April 05, 2013
WANAFUNZI SHULE YA MSINGI KWAMBE WAPEWA CHAKULA CHA MCHANA
Madhumuni
kwambe
April 04, 2013
DARASA HURU: CCM KAENI CHONJO NA JULIANA SHONZA NA MTELA MWAMPAMBA
![]() |
| Daniel Gingo |
Kuna wakati ukiangalia siasa wanazofanya Juliana Shonza na
Mwampamba (na hasa Mwampamba) wanachofanya sio siasa, wanachokifanya ni utoto!
Tena unaweza kudhani kwamba inawezekana CHADEMA walipumua baada ya hawa jamaa
kuondoka huko.
Niliwahi kusema kwamba utoto wanaoufanya sasa hivi
utakitokea puani CCM, kama baadhi yenu hamtaki kuniamini kwa kudhani kwamba
nina chuki na CCM basi mimi na ninyi tunyamaze kwa sasa, tusubiri wakati
ukifika utasema.
Kwa Juliana mpaka kesho sijui kilichomtokea, namfahamu kama
dada aliyekuwa akimpenda na kumtumikia Mungu kule Mabibo, kilichotokea kwake
sikijui, BWANA AJUA!
KWA MFANO WAULIZENI MASWALI HAYA:
1. Kama wakiwa CHADEMA walikuwa wakijua njama zote za mauaji
zilizokuwa zikipangwa au kutekelezwa na CHADEMA nini kiliwafanya washindwe
kuinuka na kusema kama kweli walikuwa wazalendo kwa Taifa hili? Kwa nini waje
waanze kutoa tuhuma hizo leo magazetini na mitandao kama humu?
2. Kama walijua njama za uhalifu zilizokuwa zikifanywa na
CHADEMA na wakaficha ‘uovu’ huo ni vipi leo watashindwa kuficha uovu wa CCM
pindi utakapofanywa? Nini kitawazuia kuficha madudu ya CCM dhidi ya wananchi wa
Tanzania?
3. Katika njama na mikakati ya ‘uovu’ ya CHADEMA wao
walishiriki kiasi gani na kwa kiwango gani? Je, ni kweli hawakushiriki mipango
iliyotelekezwa? Nini kiliwafanya wajiondoe huko huku wakijua kuwa walishiriki
kupanga njama hizo? Je, walikosa walichoahidiwa?
4. Kama waliweza kuwasiliti wenzao wa CHADEMA na leo wanakuja
kuwaanika hadharani, watuambie kwa nini tusiionye na kuitahadharisha CCM kukaa
chonjo na vijana hawa? Kama waliwasaliti CHADEMA na leo wanafichua siri ambazo
walishiriki wote Nape Nnaye ana uhakika gani kwamba nay eye hatakuja kuumbuliwa
siku za mbeleni?
MWISHO
a. Narudia leo kuionya CCM, iwe macho na vijana hawa, na sio
CCM tu, hata vyama vingine kwa ajili ustawi wa Demokrasia nchini, viache
kushabikia watu wanapoacha vyama vyao na kuja kuwa mavuvuzela kwenye vyama
vipya!
b. Sina uhakika kama CHADEMA haijawatuma vijana hawa
kuivuruga CCM, lakini mashaka yangu ni makubwa juu ya hilo.
MANABII MNAO, LAKINI HAMUWASIKILIZI!!!!
Madhumuni
siasa
KIKUNDI CHA HABARI CHAKUTANA KUWEKA MIKAKATI
Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam
NAIBU Waziri wa Sheria na Katiba, Angellah Kairuki amewataka
wanachama wa kikundi cha waandishi wa habari cha kujikomboa kiuchumi (Habari
Group) kupendana na kuaminiana ili kukifikisha kikundi hicho mbali.
Kairuki ambaye pia ni mlezi wa Habari Group, alikitaka
kikundi hicho kutokuwa wachoyo wa kusaidia waandishi wa habari wengine wenye
nia ya kuungana na kufanikiwa kimaisha.
Akizungumza na kikundi hicho Dar es Salaam juzi, alisema ili
mtu afanikiwe ni lazima awe mwenye upendo na kusaidia wengine pale penye mwanya
wa kufanya hivyo na kuwataka wanachama wote kuwa na moyo wa kujitolea kwa ajili
ya kikundi. "Sitopenda
kusikia kikundi hiki kimekufa kwa sababu ya mifarakano na chuki miongoni mwenu
kwani kwa kufanya hivyo hamtofikia malengo mliyokusudia," alisema Kairuki.
Aliongeza kuwa
wakati anaingia madarakani aliweka vipaumbele kwa wafanyakazi wa majumbani,
madereva wa aina zote, wafanyakazi wa mashambani, wahudumu wa baa na nyumba za
wageni, walinzi na waandishi wa habari.
Na kwamba ameanza kushughulikia haki mbalimbali za makundi hayo, ambapo
kwa sasa wapo kwenye mchakato wa kuishinikiza serikali kusaini mkataba wa
kuridhia haki za wasichana wa majumbani.
Aliwapongeza waandishi wa habari kwamba pamoja na changamoto
nyingi wanazokutana nazo, lakini hawakati tamaa na wamekuwa wakifanya kazi yao
kwa moyo mmoja na kwa bidii.
Kama mkakati wake wa kuwasaidia waandishi wa
habari, alisema atasimamia Habari Group ili wawe mabalozi wazuri kwenye mambo
mbalimbali kwa jamii, ikiwemo kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali, kuwapa elimu
ya umuhimu wa cheti cha kuzaliwa, sambamba na kushirikiana nao bega kwa bega
kwenye mambo muhimu ya kijamii.
"Kuwasidia kwenu ni miongoni mwa malengo yangu
niliyojiwekea ya kupigania haki ya baadhi ya makundi ambyo nimeona haki zao
kama wafanyakazi hazitekelezwi,"aliongeza.
Madhumuni
Maendeleo
MGODI UNAOTEMBEA: WAMEAMUA KUIWEKA TANZANIA KIKAANGONI.
![]() |
| Kambi Mbwana, Dar es salaam |
KABLA ya kuanza kufikiria labda kuna mkono wa mtu au Taifa
kutoka nje ya nchi yetu, vyema tukaelewa kuwa siku zote mvunja nchi ni
mwananchi mwenyewe, hasa kwa kuangalia jinsi baadhi yao wanavyokosa uzalendo
kwa kutenda vitu visivyokuwa vya kiungwana.
Watu hao wamekuwa wakiendeleza kufanya vitendo vya
kushangaza na kuogopesha kwa kiasi kikubwa, ikiwa ni njia moja wapo
inayolitangaza Taifa letu vibaya nje ya nchi.
Tangu kupata Uhuru uliopatikana kwa harakati za viongozi
wetu, akiwamo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na wapambanaji
wengine, Tanzania ilijipambanua kuwa ni kisima cha amani.
Katika kulinda msingi huo, wananchi walielimishwa au kupewa
kauli mbiu ya namna gani wanavyotakiwa waishi kwa ajili ya kuishi kwa amani na
upendo ili kukuza uchumi wa nchi yetu.
Ni kweli kabisa. Kiu hiyo ilidumu kwa miaka mingi, ingawa
sasa naanza kuona kuwa hali hiyo imekwisha. Anayesema kuwa nchi hii bado ni
kisiwa cha amani, hakika anatumia lugha nzuri kwa kuhofu anayewaeleza hivyo
wataondoa woga kwa sababu moja ama nyingine.
Kwanini nasema hayo? Taifa letu sasa lipo kwenye matatizo
makubwa ya vurugu za kidini, siasa na mambo mengine ambayo yote kwa pamoja
yanawaweka wananchi kwenye wasiwasi mkubwa.
Kumekuwa na matukio mengi ya kutisha. Katika kulielezea
jambo hilo la machafuko ya Tanzania, wengi watawataja watu maarufu au wale
ambao matukio yao yamegusa watu wengi. Lakini ukweli ni kwamba hao wanaotajwa ni wachache kati ya
wengi ambao labda kwa kutokuwa maarufu kwao, au kutojulikana kwa madhira
yaliyowakuta, kunawafanya wasionekane yale yaliyowatendewa.
Ingawa watu watawataja watu kama vile Mwandishi Daudi
Mwangosi, mtu aliyepoteza maisha kwa staili ya kutisha kupita kiasi. Mbali na
Mwangosi, bado wapo watu kama vile Daktari Stephen Ulimboka, Mhariri wa
Mtendaji wa Kampuni ya New Habari 2006 (Ltd), Absalom Kibanda ambao matukio yao
ya kutekwa na kuteswa yamewagusa watu wengi na kuendeleza msemo kuwa Tanzania
sasa si kisiwa cha amani.
Mbali na watu hao, ambao kwa mapenzi ya Mungu wameendelea
kubarikiwa uhai, wapo ambao wamepoteza maisha, akiwamo Padri Evarist Mushi wa
Kanisa Katoliki Visiwani Zanzibar. Padri huyu aliuagwa na kuibua hisia nzito sambamba na kuzidi
kueneza chuki kwa miongoni mwa jamii ya Kitanzania. Pamoja na yote hayo, bado
wapo wananchi ambao wamekuwa wakiishi bila kuvumiliana kwa sababu za ajabu,
hasa huu wimbo wa kuchinja unaoendelea kuimbwa kwa lugha za chuki na kukiathiri
kizazi cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Tangu kuzaliwa kwa Taifa hili, likipita katika vipindi
tofauti kwa viongozi tofauti waliokuwa na mapenzi makubwa kwa wananchi wao,
watu waliishi kwa upendo na kuvumiliana kupita kiasi. Si kama ukatili haukuwapo, huenda ulikuwapo, ila si kama
ulivyokuwa sasa kiasi cha watu kushikwa na mihemko na kutenda bila hata kuogopa
vyombo vya Dola katika mazingira wanayotaka wao.
Hii si njia nzuri ya kuzalisha amani kwa Watanzania. Zaidi
tunaendeleza chuki, fitina, majungu na kusababisha sumu mbaya ya vurugu ambazo kuna
siku zitashindwa kumalizwa.
Katika kutafuta nufumbuzi juu ya machafuko ambayo mengi
huibuka kwa kupita mgongo wa dini na siasa, baadhi ya watendaji wa serikali,
wanashindwa kutumia busara, hekima na utu juu ya kumaliza migogoro hiyo.
Kuna siku tutashuhudia watu wakiingia barabarani kufanya
uhalifu, maana tayari walishazoea na kuona kuwa hakuna wa kuwazuia kwa namna
moja ama nyingine.
Katika kuliangalia Taifa lenye amani, hatupaswi kuchekea
kauli za uchochezi zinazotoka kwa mtu yoyote, iwe ni mwanasiasa au kiongozi wa
dini ambaye hana uzalendo na wananchi wake. Huo ndio ukweli. Mihemko yako haiwezi kutufanya tuone upo
sahihi hata pale utakaposimama kwa kupitia cheo chako cha kidini au kisiasa
kuhamasisha vurugu hatari kwa Taifa hili.
Hatuwezi kwenda hivyo. Bado hatuna uchumi unaotufanya
tulinge kuwa tutakuwa pazuri hata kama baadhi ya watu watafanya vurugu,
wataharibu miundo mbinu yao kwasababu ya kuhamasisha ujinga kutoka kwa mtu
mmoja asiyekuwa mzalendo. Kwa mfano, wapo watu ambao wanabishana juu ya nani yupo
sahihi katika suala zima la kuchinja. Sakata hili lilibuliwa na Waziri Stephen
Wasira, alipokuwa anazungumza jijini Mwanza.
Mengi yaliendelea kuibuka hasa pale Wasira alipojikuta
akitoa ufafanuzi kuwa mwenye mamlaka ya kuchinja ni Waislamu. Kauli ya Wasira
isingeleta matatizo kama watu watatumia akili na uzalendo kufuatilia suala
hili. Kuna uwezekano mkubwa kuwa huenda Wasira amezungumza hivyo
kwasababu ndio utaratibu uliozoeleka kwa Watanzania wengi. Hata wachungaji,
mapadri walikuwa wakitaka kufanya shughuli inayoshirikisha watu wa jamii
tofauti, vitoweo vyao vilikuwa lazima vichinjwe na Waislamu.
Pamoja na yote hayo, watu ambao ni jamii ya Wakristo
hawakulazimishwa pia wachinjiwe na Waislamu kama hawajaona hilo linafaa, ingawa
tatizo litakuwa pale wanapochinja wao na kuwalisha wengine. Kumbe leo wapo watu wanaotaka wachinje, basi sakata hilo
linastahili viongozi wakae na kushirikisha makundi ya kijamii hasa kwa viongozi
wao wa dini, Mashekhe, Mapadri na wengineo.
Wakati hayo yakiendelea, watu wanahoji. Je, vurugu hizo
mwisho wake ni wapi? Ingawa wapo wanaosema kuwa vurugu hizi zina mkono wa mtu,
wakimaanisha watu wanaotumiwa na wengine kutoka nje ya nchi, lakini bado
hainifanyi nishindwe kuwataja watu hao kama majuha na wasiokuwa na uzalendo
katika Taifa lao.
Watu hao ambao lengo lao kubwa ni kuiweka nchi katika
mtihani mzito, hasa katika kiu ya kuilinda amani yake, hawastahili kuchekewa
hata mara moja, maana wanavyoendelea kuchekewa, ndivyo sumu hiyo inavyozidi
kuenea na kuota mizizi hata kwa wale wasiokuwa na tabia hiyo.
Kila mtu wakiwamo viongozi wa serikali, chini ya Rais Jakaya
Mrisho Kikwete kwa upande wa Bara na Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wa
Visiwani kuendelea kuwa wakali kwa kundi lolote, mtu yoyote anayefanya uvunjifu
wa amani kwa makusudi kwa faida anayoijua mwenyewe.
Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi pamoja na vyombo vya ulinzi
na usalama vihakikishe kuwa vinakuwa mstari wa mbele, pamoja na kutoa elimu kwa
wananchi juu ya kulinda amani na mustakabali wa Tanzania.
Leo tunaona ni kawaida, lakini ikiendelea hivi, kila mmoja
ataona ana uhuru wa kufanya kila analotaka, hivyo kusababisha machafuko, mauaji
ya watu wasiokuwa na hatia, hasa tatizo hilo linapopitia kwa mlango wa dini au
vyama vya siasa, kama vile Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama
Cha Wananchi (CUF), Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vyama vingine vya siasa
vilivyosajiliwa katika nchi yetu.
Huu ndio ukweli wa mambo. Tusipokuwa makini, kujua nini cha
kufanya kwa ajili ya nchi yetu, hakika hatutakuwa na kizazi chenye uzalendo,
kinachoithamini amani kwa ajili ya kulinda utu na heshima za watu.
Tuna wajibu wa kulijua hili, maana inapotokea machafuko
makubwa, wanaoathirika ni akina mama na watoto, hivyo ni wazi hawa wanaofanya
vitendo vya unyama kwa wenzao, wale wananaokesha kubuni namna ya kufanya vurugu
za kidini na kisiasa wafikie wakati waone imetosha kwa ajili ya kuendeleza
wimbo wetu wa Tanzania kisiwa cha amani.
MAONI: kambimbwana@yahoo.com
0712 053949
0753 806087
Madhumuni
Mgodi Unaotembea,
siasa
April 03, 2013
GHASIA ZA TUNDUMA, HALI SIO NZURI SANA
| Ghasia zinazoendelea katika mji wa Tunduma ulioko mkoani Mbeya zimechochea uharibifu kijamii. Tunduma haiko katika hali nzuri. |
Vurugu kama hizo ziliwahi kutokea mjini Mwanza na kuhusisha wamumini wa imani ya kikristo na Kiislamu. Mauaji yalitokea na serikali ilifanya juhudi kuwakamata wahusika.
Hapa mwakilishi
wa Blogu ya Lundunyasa, anaelezea kwa ufupi sana juu ya kile kinachoendelea
mjini humo.
Ni kwamba inaelekea hotuba ya Rais
Jakaya Kikwete kuhusu uchinjaji bado haijaeleweka, hivyo wakristo bado walikuwa
na msuguano na wenzao juu ya nani achinje.
Tamko la Polisi lilisema
waislamu waendelee kuchinja sasa leo alfajiri vijana wa kikristo walienda
machinjoni na kumgawia kichapo cha kutosha mchinjajiwa kiislam ambaye
alifanikiwa kutoroka.
Baada ya hapo wakristo nasikia
ndiyo wakaanza hizo fujo ikiwemo pamoja na kufunga barabara, kuharibu msikiti,
kubomoa nyumba ya polisi mmoja aliyejenga uraiani, wameandamana na biblia mikononi
kudai haki ya kuchinja.
Polisi wa Tunduma kazi
imewaelemea na ikabidi nguvu itoke mkoani na RPC yupo huko sasa hivi. Juzi
kanisani Padre mmoja alitoa kauli kuwa kama hawa watu wanataka kuchinja basi
watuchinjie na kitimoto.
Kisa kikuu ni kwamba madalali wa
mifugo wamegoma kupima nyama zinazochinjwa na wakristo, hivyo wakristo wanahoji
kwanini iwe hivyo. Pia mtaani mabucha ya nyama zilizochinjwa na waislamu
zimeganda hakuna wanunuzi.
Raia ilibidi wakimbilie
mahakamani kwa kuona kwamba ndiyo sehemu pekee ya usalama kwao, hivyo ikalazimu
mahakama kuhairishwa ili kuepusha balaa. Kale kamchezo kakuchoma matairi na
kufunga barabara kakawa ndiyo mchezo wa kawaida.
KIM POULSEN ANASTAHILI MKATABA MNONO TAIFA STARS
Hivi karibuni kocha
mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen ametoa mipango mizuri kwa maendeleo ya soka.
Kim ameliambia shirikisho la soka nchini kuwa anahitaji kuona kikosi cha timu
ya taifa ya vijana Serengeti Boys ikishiriki michuano ya Ligi Kuu Tanzania
Bara.
Kocha Kim anasema,
mpango wake ni kutaka kuona wachezaji hao wanakuwa wanacheza mechi za ushindani
kwa kila wiki ya mwezi ili kuweza kujijenga kiushindani na kimbinu. Kwa mujibu wa kocha
huyo, anasema kama wachezaji wa Serengeti Boys wataweza kucheza mechi moja kwa
wiki, kisha wakafanikiwa kushiriki michuano yote ya Ligi Kuu basi hakuna shaka
kabisa watakuwa kwenye ushindani mkali watakapopewa nafasi ya kuchezea timu ya
wakubwa.
Kocha Kim anasema,
wachezaji hao vijana wanatakiwa kuchezea timu ya taifa kwa muda kisha
wakifikisha umri wa kuvuka Serengeti
Boys basi watarudishwa kwenye klabu zao ili kupisha wengine waweze kutumika
katika kikosi hicho na kushiriki michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Dhumuni la kocha huyo
ni lilelile kuwafanya wachezaji wengi vijana wakipata nafasi na kucheza soka la
ushindani wakati wote. Pia kocha Kim
anakusudia kujenga kikosi bora cha miaka ijayo hivyo hakuna wasiwasi kuwa kati
ya mwaka 2015 au 2017 tanzania inaweza kabisa kushiriki michuano ya Kombe la
mataifa ya Afrika pamoja na kombe la dunia mwaka 2018 nchini Russia au 2022
nchini Qatar.
Nilipotafakari
programu hiyo upesi nikakumbuka namna kocha Marcio Maximo alivyoweza
kuishirikisha timu ya taifa ya vijana kwenye michuano ya kombe la taifa ambalo
linashirikisha mikoa yote ya jamhuri ya muungano wa Tanzania. Moja ya faida hizo ni
kumjengea uwezo mshambuliaji wa TP Mazembe, Thomas Ulinwengu ambaye alishiriki
kikamilifu kwenye michuano hiyo.
Kwa wengine sasa
wanaona Thomas Ulimwengu amekuwa mshambuliaji hatari na hodari zaidi, lakini
njia alizopitia zimemjengea umakini na uhodari katika soka, ambako sasa anaweza
kupambana na washambuliaji hatari klabuni kwake kama Kaluyituka, Given
Singuluma, na wengineo.
Kwa mtazamo wangu
uamuzi wa kocha Kim kuliagiza shirikisho la soka nchini TFF kuhakikisha
Serengeti Boys inashiriki mechi za Ligi Kuu Tanzania bara kuna lengo moja tu
kuhakikisha anakuwa na kikosi imara zaidi cha timu ya taifa ya wakubwa(Taifa
Stars).
Ukiangalia rekodi za
kocha Kim na namna anavyoweza kujenga kikosi chake katika timu ya taifa, hakika
amekuwa kocha wa kipekee sana. nasema hivi sio kwasababu ya matokeo mazuri,
bali muundo wake wa utendaji kazi na namna anavyoweza kutufahamisha makosa yetu
kwa hekima.
Kim anajua kabisa
tulichokosa ni misingi ya soka la vijana kwahiyo anachofanya ni kuhakikisha
tunakuwa na hazina ya kutosha katika soka la vijana kupitia timu ya taifa. Wakati Kim akisema
hayo wenyewe tunafahamu kuwa tuna michuano miwili muhimu sana ambayo inawajenga
vijana lakini bado haionekani kuwa imara kiushindani. Mfano michuano ya Copa
cocacola na michuano ya Uhai.
Hii ni michuano
inayohusisha timu za vijana ambazo kwa namna moja ama nyingine zinapata faida,
lakini hakuna mwendelezo wake. Kwahiyo kocha Kim
amegundua moja ya sababu za kushindwa kuwa na mwendelezo ni gharama za
uendeshajiu, kwahiyo anaamua kupunguza gharama hizo kwa kuitumia timu ya taifa
ili iweze kusaidia kuzalisha wachezaji imara.
Pia anaikumbusha TFF
kuwa hakuna njia ya mkato kama inataka wachezaji wazuri zaidi ya kuwekeza
ikibidi shirikisho lenyewe kuwa na kituo chake. Kwa mantiki hiyo
badala ya kuwkusanya vijana huko mitaani na kuwapeleka uwanja wa Karume, kocha
Kim anatumia timu ya taifa kama mahali pevu ambapo pataleta hamasa kwa vijana
na kuongeza ujuzi wao kipindi wakirudi kwenye klabu zao.
Pili, hii itazisaidia
timu zetu kama Yanga na Simba ambazo mara nyingi zimekuwa zikisubiri wachezaji
walioko timu ya taifa ndio wawasajili. Namna gani kocha Kim
ataweza kuwaendeleza wachezaji watakaofanya vema kwenye kikosi cha Serengeti
Boys? Hilo litateguliwa kwa kumuongezea mkataba mpya ambao utamfanya ajikite
zaidi kutengeneza timu imara za timu za taifa akishirikiana na makocha wazawa.
Nimalize kwa kusema,
hakuna jambo baya kama tutaruhusu kuondoka kwa kocha Kim Poulsen wakati huu
ambapo ametuonyesha falsafa bora kabisa ya soka letu. Ni vyema TFF na serikali
zinaona umuhimu wa kuongeza mkataba mnono kwa kocha huyu. Muhimu tuache blah
blah katika hili.
STRAIN THEOTY/CRIMENOLOGY VS UDINI NA DINI=CUHUMI?
Wataalamu
kama Robert Merton waliwahi kusistiza umuhimu wa uhalifu katika jamii. Lakini
kwa wataalamu hao hao wanasema, ikiwa njia za kujipatia pato zikibanwa au
zikibinywa uhalifu ni kitu kinachochukua nafasi ambapo watu hutafuta pato
kupitia njia zozote zile ikiwemo uhalfu.
Wakasema
kuwa kuna umuhimu wa uhalifu sababu unaileta jamii pamoja. Jamii inakuwa kwenye
kutafuta njia mwafaka kumaliza uhalifu, lakini lazima jamii hiyo ijitolesheleze
ndipo tunaweza kuufanya uhalifu kumalizika. .......
Naam
kama nchi yenu haiongelei suala la ukuzaji uchumi, itaongelea nini? Kama
tumeshuhudia watu kule Mwanza wanauana kisa HAKI YA KUCHINJA na kuvaa mavazi ya
DINI kisha kumwaga damu, nini tafsiri yako? Je, umewaona wanaoshiriki zoezi la
kuuana ni watu wa namna gani? ....je wale wanawezaje kuachwa katika faili la
UCHUMI? Hatuna uchumi imara lakini hatutakiwi kuacha kutafuta UCHUMI
imara.
@Nakupenda
sana nchi yangu TANZANIA.
Hatutendi
haki hata kidogo kutoandika 'aya' za uchumi wetu ambayo ndio msingi wa taifa
letu na kumwachia Rais wetu Kikwete akihutubia mambo machache. Labda afadhali
hayo machache kuliko kukosa kabisa. Kama tunataka kujenga utamaduni wa
kutomwambia basi tunajenga taifa la watu wasioweza kufikiri au taifa la watu
wanaopendelea mambo mepesi.
Hatukatai kuona kuwa hotuba ya rais wetu haiwezi
kuwaridhisha watu wote, lakini mimi naona kuna haja pia kuwakumbusha wale wote
wanaohusika kuwa, wajaribu na waweze kufanya kitu ambacho kinaakisi jamii yao.
Kama tunakubaliana kwamba uhalifu ni kitu kinacholeta jamii pamoja, na kwamba
lazima jamii ijitosheleze basi yatupasa kujiuliza itajitosheleza katika lipi na
kwanini?
Lazima tumfanye rais wetu awe 'mgumu' kwa maana mtu 'mzito' kwa hoja
nzito. Kwahiyo tusitegemee kuwa Rais anaweza kufanya hilo pekee bali lazima tusaidie,
lazima kumfanya awe bora sababu ni mali yetu na tunajivunia yeye. Lakini kama
kuna watu wanadhani kukosoa hotuba ya Rais ni dhambi ati sio saizi yetu hatuba
budi kusema labda akina sisi tunaokosoa tumechanganyikiwa na tunakaribia
kuchojoa nguo.
Ni jambo baya sana tunapoona kila mtu anadhani waandishi wa
hotuba ya Rais wanajua kila kitu. Lakini wanayo fursa ya kupata tafiti za
kisasa za uchumi, makabrasha na kadhalika ili kuweza kuelezea jambo la msingi
kuhusu hali ya maisha ya watu wetu.
Ni vigumu sana kuamini kuwa Rais wetu
anaandikiwa hotuba nusu, labda wenzetu walisahau, ila nakumbusha kama huijui
jamii yako basi unaelekea kuchanganyikiwa. Turuhusu waandishi wa hotuba ya rais
wawe hodari kwa kuwajengea hoja zenye maana sio kuwatusi. Tuwape nafasi ya
kujisahihisha sababu wao sio miungu hata kidogo..
SERIKALI YASHIKILIA MSIMAMO SAKATA LA LOLIONDO
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
SERIKALI kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imesema haitabidili kamwe maamuzi iliyotoa kuhusu Pori Tengefu la Loliondo, mkoani Arusha na kuwataka wanaharakati wanaochochea mgogoro wa ardhi katika eneo hilo kuacha mara moja.
Tamko hilo la serikali, limekuja muda mfupi baada ya watu mbalimbali kutoa maoni yao kwenye mitandao na vyombo vya habari kwamba uamuzi wa
serikali kuhusu pori tengefu si sahihi.
Tamko la serikali lilitangazwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki hivi karibuni kwamba, wameacha kilomita za mraba 25,000 kwa ajili ya wananchi na serikali imechukua kilomita za
mraba 15,00 kwa ajili ya kutunza rasilimali za nchi.
Alifanya hivyo kwa kwa mujibu wa Sheria ya Wanyamapori Namba 5 ya Mwaka 2009, Sehemu ya 16 Vifungu Na. 4, 5 na 6 na kwamba muda mrefu viongozi wa wizara wamekuwa wakikutana na wananchi na viongozi wa mkoa wa Arusha na Wilaya ya Ngorongoro kujua kero zilizopo ili zitatuliwe na ndio imewezesha serikali kufanya uamuzi alioufanya.
"Ukweli ni kuwa Waziri Kagasheki alifuata sheria alipotoa tamko kuhusu kupunguza eneo la pori tengefu la Loliondo kwa mujibu wa sheria inayompatia waziri mwenye dhamana uwezo wa kupitia upya mapori tengefu na kufanya marekebisho mbalimbali muhimu kwa manufaa ya wananchi bila
kuathiri uhifadhi,"alisema George Matiko, ambaye ni msemaji wa wizara.
Katika taarifa kwa vyombo vya habari jana, Matiko alisema tamko lilizingatia tafiti mbalimbali ikiwemo utafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI) na mapendekezo ya tume mbalimbali zilizoundwa kuchunguza mgogoro wa Loliondo ikiwemo ya Waziri Mkuu iliyoundwa mwaka juzi.
Aliongeza kuwa eneo la kilomita za mraba 1,500 litaendelea kumilikiwa na wizara kwa mujibu wa sheria na kwa kutambua kuwa ni sehemu ya mazalia ya wanyamapori, mapito ya wanyamapori na vyanzo vikuu vya maji kwa hifadhi mbalimbali ikiwemo Serengeti.
Alisisitiza ardhi iliyobaki baada ya kuondoa eneo la pori tengefu la Loliondo itasimamiwa na vijiji kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi ya Vijiji Namba 5 ya Mwaka 1999 na wananchi watawezeshwa ili waanzishe Eneo la Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA) katika ardhi hiyo kwa manufaa
yao.
"Tanzania inajali uhifadhi lakini pia inajali maslahi ya wananchi, ndiyo maana asilimia 25 ya eneo la nchi hii limehifadhiwa bila kuwepo migogoro. Hakuna migogoro kati ya wananchi na Serikali, kwa kuwa wananchi wanatambua umuhimu wa uhifadhi kwao na kwa vizazi vijavyo.
Ndiyo maana wananchi wanachangia kwa kiwango kikubwa katika kufanikisha uhifadhi,"alimaliza Matiko.
Madhumuni
kumbukumbu,
maisha
Subscribe to:
Posts (Atom)




