February 12, 2013

MAFUNZO YA ELIMU YA UJASIRIAMALI-IRINGA USIKOSE


BIASHARA NA UCHUMI: UNAHITAJI 'GIA' YA UVUMILIVU KUMUDU BIASHARA



Albert Sanga, Iringa
Makala haya ninayaandika leo ikiwa ni baada ya kumtembelea Bw. Frank Mwaisumbe nyumbani kwake; jumapili mbili zilizopita na kubadilishana nae mawazo. Bw. Mwaisumbe ni mfanyabiashara aliyepo mjini Iringa anaemiliki kampuni inayohusika na uwakala wa safari za Anga, iitwayo Getterland Company Limited na pia ni mmoja ya waasisi wa shirika la Mindset Empowerment linaloendesha mashindano ya mbio za Ruaha Marathon.

Nilimfahamu Bw. Mwaisumbe zamani kidogo na kuna kitu cha kusisimua hapa; kwa sababu ni mwalimu aliyenifundisha kozi ya masoko nikiwa chuo kikuu Tumaini Iringa. Wiki iliyopita mtakumbuka nilieleza namna wasomi wetu (wahadhiri, maprofesa na madaktari wa biashara) wanavyokwama kuzalisha wafanyabiashara halisi; kwa sababu wanafundisha mambo ambayo wenyewe “hawayajui kwa vitendo”.

Huyu Bw. Mwaisumbe ni mmoja ya wahadhiri ambao walinipa hamasa kubwa sana kibiashara nikiwa chuo kikuu; kwa sababu alikuwa akifundisha “biashara” halisi kwa sababu ni mfanyabiashara aliyefanya biashara nyingi sana tangu kitambo. Vyuo vyetu nchini vinawahitaji watu wa jamii ya Bw. Mwaisumbe katika kuwasaidia wahitimu wetu kujiajiri badala ya kulilia ajira ambazo “hazipo”

Ninashirikiana kwa ukaribu sana na Bw. Mwaisumbe zaidi sana katika shirika lake la Mindset Empowerment; ambapo mimi ni Mratibu (Coordinator) wa shirika hili. Katika kushirikiana huku kuna mambo mengi sana kuhusu uzoefu kibiashara ambayo nimekuwa najifunza kutoka kwake.
Jumapili hiyo niliyomtembelea tulitumia muda mwingi kujadili mipenyo, staili, mbinu na mambo yanayosababisha wafanyabiashara mbalimbali duniani kufanikiwa. Nilijifunza mengi sana katika mazungumzo yetu haya na nikakumbuka visa vingi vilivyowahi kunipata katika harakati zangu kibiashara.
Katika kujadili tulibaini kuwa hakuna mfanyabiashara yeyote duniani anaesimama mara moja kirahisi. Kila mfanyabiashara aliyefanikiwa ukimfuatilia historia yake atakueleza namna alivyoanguka-anguka na kusimama, namna alivyojaribu mambo mengi lakini akafanikiwa katika machache ama katika moja bila kusahau namna alivyopokea upinzani mkali katika kufanikisha hilo unaloliona limefanikiwa.

Binafsi ninakumbuka mtaji wangu wa kwanza niliupata (kwa jasho langu mwenyewe bila kupewa na mtu) nikiwa na miaka 19 kwa kuchuuza vitunguu kutoka pale Mang’ula Karatu na kuvipeleka Arusha mjini. Ilikuwa ni biashara niliyoipatia kweli kweli kiasi kwamba nikaweka malengo ya kuanzisha chuo cha mafunzo ya kompyuta na biashara.

Ndani ya mwaka mmoja nilifanikisha lengo langu hilo kwa kufungua chuo hicho kule wilayani Mufindi.  Nakumbuka thamani ya kile chuo ilikuwa takribani milioni ishirini. Nilijiona niliyefanikiwa na kila nilikokuwa ninapita nilikuwa ninapokea heshima na pongezi za mafanikio hayo hasa ikizingatiwa kuwa nilikuwa nimezikamata “milioni” nikingali mdogo wa miaka 20 tu tena nikiwa ndio kwanza nimehitimu kidato cha sita.

Ukweli ni kwamba saa niliyodhani kuwa “nime-win” kumbe ndio saa ambayo nilikuwa naelekea kuanguka. Ile biashara ilianguka yote; ndani ya miezi miwili tu nikawa sina kitu! Kufilisika kwangu kulitokana na mambo mawili. Mosi; wafanyakazi niliowaajiri kuendesha chuo walijigeuza miungu watu, wakaanza kuwanyanyasa wanafunzi na kuzembea kufundisha. Nilikuja kupewa taarifa mwishoni mambo yakiwa yameharibika kabisa kuambiwa kuwa kati ya wanafunzi 104 waliokuwa chuoni wamebaki wanafunzi nane tu!

Nilichanganyikawa na nikaenda haraka sana kuwatimua kazi, lakini nilishakuwa nimechelewa na mambo yalikuwa yameshaharibika. Pili; kulitokea shoti ya umeme (kwa uzembe wao) na ukaunguza sehemu kubwa ya vifaa vya chuo kile zikiwemo kompyuta na vifaa vingine. Sikuwa na ujanja zaidi ya kukifunga kile chuo na kukubali matokeo ya kufilisika.

Leo hii ninapojikumbusha kuhusu biashara ile namtafakari mwandishi aitwaye Mchungaji Daktari Robert Schuller aliyeandika kitabu kiitwacho, “Success is Never Final Failure is Never Ending”. (Kufanikiwa sio kikomo na kushindwa sio mwisho). Anachomaanisha mwandishi huyu ni kuwa ukifanikiwa usijisahau na ukianguka usikate tama.

Ukweli ni kwamba kwenye biashara kuna mapito mengi sana kiasi ambacho mfanyabiashara unahitaji uvumilivu mkubwa mno kuendelea. Biashara sio lelemama! Unaweza kutumia miaka mingi sana katika kujenga biashara zako na kukusanya mali; lakini ukaja kupoteza kila kitu ndani ya dakika chache. Huhitaji kukata tamaa, unahitaji uvumilivu na kuanza upya. Huo ndio ujasiriamali na sifa ya mjasiriamali ni kutokukata tamaa.
Unadhani mchezo umeishia hapo? La hasha! Sikukata tamaa, nilisimama na kuanza kujikongoja tena; safari hii nikaamua kufanya biashara ya kukusanya na kuuza alizeti kule wilayani Njombe katika maeneo ya Irembula. Kama kawaida; si rahisi kufanya biashara peke yako; ni lazima uwe na watu. Hata huko kwenye alizeti nilikuwa na watu niliowaamini kunikusanyia na kunitunzia.

Mwanzoni nilienda vizuri; nikajisemea moyoni; loo! Biashara si ndio hii? Kumbe nilikuwa nimepotea kwani mkasa mwingine ukanitokea. Nikiwa nimekopa fedha kutoka kwa watu na kukusanya alizeti kwa wingi huku nikijua saa ya kuuza nakuwa milionea; nikadhulumiwa mchana kweupe! Yule nilipotunza alizeti akaauza alizeti magunia yote kisha akakimbia na fedha zote na hadi leo ninapoandika makala hii ikiwa imepita miaka kadhaa sifahamu alipo.

Huu ukawa ni msiba mwingine kibiashara kwangu. Tena ni bora angekuwa alikimbia na mtaji wangu pekee; lakini aliondoka na hela hata nilizokopa; hii ina maana nilipoteza mtaji wote na nikabakiwa na madeni. Hii ndio biashara, sikukata tamaa ndio maana hadi leo “nimekomaa” na biashara. Kimsingi sina miaka mingi kiumri na wala sina miaka mingi sana katika biashara, lakini kuna visa vingi mno vya kushindwa na kufanikiwa vilivyonitokea hadi sasa; kiasi kwamba nikisema nivilete vyote gazeti zima halitatosha kwa juma moja.

Hata hivyo; katika mikasa yangu miwili niliyoileta hapo juu kuna mambo machache napenda uyajue ambayo Bw. Mwaisumbe amenisaidia sana kuyajua. Mosi unapokuwa katika biashara unatakiwa uwe na imani isiyoteteleka ya kuwa kuna siku utafanikiwa. Inawezekana ukawa unafanya biashara lakini haujui “utatoka” lini.

 Inawezekana umeshapata hasara nyingi mno katika biashara zako; lakini kama ukibaki na imani hii hakika ipo siku utafanikiwa tu. Bw. Mwaisumbe huwa anapenda kusema hivi “Mtu aliyeanguka-anguka sana katika ujasiriamali, siku akiinuka, hataanguka tena. Na mtu anaeanguka na kusimama hahofii kuanguka kesho kwa sababu anajua ataamka tu”

Pili; asilimia kubwa ya sisi wajasiriamali tunaangushwa sana na watu wengine, ediha tunaowaamini ama tunaowaajili ama tunaoamua kupanda nao tunapopanda kibiashara. Pamoja na uweli huu; haimaanishi kuwa usiwaamini watu; la hasha! Jambo la kufanya ni kuhakikisha unajitahidi kadiri uwezavyo kutafuta, kushirikiana na kuajiri watu sahihi katika ujasiriamali wako. Itakumbukwa kuwa nimewahi kuandika kupitia gazeti makala yenye kichwa; “Mjasiriamali na Sayansi ya kuajiri wafanyakazi”

Tatu; unapofanya ujasiriamali ama kama unatamani kuingia katika ujasiriamali hutakiwi kuogopa kupoteza mtaji ama hatua uliyonayo. Kitu cha thamani katika ujasiriamali sio mali ama fedha unazofanikiwa kuzipata; bali ni “akili ya fedha (financial IQ), kujiamini na uzoefu unaoupata kila unapofanya biashara. Ni vema mjasiriamali kujenga ujasiri na kujiamini (spirit) kiasi kwamba ujisemee kuwa “hata kama nikipoteza kila kitu nilichonacho leo, ninaweza kurudisha na zaidi ya nilivyokuwa navyo”.

Niandikie: stepwiseexpert@gmail.com;  0719 127 901

February 11, 2013

CHOMBEZO: KILA MTU, MTU, MTU NA HAKUNA MTU



Markus Mpangala
Hii ni hadithi  kuhusu watu wanne waitwao Kila Mtu,Mtu, Mtu na Hakuna Mtu. Kulikuwa na kazi muhimu kufanywa, na Kila Mtu alikuwa na uhakika kila mtu angefanya kazi hiyo, lakini Hakuna Mtu aliyefanya hivyo. Mtu alipata hasira kuhusu hili, kwasababu ilikuwa ni kazi ya  Mtu. Kila Mtu aliwaza kuwa kila Mtu anaweza kufanya hivyo lakini Hakuna Mtu aliyetambua kwamba kila mtu asingefanya hivyo. Na mwisho iliishia Kila Mtu kumlaumu Mtu wakati Hakuna Mtu aliyefanya  chochote ambacho Kila Mtu angeweza kufanya. Mwisho wa hadithi……
Haya sasa tafakari. Je wewe unatumia pesa zako vizuri? Je una madeni mengi? Je wewe huachishwa kazi mara kwa mara? Nini sababu zako za kuachishwa kazi? Au ni kwasababu ya kazi yenyewe au yule aliyekupa kazi? Au ni kwasababu mazoea au tabia fulani ambayo unapaswa kurekebisha?
Ikiwa hutumii vizuri pesa zako mwenyewe, je utaweza kutumia pesa za familia? Je unatazama mambo yote kwa mtazamo mbaya? Tafakari mara nyingine. Jipe nafasi ya kufanya hivyo huku ukijua kuwa kazi inahitaji uelewa, umakini na bidii.  Sote tunajua kazi ni za kila mtu hapa duniani. Hakuna mtu ambaye anatarajia kazi ya mtu itafanywa na mtu mwingine. Kila mtu anajua anahitajika kufanya kazi kwa bidii ili asimtegee mtu au kumtegemea mtu.
Na kila mtu anahitaji kazi ili aishi vema, hakuna mtu asiyehitaji familia bora. Kwahiyo ili kutimiza haya ni lazima ujifahamu. Lakini ujue wajibu wako katika kazi yako. Na ufahamu mipaka ya kazi yako. Fahamu matumizi yako ya kila siku ili usimlaumu mtu kwakuwa hakuna mtu atakayekusaidia. Fahamu bajeti yako kwa siku,juma,mwezi, na mwaka. Lazima ujifahamu kila hatua unayokwenda mbele maishani. Tambua kila mtu anafanikiwa endapo atafuata kanuni za msingi za maisha.
Hakuna mtu anayependa kuona mtu anashindwa kufanya kazi yake bila sababu, kwakuwa tu mtu anategemea kufanya hivyo. Na asipofanya hivyo inakuwa shida na inamfanya mtu awe na hasira dhidi ya kila mtu. Pesa, kazi na maisha ni lazima viwe tofauti ili kuongoza familia yako. Usitegemee mtu ataongoza familia yako. Hakuna mtu atakayewaambia wanao wasome kwa bidii.  
Ukihitaji kazi, basi hakikisha unayo hoja za kusema kwa mtu. Je umekabiliana vipi na waombaji wapya wa kazi? Wangapi wanatimiza wajibu wao katika kazi, maana kila mtu anataka kuona mtu anafanya kazi yake ipasavyo. Je unalisaidiaje taifa kutokana na kazi yako? Unafahamu kuwa kutoangalia mambo kijuu juu inakusaidia kujifahamu na kuongoza vema ofisi yako au kupata kazi mpya?
Unatambua kuwa ndani ya ofisi yako kila mtu anahitaji cheo ulichonacho? Hakika nakuambia hakuna mtu ambaye hataki kuona mtu anaishi vizuri. Kila mtu anajua ni lazima afanye kazi na apendwe na kila mtu. Mtu huona fahari pale anaposifiwa na kila mtu kutokana na kuwajibika katika kazi yake. Kazi ya kila mtu ni mtu kuifanya kazi yake kwa bidii na hakuna mtu ambaye anapenda kuharibu kazi yake.
Kwa hakika ndugu zangu mnatakiwa kuwa waelewe  wa mambo na kila mtu ajue kuwa unaelewa. Mtu mwenye bidii ya kazi na kujifunza mambo hachoki kuwatumikia watu, na kila mtu hupenda kufanyiwa kazi zake vema. Usiwe mtu unayependezwa na mambo yaleyale au kukubaliana kila jambo kwa mtindo na sababu zilezile. Uwe mtu ambaye kila mtu anafahamu kuwa akihitaji ushauri basi atakuwa wa kwanza kuwajibika mbele ya hadhira.
Jipe muda wa kujisomea, fanya tafakari kila unachojisomea. Natambua kila mtu anachoka atokapo kazini, lakini hakuna mtu ambaye anapenda kukaa tu ofisini kwake bila kufanya kazi yoyote. Timiza malengo yako kwa kuwatumia watu. Uwe mtumishi wa kila mtu kulingana na cheo chako au nafasi yako kwa jamii. Kila mtu anahitaji msaada wako wa nasaha na mengineyo, kwani duniani tupo kwaajili yaw engine.
Wengine hawa ni kila mtu ambaye anajua umuhimu wa kuwatumikia. Na hakuna mtu ambaye hajui umuhimu wa hili. Je unadhani kazi ya mtu ni ipi? Na hadithi hii ya kila mtu inakupa funzo lolote? Na inawezekana ndugu yangu umekata tama ya maisha. Lakini tambua kila mtu amepitia kwenye milima na mabonde. Hakuna mtu aliyefika kileleni bila kuanguka.
Kila mtu anayepanda mlima Kilimanjaro kuna mahali aliteleza au kuanguka. Hakuna mtu ambaye amefanikiwa bila kuchoka, lakini unahitaji nidhamu zaidi ya kuchoka kuliko kuendelea kudhani kila mtu anaweza tu kufanikiwa akikaa sebuleni na kuota amefanikiwa.
Unachotakiwa kufanya ni kusema katika kazi za mtu basi wewe ni kila mtu na hakuna mtu anayeweza kuifanya kazi hiyo zaidi yako. Waingereza wanaomsemo wao,  simama uhesabiwe vinginevyo kaa chini usahauliwe. Kwa maneno hayo inamaana hakuna mtu muhimu katika maisha yako zaidi ya wewe. Hebu rudi juu usome falsafa ya leo ya Kila Mtu, Mtu, Mtu na Hakuna Mtu. Halafu jifahamu wewe ni nani kati ya hao wanne.

February 07, 2013

MVUA KUBWA YANG'OA MADARAJA BARABARA YA LITUHI-MBAMBA BAY


Na Egbart Jeremy, Nyasa

Mvua mkubwa iliyonyesha mapema mwezi huu imesababisha baadhi ya miundombinu kuharibiwa. Miongoni mwa maeneo yaliyoharibiwa kabisa ni Daraja la Mbaha, na barabaraba ya Lituhi kwenda Mbamba kwa ujumla, ambapo imejifunga kutokana na kukosekana kwa vivuko vingine. 
Moja ya maeneo yaliyoharibiwa kutokana na mvua kubwa iliyonyesha wilayani Nyasa
Mvua hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa ukosefu wa mawasiliano baadhi ya vijiji hadi vijiji katika mwambao wa ziwa Nyasa. Sio madaraja pekee, bali ukuna uharibifu mkubwa sana vyanzo vya miradi ya maji hususani katika kijiji cha Lundu. 
Hadi sasa hali haijatengemaa kiasi amabcho wakazi wa maeneo yaliyokumbwa na uharifu wanakosa huduma muhimu kutokana na ukosefu wa usafiri kutoka eneo moja kwenda jingine. Ikumbukwe miradi ya maji katika kijiji cha Lundu ni moja ya miradi mipya iliyokamilishwa mapema mwishoni mwa mwaka jana hivyo kuleta nafuu kwa wakazi wake. Lakini kutokana na uharibifu uliotokana na mvua kubwa kunyesha utalazimisha miradi hiyo kuanza kukarabatiwa upya.