Showing posts with label Mgodi Unaotembea. Show all posts
Showing posts with label Mgodi Unaotembea. Show all posts

November 02, 2017

KAMPUNI YA MKUKI NA NYOTA WAINGIA SOKO LA VITABU CHINA


NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

KAMPUNI ya Mkuki na Nyota ambayo hujishughulisha na uchapaji wa vitabu imetanua wigo wa soko lake la uchapishaji na utangazaji wa vitabu baada ya kusaini makubaliano na Shirika la World Affairs Press (WAP) la nchini China.
 
Akizungumza baada ya kusaini makubaliano hayo Mkurugenzi wa MNN, Mkuki Bgoya amesema kuwa wamesaini Makubaliano na Shirika la World Affairs Press (WAP) ya China kufanya kazi pamoja katika miradi mbalimbali ya kuchapisha na kuvitangaza vitabu ikiwa ni njia mojawapo ya kutanua soko la kampuni hiyo barani Asia.

Mkuki na Nyota ni kampuni mashuhuri kwa uchapaji wa vitabu ambayo ilianzishwa mwaka 1992 jijini Dar es salaam. Mwanzilishi wa kampuni hiyo ni Walter Bgoya ambaye alitumia uzoefu wake wa miaka 18 ya kuwa Meneja Mkuu wa Tanzania Publishing House. 

October 27, 2017

KWANINI WILAYA YA NYASA IMESHIKA MKIA KATIKA MATOKEO YA DARASA LA SABA?



RAYMOND NDOMBA, SONGEA
WILAYA ya Nyasa iliyopo mkoa wa Ruvuma imekuwa ya mwisho katika matokeo ya darasa la saba mwaka huu 2017 kimkoa. Swali la kujiuliza ni kwanini hali hiyo imetokea. 


Mawazo yangu ni haya; Pamoja na sababu nyingi zilizosababisha matokeo hayo ya aibu kubwa. Wazazi wanapaswa kubeba lawama kubwa. Wengi wao hawafuatilii maendeleo ya watoto wao, pia makuzi na malezi mabaya.

Miaka ya hivi karibuni (kuanzia mwaka 2000), Wazazi wengi katika wilaya ya Nyasa hawajali elimu, hawajigusi katika ufuatiliaji wa watoto wao kielimu na hata kitabia (Angalia matokeo ya mitihani ya Taifa ya shule za msingi na sekondari kunzia miaka hiyo ya 2000 kwa shule kongwe ndani ya wilaya). 

October 17, 2017

MAONI YA MHARIRI: KWA WILAYA YA NYASA DUNIA HAIJABADILIKA?

Majuzi nimeona picha ya mwanadada mashuhuri katika mtandao wa Instagram, Mange Kimambi akionyesha majengo ya hospitali ya Lumeme wilayani Nyasa ikiwa na mazingira mabaya ya kufanyia kazi na ukosefu wa huduma muhumu. Pamoja na jengo lenyewe kutokamilika, lakini limekuwa likitumika hivyo hivyo.

Kwangu mimi ile ilikuwa habari kubwa sana kwa wilaya yetu ya Nyasa. Kama mwanahabari naamini kuripotiwa matukio au masuala yasiyofaa  ndani ya jamii ambayo haitoi habari za kutosha ni njia mojawapo kubwa ya kubadili mwenendo.

HAPA CHINI kuna Blogu ya JIMBO LA NYASA. Lakini habari za Jimbo husika ziliwekwa mara ya mwisho Januari mwaka huu. Nimejiuliza wasaidizi wa Mbunge wanafanya nini kama hawawezi kutoa taarifa za ofisi ya mbunge? Najiuliza hivi hatuoni umuhimu wa habari zetu zikiwa hadharani bila kujali mbaya au nzuri?

Je waanzilishi wa blogu ya JIMBO walikusudia tamasha au nini? BONYEZA HAPA KUTAZAMA.  Kimsingi habari za Jimbo la Nyasa ni lazima zitolewe wala kwa wananchi. Pili inadhihirisha "kuamini" kuwa NYASA ni ileile ambayo inaishi pasipo kuwa na habari zozote. Mtazamo huo si sahihi ndio maana wahusika wanaona "bora liende tu" huku wakisahau na kushindwa "KUMUUZA" mbunge. 

Nimejiuliza hadi leo hata kutengeneza ukurasa wa habari za mbunge kwenye mitandao hatuwezi kweli?  Hivi mahusiano ya mbunge na wapigakura wake yana maana gani? Naandika hapa kwasababu naamini wapo wahusika wanaofikisha ujumbe. Ningependa kuwakumbusheni kuwa "kutomuuza mbunge" katika ulimwengu wa kidigitali ni uzembe. Labda tunaweza kutembelea wananchi kila kona ya jimbo, lakini tunapawa kuelewa kuwa taarifa za huko ziwekwe sehemu maalumu kutunza kumbukumbu sio mambo ya "MASJALA" tena (hizo ni zama za kale mawe).

Kwa heshima nawakumbusha wasaidizi wa mbunge, kutoitendea haki blogu, kutozungumzia hata utalii ambao ni chachu ya kukuza mzunguko wa fedha wilayani kwetu ni UDHAIFU unaopaswa kurekebishwa.
Ninawatakieni majukumu mema. 
HABARI NI BIASHARA. HABARI NI UCHUMI.

MARKUS MPANGALA,
Oktoba 17/ 2017
Dar es salaam

April 04, 2013

MGODI UNAOTEMBEA: WAMEAMUA KUIWEKA TANZANIA KIKAANGONI.

Kambi Mbwana, Dar es salaam

KABLA ya kuanza kufikiria labda kuna mkono wa mtu au Taifa kutoka nje ya nchi yetu, vyema tukaelewa kuwa siku zote mvunja nchi ni mwananchi mwenyewe, hasa kwa kuangalia jinsi baadhi yao wanavyokosa uzalendo kwa kutenda vitu visivyokuwa vya kiungwana.

Watu hao wamekuwa wakiendeleza kufanya vitendo vya kushangaza na kuogopesha kwa kiasi kikubwa, ikiwa ni njia moja wapo inayolitangaza Taifa letu vibaya nje ya nchi.

Tangu kupata Uhuru uliopatikana kwa harakati za viongozi wetu, akiwamo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na wapambanaji wengine, Tanzania ilijipambanua kuwa ni kisima cha amani.
Katika kulinda msingi huo, wananchi walielimishwa au kupewa kauli mbiu ya namna gani wanavyotakiwa waishi kwa ajili ya kuishi kwa amani na upendo ili kukuza uchumi wa nchi yetu.
Ni kweli kabisa. Kiu hiyo ilidumu kwa miaka mingi, ingawa sasa naanza kuona kuwa hali hiyo imekwisha. Anayesema kuwa nchi hii bado ni kisiwa cha amani, hakika anatumia lugha nzuri kwa kuhofu anayewaeleza hivyo wataondoa woga kwa sababu moja ama nyingine.
Kwanini nasema hayo? Taifa letu sasa lipo kwenye matatizo makubwa ya vurugu za kidini, siasa na mambo mengine ambayo yote kwa pamoja yanawaweka wananchi kwenye wasiwasi mkubwa.

Kumekuwa na matukio mengi ya kutisha. Katika kulielezea jambo hilo la machafuko ya Tanzania, wengi watawataja watu maarufu au wale ambao matukio yao yamegusa watu wengi. Lakini ukweli ni kwamba hao wanaotajwa ni wachache kati ya wengi ambao labda kwa kutokuwa maarufu kwao, au kutojulikana kwa madhira yaliyowakuta, kunawafanya wasionekane yale yaliyowatendewa.

Ingawa watu watawataja watu kama vile Mwandishi Daudi Mwangosi, mtu aliyepoteza maisha kwa staili ya kutisha kupita kiasi. Mbali na Mwangosi, bado wapo watu kama vile Daktari Stephen Ulimboka, Mhariri wa Mtendaji wa Kampuni ya New Habari 2006 (Ltd), Absalom Kibanda ambao matukio yao ya kutekwa na kuteswa yamewagusa watu wengi na kuendeleza msemo kuwa Tanzania sasa si kisiwa cha amani.

Mbali na watu hao, ambao kwa mapenzi ya Mungu wameendelea kubarikiwa uhai, wapo ambao wamepoteza maisha, akiwamo Padri Evarist Mushi wa Kanisa Katoliki Visiwani Zanzibar. Padri huyu aliuagwa na kuibua hisia nzito sambamba na kuzidi kueneza chuki kwa miongoni mwa jamii ya Kitanzania. Pamoja na yote hayo, bado wapo wananchi ambao wamekuwa wakiishi bila kuvumiliana kwa sababu za ajabu, hasa huu wimbo wa kuchinja unaoendelea kuimbwa kwa lugha za chuki na kukiathiri kizazi cha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tangu kuzaliwa kwa Taifa hili, likipita katika vipindi tofauti kwa viongozi tofauti waliokuwa na mapenzi makubwa kwa wananchi wao, watu waliishi kwa upendo na kuvumiliana kupita kiasi. Si kama ukatili haukuwapo, huenda ulikuwapo, ila si kama ulivyokuwa sasa kiasi cha watu kushikwa na mihemko na kutenda bila hata kuogopa vyombo vya Dola katika mazingira wanayotaka wao.

Hii si njia nzuri ya kuzalisha amani kwa Watanzania. Zaidi tunaendeleza chuki, fitina, majungu na kusababisha sumu mbaya ya vurugu ambazo kuna siku zitashindwa kumalizwa.
Katika kutafuta nufumbuzi juu ya machafuko ambayo mengi huibuka kwa kupita mgongo wa dini na siasa, baadhi ya watendaji wa serikali, wanashindwa kutumia busara, hekima na utu juu ya kumaliza migogoro hiyo.

Kuna siku tutashuhudia watu wakiingia barabarani kufanya uhalifu, maana tayari walishazoea na kuona kuwa hakuna wa kuwazuia kwa namna moja ama nyingine.
Katika kuliangalia Taifa lenye amani, hatupaswi kuchekea kauli za uchochezi zinazotoka kwa mtu yoyote, iwe ni mwanasiasa au kiongozi wa dini ambaye hana uzalendo na wananchi wake. Huo ndio ukweli. Mihemko yako haiwezi kutufanya tuone upo sahihi hata pale utakaposimama kwa kupitia cheo chako cha kidini au kisiasa kuhamasisha vurugu hatari kwa Taifa hili.

Hatuwezi kwenda hivyo. Bado hatuna uchumi unaotufanya tulinge kuwa tutakuwa pazuri hata kama baadhi ya watu watafanya vurugu, wataharibu miundo mbinu yao kwasababu ya kuhamasisha ujinga kutoka kwa mtu mmoja asiyekuwa mzalendo. Kwa mfano, wapo watu ambao wanabishana juu ya nani yupo sahihi katika suala zima la kuchinja. Sakata hili lilibuliwa na Waziri Stephen Wasira, alipokuwa anazungumza jijini Mwanza.

Mengi yaliendelea kuibuka hasa pale Wasira alipojikuta akitoa ufafanuzi kuwa mwenye mamlaka ya kuchinja ni Waislamu. Kauli ya Wasira isingeleta matatizo kama watu watatumia akili na uzalendo kufuatilia suala hili. Kuna uwezekano mkubwa kuwa huenda Wasira amezungumza hivyo kwasababu ndio utaratibu uliozoeleka kwa Watanzania wengi. Hata wachungaji, mapadri walikuwa wakitaka kufanya shughuli inayoshirikisha watu wa jamii tofauti, vitoweo vyao vilikuwa lazima vichinjwe na Waislamu.

Pamoja na yote hayo, watu ambao ni jamii ya Wakristo hawakulazimishwa pia wachinjiwe na Waislamu kama hawajaona hilo linafaa, ingawa tatizo litakuwa pale wanapochinja wao na kuwalisha wengine. Kumbe leo wapo watu wanaotaka wachinje, basi sakata hilo linastahili viongozi wakae na kushirikisha makundi ya kijamii hasa kwa viongozi wao wa dini, Mashekhe, Mapadri na wengineo.

Wakati hayo yakiendelea, watu wanahoji. Je, vurugu hizo mwisho wake ni wapi? Ingawa wapo wanaosema kuwa vurugu hizi zina mkono wa mtu, wakimaanisha watu wanaotumiwa na wengine kutoka nje ya nchi, lakini bado hainifanyi nishindwe kuwataja watu hao kama majuha na wasiokuwa na uzalendo katika Taifa lao.

Watu hao ambao lengo lao kubwa ni kuiweka nchi katika mtihani mzito, hasa katika kiu ya kuilinda amani yake, hawastahili kuchekewa hata mara moja, maana wanavyoendelea kuchekewa, ndivyo sumu hiyo inavyozidi kuenea na kuota mizizi hata kwa wale wasiokuwa na tabia hiyo.

Kila mtu wakiwamo viongozi wa serikali, chini ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa upande wa Bara na Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wa Visiwani kuendelea kuwa wakali kwa kundi lolote, mtu yoyote anayefanya uvunjifu wa amani kwa makusudi kwa faida anayoijua mwenyewe.

Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama vihakikishe kuwa vinakuwa mstari wa mbele, pamoja na kutoa elimu kwa wananchi juu ya kulinda amani na mustakabali wa Tanzania.

Leo tunaona ni kawaida, lakini ikiendelea hivi, kila mmoja ataona ana uhuru wa kufanya kila analotaka, hivyo kusababisha machafuko, mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, hasa tatizo hilo linapopitia kwa mlango wa dini au vyama vya siasa, kama vile Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama Cha Wananchi (CUF), Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vyama vingine vya siasa vilivyosajiliwa katika nchi yetu.

Huu ndio ukweli wa mambo. Tusipokuwa makini, kujua nini cha kufanya kwa ajili ya nchi yetu, hakika hatutakuwa na kizazi chenye uzalendo, kinachoithamini amani kwa ajili ya kulinda utu na heshima za watu.

Tuna wajibu wa kulijua hili, maana inapotokea machafuko makubwa, wanaoathirika ni akina mama na watoto, hivyo ni wazi hawa wanaofanya vitendo vya unyama kwa wenzao, wale wananaokesha kubuni namna ya kufanya vurugu za kidini na kisiasa wafikie wakati waone imetosha kwa ajili ya kuendeleza wimbo wetu wa Tanzania kisiwa cha amani.

MAONI: kambimbwana@yahoo.com
0712 053949
0753 806087

January 23, 2013

SAKATA LA GESI LIMEZUA JIPYA MKOANI MTWARA-Mgodi Unaotembea


Kambi Mbwana

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

HALI ya mkoani Mtwara ni dhahiri inatishia amani, hivyo kuna kila sababu ya serikali na wadau wote kukaa na kuliangalia suala hilo kwa marefu. Nikiwa kama Mtanzania, nimekuwa nikifuatilia kwa karibu mno sakata hilo la gesi inayopingwa na wadau kuletwa jijini Dar es Salaam, badala yake wanataka ibaki mkoani Mtwara, ingawa wenye akili ndogo wanapinga au kutukashifu kadri ya uwezo wao, wakijidanganya kuwa sipaswi kufuatilia mambo ya Mtwara na Lindi.
Huu ni udhaifu na hauwezi kuchekewa, maana ni dhahiri Mtwara, Lindi ni sehemu ya Tanzania kama ilivyokuwa Tanga, Arusha, Kilimanjaro na kwingineko. Wananchi hao waliojikusanya kwa ajili ya kupigania sakata hilo, wamefikia kubadilisha kabisa hisia zao, bila woga wowote katika kulizungumzia suala la gesi.
Kama nilivyowahi kuhoji hapo nyuma, kuwa tatizo ni gesi, choyo, siasa au ubaguzi? Makala haya yalitoka katika blog hii ya Handeni Kwetu na kupokea maoni mbalimbali. Na haya ndio maoni ya Watanzania hao wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Mwanzo wa ugaidi Tanzania ni mwisho wa amani. Kusini hawaogopi jeshi. Kauli ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete ipo kwenye mioyo yao. Leo nasema, ila wana Mtwara watasema kwa sauti zao, maana vitisho kwao ni kama kuitukana maiti.
Chochote kitatokea iwe ni vita vyovyote vile 2015 hatutaki uchaguzi na hatutaki pia tuletewe kiongozi na ole wenu, +255712897794
Maandamano Mtwara
Kaka nimefurahishwa na makala yako isemayo Tatizo ni ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Inaonekana na wewe pia umeandika makala hii kwa lengo lako binafsi. Umeshindwa kutoa uhalisia wa jambo lenyewe, badala yake umeandika kwa lengo la kutaka kumfurahisha ama kuwafurahisha watu fulani. Rudi nyuma angalia wanachofanyiwa wakulima wa korosho wa Mtwara je ni sahihi? Lile zao halisaidii kuinua pato la Taifa? Angalia hali ya maisha ya wakazi wa Mtwara. Nadhani umekurupuka na si mawazo yako kuna mkono wa mtu nyuma yako.
Nenda kazunguuke na kufanya utafiti wa kina utapata majibu sahihi kwa wenyeji. +255657614354.
 Tatizo la mikoa ya Kusini sio gesi bali ni kusahauliwa kwa miaka 51 ya Uhuru. Korosho, reli, Bandari, miundo mbinu, tatizo la elimu na kuwa waanga wa ukombozi wa nchi zilizopo kusini mwa Afrika.
Wanasiasa kujiingiza katika hoja si ajabu kwasababu duniani kote wanasiasa ndio huibua matatizo ya wananchi , maana wasomi wetu wengi hawana meno ya na ndio wanaopitisha  mikataba mibovu .
Sio choyo, lakini tunafikia wakati tunajuta kwa nini sisi Mtwara Lindi tumekuwa sehemu ya Tanzania. Tuna rasilimali tosha za kuweza kuitwa, kama vile Bandari, Bahari, Ardhi yenye rutuba, watu, mito, madini, korosho, ufuta, mhogo na nyinginezo. Kusini tuna haki ya kumdai mume wetu Tanzania haki zetu za msingi, maana tumevumilia mno hadi kilio cha kwi kwi. Ni mimi mwanaharakati,  Amoni, wa Kata Msangamkuu, Mtwara Vijijini. +255652221100.
Ninaomba uelewe lengo la wananchi wa Mtwara na Lindi sio kwamba hawataki gesi isitumiwe na wengine hapana, wao wanataka kiwanda kitengenezwe Mtwara. Kule itoke gesi safi, maana wanakataa mambo yasijekuwa kama ya madini ya Geita ambayo mwekezaji anachimba anaenda kuhakiki Mwanza na kulipa kodi ya uwongo na kuiibia nchi na kuwa masikini, huku wakifaidi watu kutoka nje.
Nimesoma makala yako, inayosema tatizo ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Mimi nimeisoma na kwa utafiti wangu, nimegundua kwamba wewe ni CCM na ndio maana ukaona eti ni siasa. Hapana, ni kwasababu vyama vya upinzani vinapenda maendeleo ya Watanzania.
Mbona hawakuhamisha miwa kutoka Kagera na kuileta Dar es Salaam ili itengenezwe hapa? Pili, hebu fikiria gharama za kuweka bomba ni kiasi gani? Tatu, kumbuka msongamano mkubwa wa watu, ina maana wakiongeza viwanda wanazidisha msongamano. Nne, kwanini wasiwaachie watu wa Mtwara na Lindi na wao wapate ajira? Tano, kila kilichokuwapo Dar es Salaam, Mtwara kipo kama vile Bandari na mengineyo. +255713221244.
Ingawa hujaonyesha wazi ujumbe unaopeleka kwa wana Mtwara, lakini ninachofahamu, Taifa halina rasilimali. Mikoa, wilaya, vijiji, ndivyo vyenye rasilimali, kama vile mbuga za wanyama, madini, mazao na mengineyo ambayo mapato yake hukusanywa na kuwa pato la Taifa. Gesi ni kama rasilimali nyingine tu. Ikiwa Mtwara, Lindi, Kigoma, Mbeya au popote nchini, tueleze ni vipi italinyima Taifa letu pato? Au italigawa vipi Taifa? +255717757797.
Hongera bwana Kambi Mbwana kwa makala yako. Endelea kuwapa elimu Watanzania wenzetu wasioelewa. Naitwa Moi, +255757295249.
Unajua sisi tunaotoka Mtwara tunafananishwa na nyani katika Taifa hili. Hatuna thamani mbele ya makabila mengine toka Uhuru. Barabara haijaisha, mazao yetu hayana usimamizi na hatuna huduma za jamii zilizo bora. Tukipata wakarimu, sio bora pamoja na watumishi wote. Sisi ni jamii ya mwisho katika Taifa hili, hujiulizi gesi na mafuta aliyotupatia Mwenyezimungu ingekuwa sehemu nyingine ingehamishwa? Kwakuwa sisi nyani, hatuna thamani, gesi itaondoka na mafuta pia yataondoka, maana hawa hawatatuthamini milele. +255712848839.
Asante kwa makala yako, lakini usiwe mwandishi mwoga anayeogopa watawala walioshindwa kuwaondolea wananchi umasikini na kuligawa Taifa, kati ya wenye nacho na wasiokuwa nacho. Jitahidi kuwa mkweli ili upate mafanikio maishani mwako. +255755045295. Kijana mbona unakuwa kama popo asiyejulikana kama ni mnyama au ndege. Ya Handeni Kwenu yamekushinda sasa umehamia kwenye gesi.
Nasikitika ujumbe huu uliotumwa kwa namba +255757602075. nimeufipisha kwa sababu za kimaadili, maana ulijaa matusi na kashfa kutoka kwa mtumaji, ambaye pia hakujitambulisha jina lake. Kaka nimesoma makala zako nyingi, nimegundua wewe ni kada wa CCM na usiyejua nini wanachokitaka Watanzania.  Hata hujui huko vijijini watu wanaishi vipi. Unaogopa ya Daudi Mwangosi na Amina Chifupa na huo sio uzalendo, hivyo hupaswi kuwa mwandishi.
Hivi unajua CCM wanaiendashaje nchi hii? Umeshahoji wananchi wangapi kuhusu maisha yao badala yake unamfuata Nape Nnauye, unataka CCM ndio waiongoze nchi milele na milele kwakuwa wewe si mzalendo. Ujumbe huu ulitoka kwa namba +255652273836. Nashukuru brother kwa kuweza kupata fursa ya kuweza kusoma makala yako.
Ni kweli hoja zako ulizozisema zinaweza kushabihiana na ukweli,  ila kutokana na vile hali ilivyo naweza (kudetermine ya words) nazo yanatokana na siasa pia. Hebu nambie kaka angu, umaskini uliopo katika mikoa ya kusini, moja kwa moja tumekuwa maskini na hii ilikua nafasi pekee ya kuweza kupata ahueni.
Hebu jamani isifike wakati tukawa tunaangalia swala hili kijuu juu, hali ni mbya kusini hatuna pa kushikia, serikali ilibidi iangalie gesi hii pia katika kutafuta namna ya kuikomboa miji hii ya kusini.
Ni wazi kuwa serikali imekua ikifurahia tu kupata neema hiyo kuendesha mambo yao na si kusaidia kuondosha umaskini.
Nyinyi waandishi tunawategemea kutoa hoja za kusaidia kuondokana na majanga ya kimaskini. Ujumbe huu ulitumwa kwa njia ya barua pepe kutoka kwa Raya Juma, Nashkuru Haya ni baadhi ya maoni yaliyoingia mara baada ya kuandika makala ile, huku watu wakiingia moia kwa moja katika hoja yangu ya siasa, ubaguzi na choyo nilizokemea. Kwanini nasema siasa? Ukiangalia hapo, wapo waliotuma ujumbe huo wakiwa na chukia serikali ya CCM. Hata hivyo, kuyaanika maoni yao si kuwaletea matatizo, bali kusoma mawazo ya watu wa Mtwara.
Wao ndio wahusika. Ndio wenye kupigania suala la gesi, hivyo inaweza kuwa njia muafaka ya kuepusha shari inayozidi kujengeka mioyoni mwa Watanzania, hususan wale wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Watu wamekuwa na mawazo tofauti juu ya sakata hilo. Wapo wale wanaofikia kutamani Mtwara iwe na utawala wake, jambo ambalo hakika si la kuchekea.
Rasilimali za Tanzania zinaanza kutugawa kadri siku zinavyozidi kwenda mbele, ndio maana nikaamua kuyaanika mawazo ya ndugu zetu hao. Kwa kumalizia tu, sakata la gesi linaweza kujadiliwa upya kwa kuwashirikisha wadau na wananchi wa Mtwara, hasa kwa kupewa mikakati ya namna ya serikali kuwapelekea maendeleo maana ni wajibu wao.
Masuala ya chokochoko ya gesi yasiachwe tu kwa wanasiasa ambao wamekuwa wabunifu kuingia kwenye hoja zinazoshirikisha watu kwa ajili ya kujijenga kisiasa, jambo ambalo si zuri.
Na sisi tunaofikia kujadili suala la gesi, wakiwamo wana harakati, wasitumie maneno makali, maana siku zote jazba inaondosha maana husika. Maoni mengi ya Watanzania nimeshindwa kuyaandika kwa kwasababu hayajatolewa kiungwana, huku niliyoaandika nikiyafanyia marekebisho mengi mno.
Katika hili, serikali kwa kupitia Waziri wake wa Nishati na Madini, Professa Sospeter Muhongo, anapaswa kukaa na kulijadili jambo hili kwa mapana yake.

kambimbwana@yahoo.com
www.handenikwetu.blogspot.com
+255712053949
+255753806087