May 12, 2013

UDINI, UGAIDI MPAKA KUZIBA PANCHA ZA MITIHANI

Na Markus Mpangala, Dar es Salaam

Ulianza UDINI. Tukaambiwa chama fulani cha siasa ni cha kidini. Baadaye tukaelezwa kuwa kinafadhili au kutunza magaidi hapa nchini. Tukaambiwa wanaleta visu, silaha na kadhalika. Baadaye tukaambiwa chama fulani ni cha waumini wa dini fulani. Yalikuwepo mwaka 1995. Yakawepo mwaka 2000. Yakaongezwa mwaka 2005. Yakarutubishwa mwaka 2010 kwamba chama fulani cha waumini fulani. Sasa Bungeni tunasikia na kuambiwa chama fulani ni Magaidi. Halafu wale wa chama hicho nao wanasema chama fulani ni Magaidi.
Ndugu zangu, kuchanganyikiwa huku na hitilafu ya kijamii ilisababishwa na watu. Ni watu waliopika kwa juhudi UDINI. Wakapika kwa maarifa na jasho la kipumbavu. Baadaye wameanza kupikana kwa UGAIDI bungeni. Hili suala lilianza zamani sana juu ya Magaidi hapa kwetu (tukumbuke zama za uongozi wa mzee wetu Omar Mahita). 

Sote kinachotokea tunakiona, na tunalaghaiwa sana sababu tumekubali kulaghaiwa. Hakuna njia ya mkato kwamba kuchanganyikiwa huku kwa jamii yetu na kile kilichosababisha kufutwa kwa mitihani ya kidaoto cha nne, nadhani nako ni kuchanganyikiwa kulekule. Yaani tumejikuta tumechanganyikiwa kiasi ambacho hata binadamu aliye mbele yako ni adui bila kujua sababu zako za kufikiria yeye ni adui. 

Mapishi ya kuwagawa wananchi wa Tanzania yapo mengi na kwa kila namna. Sote tunashuhudia hili kila kona na hakuna aliye tayari kukiri kuwa alihusika ama yeye ndiye mhusika. Serikali inawalaumu wananchi wake, hali kadhalika Wananchi wanailaumu serikali yao. Chama tawala wanawalaumu vyama vya upinzani, hali kadhalika vyama vya upinzani wanakilaumu chama tawala.
Idara za serikali zinawaambia watu na kuwatisha kuwa wakijadili uchochezi watakamatwa. Mimi nasema hatukufikia kujadili fikra za kichochezi hivi hivi kama sio kujilemeza na kutawaliwa kwa njia ambazo zinaleta ukakasi.
Wimbo wa uchochezi ni matokeo ya kujaribu kufifisha fikra huru zenye kujadili mambo ya msingi, maana kinachofanywa ni kujumuisha sote tumekuwa wachochezi. Daima utawala mbovu husingizia na kulaumu kuwa kuna watu wachochezi, na mwishowe kila mara kazi yake ni kujitetea kila uchao. Hakika tumechanganyikiwa mno. 

Leo hii tumeruhusu watu wajione waathirika wa masuala ya kufikirika. Leo tumeruhusu kugombana sababu ya kuchinja. Leo tunagombana sababu ya imani za dini. Leo tunatishia uhai na kuitana majina mabaya ndani ya Ukumbi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Spika wetu mheshimiwa naye anasikia kauli chama fulani cha kigaidi na mlalamikiwa naye anakuja juu akisema chama fulani ni magaidi. 

Malumbano haya yanapoachiwa kwenye jengo la Bunge nadhani watu huku pembeni wanaendelea kulishwa kwamba tishio letu ni ugaidi na sio umasikini wa kipato. Hakuna aliye tayari kuona ghasia za uchumi duni, shida zilizojaa pomoni kwa mwananchi wa Tanzania, ambao unachochea kuchanganyikiwa kijamii. 

Na kuchanganyikiwa huku hata askari wetu wametuhumiwa kupora milioni 150 za majambazi waliokamatwa. Sote tunaona. Hii ni ishara kwamba kuchanganyikiwa huku ni kukubwa mno. Tumechanganyikiwa kijamii na madhara yake hata kwenye uongozi ndiko kumechanganyikiwa kabisa, kumepumbaa,wameduwaa hawajui tufanye nini katika Tanzania ya leo kuondokana na vijitukio vya kuhasimiana nchini.
Na hakika kuchanganyikiwa huku ni kukubwa kuliko kitu chochote. Wimbi la nyumba za ibada ni kubwa mno lakini cha ajabu matendo yenye dhambi yanazidi kushamiri. Hakuna hata lenye kificho kwamba, kama serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haichukui wakati kujisaili yenyewe basi itakuwa kila hotuba za kila mwezi ni kujitetea kwingi zaidi na zaidi.
Istilahi za kuishi kisungura kumetufanya tuone tofauti zetu za kidini ni moja ya mambo yanayotakiwa kuchukiwa badala ya kuishi kwa amani na upendo huku tukikubali kuwa hilo ni suala la imani ya mtu. Serikali huwa inatamba ina mkono mrefu, lakini leo hii tunashindwa, tumelemaa, tumekwama hata kuchunguza masuala mepesi, lakini kinachofanyika ni walete FBI au CIA na kadhalika. 

Lakini hawa hawa FBI, CIA ndio waliofanikiwa kuivuruga Afhanistan iliyokuwa imetulia chini ya Maflme Najibullah. Kwa vigezo vya nchi zao wakadhani utawala wa kifalme Afghanistan haina demokrasia. Ulaghai huu ukajikita, Mfalme Najibullah hayupo leo, Hamid Karzai amebaki kuwa kibaraka wa Marekani na sasa tuhuma kubwa ya kupokea fedha kutoka CIA ni kubwa mno. 

Gazeti la The New York Times limeripoti tuhuma hizi kwa kirefu sana wiki iliyopita, na kumtia kigugumizi Rais Hamid Karzai. Yote haya yanafanyika kwa udhamini huu huu wa kudhani FBI au CIA ni wapendwa sana. Tumechanganyikiwa hata makachero wetu hatuwaamini wakati tunatumia fedha nyingi kuwasomesha ughaibuni na hapa nchini.
Makachero ambao tumewapa mafunzo ya kila namna lakini tunawakejeli kwa kuwaletea FBI. Ugonjwa uleule wa ukoloni tunajaribu kuurudisha kwa mlango wa nyuma. Na sifa ya ukoloni kwa sasa ni kurejea katika njia za utamu utamu na vitu vyote vyenye utamu. Kuchanganyikiwa kwetu huku ni kukubwa sana. Mimi nadhani lazima tuchukue hatua za msingi na kuwa wakali. 

Serikali ya nchi yoyote sio lazima ipendwe kwakuwa inawajali wananchi kwa kuwaachia wajichane na kustarehe kwa uhuru, bali hata ukali na kuwaadabisha raia wake ni njia moja wapo ya kupendwa kwa serikali. Wimbi la uchochezi linaibuka katikati ya kulemaa kwa kusimamia masuala ya msingi. Tunazo sheria za kila namna lakini tilichoweza kukifanya ni kuachia mambo yajiongoze yenyewe halafu baadaye tuseme kila mwezi kwa hotuba dhaifu na kujitetea. 

Benjamin Mkapa alinukuliwa siku za karibuni kuwa viongozi wa kizazi kipya wameshindwa kazi hivyo wanachotakiwa ni kuwapisha wale kizazi cha kale. Lakini kwa upande wake Mheshimiwa Zitto Kabwe aliwahi kudokeza kuwa nchi yetu haiwezi kujikwamua hapa ilipo kwa kutegemea uongozi au kiongozi aliyetokana na zama za ukoloni yaani waliozaliwa kipindi hicho. 

Shida hapa sio kuzaliwa lini, bali namna gani hatua stahiki zitatuondoa kwenye kuchanganyikiwa huku ndani ya jamii yetu. Tumechanganyikiwa kiasi kwamba suluhu yake ni kuziba pacha za mitihani kwa kuwadekeza wanafunzi waliochora zombi, Messi na kadhalika. Uonevu huu baadhi ya wananchi wananiuliza, tumeikosea nini nchi hii? Kuchanganyikiwa kwetu huku ni kukubwa mno hata nashangazwa na Baraza la Mawaziri kuidhinisha kufutwa mitihani. Kisa? Hakuna jingine zaidi ya kuchanganyikiwa kiuongozi. Tuko pabaya sana, lakini tunaelekea mahali pazuri sana kadiri tunavyozidi kuchanganyikiwa. Amani iwe nasi daima.

Baruapepe; mwanazuoni27@gmail.com

No comments:

Post a Comment

Maoni yako