ofisi yako inahitaji uwajibikaji wa pamoja. 
Taswira ya Mungu
Amua sasa kama unaona mkataba wako haukunufaishi, basi achana nao kwa nia njema kabisa kuliko kuwaghilibu wenye kampuni kuwa u mfanyakazi mwenye hamu ya kuendelea kufanya nao kazi. 
Kuna mambo maishani ni lazima yafanyiwe uamuzi. 
Ni muhimu kuyaangalia kila leo maana ya kesho huwezi kuyaona kwakuwa mshale wa saa unakuwa na mambo mengine zaidi ya hayo. Najua wapo wengine wenye matatizo ya kiafya,mali na mengineyo. Lakini hakuna jambo zuri kwenye maisha kama kufanya uamuzi juu ya hali uliyonayo.
Endapo wewe huna kazi, amua kuwa unahitaji kazi inayoweza kukufanya ukafanya mambo mazuri zaidi. Au unaweza kuamua kwa kuwa mchuuzi maana kushindwa yule si kushindwa kwa wewe. 
Jukumu lako ni kuamua namna ya kuishi kwenye hii sayari yetu ya dunia. Ni muhimu kuyafanya maisha yako kuwa bora kwakuwa hakuna kizuizi chochote. 
Hakuna awezaye kukuzuia ikiwa unafuata taratibu halali za maisha yako. Ni mwenyezi Mungu pekee anaweza kukuzuia lakini mafanikio yako yapo mikononi mwako. Juhudi zako ndizo zitakufanya uwe bora kila siku. 
Amua moja kusuka ama kunyoa, kufunga pingu za maisha au kukaa kuoa. Kuishi vizuri au kuishi kipuuzi. Ni wewe unaweza kuamua namna ya kuishi kwenye hii dunia. Amua moja tu ndugu yangu. Amua ukijua kuwa uamuzi wako unastahili kuheshimiwa na watu wote. 
Usifanye jambo ambalo linaumiza nafsi yako. Amini uamuzi wako unastahili kukufanya uishi vizuri zaidi ya leo. Ni wakati wako wa kufanya uamuzi ili uweze kujua unakokwenda na namna gani unaweza kuishi kwa amani. Amua sasa. 
Misingi ambayo itakufanya uwe na nyumba bora, familia bora na yenye amani ila siku. Familia yenye heshima na wingi wa upendo. Lakini muhimu ni kuamua namna ya kuwa familia hiyo.  Huwezi kupanga kuwa na familia yenye upendo ikiwa hujawa sehemu ya upendo huo. 
Huwezi kuota kuwa na mke mwema/mume ikiwa matendo yako hayaambatani na wema/upendo. Unatakiwa kujiuliza sana kila unavyoishi. Jaribu kujenga picha ambayo mbele yako unajiona na kujisemea kuwa unajipenda. 
Basi vivyo hivyo unatakiwa kuwapenda wengine ama famili yako. Yote haya yanakujia ikiwa tu umeamua kupenda na kutazama njia zenye mustakabali mwema maishani. Hebu  jiulize kwanini wewe huwi mfano wa kuigwa bali unabaki kusema kwamba unataka kumuiga fulani? Kwanini usiamue kuwa wewe unayeigwa badala ya kuwatazama wengine? 
Amua sasa kuwa maisha yako yatakuwa mfano wa kuigwa zaidi kadiri unavyokwenda maana ni wewe tu uwezaye kusuka taswira ya maisha yako. Uwe mfano zaidi kila siku ili utambue thamani ya kuigwa. Sasa ili kuweza kuamua maisha yako basi ni lazima utambue kuna kanuni zinazoongoza maisha ya wale unaowaiga kwa maisha yao mazuri na mema. 
Ni misingi 6 tu ya kuamua namna ya kuishi kutenda mema ama mabaya. Bila shaka utanielewa vema. Na uichunge misingi 6 hii iwe dira yako maishani mwako ili ufanikiwe.
1.Usimchukie yeyote hata kama atakukosea vipi.
2.Ishi maisha ya kawaiada hata kama upo juu kwa kiasi kikubwa.
3. Tarajia heri hata kama mitihani inakusakama.
4. Toa kwa wingi hata kama wewe umenyimwa.
5. Onesha tabasamu hata kama moyo  unavuja damu
6. Usiache kumuabudu mungu.
Nakutakia siku njema na afya nje. Usisahau kuwa yaliyotokea jana yanakufahamisha kwamba aidha ujirekebishe au unapaswa kusonga mbele kutokana na hali ilivyo sasa. Ichunge misingi hiyo muhimu maishani. AMUA SASA.

HAKUNA AJUAYE SIKU YA MWISHO WA DUNIA


Na Markus Mpangala, Nyasa
Mchungaji Harold Camping wa Family Radio alisema kuwa mwisho wa dunia ungelikuwa ni Mei 21/2011. Akaongeza kwa kusema siku hiyo Watakatifu watakwenda mbinguni na hapo ndipo mwisho wa dunia utatokea. Katika mahubiri wa Mchungaji Harold Camping moja kwa moja yanashabihiana na yale ya Mchungaji Benny Hinn, naye mwenyeji wa Marekani.

Mchungaji Benn Hinn naye akafuata mkondo wa Harold Camping kwa kubashiri mambo mbalimbali, kwamba yatatokea, lakini hakuna lililojiri hata moja. Ubashiri wa Mchungaji Harold Camping ameweka kwenye kitabu chake cha  Time has an end. Na amehubiri kuwa Mei 21, 2011 ndiyo mwisho wa dunia.

Lakini naomba niwaambie neno hili; “Watu huniheshimu kwa midomo yao, ila mioyo yao iko mbali nami. Nao huniabudu bure wakifurahisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu” (Mathayo 15;8). 

Tunaishi nyakati hizi lakini hatujui tushike kitu gani kumuabudu Mwenyezi Mungu. Tumekuwa watu wa kutangatanga kwa kila aina ya mahubiri. Lakini haigombi kuyasikiliza ila mwana mwema husikiliza na kufanya tafakuri juu ya yale maagizo ya Baba wa Mbinguni. Pia niharakishe kusema sikupendelea kujikita katika dini hivi kwani wasomaji wetu wengine ni waumini wa dini zingine. Kwakuwa tunavunja mlango ili tujenge nyumba basi leo waniwie radhi nitasema machache.
Je, Biblia anayosoma Mchungaji Harold Camping ni ile ambayo sote tuisomayo? Hilo la kwanza, na kama jawabu ni ndiyo ni kwanini anataka kupingana na Biblia anayohubiri na kuwafundisha watu wake?
Je, tujiulize alifanya hivyo kwa Nasibu kwamba Mei 21, 2011 kuwa mwisho wa dunia? Ni muujiza ama neema gani aliyoshushiwa hata akasema kuwa siku hiyo ndiyo ile ambayo Mwana wa Adamu alisema kuwa ni Baba wa Mbinguni pekee aijuaye siku hiyo?

Iliandikwa hivi; “Walakini habari ya siku ile hakuna aijuaye, hata Malaika walio Mbinguni wala Mwana, ila Baba peke yake” (Mathayo 24:36). Kwa vyovyote itakavyokuwa na kwa namna yoyote yanavyokujia mahubiri ya namna hii, kitu cha kwanza yanakupa hofu. Kwahiyo matokeo yake ni kuchanganyikiwa kwamba unabii unakuja tarehe hiyo ya Harold Camping?
Lakini tutumia Biblia hiyo kuangalia unabii unaohubiriwa, kama ambavyo tulivyoona Injili ya Mathayo kwamba ‘WALAKINI’ hakuna aijuaye siku ile, bali Baba peke yake. Hivyo angalia neno la Mungu linasema; “Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni, mmoja atwaliwa, mmoja aachwa, wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa”, (Mathayo 24; 40-41).
Kuna mambo mengi ynasemwa kuwa ni mwisho wa dunia, lakini mara zote hakuna ukweli wowote kwani hakuna ajuaye siku ile. Mwaka 1999 lilitokea shirika fulani la Bima huko Marekani, ambalo likuwa linachukua mali za watu waliosadiki kuwa mwisho wa dunia ni mwaka 2000.
Sijui ni kitu gani kilichowafanya waamini hivyo lakini ukweli haikutokea, ni Mungu pekee ajuaye. Wakaishia kuendelea kuishi kwa kubashiriwa, hata hivyo ilisemwa na mwana wa Adamu kuwa angalieni mtu asiwadanganye. Kwasababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi.

Kwa mambo yanavyotokea na kwa jinsi tunavyojipa hangaiko ndivyo tunavyozidi kuona akina Harold Camping ndiyo tumaini letu. Waandishi wa Biblia hawakuwa magwiji wa Theolojia, hawakuwa Maprofesa wala madaktari walau wasanifu wa habari bali walielewa mafunzo ya Kristo wakayaandika na kuyafundisha kwa uhuru ili watu wajue na kurudisha waliopotea.
Na wakasisitiza kuwa  mkisikia yuko Jangwani asilani msitoke, wala mkisikia yumo ndani ya nyumba fulani, msihangaike kutoka. Sikiliza ndugu msomaji; ilisemwa kwamba desemba 31, 1999 utakuwa mwisho wa dunia, lakini haukutokea hivyo.

Ikasemwa Desemba 31, 2000 utakuwa mwisho wa dunia, lakini haikutokea hivyo. Sisiti kusema haya ni mafunzo ya akina Kibwetere wa Uganda na miungu bubu ya wahuni inayopigiwa kelele.

Mfano wa pili ni waumini wa UFO, ambao walikufa kwenye mji wa San Diego, Marekani mnamo Mei 26, 1997 kwa madai kuwa walikuwa wakisubiri kwenda mbinguni kwa dhehebu lao la ‘Lango la Mbinguni’.

UFO ni itikadi juu ya vitu vya anga visivyotambuliwa, wanaamini kuliko imani yenyewe, inatisha kweli kweli! Neno hili UFO ni kirefu cha Unidentified Flying Objects. Mwisho wa waumini hawa wa UFO wakawa ni kama akina Harold Camping wanaohubiri mwisho wa dunia ungelikuwa ni Mei 21, 2011.

Mfano wa tatu; Mchungaji Jim Jones wa nchini Marekani katika dhehebu lake walikufa watu 914 mwaka 1978 kutokana na imani hizo za mwisho wa dunia kuwa ni siku fulani. Dhehebu jingine lilijiita ‘Tawi la Daudi’, ambalo ilikuwa mjini Waco jijini Texas, yapata April 19, 1993 nchini Marekani lilikuwa katika mashambuliano ya risasi dhidi ya jeshi la Polisi na wengi wakauawa.
Sababu kubwa ilikuwa kuamini siku ya mwisho ni hii hapa, au ile kule na zaidi ipo pale. Hivyo hata kutii sheria za nchi tabu! Mahubiri ya Harold Camping siyo mageni, kwani Yuda alikwisha kuwavuta watu siku ile wakamsadiki kisha akawahadaa.

“Hata kabla ya hapo alipoondoka Theudia, akajidai kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu” (Matendo 5; 36-37).

Hivyo ukitazama wafuasi wa wachungaji hao waliangamizwa kabisa hawakusalia hata chembe. Na imeandikwa “Msimwamini rafiki, msimwekee kiongozi tumaini” (Mika 7:5). Ni upendo wa mwenyezi Mungu.
Lakini wafuasi wanaoamini kwamba siku hiyo ni ile aliyoitaja mhubiri Harold Camping, angalieni kwamba watambaratika hakuna akayesalia. Wengi hawajui kwamba wanadanganywa, wameweka kila kitu mikononi mwa Harold Camping wala hawajisumbui kujua ukweli. Na hao wengi ‘watakuwa siyo kitu.’

Ni dhahiri kwamba siku ya mwisho itawadia katika ulimwengu huu na hakuna atakayesalia. Bibilia inasema hivi; ‘Halitasalia jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa’. Na hakuna kiumbe hai atakayesalia kati yetu tuliomo.

Imeandikwa “Basi alikaribia mahali niliposimama; nami niliogopa alipokaribia nikaanguka kifudifudi; lakini aliniambia fahamu, Ee mwanadamu, kwa maana maono haya ni ya wakati wa mwisho” (Daniel 8:17).
Wakati watu wakiwa katika mshangao huo wa siku ile (nasema ile maana haikutajwa siku rasmi katika Biblia) viumbe wote wataondolewa katika ulimwengu huu na kupotezwa kabisa. “Basi yoyote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi” (Mathayo 24:3).

Vilevile imesemwa “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,”(2 Timotheo 3:1-2).

“Lakini siku ya bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea. Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa, mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuhimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka? (2 Petro 3:10-12).

Na imeandikwa kwamba; “Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na  kusema iko wapi ahadi ya kuja kwake? Kwa maana tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali hiyo tangu mwanzo wa kuumbwa” (2 Petro 3:3-4).

Sasa kwakuwa mahubiri ya Harold Camping yalida kuwa siku ya mwisho kuwa ni Mei 21, 2011 basi tutafakari mwenendo hu unaashiria nini. Kwa imani ya mwenyezi mungu na kwa mwongozo wa Biblia tumwachie Mungu aamue. Imeandikwa “Mbingu na nchi zitapita Kamwe; lakini maneno yangu hayatapita kamwe,” (Mathayo 24:35).

“Mungu si mtu, aseme uwongo; wala si mwanadamu, ajute; iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? (Hesabu 23:19).

Je, ni Yesu yupi na Mungu yupi aliyetaja siku hiyo hata Harold Camping akatubashiria kuwa ilikuwa ni Mei 21, 2011 na kwanini haijatokea? Na hata kama tutajiuliza siku hiyo ni lini, hakuna anayejua. Tumeonywa kwamba dai la kujua siku ile lipo tangu zamani za wanafunzi wa Yesu, lakini hawakupata kuijua, na hakuna aliyeijua baadaye hata ufufuko wa Yesu.

“Si juu yenu kupata ujuzi wa nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe” (Matendo 1:7). “Nani ni mshauri wa Bwana? “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! Hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani,” (Warumi 11:33-34). 

“shauri la Bwana lasimama milele, makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi” (Zaburi 33:11). Imesemwa kwamba mawazo ya bwana siyo mawazo yetu, na kamwe siyo mawazo ya Harold Camping yatafikisha ulimwengu mwisho. Soma Isaya 55:8-11.

Na tumefundishwa katika; 2 Timotheo 3:1-5).  Watu wamepoteza maisha yao, kwakuwa wanasadiki kuwa siku hiyo ni ile aliyotaja Mchungaji Harold Camping.
Amri ya Bwana haina mshauri, yeye hutenda awezavyo na apendavyo ndiyo maana hakuna binadamu aliyetajiwa siku ile. Na ‘WALAKINI’ hakuna aijuaye wala Malaika wa Mbinguni, wala Mwana wa Adamu, bali ni Baba peke yake.

JE WAJUA ZANZIBAR ILIFANIKIWA KUWA MWANACHAMA WA UMOJA WA MATAIFA?


Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Siku kama ya Jana (Tarehe 16 Mwezi wa 12) miaka 49 iliyopita (mwaka 1963) Bendera ya lililokuwa Taifa la Zanzibar (sasa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania) na Bendera ya Jamhuri ya Kenya zilipandishwa Hewani katika Viwanja vya Umoja wa Mataifa huko New York, Marekani ikiwa ni ishara ya kutambulika Rasmi kwa Mataifa hayo kama Wanachama wapya wa Umoja wa Mataifa.

Zanzibar ilipata Uhuru wake Disemba 10, mwaka 1963 chini ya Utawala wa Sultan kama Mkuu wa Nchi na Uongozi wa Shughuli za Serikali wa Waziri Mkuu Sheikh Mohammed Hamad Shamte wa Ushirikiano wa Vyama vya Zanzibar & Pemba Peoples Party (ZPPP) na Zanzibar Natiolist Party (ZNP) au "Hizbu" cha aliyekuwa Waziri wa Kwanza Mambo ya Nje wa Zanzibar Sheikh Ali Muhsin Barwany.
Balozi Hilal Mohammed Hilal Al-barwan aliteuliwa kuwa Balozi wa Kwanza wa Zanzibar katika Umoja wa Mataifa ambapo Disemba 16, 1993 Waziri Mkuu Mohammed Hamad Shamte alilihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika Hotuba yake ya kuitambulisha Zanzibar kama Mwanachama Mpya wa Umoja wa Mataifa.

Tarehe 17 Disemba, 1963 Balozi Hilal Mohammed Hilal Al-Barwan aliwasilisha Hati zake za Utambulisho kama Balozi wa Kudumu wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana U Thant.

Serikali husika (iliyokabidhiwa Uhuru) ilidumu kukaa Madarakani kwa muda Mchache tu kabla ya kufanyika Mapinduzi yaliyoongozwa na Makomredi wa ASP na wale wa Chama cha Ummah Party kwa Msaada Mkubwa wa Serikali ya Chama cha Tanu ya iliyokuwa Nchi ya Tanganyika (sasa Tanzania Bara, ikiwa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania).

Mapinduzi hayo yalimleta Madarakani Sheikh Abedi Amani Karume kama Rais Mpya wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika Serikali iliyoundwa kwa ubia wa Wanachama wa Chama cha ASP na wale wa Ummah Party cha Komredi Abdulrahman Mohammed Babu.

MCHAKATO ULIPOANZIA.

Mchakato wa Zanzibar kuwa Mwanachama wa Umoja wa Mataifa ulianza Mwaka 1960 ambapo aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Dag Hamaskold aliitembelea Zanzibar Tarehe 6, Januari, mwaka 1960 wakati akielekea katika Ziara yake Maalum ya Kikazi Nchini Zaire (Sasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo).

Pichani ni Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Dag Hamaskold akiwa pamoja na Viongozi Mbalimbali pamoja na Wajumbe wa Baraza la kutunga Sheria la Zanzibar (Legco) katika Viwanja vya Bustani ya Victoria huko Zanzibar wakati wa Ziara yake hiyo, ambapo Picha hii hutajwa kama Picha ya Mwisho ya Bwana Darg na jopo lake kabla ya Ndege yake kuanguka huko Rhodesia ya Kusini (sasa Zambia) wakati akielekea Zaire.

Wengine kwenye Picha waliosimama kutoka kushoto kwenda kulia ni Sheikh Dahman (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia chama cha ZNP), Sheikh Ali Sharif (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia Chama cha ASP), Bwana N.V.Patel (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia ASP), Bwana Master (Mjumbe katika Msafara wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Sheikh Rashid Al-Ghaithy (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia ZNP) na Sheikh Juma S. Al-Mugheiry (Karani wa Baraza la kutunga sheria, LEGCO).

Waliokaa kutoka Kushoto kwenda kulia ni Sheikh Juma Aley (Waziri kupitia Chama cha ZNP), Sheikh Abeid Amani Karume (Waziri kupitia ASP) Bwana Dag Hamaskold (Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Bwana Smithson (Waziri katika Serikali ya Uingereza), Bwana Kirk Madan (Katibu Mkuu Kiongozi), Bwana Hilal Mohammed Hilal Al-Barwani (Waziri, ZNP na Pia Balozi wa Kwanza wa Zanzibar Umoja wa Mataifa) na Sheikh Ameir Tajo (Waziri, ASP).

ZANZIBAR NA TANGANYIKA ZAPOTEZA UANACHAMA WAKE KATIKA UMOJA WA MATAIFA.

Tanganyika imekuwa Mwanachama wa Umoja wa Mataifa tokea Disemba 14, mwaka 1961 mara baada ya kupata Uhuru wake tarehe 9 Disemba, mwaka 1961 kutoka kwa Wakoloni wa Kiingereza ambapo Dr. Vedastus Kyaruzi alikuwa Balozi wa Kwanza wa Tanganyika katika Umoja wa Mataifa akifuatiwa na Balozi A. Z. Nsilo Swai na kisha Chifu Erasto A. M. Mang'enya kuwa Balozi wa Mwisho wa Tanganyika katika Umoja wa Mataifa. 
Mara baada ya Muungano wa Nchi za Tanganyika na Zanzibar Mwaka 1964 na kuundwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Nchi ya Zanzibar pamoja na Nchi ya Tanganyika zilipoteza Viti vyake katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambapo kilitengwa kiti kipya kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kiti ambacho kimeendelea kuwepo mpaka leo kikiiwakilisha Tanzania huko Umoja wa Mataifa. 
Tarehe 19 Mwezi Novemba Mwaka 1964 Bwana John Samuel Cigwensisi Malecela aliteuliwa Kuwa Balozi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Tanzania. Mabalozi wengine waliowahi kuiwakilisha Tanzania katika Umoja wa Mataifa ni Balozi Akil B.C. Daniel, Balozi Salim Ahmed Salim, Balozi Paul M. Rupia, Balozi Mohamed Ali Foum, Balozi Dr.Wilbert K. Chagula, Balozi Anthony B. Nyaki, Balozi Daudi N. Mwakawago, Balozi Dr.Augustine P. Mahiga, Balozi Ombeni Y. Sefue na huyu Mpya Balozi Tuvako Manongi.

CHANGAMOTO ZA MUUNGANO.

Miongoni mwa mambo ambaye yamekuwa yakiibuliwa kama moja ya malalamiko ya baadhi ya Wazanibari juu ya kero za Muungano ni ukweli kuwa Ushirikiano wa Kimataifa halikuwa katika moja ya Mambo yaliyokubalianwa katika Mkataba wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar (Kimsingi Mambo ya Nje ndio moja ya yaliyokubalianwa katika Mkataba wa Muungano).
Hivyo basi kuingizwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa katika Mambo ya Muungano kinyume na Makubaliano ya Muungano huonekana kama ni batili na sehemu ya kuiminya Zanzibar katika Muundo wa Muungano (ukitolewa Mfano kuwa katika Mabalozi wote waliowahi kuiwakilisha Tanzania katika Umoja wa Mataifa tokea Muungano Wawili tu ndo Wazanzibari na waliobaki wote ni Watanganyika).
Kwa kiasi flani hali hii (ya kuingizwa kinyemela kwa Ushirikiano wa Kimataifa kwenye Mambo ya Muungano na kutokuwepo kwa uwiano wa kuridhisha wa Uteuzi wa Mabalozi wa Kudumu katika Chombo hiki kikuu cha Ushirikiano wa Kimataifa Duniani) inatumika kama moja ya sababu kuu za Msingi za wanaodai Zanzibar huru na kuvunja Muungano, lakini pia imekuwa Moja ya madai makuu ya wanaotaka kuendelea kwa Mashirikiano na Muungano wenye Utu na Heshima kati ya Tanganyika na Zanzibar kwa Kuboresha Muundo na kuondoa zile ambazo zinaonekana kuwa ni kero za Muungano. 
Jambo hili ni zito na lina Mantiki makubwa katika mustakabali wetu kama Nchi, Kwa nafasi yetu kila mmoja ana wajibu wa kulitafakari hili na kuja na majibu ya msingi kulingana na uelewa wake, mifano kuntu na uzoefu juu ya hali hii kutoka katika Mataifa mbalimbali yenye Mashirikiano kama yetu.

Naamini Tutafanikiwa, Mungu Ibariki Tanzania.

Picha ni kwa Hisani kubwa ya Bwana Shafiq Sanya na Maelezo ni Kwa Hisani Kubwa ya Seif Abalhassan wa Watanzania Mashuhuri.

MHADHIRI WA MAPENZI DUNIANI


''Unapoongelea Utaalamu wa Mapenzi,Unapoongelea Uponywaji wa Hisia zako,Unapowaza upate wapi mbinu kuendesha Mapenzi yako ili yawe Matamu...Meseji yake moja tu ni dawa tosha kwa Kwa Machozi yako,Ni dawa tosha ya relationship yako isiyoeleweka...Dawa tosha ya Kurudisha Smile yako iliyopotea...Muite Seth aka Doctor Love
JIUNGE LEO,Your Love Life will never be the same

January 24, 2013

HAPPY BIRTHDAY CHADEMA


Ben Saaanane

Na Ben Saanane, Dar es Salaam
Hebu tuone:Chama cha Patriotic Front cha Zambia(Ninakifananisha na CHADEMA katika Historia na Harakati zake Kuchukua Dola) kilichoanzishwa Mwaka 2001 kimeweza kuwa chama imara kwa kuwachukulia hatua wasaliti bila kujali cheo au nafasi ya mtu.
Leo hii tunapoandika hapa waziri wa mambo ya nje Given Lubinda anajiandaa kukutana na kamati ya Nidhamu ya chama hicho kwa tuhuma za kukisaliti chama hicho na kushirikiana na vyama hasimu.
Akipatikana na hatia kwenye kamati kuu ya PF atafukuzwa uanachama moja kwa moja.
Pia wakati huo huo kiongozi wa upinzani Hakainde Hichilema wa chama cha UPND(nilishawahi kukifananisha na chama cha CUF) anakabiliwa na mashtaka ya defamation huku chama Tawala cha Zamani cha MMD(CCM ya Zambia iliyounda aliiance na UPND kuihujumu PF) kikipambana kujinusuru kisifutwe kwa kukiuka sheria na kuhodhi mali za umma.Huu ni mfano mzuri wa kufuata misingi na sio kufuata watu.
Hakuna aliyewahi kuwa juu ya chama.Chama cha ODM nchini Kenya kilichoanzishwa mwaka 2005 kilionyesha njia kuwaondoa akina Ruto,Chama cha MDC nchini Zimbabwe kilichoanzishwa mwaka 1999 kilionyesha njia kwa kuwaacha akina prof.Arthur Mutambara,CCM Chini ya uenyekiti wa Mwl.Nyerere kilifuata Misingi kwa kumfukuza Maalimu Seif akiwa waziri kiongozi(NASIZITIZA CCM ya NYERERE)....CHADEMA leo kimefikisha miaka 20 Rasmi tangu kisajiliwe.
Tuendelee kufuata misingi kwa mifano hii.Happy Birthday CHADEMA,Viva M4C

JOHN STEVEN AKHWARI ANASTAHILI HESHIMA


Na Hance Forogo, Dar es salaam
Mzee wetu tunayempa Heshima leo alizaliwa mwaka 1938 katika wilaya ya Mbulu iliyoko mkoa wa Arusha....hapa namzungumzia mzee John Steven Akhwari!....akiwa kijana mdogo kabisa alianza kujiingiza katika mchezo wa riadha na haikumchukua muda mrefu kuwa mwanariadha wa mbio ndefu wa kutegemewa na Taifa la Tanzania akishiriki mashindano mengi ndani na nje ya Tanzania na amewahi kuwa bingwa wa mbio ndefu wa bara la Afrika,pia mwaka 1970 alimaliza mbio akiwa na 05 katika mashindano ya mbio ndefu kwa nchi za jumuia ya madola!....
Akitumia muda wa 2:15:05 wakati mshindi alitumia muda wa 2:09:28,inaaminika kuwa alikuwa ni mkimbiaji "World Class" mwenye hadhi ya dunia kati ya miaka ya 1960 na 1980!....
Katika tukio la kihistoria,mzee Akhwari katika mashindano ya Olimpiki mwaka 1938 nchini Mexico,katika mji wa Mexico akiwa wanafanya utani na wakimbiaji wa kuviziana na wakimbiaji wengine ili kupitana na kuwania ushindi alianguka ghafla akiwa amemaliza 19km kati ya 42km.
Baada ya kubanwa na misuli tatizo lililotokana na hali ya hewa kwani kabla hakuwa amefanya mazoezi katika mazingira yenye hali ya miinuko na hali ya nchi kama ya Mexico.
Kutokana na tukio hilo aliteguka goti na kupata jeraha kubwa pia alipata maumivu makali kwenye bega lake!.....hata hivyo aliendelea na mashindano na kumaliza wa mwisho akitumia muda wa 3:25:27 kati ya 57 waliomaliza mbio wakati wanariadha 18 hawakuweza kumaliza mbio huku mshindi Mamo Wolde toka Ethiopia akitumia muda wa 2:20:26!....baada ya muda mfupi kumaliza mbio zake,waandishi walimfuata na kumuuliza kwa nini aliendelea na mbio wakati alikuwa ameumia sana!?....
akajibu kuwa "Nchi yangu(Tanzania) haikunituma kushiriki maili 5000,imenituma nije kumaliza mbio za maili 5000" Jina lake linatumiwa na taasisi ya John Steven Akhwari Athletic Foundation ambayo inatumika kuandaa wanamichezo wanaojiandaa kwa mashindano ya Olimpiki,mwaka 2000 alialikwa kwenye mashindano ya Olimpiki yaliyofanyika Sydney nchini Australia na baada ya hapo alichaguliwa kuwa balozi wa heshima katika maandalizi ya mashindano ya Olimpiki jijini Beijing,China,pia 13/04/2008 alihusika na ubebaji wa Mwenge wa Olimpiki ulipokuja Tanzania katika maandalizi ya Olimpiki!....
Licha ya kwamba mwaka 1983 mzee wetu alitunukiwa medal ya heshima kama shujaa wa Taifa "National Hero Medal of Honor" hatuna budi nasi pande hizi KUMPA HESHIMA ZAKE kwa juhudi kubwa na uzalendo alioufanya kwa ajili ya nchi yake!....ameitangaza nchi kupitia mchezo wa riadha!.....
Huyo ndiye mzee John Steven Akhwari ambaye kwa sasa ni mkulima stadi,hakika anastahili HESHIMA!....Thanx!...