February 04, 2013

TOFAUTI ZETU ZA DINI, ZISITUFIKISHE KWENYE UHASAMA


Na Markus Mpangala, Dar es salaam

Niwe mkweli, nasikitishwa sana na baadhi ya watanzania wenzetu wanavyochukulia mambo kwa njia HASI. Huwa sichelewi kabisa kupambana nao ili kuokoa hali mbaya inayoweza kujitokeza. Kuna wakati baadhi ya wananchi katika mkoa fulani(sitataja) waliwahi kutoa maoni yao kwa tume ya Kukusanyasa Maoni ya Katiba kwamba katiba iangalie pia suala la Machinjio kwanini kuna Waislamu pekee. 
Hawa ni rafiki zangu nilipokuwa UDSM. Hapa wapo waumini wa dini tofauti, lakini wameishi kwa upendo na amani bila kuulizana masuala ya DINI zao kuwa tofauti. Wanaishi kwa raha
Sijui mwananchi yule alipata wapi utafiti na kuhimisha kiasi kile, lakini ni wazi kuwa tupo katika kipindi kibaya au mwanzo wa kipindi kibaya kabisa. Natambua kuwa nyakati mbaya huwa haziishi ila watu wabaya huisha, lakini hakuna ubaya zaidi kama kufikiria mabaya na kuilisha jamii ubaya. Ni wazi kuwa kila mwananchi anao mtazamo wake kuhusu DINI, lakini mitizamo hii isitufanye tugawane mbao za nchi yetu eti wewe MKRISTO au wewe MWISLAMU. 
Nchi hii sio ya Waislamu na Wakristo pekee, bali kuna wapagani, wahindu na wabuddha pia. Kuna watu wa dini mbalimbali, hivyo haipendezi kuonyesha kwamba waislamu na wakristo ndio wapiga filimbi ya kujidhania wao ndio Tanzania. Januari 14, 2013 nilitumiwa ujumbe kuwa niwe sehemu ya watu wanaopinga kuanzishwa Mahakama ya Kadhi. Nakiri niliudhika kwa ujumbe huo na mara moja nikauripoti sehemu zinazohusika. 

Mpaka sasa natambua ujumbe ule ulishaandikiwa ripoti na uchunguzi unaendelea hadi sasa. Sina shaka kuwa hatua iliyofikiwa ni nzuri na siku sio nyingi tutabainishwa kuwa wahusika ni akina nani wanaosambaza ujumbe huo ili kuwahamasisha wakristo etu wapinge Mahakama ya Kadhi ambayo kimsingi utaratibu wake uko wazi kabisa. 

Lakini leo hii Ferbruari 04, 2013 niliambiwa kuwa niwe sehemu ya wanaponga suala la MACHINJIO kwa kuandika na kuchambua zaidi. Mtu aliyeniambia hilo natambua anafahamu kuwa anasoma magazeti na ananisoma mada zangu nyingi ninazoandika. Yeye anataka niandike mada juu ya Machinjio na anadai kuwa kuna KITU KIMEJIFICHA.

 Hakika hili ni jambo la ajabu na nimeshangaa sana. Inakuwaje mtanzania amefika mahali kuona watanzania wenzake wa dini nyingine kuwa kero. Pai ni kitu gani kinachomshukuma mtu huyu kusema kuwa kuna jambo limejificha katika madai ya uchinjwaji wa nyama unapofanywa na waislamu huku walaji wengine wakiwa Wakristo, au Waislamu wanavyokataa kula nyama iliyochinjwa na mkristo ama mwenye imani tofauti na wao.

 Wengi wanatumia kigezo hiki kwamba mnyama anapochinjwa na mwislamu ni halali na pale anapochinjwa na asiyekuwa mwislamu ni haramu. Kimsingi haya ni mawazo yenye uozo mkubwa. Ni aibu, ni mafunzo ya kishetani kudai kuwa mnyama anapochinjwa na mwislamu ni nongwa hivyo nasi wakristo tuanze kupinga kwa kuingiza hoja hizi. 

Ndugu zangu, dini zililetwa kwaajili ya amani na upendo sio kugombana na uhasama. Ni umasikini na upumbavu mkubwa kudai kuwa eti mnyama aliyechinjwa na mwislahu anatakiwa kupingwa na mkristo sababu tu waislamu wanaona haramu. 

Kama waislamu wanaona haramu ni wao, na hakuna sababu ya kuchukulia kama nyenzo ya uhasama.  Ndugu zangu, sijui nini kinamfikisha mtu kufikiria hilo. ...NAWAULIZA MASWALI HAYA ..........Unataka Nyama au Mchinja Nyama? .... Ndio, nasikia mmeanza kuhoji kwanini wanaochinja Wanyama kwenye machinjio ni Waislamu na kwanini wenye Mabucha ya Nyama ni Waislamu......... naendelea kuwasikiliza ..... Hivi Ng'ombe ana DINI?

 Mbuzi ana DINI? Unakula DINI au Nyama? Kisu kina DINI? Supu ina DINI? Kuku ana DINI? ... Kama wewe huli mnyama aliyechinjwa na Mkristo unadhani itabadilika na kutokuwa Nyama? Kwanini mnyama aliyechinjwa na Mwislamu itabadilika kutokuwa Nyama? ... SIRI iko wapi hapo? Umelazimishwa kula? Kitu kimoja rahisi ni kujiuliza tatizo hapo ni nyama ama mchinjaji? Na kama unaona mchinjaji ni tatizo kwanini usianzishe bucha lako ambalo litakuondolea kwenye ukakasi eti waislamu ndio wachinjaji? 

Kwanini usinunue ng'ombe wako au mnyama wako ukamchinja mwenyewe kwa raha zako ili kuepusha uhasama huu? Ndugu zangu hakuna kitu kibaya kama hatua tuliyofikia. Inapofika watu wanaanza kuhoji mambo yenye uozo kama haya ni wazi kushiba kwao ni tumboni tu sio akilini. Ubongo wa wanafikiria haya haujashiba hata kidogo ndio maana wanaona hilo la mchinja wanyama ni kero kama zilivyo kero za kukosa pesa, kukosa chakula, kukosa mahitaji muhimu au la. Hakuna mwanadamu atakayekufa kwa kutokula nyama. Hakuna mtanzania ambaye atapoteza uhai kwa kukosa nyama. 

Matatizo haya tutafika mahali hata wakristo wenyewe wataanza kusema, hawali nyama yoyote iliyochinjwa na mpetekoste, mkatoliki, mlokole, mlutheri na wengineo, vivyo hivyo tutafika mahali tunanyoosheana vidole mbona hawa wanacheka na wale wamenuna. Upuuzi huu hakika unapaswa kukemewa, na wala haifai kabisa kuwa endapo mtu amenunua nyama kisha akagundua mchinjaji ni mwislamu, basi aitupilie mbali. Huu ni uozo wa akili zetu, na ukosefu wa kushiba kifikra. Tatizo hili lisipokemewa mwishowe tutakuwa tunaishi kwa kumwaga damu kila siku.  

CHOMBEZO: WEKA MALENGO MAISHANI

Markus Mpangala

Ni mwenyezi Mungu anayetuweka hai kwenye hii dunia huku wenyewe tukichukua jukumu la kujilinda dhidi ya hatari zozote. Leo ninapenda kukuelezea jambo lililonishangaza zaidi ingawaje nilikwisha simuliwa nyakati fulani na baadhi ya wanazuoni, na lenye elimu muwali. Jambo hili ndilo linalenga kukuuliza maswali haya; wewe ni mfanyakazi kwenye ofisi fulani, hivi unafanya kazi ili iweje? Labda wewe huna kazi, unaishi ili iweje? Kwanini huna kazi au shughuli yoyote? Lau umri wako mdogo au hujapata kazi, unadhani kuna umuhimu wa kazi? Na kwanini unaona kuna umuhimu wa kuishi kama ulivyo? Wengine ni wafanyabiashara na mengineyo; hivi katika maisha yako una malengo gani? Yaani unaamka mapema, unakwenda kazini aidha kwa usafiri wako au wa jamii (Daladala).
Unakwenda ofisini kufanya nini? Lengo lako hasa ni nini kadiri mshale wa saa unavyokwenda hapa duniani? Unaishi ili kufanya nini? Kwanini unadhani una haki ya kuishi na si yule au mimi? Lengo lako la kuishi liko wapi? Sababu yako ya kufanya kazi iko wapi? Ndiyo, unapenda cheo, halafu iweje? Ukishakupata cheo hicho unalengo gani na maisha yako?
Unadhani cheo chako kitaisaidia nini ofisi yako? Kwanini wewe unapenda sana kupendelewa? Unapotaka kupendelewa je, wewe umewafanyia upendeleo wenzako? Unadhani ukipendelewa wewe ni muhimu kuliko yule na mimi? Lengo lako la kupendelewa ni nini? Unapenda kupewa kuliko wewe kutoa? Lengo lako ni nini hasa?

Jiulize sana msomaji ili tuende sambamba nikupe jambo hili. Tueleweshane hapa kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuweka malengo katika maisha yetu haya. Kama wewe huna ndoto basi hutafanikiwa. Kama wewe huna maono maishani, basi una kazi kubwa kujitambua. Una kazi kubwa ya kutambua uendako. Ni lazima uanze kufikiri sasa, maana mtu mwerevu huzifikiria hatua zake. Basi tusiende mbali msomaji mpenzi, nakupenda sana, tambua hilo.
Shaban akitimiza majukumu yenye malengo ofisini kwake
Sikiliza sasa, Aprili 19 mwaka huu nilinunua kitabu cha “Barrack Obama: Yes, We Can”, kimeandikwa na Lila Luce. Mambo yaliyomo kitabuni ndiyo yananifanya nitafakari nawe leo kupitia safu hii. Rudi juu anza kusoma upya halafu uelewe zaidi. Kwenye kitabu hiki kuna mambo ambayo sikujua kuhusu Rais huyu wa Marekani. Inachekesha na kuelimisha, lakini ukweli maisha aliyopitia Barrack Hussein Obama (jina lake la utani Barry O’Bomber) kuna mengi ya kujifunza.
Ukisema mitishamba, Obama amenyweshwa sana kule Kogelo, Kenya. Ukisema Daladala, basi Obama amepanda sana pale Kenya (huita Matatu). Obama alikuwa mtumiaji wa madawa ya kulevya (teja) enzi za ujana wake, tafakari hilo.

Obama ana kauli mbiu ya “Mabadiliko”. Mabadiliko ni dhana ambayo ilitokana na aliyoona na kuishi maishani mfano Kogelo na Indonesia. Tusione Obama anaongoza Marekani, alilumbana na mkewe (Michelle Obama) kwa wazo la Urais. Michelle akamwita msaliti, hamwelewi anafikiria nini juu ya familia, alimwambia; “mume wangu nitawezaje kulea mabinti hawa wawili (Natasha na Malia) peke yangu?

Lakini Obama alimjibu mkewe, “tafadhali hii ni mara yangu ya mwisho, kabla ya kuishi kwa utulivu mke wangu, niruhusu.” Msomaji unapaswa kutambua kuwa wakati anagombea kuwa Useneta alitofautiana na mkewe, lakini aliruhusiwa kwa ahadi hatawania kiti kingine.
Obama anakufunza mengi; alifundishwa imani ya Ukristu na akawa mkristu, akajifunza Uislamu alipokuwa Indonesia, kwahiyo dini zote kazipitia kabla ya kufunga pingu za maisha kwa Mchungaji Jeremiah Wright. Alifundishwa mila na desturia za Wamasai. Alishatumia Vibatari kule Kogelo, Kenya. Alitembea kwa miguu vijijini, hakika ni mengi mno. Hata hivyo kauli aliyomwambia mkewe wakati anaomba amruhusu kuwani Urais ndiyo inatuleta hapa leo msomaji.

Awali alisema, ‘Nimeona nafasi ya kushinda’. Hii ilitokana na malengo yake aliyoweka ili kutimiza ndoto zake. Akamjibu mkewe, ‘hii ni nafasi ya mwisho mke wangu. Nahitaji kuyafanyia kazi mawazo yangu kabla sijatulia na kuishi kwa amani kwenye familia yetu.”  
Hii inakuonyesha ndoto zake maishani. Inakuonyesha malengo yake maishani. Inakupa mwanga wa kutengeneza sura mpya na kuacha ya kale. Inakupa matumaini mapya ambayo lazima utayatendee kazi.
Rafiki yangu Shaban a.k.a Don King, akiwa ofisini kwake
Lazima uwe na malengo maishani msomaji. Ujue dhumuni lako maishani. Tambua hakuna aliyeandikiwa kufanikiwa au kupewa uhalali wa kukusanya mafanikio yote. Hayupo binadamu aliyeshushiwa mafanikio kutoka mbinguni bila kuweka mkazo kwenye malengo yake. Anza kutimiza ndoto zako kwa kuweka malengo yafanyayo kazi. Amini juhudi zako na mawazo yako ni muhimu mno kwa jamii. 
Jamii inahitaji mawazo yako ambayo unatakiwa kuyatendea kazi. Fanya kazi kwa bidii ukiwa unajua dhumuni lako ni lipi. Tumia kipato chako kwa uangalifu maana huwezi kujenga nyumba ukiwa mwingi wa starehe. Wapo wajinga wachache hawaweki akiba na kila kukicha wanalalamika maisha magumu. Ndugu yangu kama huna malengo maishani ni bure. Utaishi kulingana na mazoea tu yaliyomo.
Unakwenda kazini, mwisho wa mwezi ukifika mshahara wote unalipa madeni. Halafu eti unataka kulingana na tajiri wa Mexico Carlos Slim au Tokyo Sakswalle wa Afrika Kusini. Mafanikio hutengenezwa, katu mafanikio hayakutengezi wewe. Ukitaka kufanikiwa lazima ujue njia zake halali na kubuni mpya ambazo zitakupa sura mpya ya maisha yako. Ndoto zako zitakupa msukumo wa kufanikiwa.
Anza sasa kupanga vipaumbele. Pima kipato chako kama kinakuruhusu kufanya yanayokuzidi. Mawazo yako mazuri yakuongoze ili ufanikiwe. Tumia 80% kufuatilia fursa zilizopo na mpya.

WADAU WA HANDENI KUKUTANA IJUMAA LEADERS CLUB


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

WAKAZI wa Dar es Salaam wenye asili ya wilayani Handeni, mkoani Tanga, pamoja na maswahiba zao, wamepanga kukutana Ijumaa ya Februari 8, katika Viwanja vya Leaders Club, kuanzia saa 10 za jioni ili kutafuta namna ya kusaidia watu wasiojiweza wilayani humo.
Kikao hicho ni cha kwanza kufanywa na watu wa asili ya Handeni, katika jiji hili ambalo wananchi wengine kutoka mikoa na wilaya mbalimbali wamekuwa wakikutana na kujadili hali ya maisha inayowakabili.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, mmoja wa wajumbe wanaoandaa kikao hicho, kilichopewa jina la ‘Handeni Kwetu’, Kambi Mbwana, alisema kwamba kukutana kwa wadau hao ni sehemu maalum ya kutafuta namna pia ya kusaidiana na viongozi wao kwa ajili ya maendeleo yao.
Alisema kwamba Wilaya ya Handeni imekuwa ikikabiliwa na matatizo ya kila aina, ikiwamo njaa na shida ya maji, hivyo kwa wananchi hao kukutana pamoja, wanaweza kupata ufumbuzi katika baadhi ya mambo.
“Wakati Handeni ikiendelea kutajwa kama wilaya zisizokuwa na maendeleo kwa miaka 51 ya Uhuru, sisi tunakutana na kutoa kauli moja yenye tija kwa watu wote.
“Bila kuangalia nafasi zetu, vipato vyetu au heshima katika jamii, naamini moyo tu wa kukaa na kuzungumza au kuimba wimbo mmoja wa maendeleo, naamini mambo yatakuwa mazuri, hasa pale kitakapofanyika kilichojadiliwa na wote,” alisema.
Handeni, inayoongozwa na Muhingo Rweyemamu kama Mkuu wa Wilaya na Mbunge wake Abdallah Kigoda, imetajwa kukumbwa na baa la njaa na kulazimika baadhi ya wakazi wake kulalia mboga mboga pamoja na shida ya maji, jambo linalohitaji kujitolea kwa kila mmoja kwa nafasi yake.

February 01, 2013

CHOMBEZO: FIKIRIA VITU ULIVYONAVYO


Ni muhimu kujua kwamba maisha yetu yanaweza kubadilika na kuwa aidha mabaya ama mazuri kutokana na mitazamo yetu. Mitazamo ambayo inatupatia njia nyingine ama zilezile kufanikisha ama kutofanikisha malengo yetu.

Unamaliza wiki nyingine na kutafuta saa nyingine kwa mkondo uleule wenye kilio kwamba huna kitu. Kila siku unaona huna jambo linaloonyesha linakupa faraja ama burudani. Lakini hebu fikiri kwa bidii na kuyaangalia mazingira yako.

Angalia kitu gani unacho halafu jaribu kukizingatia kila dakika iendayo kwa mola wako. Jambo la maana ni kwamba jaribu kukazia fikra kwa vitu ulivyo navyo wala usihangaike kutilia mkazo kwa vitu usivyo navyo.
Kampuni ya amsuala ya habari,sanaa,budrudani,michezo na kadhalika. Chini ya mkurugenzi Kambi Mbwana.
Pengine unafikiria namna ya kumiliki vitu vingi sana, na unaamini vitu hivyo vitakupa fursa ya kupata vingine au kujisikia poa sana. Lakini angalia hakuna sababu ya kujiumiza kwasababu ya vitu usivyonavyo. Vitu kama vile nyumba nzuri, familia bora yenye upendo na mali kedekede.
Tambua hivi vyote haviwezi kukufanya wewe, bali wewe unaweza kuvifanya vitu hivi kuwa nyenzo maishani. Wahenga walipata kusema, afadhali chakula cha mboga za majani penye upendo kuliko ng’ombe dume aliyenoneshwa kwa chuki.

Jaribu kuwa na upendo wa hali ya juu kwa vitu ulivyo navyo, weka mkazo zaidi kila siku kwani hii itakusaidia kuvitafuta vile usivyo navyo. Pengine unajua familia yenu si bora, labda haina pesa, haina mali, haina elimu na hakuna uhakika wa chakula kwa siku.

Huenda mnaishi kwenye nyumba ambayo ikinyesha mvua tu inavuja. Wapo wanaolala kwenye vibanda. Labda wewe huna mavazi mazuri na ungelipenda kuwa na mavazi bora kama binadamu wengine wenye ukwasi. Natambua kuwa unachoshwa na aina yako ya maisha ya kukosa vitu muhimu ambavyo unadhani ndivyo vitakufanya ujisikie vema.

Pengine unatamani kula vyakula vya bei ghali kama na nyenye virutubisho anuai ili uende sambamba na wakati. Wapo watu wanahitaji kuwa na mwonekano mpya kila siku, na wanahitaji kujisikia bora kila dakika iendayo kwa mola.

Wapo wanaochukia nafsi zao kwa kukosa kufanya jambo fulani ama kukosa vitu fulani ambavyo vinawafanya wawe tofauti kila siku. Hebu tafakari ndugu yangu, kitu gani ukikipata kitakufanya umalize kuhitaji vitu vingine?

Kwanini unadhani kukosa kitu kile kunakufanya ushindwe kukitunza kitu hiki ulichonacho? Kwanini unakumbwa na hisia za unyonge kwakuwa umekosa kitu fulani? Nakuomba badili mtazamo huo, weka fikra zako kwenye vitu ulivyonavyo si vile usivyonavyo. Hebu fikiria, hivi unahitaji sana mavazi ya kisasa kuipendeza nafasi yako? 

Je unahitaji mapochopocho ili kuishi na kuwa na afya njema? Wapo watu ambao wakati mwingine wanajisikia kuwa wako kwenye minyonyoro ya umasikini kwa kuwa wanakosa vitu mbalimbali maishani. Wapo wengine huamua kujiingiza kwenye ulevi au matendo mabaya kwakuwa wanakosa pesa, mali, na vitu vingine.

Lakini hawazingatii vitu walivyo navyo. Lakini unapojiwekea mitazamo kwamba huna kitu fulani unajijengea mitazamo hasi ambayo itakuathiri mwili wako kila siku. Unatakiwa kutotoa nafasi kwa kufikiria vitu usivyo navyo. Unatakiwa kuweka mkazo wenye malengo yako na kwa vitu unavyomiliki.

Unaweza kudhani huna jambo au kitu unachomiliki lakini kwa hakika wewe unaweza kuwa ndiye mkombozi wa maisha yako kwa kuweka msingi kwamba hakuna kitu chochote bora bila wewe. Hakuna mtu yeyote atakayekufanya uwe bora zaidi, kuliko wewe mwenyewe. Unatakiwa kujiambia kuwa wewe ni bora kuliko kitu unachokikosa sasa na baadaye.

Ndugu yangu, nyakati zile ambazo unaona huna kitu, basi unatakiwa kujiheshimu sana matendo yako. Jiheshimu sana kwenye nyakati unazokumbwa na mitazamo mibaya juu ya kukosa vitu fulani.
Unapokosa vitu haina maana kwamba wewe si bora, bali unaweza kuheshimu suala hilo huku ukinuia kuwa bora kwa kutafuta vitu. Unaweza kujitolea katika asasi nyingi tu kwani hii inakupa fursa ya kupata mwanga mpya na matumaini mapya.
Kwani hii inakupata ridhiko na kujitambua kwamba familia yenu ina uwezo mdogo wa kifedha na kwamba huwezi kupata kila kitu. Njia nyingine mbali na kujiheshimu ni kuondoa wingu jeusi ulilonalo kwamba ukivipata vitu hivyo ni mafanikio makubwa.
Lakini unasahau kuwa kadiri unavyohitaji vitu ndivyo unavyoweza kufanikiwa kutohangaikia vitu. Kama nilivyokuasa wiki jana kwamba weka vipaumbele usiwe mtu unayeishi bila kujua unakokwenda.
Unajikuta unafanya kazi kila siku mshahara unalipa madeni kwa kuwa una hulka ya kutaka kumiliki vitu ambavyo huvimiliki na vinakuzidi uwezo. Panga njia za kuweka akiba ili uweze kujijengea uwezo zaidi. Safisha roho yako ili usiwe mtumwa wa matukio au vitu.
Maana watu wengi siku hizi ni watumwa wa vitu au matukio, pengine kuna harusi, sherehe na mambo mengine. Kama uwezo wako hauruhusu basi usitake kulingana na wale wenye uwezo mkubwa. Tafakari sana vitu ulivyo navyo na uvipatie heshima kwamba ni vitu vizuri na vinapaswa kuheshimiwa daima.

Ni wakati wa kujiangalia mwenendo wako kwani inakupa fursa nzuri ya kuukarabati ubongo wako na kujua namna ya kufanikisha kuvipenda vitu vyako. Penda kila kitu ulichonacho kwani kitakupa mwangaza zaidi wa kuyaona matumaini mapya. Matumaini haya yataanza kwa kuvitazama vitu ulivyo navyo au kazi uliyonayo ambayo inakupa wasaa wa kutafakari zaidi.
Inawezekana kuwa huoni mwelekeo kwa kuwa unapata maslahi duni, lakini kumbuka hakuna kizuri kinachokujia bila kuwepo kwa kingine. Hivyo ni wakati wako wa kujiheshimu na kutazama yale uliyonayo kuliko yale usiyonayo.

Tazama mbele zaidi wala usiumizwa na hali uliyonayo sasa, kwani saa yaja, mafanikio yako yanakuja. Nisikuchoshe msomaji, hili ndilo somo letu la leo. Mimi nakuacha hapa, naenda kuendelea kusoma riwaya nzuri na ya kusisimua iitwayo ‘Nyuso za Mwanamke.’ Je wewe umesoma vitabu vingapi mwaka huu na vimekupa maarifa. Hebu muulize mwenzio hapo! Tukutane wiki kesho.

January 29, 2013

VURUGU ZA MTWARA HEBU TUKUMBUKE KAULI YA MWAKA 2011 KUHUSU MRADI WA UMEME MKOANI MTWARA. ........?


• Mradi kabambe wa umeme kujengwa
• Rais Kikwete apokea ripoti ya maandalizi
• Utagharimu mabilioni ya fedha
• Utaunganisha mikoa yote kwenye Gridi ya Taifa

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatano, Oktoba 12, 2011, amepokea ripoti kutoka makampuni mawili ya kimataifa kuhusu Mpango Kabambe ya mradi mkubwa wa umeme ambao utaunganisha kwenye Gridi ya Taifa mikoa yote sita ambayo kwa sasa haiko kwenye gridi hiyo.

Rais Kikwete amepokea ripoti hiyo kutoka makampuni ya China National Machinery & Equipment Import & Export Corporation (CMEC) ya China na Siemens ya Ujerumani ambayo kwa pamoja yanatarajia kujenga kituo kikubwa cha kuzalisha umeme kutokana na gesi katika eneo la Mnazi Bay, mjini Mtwara na pia kujenga njia ya kusafirisha umeme ya kilomita 1,100 kutoka Mtwara hadi Singida.

Mradi huo mkubwa wa umeme wa megawati 300 utakaogharimu karibu dola za Marekani milioni 684 na utakaozalisha umeme wa moja kwa moja na wenye nguvu kubwa ya 300 kV (300 kV High Voltage Direct Current – HVDC) utagharimiwa kwa pamoja na mkopo kutoka Benki ya Exim ya China na Serikali ya Tanzania.

Umeme kutokana na mradi huo utaunganishwa kwenye gridi ya taifa na kutoka Singida hatimaye utavutwa kupelekwa katika mikoa ya Kaskazini Magharibi mwa Tanzania ya Kagera, Kigoma na Rukwa ambako pia utaongeza upatikanaji wa umeme katika machimbo ya madini yaliyoko katika mikoa hiyo.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mbali na mikoa hiyo mitatu, pia mikoa ya Lindi na Mtwara ambayo nayo haiko katika Gridi ya Taifa nayo itaunganishwa katika Gridi hiyo kupitia umeme huo.

Kuunganishwa kwa mikoa hiyo sita katika Gridi ya Taifa kupitia umeme wa mradi huo pamoja na Mkoa wa Ruvuma ambao utaunganishwa katika Gridi hiyo kwa mradi unaogharimiwa na Serikali ya Sweden kutakamilisha mpango wa Serikali ya Awamu ya Nne kuunganisha mikoa yote ya Tanzania kwenye umeme wa Gridi ya Taifa.

Kwa sasa Mkoa wa Kagera unahudumiwa na umeme kutoka Uganda, wakati Mikoa ya Kigoma na Rukwa inahudumiwa na umeme wa mafuta ya dizeli. Mikoa ya Mtwara na Lindi inapata umeme wake kutoka kampuni ya Wentworth ambao haujaunganishwa kwenye gridi ya taifa.

Kuunganisha mikoa yote ya Tanzania kwenye Gridi ya Taifa ilikuwa moja ya ahadi kubwa zilizotolewa na Serikali ya Rais Kikwete wakati anaingia maradakani na kwa kuuunganisha mikoa hiyo sita kwenye Gridi hiyo, Serikali hiyo itakuwa imetimimiza ahadi hiyo.

Akipokea ripoti hiyo, Rais Kikwete ameishukuru Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati na Madini pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa juhudi zao zilizofanikisha makubaliano ya kujengwa kwa mradi huo mkubwa wa umeme ambao utachangia kuongeza wingi wa umeme nchini katika kipindi ambacho kwa miezi kadhaa Tanzania imekabiliwa na mgawo wa umeme kutokana na ukame uliokausha maji kwenye mabwawa makubwa ya uzalishaji umeme nchini.

Rais Kikwete pia ameitaka Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Benki ya EXIM ya China kuhakikisha kuwa fedha za kutekeleza mradi huo zinapatikana haraka iwezekanavyo na pia ameitaka TANESCO na makampuni ya CMEC na Siemens baada ya kupatikana kwa fedha kuanza ujenzi wa mradi huo kwa kasi na kuukamilisha katika muda na ubora unaotarajiwa.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu
DAR ES SALAAM.

12 Oktoba, 2011

IMECHUKULIWA KUTOKA WANABIDII FORUM hii leo jumanne.

WATOTO/VIJANA WASOMAO NJE YA NCHI



Haika Lawere
Na Haika Lawere, via Facebook

Huwa nawatazama wazazi wengi hapa Tz wanavyojinyima usiku na mchana ili kupata ada kuwalipia watoto wao school fees uko nje eg USA/UK,India,Malysia,SA nk nk,wengine huiba ktk ofisi zao ili tu mtoto asome,wengine watauza properties ili mtoto ailimike,wengine hukopa,wengine hata maendeleo binafis yana simama ili vijana wasome!!! 
ila sasa...huko waliko hawa watoto,baadhi yao hawasomi,wengine huishia kuzaa na foreigners ili kupata papers,wengine hu-cohabitate na strangers ili kupata unafuu wa kodi,wengine ni mwaka wa 10 na zaidi hata Certificat/Diploma hawana hata darasa hawajawahi kuingia!!wingine wameshajilipua hata wazazi wakiumwa/kufa hawaji kuwaona!!
Wengine huaribikiwa kabissaaa kitabia/ kiakili/ki-mtazamo na wanakuwa hawa-fit mazingira ya uku!!mi niwasihi tu wadogo zetu ambao wazazi wenu wana-sacrifice kuwasomesheni nje muwe apprecitive,waoneeni wazazi wenu huruma wanavyoteseka,bongo pagumu jamani!! someni na muelimike na mkimaliza shule, ni vizuri mkarudi kutumikia nchi yenu,jamii yenu na kuwatunza wazazi wenu hapo watakapozeeka!!!msizamie nchi za watu wakati kwenu kuna-oppoturnities chungu-mzima!!!simhukumu mtu,ni mtazamo tu anyone can challenge!!

SOKA AFCON; CAPE VERDE, WANAJIAMINI WANAJUA SOKA


Na Markus Mpangala, Dar es salaam

Angola imechapwa magoli 2-1 na Cape Verde, taifa ambalo taifa linalokadiriwa kuwa na idadi ya watu 500,000 tu kulingana na sense zao. Cape Verde imeingia robo fainali huku kocha wake, Lucio Antunes akiongeza sifa katika kazi yake ya ukocha. Ingawa nahodha wake Fernando Neves alijifunga bao la kwanza, lakini aliongoza vema kikosi chao kuishinda Angola kisha kutinga robo fainali. Ni mafanikio makubwa kwao.

Cape Verde inashiriki michuano ya mataifa ya afrika yanayoendelea nchini Afrika Kusini. Kama tujuavyo michuano hii ilitakiwa kufanyika nchini Libya, lakini kutokana na matatizo ya kisiasa yaliyotokea nchini humo yalisababisha majadiliano baina ya chama cha soka cha Afrika kusini na kile cha Libya hivyo kubadilisha michuano.
Kocha wa Cape Verde, Lucio Antunes
Kimsingi Afrika Kusini ilitakiwa kuwa mwenyeji wa michuano ya mwaka 2015, hivyo basi kwakuwa imekuwa mwenyeji mwaka huu basi michuano ijayo itafanyika nchini Libya. Tukiitazama Cape Verde inayoshiriki michuano hiyo ikiwa na wachezaji wengi vijana wameonyesha soka safi ambalo liliwafanya waweze kufuzu kwa michuano hiyo.

Cape Verde imetinga fainali hizo ikiwa na kumbukumbu ya kuisambaratisha Cameroon kwa mabao 4-0 wakati wa kuwania kufuzu kwa AFCON. Kwa sasa wengi wanaitazama Cape Verde kama somo la kuendeleza soka. Idadi ndogo ya watu, kujiamini, kujua soka, lakini imejikuta ikikosa jambo moja tu uzoefu wa mashindano ya kimataifa kama AFCON. Pambalo la kwanza la Cape Verde lilikuwa baina yao na wenyeji Bafana Bafana. Pambano hilo lilimalizika kwa suluhu ya kutofungana hali ambayo iliibua maswali kwa wadau wa soka wa kote afrika hususani wenyeji waafrika kusini.

Matokeo ya pambano hilo ilimlazimu kocha wa Afrika kusini, Gordon Ingesund kufanya mabadiliko katika kikosi chake. Awali alimweka benchi mshambuliaji hatari Katlego Mphela na kumwanzisha Majoro hali ambayo iliwakuta wakishindwa kufurukuta mbele ya ngome ya Cape Verde inayoongozwa na nahodha Neves na T. Varela.

Pambano la kwanza kwa Cape Verde lilionyesha ushahidi kuwa ilijiandaa kwa AFCON mwaka huu na ilipania kufanya vema. mpaka sasa Cape Verde wamejikusanyia pointi mbili, wakiwa nyuma kwa pointi mbili kutoka kwa vinara Afrika kusini. Cape Verde ilitoka sare ya mabao 1-1 dhidi ya Morocco, hivyo kushika nafasi ya pili. Huku Morocco ikishika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi mbili na bao moja baada ya kutoka suluhu na Angola.

Aidha, pambano la pili Afrika Kusini iliichapa Angola kwa mabao 2-0, huku mshambuliaji Siyabongwa Sangweni wa Afrika Kusini akiibuka shujaa kutokana na mchezo mzuri uliomfanya apachike bao la kwanza. Afrika kusini iliingia pambano la pili ikimwanizhs beki wake hodari Tsepo Masilela ambaye alikosekana kwenye pambano la kwanza. Hali hii ilimsaidia sana nahodha wao Khumalo kucheza kwa kujiamini na kuongoza jahazi la nchi hiyo kwa ufanisi.

Lakini kwa Cape Verde ni wazi imeingia kwenye michuano hii ikielewa kuwa ni sehemu ya kujifunza licha ya kushindana kwa dhati. Washambuliaji wake Platini, Ryan Mendes wamekuwa kivutio kwa mashabiki wa soka wanaoifuatilia timu hiyo. Ryan Mendes akicheza kama shambuliaji wa pili katika mfumo 4-3-3, ameng’ara sana kutokanana kujaliwa kipaji kikubwa cha soka. Platini licha ya kuwa mshambuliaji mwenye kipaji anakabiliwa na ukosefu wa stamina ambayo ingelimwezesha kufanya maajabu mbele ya lango la adui.

Kwa upande wa kushoto beki Nivaldo anaonekana kucheza kwa utulivu lakini anaoksa kasi ya mchezo. Yeye ni beki aina ya Timothee Atouba, wanaocheza soka la taratibu sio kasi kasi kama Essou Ekotto. Lakini moja ya mabeki wanavutia kuwatazama jinsi wanavyoshughulikia washambuliaji ni nahodha wa Cape Verde, Neves  na Gege ambaye ni beki wa kulia wa timu hiyo.
wachezaji wa Cape Verde wakishangilia
Wanacheza soka la nguvu na vipaji. Wanajua namna ya kukabiliana na washambuliaji hatari kama Belhanda wa Morocco, mawinga hatari kama Siphiwe Tshabalala  wa Afrika kusini. Kila unapoitazama Cape Verde ikitandaza soka, utaona kwua inao vijana wanaojiamini sana, na wanajua kucheza soka. Mpangalio wao wa mashambulizi mara nyingi hutegemea kasi ya Ryan Mendes, ambaye amekuwa mchezaji kivutio zaidi na mwenye kilifahamu lango la adui kwa ufasaha.
Pia Cape Vaerde inayo bahati moja kubwa, viungo Soares na Mendes wake wanajua kupiga mashuti makali wakiwa na lengo la kujaribu kufunga. Mashuti hayo yanaweza kulenga goli (on target) au kutoka nje ya goli(off target) lakini jambo la msingi wanajaribu kutuonyesha kile walichonacho katika soka. Kwenye safu ya ushambuliaji Platini na Tavares wamekuwa tishio kwa kiwango cha kuridhisha, lakini wanaosa uzeofu tu. 

Tavares anatumika kama mshambuliaji wa kupambana na mabeki, huku Platini akiwa mshambuliaji wa pili maalumu wa kupachika mabao. Ni sababu hii inaonekana timu pinzani zinamfanya rafu mbaya sana Platini kuliko mchezaji mwingine yeyote wa Cape Verde. Kila dakika wanayocheza dimbani wanavutia, wanaburudisha na kujenga taswira mpya ya soka baada ya vigogo kama Cameroon na Senegal kukosekana kwenye michuano hii. Kwa watanzania wanaikumbuka Cape Verde iliyotuchapa mabao 2-1 wakati Taifa Stars ilipokuwa ikinolewa na Marcio Maximo.

Ni wazi wakati ule Cape Verde nayo ilikuwa kwenye kipindi cha mpito cha kujitengenezea njia ya mafanikio kisoka. Hatimaye mwaka huu wanashiriki AFCON, na wametuonyesha kuwa vipaji, kujiamini na kupangilia mambo ni msingi mkubwa wa mafanikio. Jambo lililo wazi na kufurahisha ni kwamba mfumo wa Cape Verde wa 4-3-3 uko wazi sana na unaonekana kwa uwazi ambao timu pinzani zinaweza kuichapa mabao mengi. Lakini Cape Verde wana nidhamu sana katika mchezo. Wanajua soka, wanajiamini lakini safu ya ulinzi inahitaji uzoefu zaidi. Platini anahitaji stamina, Mendes atakuwa bonge la kiungo siku za mbele. Tujifunze, na ku-graduate.