April 05, 2013

WANAFUNZI SHULE YA MSINGI KWAMBE WAPEWA CHAKULA CHA MCHANA


WANAFUNZI WA SHULE YA MSINGI KWAMBE WILAYA YA NYASA WAKIPATA MLO WA MCHANA SHULENI HAPO,JITIHADA ZA AFISA ELIMU NDUGU MATHIAS MKALI KUPUNGUZA UTORO MASHULENI KWA KUANZISHA SHULE ZOTE WILAYANI MBINGA ZITOE CHAKULA CHA MCHANA.HONGERA KWA NYANJA BOY HUYO

April 04, 2013

DARASA HURU: CCM KAENI CHONJO NA JULIANA SHONZA NA MTELA MWAMPAMBA

Daniel Gingo

Kuna wakati ukiangalia siasa wanazofanya Juliana Shonza na Mwampamba (na hasa Mwampamba) wanachofanya sio siasa, wanachokifanya ni utoto! Tena unaweza kudhani kwamba inawezekana CHADEMA walipumua baada ya hawa jamaa kuondoka huko.

Niliwahi kusema kwamba utoto wanaoufanya sasa hivi utakitokea puani CCM, kama baadhi yenu hamtaki kuniamini kwa kudhani kwamba nina chuki na CCM basi mimi na ninyi tunyamaze kwa sasa, tusubiri wakati ukifika utasema.

Kwa Juliana mpaka kesho sijui kilichomtokea, namfahamu kama dada aliyekuwa akimpenda na kumtumikia Mungu kule Mabibo, kilichotokea kwake sikijui, BWANA AJUA!

KWA MFANO WAULIZENI MASWALI HAYA:
1. Kama wakiwa CHADEMA walikuwa wakijua njama zote za mauaji zilizokuwa zikipangwa au kutekelezwa na CHADEMA nini kiliwafanya washindwe kuinuka na kusema kama kweli walikuwa wazalendo kwa Taifa hili? Kwa nini waje waanze kutoa tuhuma hizo leo magazetini na mitandao kama humu?

2. Kama walijua njama za uhalifu zilizokuwa zikifanywa na CHADEMA na wakaficha ‘uovu’ huo ni vipi leo watashindwa kuficha uovu wa CCM pindi utakapofanywa? Nini kitawazuia kuficha madudu ya CCM dhidi ya wananchi wa Tanzania?

3. Katika njama na mikakati ya ‘uovu’ ya CHADEMA wao walishiriki kiasi gani na kwa kiwango gani? Je, ni kweli hawakushiriki mipango iliyotelekezwa? Nini kiliwafanya wajiondoe huko huku wakijua kuwa walishiriki kupanga njama hizo? Je, walikosa walichoahidiwa?

4. Kama waliweza kuwasiliti wenzao wa CHADEMA na leo wanakuja kuwaanika hadharani, watuambie kwa nini tusiionye na kuitahadharisha CCM kukaa chonjo na vijana hawa? Kama waliwasaliti CHADEMA na leo wanafichua siri ambazo walishiriki wote Nape Nnaye ana uhakika gani kwamba nay eye hatakuja kuumbuliwa siku za mbeleni?

MWISHO
a. Narudia leo kuionya CCM, iwe macho na vijana hawa, na sio CCM tu, hata vyama vingine kwa ajili ustawi wa Demokrasia nchini, viache kushabikia watu wanapoacha vyama vyao na kuja kuwa mavuvuzela kwenye vyama vipya!
b. Sina uhakika kama CHADEMA haijawatuma vijana hawa kuivuruga CCM, lakini mashaka yangu ni makubwa juu ya hilo.

MANABII MNAO, LAKINI HAMUWASIKILIZI!!!!

KIKUNDI CHA HABARI CHAKUTANA KUWEKA MIKAKATI


Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam

NAIBU Waziri wa Sheria na Katiba, Angellah Kairuki amewataka wanachama wa kikundi cha waandishi wa habari cha kujikomboa kiuchumi (Habari Group) kupendana na kuaminiana ili kukifikisha kikundi hicho mbali.


Kairuki ambaye pia ni mlezi wa Habari Group, alikitaka kikundi hicho kutokuwa wachoyo wa kusaidia waandishi wa habari wengine wenye nia ya kuungana na kufanikiwa kimaisha.

Akizungumza na kikundi hicho Dar es Salaam juzi, alisema ili mtu afanikiwe ni lazima awe mwenye upendo na kusaidia wengine pale penye mwanya wa kufanya hivyo na kuwataka wanachama wote kuwa na moyo wa kujitolea kwa ajili ya kikundi.  "Sitopenda kusikia kikundi hiki kimekufa kwa sababu ya mifarakano na chuki miongoni mwenu kwani kwa kufanya hivyo hamtofikia malengo mliyokusudia," alisema Kairuki.


 Aliongeza kuwa wakati anaingia madarakani aliweka vipaumbele kwa wafanyakazi wa majumbani, madereva wa aina zote, wafanyakazi wa mashambani, wahudumu wa baa na nyumba za wageni, walinzi na waandishi wa habari.  Na kwamba ameanza kushughulikia haki mbalimbali za makundi hayo, ambapo kwa sasa wapo kwenye mchakato wa kuishinikiza serikali kusaini mkataba wa kuridhia haki za wasichana wa majumbani.

Aliwapongeza waandishi wa habari kwamba pamoja na changamoto nyingi wanazokutana nazo, lakini hawakati tamaa na wamekuwa wakifanya kazi yao kwa moyo mmoja na kwa bidii. 

Kama mkakati wake wa kuwasaidia waandishi wa habari, alisema atasimamia Habari Group ili wawe mabalozi wazuri kwenye mambo mbalimbali kwa jamii, ikiwemo kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali, kuwapa elimu ya umuhimu wa cheti cha kuzaliwa, sambamba na kushirikiana nao bega kwa bega kwenye mambo muhimu ya kijamii.

"Kuwasidia kwenu ni miongoni mwa malengo yangu niliyojiwekea ya kupigania haki ya baadhi ya makundi ambyo nimeona haki zao kama wafanyakazi hazitekelezwi,"aliongeza.

MGODI UNAOTEMBEA: WAMEAMUA KUIWEKA TANZANIA KIKAANGONI.

Kambi Mbwana, Dar es salaam

KABLA ya kuanza kufikiria labda kuna mkono wa mtu au Taifa kutoka nje ya nchi yetu, vyema tukaelewa kuwa siku zote mvunja nchi ni mwananchi mwenyewe, hasa kwa kuangalia jinsi baadhi yao wanavyokosa uzalendo kwa kutenda vitu visivyokuwa vya kiungwana.

Watu hao wamekuwa wakiendeleza kufanya vitendo vya kushangaza na kuogopesha kwa kiasi kikubwa, ikiwa ni njia moja wapo inayolitangaza Taifa letu vibaya nje ya nchi.

Tangu kupata Uhuru uliopatikana kwa harakati za viongozi wetu, akiwamo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na wapambanaji wengine, Tanzania ilijipambanua kuwa ni kisima cha amani.
Katika kulinda msingi huo, wananchi walielimishwa au kupewa kauli mbiu ya namna gani wanavyotakiwa waishi kwa ajili ya kuishi kwa amani na upendo ili kukuza uchumi wa nchi yetu.
Ni kweli kabisa. Kiu hiyo ilidumu kwa miaka mingi, ingawa sasa naanza kuona kuwa hali hiyo imekwisha. Anayesema kuwa nchi hii bado ni kisiwa cha amani, hakika anatumia lugha nzuri kwa kuhofu anayewaeleza hivyo wataondoa woga kwa sababu moja ama nyingine.
Kwanini nasema hayo? Taifa letu sasa lipo kwenye matatizo makubwa ya vurugu za kidini, siasa na mambo mengine ambayo yote kwa pamoja yanawaweka wananchi kwenye wasiwasi mkubwa.

Kumekuwa na matukio mengi ya kutisha. Katika kulielezea jambo hilo la machafuko ya Tanzania, wengi watawataja watu maarufu au wale ambao matukio yao yamegusa watu wengi. Lakini ukweli ni kwamba hao wanaotajwa ni wachache kati ya wengi ambao labda kwa kutokuwa maarufu kwao, au kutojulikana kwa madhira yaliyowakuta, kunawafanya wasionekane yale yaliyowatendewa.

Ingawa watu watawataja watu kama vile Mwandishi Daudi Mwangosi, mtu aliyepoteza maisha kwa staili ya kutisha kupita kiasi. Mbali na Mwangosi, bado wapo watu kama vile Daktari Stephen Ulimboka, Mhariri wa Mtendaji wa Kampuni ya New Habari 2006 (Ltd), Absalom Kibanda ambao matukio yao ya kutekwa na kuteswa yamewagusa watu wengi na kuendeleza msemo kuwa Tanzania sasa si kisiwa cha amani.

Mbali na watu hao, ambao kwa mapenzi ya Mungu wameendelea kubarikiwa uhai, wapo ambao wamepoteza maisha, akiwamo Padri Evarist Mushi wa Kanisa Katoliki Visiwani Zanzibar. Padri huyu aliuagwa na kuibua hisia nzito sambamba na kuzidi kueneza chuki kwa miongoni mwa jamii ya Kitanzania. Pamoja na yote hayo, bado wapo wananchi ambao wamekuwa wakiishi bila kuvumiliana kwa sababu za ajabu, hasa huu wimbo wa kuchinja unaoendelea kuimbwa kwa lugha za chuki na kukiathiri kizazi cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tangu kuzaliwa kwa Taifa hili, likipita katika vipindi tofauti kwa viongozi tofauti waliokuwa na mapenzi makubwa kwa wananchi wao, watu waliishi kwa upendo na kuvumiliana kupita kiasi. Si kama ukatili haukuwapo, huenda ulikuwapo, ila si kama ulivyokuwa sasa kiasi cha watu kushikwa na mihemko na kutenda bila hata kuogopa vyombo vya Dola katika mazingira wanayotaka wao.

Hii si njia nzuri ya kuzalisha amani kwa Watanzania. Zaidi tunaendeleza chuki, fitina, majungu na kusababisha sumu mbaya ya vurugu ambazo kuna siku zitashindwa kumalizwa.
Katika kutafuta nufumbuzi juu ya machafuko ambayo mengi huibuka kwa kupita mgongo wa dini na siasa, baadhi ya watendaji wa serikali, wanashindwa kutumia busara, hekima na utu juu ya kumaliza migogoro hiyo.

Kuna siku tutashuhudia watu wakiingia barabarani kufanya uhalifu, maana tayari walishazoea na kuona kuwa hakuna wa kuwazuia kwa namna moja ama nyingine.
Katika kuliangalia Taifa lenye amani, hatupaswi kuchekea kauli za uchochezi zinazotoka kwa mtu yoyote, iwe ni mwanasiasa au kiongozi wa dini ambaye hana uzalendo na wananchi wake. Huo ndio ukweli. Mihemko yako haiwezi kutufanya tuone upo sahihi hata pale utakaposimama kwa kupitia cheo chako cha kidini au kisiasa kuhamasisha vurugu hatari kwa Taifa hili.

Hatuwezi kwenda hivyo. Bado hatuna uchumi unaotufanya tulinge kuwa tutakuwa pazuri hata kama baadhi ya watu watafanya vurugu, wataharibu miundo mbinu yao kwasababu ya kuhamasisha ujinga kutoka kwa mtu mmoja asiyekuwa mzalendo. Kwa mfano, wapo watu ambao wanabishana juu ya nani yupo sahihi katika suala zima la kuchinja. Sakata hili lilibuliwa na Waziri Stephen Wasira, alipokuwa anazungumza jijini Mwanza.

Mengi yaliendelea kuibuka hasa pale Wasira alipojikuta akitoa ufafanuzi kuwa mwenye mamlaka ya kuchinja ni Waislamu. Kauli ya Wasira isingeleta matatizo kama watu watatumia akili na uzalendo kufuatilia suala hili. Kuna uwezekano mkubwa kuwa huenda Wasira amezungumza hivyo kwasababu ndio utaratibu uliozoeleka kwa Watanzania wengi. Hata wachungaji, mapadri walikuwa wakitaka kufanya shughuli inayoshirikisha watu wa jamii tofauti, vitoweo vyao vilikuwa lazima vichinjwe na Waislamu.

Pamoja na yote hayo, watu ambao ni jamii ya Wakristo hawakulazimishwa pia wachinjiwe na Waislamu kama hawajaona hilo linafaa, ingawa tatizo litakuwa pale wanapochinja wao na kuwalisha wengine. Kumbe leo wapo watu wanaotaka wachinje, basi sakata hilo linastahili viongozi wakae na kushirikisha makundi ya kijamii hasa kwa viongozi wao wa dini, Mashekhe, Mapadri na wengineo.

Wakati hayo yakiendelea, watu wanahoji. Je, vurugu hizo mwisho wake ni wapi? Ingawa wapo wanaosema kuwa vurugu hizi zina mkono wa mtu, wakimaanisha watu wanaotumiwa na wengine kutoka nje ya nchi, lakini bado hainifanyi nishindwe kuwataja watu hao kama majuha na wasiokuwa na uzalendo katika Taifa lao.

Watu hao ambao lengo lao kubwa ni kuiweka nchi katika mtihani mzito, hasa katika kiu ya kuilinda amani yake, hawastahili kuchekewa hata mara moja, maana wanavyoendelea kuchekewa, ndivyo sumu hiyo inavyozidi kuenea na kuota mizizi hata kwa wale wasiokuwa na tabia hiyo.

Kila mtu wakiwamo viongozi wa serikali, chini ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa upande wa Bara na Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wa Visiwani kuendelea kuwa wakali kwa kundi lolote, mtu yoyote anayefanya uvunjifu wa amani kwa makusudi kwa faida anayoijua mwenyewe.

Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama vihakikishe kuwa vinakuwa mstari wa mbele, pamoja na kutoa elimu kwa wananchi juu ya kulinda amani na mustakabali wa Tanzania.

Leo tunaona ni kawaida, lakini ikiendelea hivi, kila mmoja ataona ana uhuru wa kufanya kila analotaka, hivyo kusababisha machafuko, mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, hasa tatizo hilo linapopitia kwa mlango wa dini au vyama vya siasa, kama vile Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama Cha Wananchi (CUF), Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vyama vingine vya siasa vilivyosajiliwa katika nchi yetu.

Huu ndio ukweli wa mambo. Tusipokuwa makini, kujua nini cha kufanya kwa ajili ya nchi yetu, hakika hatutakuwa na kizazi chenye uzalendo, kinachoithamini amani kwa ajili ya kulinda utu na heshima za watu.

Tuna wajibu wa kulijua hili, maana inapotokea machafuko makubwa, wanaoathirika ni akina mama na watoto, hivyo ni wazi hawa wanaofanya vitendo vya unyama kwa wenzao, wale wananaokesha kubuni namna ya kufanya vurugu za kidini na kisiasa wafikie wakati waone imetosha kwa ajili ya kuendeleza wimbo wetu wa Tanzania kisiwa cha amani.

MAONI: kambimbwana@yahoo.com
0712 053949
0753 806087