January 31, 2018

UCHAMBUZI WA KITABU: "AMEZIDI"

MWANDISHI: SAID AHMED MOHAMED

MCHAMBUZI: KIZITO MPANGALA

AMEZIDI ni tamthiliya iliyopgwa chapa na East African Educational Publishers (Nairobi, Kampala, na Dar es Salaam) ambapo chapa ya kwanza ilitolewa mwaka 1995. Kitabu hiki kimesajiliwa kwa namba za usajili ISBN 9966-46-752-1.

Tamthiliya hii imegawanyika katika maonyesho kumi ya jukwaani ambapo kila onyesho lina ujumbe ambao unailenga jamii ya Afrika kwa ujumla hasa katika suala la maendeleo ya liuchumi, kielimu kijamii na kadhalika. Wahusika wakuu wa tamthiliya hii ni Ame na Zidi. Maonyesho haya yote na tamthilya yenyewe kwa ujumla ni cmhezo wa mawazoni tu!
Ame na Zidi wanajikuta katika umasikini mkubwa katika bahari iliyojaa mali. Katika hali hii ya uhitaji wanatambua kuwa hawana lingine la kufanya ila kuomba misaada ili wayatosheleze mahitaji yao. Msaada unapokuja unaleta madhara mengi zaidi.

Onyesho la kwanza linaonyesha Zidi akiwa anamwamsha nduguye Ame aliyekuwa amelala kukiwa kumeshakuchwa. Zidi anamwonyesha Ame mihogo miwili aliyotoka kuitafuta ili wapate kuila.

Onyesho la pili linaonyesha Ame na Zidi wakiwa katika kasri lao wanalisifia kasri hilo lililojaa samani nyingi kutoka Paris (Ufaransa) na vito mbalimbali pamoja na mazuria kutoka Iran.

Onyesho la tatu linaonyesha Zidi akiwa na mpenzi wake Mariam ambaye alizoeleka kuitwa Mari. Wapo katika kasri la akina Zidi huku mari akiwa amejiremba na kujiita msichana wa kileo! Zidi na Mari wanazungumza kuhusu umasikini ambao unawatafuna Zidi na Ame huku mawazoni mwao wakijinadi kwamba wana mali nyingi zenye thamani lakini si kweli.

Onyesho la  nne linaonyesha Zidi akiwa mwalimu na wanafunzi darasani katika kipindi cha somo la sayansi. Wanafunzi wanamuuliza mwalimu maswali ili wapate kujua lakini mwalimu naye hajui kitu ila anajilinda haiba yake kwa bakora!
Onyesho la tano, Ame mkuu wa ofisi fulani akiwa na msaidizi wake Zidi wakiwa ofisini wakijadiliana mambo mbalimbali na jambo kuu ni kughushi nyaraka ili kujipatia fedha kinyume na utaratibu wa kasri lao. Onesho la sita ni mwndelezo wa omyesho la tano.

Onyesho la saba Mari amerejea kutoka mbali kumtembelea mpenzi wake aliyemuacha siku nyingi. Zidi na Mari wanashangaana na kisha kila mmoja anamuona mwenzake amebadilika lakini Mari anamwambia Zidi kuwa hajabadilika kimawazo kwa kuwa bado yu masikini. Mari amekuwa na mwonekano wa kizungu na ngozi amejichubua.

Onyesho la nane, Ame na Zidi wanajadiliana masuala mbalimbali kuhusu kasri lao iliwaondokane na utegemezi wa misaada kutoka mbalia. Kubwa hasa wanajadiliana kutokomeza ugonjwa wa maleria.

Onesho la tisa, Zidi anaugua tumbo baada ya kula nyama ya ngombe iliyoletwa kwa msaada kutoka Jumuiya ya Umoja wa nchi za Ulaya (EC). Nyama hiyo ilikuwa imevunda lakini waliiparamia tu na kuila kutokana na njaa. Baadae Zidi anakufa.
Onyesho la kumi, Ame naye anaugua tumbo baada ya kuharisha kwa muda mrefu, hivyo kipindupindu kimemshika na yeye pia anakufa. Usingizi unamkosesha Ame morali ya kufanya kazi kwa bidii hivyo anabaki kitandani akiwa mvivu kuamka. Usingizi aliouzungumza mwandishi hapa huenda si ule wa kuliparamia godoro tu bali ni kuwa katika hali isiyo na mabadiliko katika kitu licha ya kubadilika kwa nyakati. Mwandishi ananuia kusema kuwa usingizi wa mawazo ni mzito ziadi kuliko usingizi wa kuparamia godoro. Tuamke katika fikra ili kujiendeleza.

Suala la elimu ni suala ambalo linajadiliwa kwa kiasi kikubwa katika nchi nyingi barani Afrika. Mwandishi aeonyesha kwamba upo uwezekano mkubwa wa baadhi ya walimu kufundisha mabo wasiyokuwa na ujuzi nayo, hivyo ni vema kila mwalimu angeshika somo moja tu kwa siku na afundishe madarasa mawili tu. Somo hilo awe analimudu vizuri. Pia maarifa wanayofundishwa wanafunzi yalenge jamii kwa ujumla, si vema mhitimu wa uhandisi wa umeme ashindwe hata kurekebisha pasi ikiwa na hitilafu. Mhandisi wa majengo kwenye makaratasi atafundishwa ubora wa kuchanganya zege lakini akiletewa theruji, lipu, mchanga, kokoto na maji anshindwa kufanya vipimo. Elimu yetu ina hitaji mabdiliko. Udadisi wa wanafunzi nao uheshimiwe!

Tunahitaji kuthamini bidhaa za ndani. Tuna samani nyingi zimejaa maeneo mbalimbali zinasota kwa siku nyingi tu. Tunaona vema kununua meza na viti vya vioo kutoka Uchina, Paris, Italia ili kuviweka ndani mwetu lakini samani bora za mbao zinazodumu kwa muda mrefu twaziona ni bure ka bisa. Mwandishi ananuia kusema kuwa tunapaswa kutahamini vitu vyetu kama vile tunavyothamini vya ughaibuni.

Ulimbwende siyo lazima kukoboa ngozi. Kwa wanawake, wanaweza kuwa warembo wazuri bila kukoboa ngozi zao na kuwa na rangi ya bandia inayoleta matatizo mwilini. Mari ni mrembo bandia aliyekoboa ngozi na kunyoa upala kisha kuvaa mawigi ya katani au ya nywele za watu waliokufa na pia amenyoa kope zote na kubandika kope za plastiki zilizotengenezwa Kanada. Tabia hii mwandishi ameisema kwa muda muafaka, na wengi wanaofanya hivyo hupata matatizo mbalimbali katika miili yao.

Wanafunzi huko vyuoni wasome kwa ujuzi wa mambo lakini si tu kupata GPA yenye alama za juu. Ikiwa ujuzi wa mambo hautazingatiwa basi hata fundi wa kuziba pancha ataitwa kutoka Ujerumani. Tunafurahi nini kutoa tenda kwa kandarasi nyingi za nje? Kama tunazo za kwetu kwa nini hatuziimarishi kwa kuziamini na kuzipatia tenda hizo? Barabara nyingi katika nchi za Afrika zimejengwa na kandarasi za ughaibuni. Basi kwa msaada wa tamthiliya hii ya AMEZIDI tusizidi tu kutegemea mbali na nyumbani kwetu.
Hakuna haja ya kughushi nyaraka ili kujipatia mali kinyemela. Tukijivika kanzu la kufanya mambo ipasavyo na kwa kanuni maalumu basi kanuni ile itaiishi na itatusaidia tukiisimamia ipasavyo. Hivi zisingekuwepo Marekani, Kanada, Ujerumani, Italia, Ujapani, Ubelgiji, Ufaransa, na kadhalika tungenyosha wapi mikono yetu zaidi? Tunekubali kwenda Haiti au Tahiti kuomba?

Afrika tuna changamoto nyingi, kuzitatua kunahitaji umakini wa kufikiri. Semina, mikutano, makongamano, maandamano, na mabango ni mitazamo tu kuhusu utatuzi lakini “mtazamo hauliwi hata tukitumbuliana macho namna gani”. Tuimarishe sera, na elimu tuijali kwa kina.

© Kizito Mpangala (0692 555 874)

18 comments:

  1. Nimependa mtiririko wa mawazo Haya.. Shukrani Kwako bwana Mpangala

    ReplyDelete
  2. Kazi nzuri mno imenisaidia kuielewa tamthilia Amezidi

    ReplyDelete
  3. Kazi nzuri mno imenisaidia kuielewa tamthilia Amezidi

    ReplyDelete
  4. Kazi nzuri sana bwana mpangala

    ReplyDelete
  5. Kazi ya Safi saana, kwa ufupi umasikini Ni mbaya

    ReplyDelete
  6. Kazi nzuri sana shukran

    ReplyDelete
  7. Excellent thanks đź‘Ťđź‘Ťđź‘Ťđź‘Ťđź‘Ť☺️

    ReplyDelete
  8. Heko Bw. Mpangala

    ReplyDelete
  9. Daaah bila ya kupitia hilo dodoso ,kwa kweli kitabuni nilikua naona kimendikwa kichina tuu baaada ya kiswahili

    ReplyDelete
  10. Anonymous09 May, 2023

    umejitahidi san kuchambua kitabu hiki hongera

    ReplyDelete
  11. Anonymous23 June, 2023

    Shukraniii sanaa

    ReplyDelete
  12. Kazi nzuri

    ReplyDelete
  13. Shwari kabisa,,kazi njema

    ReplyDelete
  14. Kazi nzuri

    ReplyDelete
  15. Kazi nzuri nimevutiwa nayo

    ReplyDelete

Maoni yako