Showing posts with label Mtwara. Show all posts
Showing posts with label Mtwara. Show all posts

February 23, 2018

AFYA: WATANI ZETU WANA NACHINGWEA, SHIRIKINI KATIKA ZOEZI LA MATIBABU YA WATOTO WENYE VICHWA VIKUBWA

January 01, 2018

SALAM ZA MWAKA MPYA 2018; KOROSHO MTWARA

NA GABRIEL MWANG’ONDA
 
KAMA ilivyo kwenye korosho kule Mtwara, basi kwa wale wahenga wenzangu wa mji wa Tukuyu mtakuwa mnajua zile karanga za mitini kwa watu wa mjini na sehemu zinginezo wanaweza kudhani nadanganya, lakini la hasha ni kweli kuna karanga humea mitini na ni miti mikubwa kabisa, kwa kinyakyusa zinaitwa (Macadamia). Hizi zina vinasaba vya korosho kwa mbali, ni very delicious and healthy vilevile. 

Wakati bei ya korosho ikipanda mpaka kufikia elfu nne kwa kilo kule Nangwanda Sijaona kunako Mtwara, watani wetu wa jadi hapo Kenya wameamua kuachana na mashamba ya Chai na kukazania kilimo cha Karanga za mtini ambazo zimefikia kilo moja Tshs 21,000.00 nakuendelea. 


January 23, 2013

SAKATA LA GESI LIMEZUA JIPYA MKOANI MTWARA-Mgodi Unaotembea


Kambi Mbwana

Na Kambi Mbwana, Dar es Salaam

HALI ya mkoani Mtwara ni dhahiri inatishia amani, hivyo kuna kila sababu ya serikali na wadau wote kukaa na kuliangalia suala hilo kwa marefu. Nikiwa kama Mtanzania, nimekuwa nikifuatilia kwa karibu mno sakata hilo la gesi inayopingwa na wadau kuletwa jijini Dar es Salaam, badala yake wanataka ibaki mkoani Mtwara, ingawa wenye akili ndogo wanapinga au kutukashifu kadri ya uwezo wao, wakijidanganya kuwa sipaswi kufuatilia mambo ya Mtwara na Lindi.
Huu ni udhaifu na hauwezi kuchekewa, maana ni dhahiri Mtwara, Lindi ni sehemu ya Tanzania kama ilivyokuwa Tanga, Arusha, Kilimanjaro na kwingineko. Wananchi hao waliojikusanya kwa ajili ya kupigania sakata hilo, wamefikia kubadilisha kabisa hisia zao, bila woga wowote katika kulizungumzia suala la gesi.
Kama nilivyowahi kuhoji hapo nyuma, kuwa tatizo ni gesi, choyo, siasa au ubaguzi? Makala haya yalitoka katika blog hii ya Handeni Kwetu na kupokea maoni mbalimbali. Na haya ndio maoni ya Watanzania hao wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Mwanzo wa ugaidi Tanzania ni mwisho wa amani. Kusini hawaogopi jeshi. Kauli ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete ipo kwenye mioyo yao. Leo nasema, ila wana Mtwara watasema kwa sauti zao, maana vitisho kwao ni kama kuitukana maiti.
Chochote kitatokea iwe ni vita vyovyote vile 2015 hatutaki uchaguzi na hatutaki pia tuletewe kiongozi na ole wenu, +255712897794
Maandamano Mtwara
Kaka nimefurahishwa na makala yako isemayo Tatizo ni ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Inaonekana na wewe pia umeandika makala hii kwa lengo lako binafsi. Umeshindwa kutoa uhalisia wa jambo lenyewe, badala yake umeandika kwa lengo la kutaka kumfurahisha ama kuwafurahisha watu fulani. Rudi nyuma angalia wanachofanyiwa wakulima wa korosho wa Mtwara je ni sahihi? Lile zao halisaidii kuinua pato la Taifa? Angalia hali ya maisha ya wakazi wa Mtwara. Nadhani umekurupuka na si mawazo yako kuna mkono wa mtu nyuma yako.
Nenda kazunguuke na kufanya utafiti wa kina utapata majibu sahihi kwa wenyeji. +255657614354.
 Tatizo la mikoa ya Kusini sio gesi bali ni kusahauliwa kwa miaka 51 ya Uhuru. Korosho, reli, Bandari, miundo mbinu, tatizo la elimu na kuwa waanga wa ukombozi wa nchi zilizopo kusini mwa Afrika.
Wanasiasa kujiingiza katika hoja si ajabu kwasababu duniani kote wanasiasa ndio huibua matatizo ya wananchi , maana wasomi wetu wengi hawana meno ya na ndio wanaopitisha  mikataba mibovu .
Sio choyo, lakini tunafikia wakati tunajuta kwa nini sisi Mtwara Lindi tumekuwa sehemu ya Tanzania. Tuna rasilimali tosha za kuweza kuitwa, kama vile Bandari, Bahari, Ardhi yenye rutuba, watu, mito, madini, korosho, ufuta, mhogo na nyinginezo. Kusini tuna haki ya kumdai mume wetu Tanzania haki zetu za msingi, maana tumevumilia mno hadi kilio cha kwi kwi. Ni mimi mwanaharakati,  Amoni, wa Kata Msangamkuu, Mtwara Vijijini. +255652221100.
Ninaomba uelewe lengo la wananchi wa Mtwara na Lindi sio kwamba hawataki gesi isitumiwe na wengine hapana, wao wanataka kiwanda kitengenezwe Mtwara. Kule itoke gesi safi, maana wanakataa mambo yasijekuwa kama ya madini ya Geita ambayo mwekezaji anachimba anaenda kuhakiki Mwanza na kulipa kodi ya uwongo na kuiibia nchi na kuwa masikini, huku wakifaidi watu kutoka nje.
Nimesoma makala yako, inayosema tatizo ni gesi, siasa, choyo au ubaguzi? Mimi nimeisoma na kwa utafiti wangu, nimegundua kwamba wewe ni CCM na ndio maana ukaona eti ni siasa. Hapana, ni kwasababu vyama vya upinzani vinapenda maendeleo ya Watanzania.
Mbona hawakuhamisha miwa kutoka Kagera na kuileta Dar es Salaam ili itengenezwe hapa? Pili, hebu fikiria gharama za kuweka bomba ni kiasi gani? Tatu, kumbuka msongamano mkubwa wa watu, ina maana wakiongeza viwanda wanazidisha msongamano. Nne, kwanini wasiwaachie watu wa Mtwara na Lindi na wao wapate ajira? Tano, kila kilichokuwapo Dar es Salaam, Mtwara kipo kama vile Bandari na mengineyo. +255713221244.
Ingawa hujaonyesha wazi ujumbe unaopeleka kwa wana Mtwara, lakini ninachofahamu, Taifa halina rasilimali. Mikoa, wilaya, vijiji, ndivyo vyenye rasilimali, kama vile mbuga za wanyama, madini, mazao na mengineyo ambayo mapato yake hukusanywa na kuwa pato la Taifa. Gesi ni kama rasilimali nyingine tu. Ikiwa Mtwara, Lindi, Kigoma, Mbeya au popote nchini, tueleze ni vipi italinyima Taifa letu pato? Au italigawa vipi Taifa? +255717757797.
Hongera bwana Kambi Mbwana kwa makala yako. Endelea kuwapa elimu Watanzania wenzetu wasioelewa. Naitwa Moi, +255757295249.
Unajua sisi tunaotoka Mtwara tunafananishwa na nyani katika Taifa hili. Hatuna thamani mbele ya makabila mengine toka Uhuru. Barabara haijaisha, mazao yetu hayana usimamizi na hatuna huduma za jamii zilizo bora. Tukipata wakarimu, sio bora pamoja na watumishi wote. Sisi ni jamii ya mwisho katika Taifa hili, hujiulizi gesi na mafuta aliyotupatia Mwenyezimungu ingekuwa sehemu nyingine ingehamishwa? Kwakuwa sisi nyani, hatuna thamani, gesi itaondoka na mafuta pia yataondoka, maana hawa hawatatuthamini milele. +255712848839.
Asante kwa makala yako, lakini usiwe mwandishi mwoga anayeogopa watawala walioshindwa kuwaondolea wananchi umasikini na kuligawa Taifa, kati ya wenye nacho na wasiokuwa nacho. Jitahidi kuwa mkweli ili upate mafanikio maishani mwako. +255755045295. Kijana mbona unakuwa kama popo asiyejulikana kama ni mnyama au ndege. Ya Handeni Kwenu yamekushinda sasa umehamia kwenye gesi.
Nasikitika ujumbe huu uliotumwa kwa namba +255757602075. nimeufipisha kwa sababu za kimaadili, maana ulijaa matusi na kashfa kutoka kwa mtumaji, ambaye pia hakujitambulisha jina lake. Kaka nimesoma makala zako nyingi, nimegundua wewe ni kada wa CCM na usiyejua nini wanachokitaka Watanzania.  Hata hujui huko vijijini watu wanaishi vipi. Unaogopa ya Daudi Mwangosi na Amina Chifupa na huo sio uzalendo, hivyo hupaswi kuwa mwandishi.
Hivi unajua CCM wanaiendashaje nchi hii? Umeshahoji wananchi wangapi kuhusu maisha yao badala yake unamfuata Nape Nnauye, unataka CCM ndio waiongoze nchi milele na milele kwakuwa wewe si mzalendo. Ujumbe huu ulitoka kwa namba +255652273836. Nashukuru brother kwa kuweza kupata fursa ya kuweza kusoma makala yako.
Ni kweli hoja zako ulizozisema zinaweza kushabihiana na ukweli,  ila kutokana na vile hali ilivyo naweza (kudetermine ya words) nazo yanatokana na siasa pia. Hebu nambie kaka angu, umaskini uliopo katika mikoa ya kusini, moja kwa moja tumekuwa maskini na hii ilikua nafasi pekee ya kuweza kupata ahueni.
Hebu jamani isifike wakati tukawa tunaangalia swala hili kijuu juu, hali ni mbya kusini hatuna pa kushikia, serikali ilibidi iangalie gesi hii pia katika kutafuta namna ya kuikomboa miji hii ya kusini.
Ni wazi kuwa serikali imekua ikifurahia tu kupata neema hiyo kuendesha mambo yao na si kusaidia kuondosha umaskini.
Nyinyi waandishi tunawategemea kutoa hoja za kusaidia kuondokana na majanga ya kimaskini. Ujumbe huu ulitumwa kwa njia ya barua pepe kutoka kwa Raya Juma, Nashkuru Haya ni baadhi ya maoni yaliyoingia mara baada ya kuandika makala ile, huku watu wakiingia moia kwa moja katika hoja yangu ya siasa, ubaguzi na choyo nilizokemea. Kwanini nasema siasa? Ukiangalia hapo, wapo waliotuma ujumbe huo wakiwa na chukia serikali ya CCM. Hata hivyo, kuyaanika maoni yao si kuwaletea matatizo, bali kusoma mawazo ya watu wa Mtwara.
Wao ndio wahusika. Ndio wenye kupigania suala la gesi, hivyo inaweza kuwa njia muafaka ya kuepusha shari inayozidi kujengeka mioyoni mwa Watanzania, hususan wale wanaoishi mkoani Lindi na Mtwara. Watu wamekuwa na mawazo tofauti juu ya sakata hilo. Wapo wale wanaofikia kutamani Mtwara iwe na utawala wake, jambo ambalo hakika si la kuchekea.
Rasilimali za Tanzania zinaanza kutugawa kadri siku zinavyozidi kwenda mbele, ndio maana nikaamua kuyaanika mawazo ya ndugu zetu hao. Kwa kumalizia tu, sakata la gesi linaweza kujadiliwa upya kwa kuwashirikisha wadau na wananchi wa Mtwara, hasa kwa kupewa mikakati ya namna ya serikali kuwapelekea maendeleo maana ni wajibu wao.
Masuala ya chokochoko ya gesi yasiachwe tu kwa wanasiasa ambao wamekuwa wabunifu kuingia kwenye hoja zinazoshirikisha watu kwa ajili ya kujijenga kisiasa, jambo ambalo si zuri.
Na sisi tunaofikia kujadili suala la gesi, wakiwamo wana harakati, wasitumie maneno makali, maana siku zote jazba inaondosha maana husika. Maoni mengi ya Watanzania nimeshindwa kuyaandika kwa kwasababu hayajatolewa kiungwana, huku niliyoaandika nikiyafanyia marekebisho mengi mno.
Katika hili, serikali kwa kupitia Waziri wake wa Nishati na Madini, Professa Sospeter Muhongo, anapaswa kukaa na kulijadili jambo hili kwa mapana yake.

kambimbwana@yahoo.com
www.handenikwetu.blogspot.com
+255712053949
+255753806087

January 15, 2013

MIKOA YA MTWARA,LINDI NA RUVUMA TAFUTENI SULUHU KUFELI MITIHANI

Na Hamisi Magendela , Dar es Salaam
SIKU chache zilizopita wananchi wa mikoa ya kusini waliandamana kupinga uchimbaji wa bomba la gesi kutoka huko kwenda Dar es Salaam ambacho ingetumika kwa ajili ya kuzalisha umeme.
wanafunzi wakiwa darasani katika moja ya shule za msingi wilayani Nyasa
Umeme huo ambao ungezalishwa jijini Dar es Salaam ungetumika katika mikoa mbalimbali ya Tanzania hali ambayo inaaminika kuwa itasaidia kupungua ghalama za umeme na kufanya ukali wa maisha kupungua.
Sipingi mawazo yao kwani kila mmoja anafikilia kwa utashi wake japo ni vema wakaangalia faida kuliko na mafanikio yatakayopatika siku za usoni ikiwa gesi hiyo itasafilishwa kwa njia ya bomba kwenda Dar es Salaam.
Kikumbwa ambacho naweza kusema ni kwa wananchi wa mikoa ya kusini wanatatizo makubwa zaidi ya kuandamana kutaka manufaiko ya gesi wakati suala zima la elimu likiwa limewatupa mkono kiasi kwamba inatia simanzi kuona inashika nafasi 10 za mwisho katika ufauru wa matokeo ya kidato cha pili yalitangazwa juzi na Wizara ya Elimu na Mafunzo jijini Dar  es Salaam jana.
Licha ya kuwa ni aibu kwa wananchi pamoja na viongozi wa mkoa huo lakini naweza kusema kuwa ni kashfa ambayo katika miaka 50 ya Uhuru ijayo inatakiwa kufanyiwa kazi ili kuhakikisha wanapata elimu ya kutosha na kuondoka na ujinga wa kukosa elimu.
Ingekuwa vema zaidi badala ya kulalamikia kuhusu gesi wangepiga kelele kwa kukosa elimu bora kwa wanachi wengi wa mikoa hiyo hali inawafanya kukosa nafasi nzuri katika viwanda vinavyojengwa katika mikoa.
Kwa maana nafasi nzuri ya ajira itakuwa ikishirikiliwa na wageni ambao wana elimu ya kutosha ya kukidhi mahitaji ya kazi inayohitajika kwa wakati huo na kufanya wenyeji kufanya kazi za hali ya chini kila siku.
Pia wananchi wa mikoa ya kusini umefikia wakati wa kusimama kidete kuhakikisha fursa iliyotangazwa na Serikali kuwa kuanzia sasa hakutakuwa na mwalimu atakaepangiwa kazi mijini kwa wanaotoka vyuoni.
Kwa maana hiyo ikiwa viongozi wa mikoa hiyo wakitumia fursa hiyo kuwahamasisha wananchi wa kuzingatia elimu badala ya kung'ang'ani masuala ambayo kwa sasa hayasaidii sana katika miaka 50 ijayo.
Kusudio hilo la Serikali kupeleka walimu vijini linatokana na malalamiko kutoka sehemu hizo kuwa zimesahaurika kielimu kutokana na kukosa walimu wa kutosha hali inayofanya mikoa hiyo kushikia mikia katika matokeo ya mwisho kama ilivyo sasa kwa mikoa ya kusini.
Serikali kupitia Wizara ya Elimu ilisema lengo la kufanya hivyo ni kupata uwiano wa mwalimu mmoja kwa wanafunzi 10 hali itakayosaidia kunyanyua kiwango cha elimu katika mikoa iliyo pembezoni mwaka nchi.
Hivyo naamini fursa hiyo ikiwa itatumiwa vema na wananchi wa huko itafanya viwanda vinavyojengwa sasa katika mikoa hiyo wenyeji kunufaika kazi zaidi kuliko wageni ndio madhumuni makubwa ya baadhi ya wawekezaji.
Kwa maana wapo wanaotoa ahadi kuwa ikiwa viwanda vyao vitamalizika waajili wenyeji kwa asilimia zaidi ya 60, lakini ikiwa hali ya elimu itaendelea kuwa hivyo ni dhairi wageni watakuwa na nafasi kubwa kuliko wazawa.
Viongozi wa mikoa ya pembezoni mwa Tanzania ikiwemo ya kusini kazi kwenu kuhakikisha mnahamasisha wananchi wenu wanatumia fursa inayotolewa na Serikali kupeleka walimu vijijini inatumiwa vizuri na matunda yaonekana.
Pia kwa Serikali ni vema ikatambu kuwa si walimu pekee wanahitajika katika mikoa hiyo iliyo pembezoni mwa Tanzania bali vyenzo za kufundishi nazo ni muhimu, itakuwa haina maana kupeleka walimu bila ya vitendea kazi na kuwajengea miondo mbinu mingine ikiwemi malazi bora.
Kwani upo uhushuhuda kuwa walimu wengi wanakacha kwenda kufundisha vijini kutokana na kutopatiwa mahitaji muhimu ya kibinadamu ikiwemo usafiri, nyumba nzuri za kuishi na kuishi katika maboma.
 Maoni: 0782839898

December 29, 2012

UTAJIRI WA GESI ASILIA: TUWASIKILIZE WATANZANIA WA MTWARA NA LINDI. TUSIWAPUUZE



Na Zitto Kabwe, Dar es Salaam
Maandamano ya amani yaliyofanyika mjini Mtwara siku ya alhamis wiki hii yameibua hoja mbali mbali kutoka kwa viongozi, wananchi, vyombo vya habari na mjadala wa siku nzima kwenye mitandao ya kijamii hasa facebook, twitter na JamiiForums. Mkuu wa Mkoa wa Mtwara ameita waandamanaji wapuuzi na Waziri wa Nishati na Madini amewaita watu hatari na wahaini. CHADEMA tumetoa kauli kupitia kwa Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kwamba udhaifu wa utendaji serikalini ndio chanzo cha maandamano haya.
Lakini kuna tatizo kubwa zaidi ambalo linaonekana siyo katika sekta hii tu bali pia katika sekta nyingine ambapo tunaona matokeo yake katika maisha ya watu wetu na naweza kusema ni dalili za kushindikana kwa sera za CCM. Sera hizi ndizo ambazo zimelifikisha taifa hili hadi hapa. Kama hadi wananchi wa Mtwara ambako kwa muda mrefu imekuwa ni ngombe ya CCM wanaanza kuhoji matokeo ya sera za chama tawala basi ni dalili kuwa Watanzania wamefungua macho yao na wanaona. 
Wanaona katika nishati, wanaona katika utawala bora, wanaona katia elimu (kuanzia ya msingi hadi ya juu kabisa!), wanaona katika afya, wanaona katika utendaji wa jeshi la polisi wanaona katika madini. Sera za CCM zimeshindwa. Zimeshindwa kuinua maisha yao na zinaonekana kuendelea kushindwa.
Mtwara na Lindi wanataka nini?
Watu wa Mtwara wanataka gesi isiondoke Mtwara na badala yake viwanda na mitambo ijengwe Mtwara kisha kama ni umeme au mbolea isafirishwe kupelekwa sehemu nyingine ya nchi. Watu wa Mtwara hawasemi kwamba Gesi yote na mazao yake vibaki Mtwara na Lindi. Wanasema umeme uzalishwe Mtwara usambazwe nchi nzima. Mbolea izalishwe Mtwara na kusambazwa nchi nzima. Wanataka Bandari ya Mtwara iboreshwe na kuhudumia mikoa ya Kusini. Watu wa Mtwara hawasemi kwamba mapato yote ya Gesi yatumike Mtwara tu la hasha.
Sio dhambi hata kidogo kwa watu wa Mtwara kudai masuala haya. Watu wa Mtwara wamefanya maandamano kwa amani kabisa bila kuharibu mali na kutoa maoni yao. Kwanini tuwasute na kuwasusubika kwa madai yao haya? Kwa nini tusiwasikilize? Kosa lao nini kudai viwanda ili wapate ajira? Tumesahau kuwa mikoa ya Lindi na Mtwara ni mikoa masikini kabisa nchini? Tumesahau kuwa mikoa ya Lindi na Mtwara ilitumika kwa ukombozi wa kusini mwa Afrika kiasi cha kuwa katika hatari kabisa? 
Tumesahau ‘sacrifice’ ya watu wa Mtwara na Lindi dhidi ya usalama wa nchi yetu? Tumesahau kuwa Korosho imekuwa zao kubwa la biashara na linaloingiza mapato mengi sana ya Fedha za kigeni? Waziri Muhongo anasema Mtwara warudishe Fedha za Mkonge na Kahawa. Mbona hataji fedha za Korosho? Mwaka 2011 Korosho ilikuwa zao la pili kwa kuingiza fedha nyingi za kigeni baada ya Tumbaku.
Lakini tujiulize, watu wa Mtwara na Lindi walifadi fedha za Mkonge? Walifaidi fedha za Kahawa? Wamefaidi fedha zao za Korosho? Tumesahau hata Reli iliyoachwa na Mkoloni ya Nachingwea – Mtwara iling’olewa na Serikali huru ya Tanzania? Tujiulize zaidi, hivi watu wa Nzega wamefaidika vipi na Mgodi wa Resolute pale Lusu? Mgodi umefungwa ukiwa umezalisha na kuuaza dhahabu ya thamani ya dola za marekani 3.3 bilioni. Hivi katika uhai wa mgodi huu Serikali Kuu imekusanya kodi kiasi gani? Halmashauri ya Wilaya ya Nzega imepata ushuru kiasi gani? Watu wa Mtwara wanayaona haya yaliyotokea Nzega na yanayotokea Tarime, Biharamulo, Kahama na Geita. Watu wa Mtwara wana Haki kuandamana kuzuia haya yaliyotokea wenzao yasiwatokee wao kwenye Gesi asilia.

Mtwara na Lindi wanakosea wapi?
Madai yao halali na mimi binafsi na chama changu tunayaunga mkono. Lakini kuna mahala lazima waelimishwe. Watu wa Mtwara pia wanapaswa kuelewa kuwa juhudi zao zisiwatenganishe na Watanzania wengine kwani bado utajiri wa Taifa unafadisha kikundi cha Watanzania wachache sana. Watu wa Mtwara wanahitaji kuungana na watu wa Mara, watu wa Mwanza, watu wa Shinyanga na watu wa Kagera kudai utajiri wa nchi utumike kwa maendeleo ya watu badala ya kunufaisha kundi dogo la watu. Watu wa Mtwara wanapaswa kuunganisha nguvu na Watanzania wengine kuzuia uporaji wa rasilimali ya nchi dhidi ya kizazi kijacho. Watu wa Mtwara wasijitenge wakawa peke yao na Gesi yao. Nguvu ya mnyonge ni umoja.
Serikali isiyosikia
Serikali ina hoja kuhusu kujenga Bomba la Gesi kwa ajili ya kuzalisha umeme kwa gharama nafuu. Umeme unaotumiwa na asilimia 14 tu ya Watanzania. Kwa kuwa hii asilimia 14 ndio wenye sauti basi watu wa Mtwara wataonekana hawana hoja kabisa. Lakini Serikali imejiuliza mara mbilimbili kuhusu mradi huu wa Bomba? Tunaambiwa na Wataalamu kwamba kuna uwezekano mkubwa mwakani gesi asilia ya kiasi cha futi za ujazo trillioni 20 itakuwa imegunduliwa katika Kitalu namba 7( block 7) ambacho kipo mkoani Dar es Salaam katika Wilaya ya Temeke. Iwapo gesi nyingi hivi itakuwa hapa Dar karibu kabisa na mitambo ya kuzalisha umeme, mradi huu wa Bomba unaojengwa kwa trillioni za shilingi utakuwa na maana tena? Huu mkopo utakuwa na tija?
Serikali imewaambia watu wa Mtwara gharama za kuleta bomba Dar dhidi ya gharama za kujenga mtambo wa kuzalisha umeme Mtwara na kuusafirisha umeme kwenda maeneo mengine ya Tanzania? Serikali imeangalia faida ya kujenga gridi nyingine badala ya kuwa na gridi moja tu yenye kushikwa na bwawa la Mtera? Leo bwawa la Mtera lisipozalisha hata megawati moja hata Dar es Salaam izalishe megawati alfu kumi umeme hautakuwapo maana uti wa mgongo wa gridi ni Mtera! Kwa nini tusiwe na gridi nyingine yenye uti wa mgongo Lindi au Mtwara?
Picha zote kwa hisani ya Said Msonga
Tuwasikilize watu wa Mtwara
Watanzania sio mabwege tena. Kuwaita watu wa Mtwara ni wahaini, wapuuzi au watu hatari haisaidii kujenga Taifa moja lenye watu huru. Serikali na wadau wote wa sekta ya Gesi likiwemo Bunge washirikiane na watu wa Mtwara kuhusu miradi ya gesi asilia. Tuwe na Azimio la Mtwara, tamko la kuelekeza namna bora ya kutumia utajiri wetu wa Gesi bila kuathiri umoja wa Taifa letu.
Ujio wa Sera, Maono na Uongozi Mbadala
Sasa hivi wananchi wa Mtwara kama wananchi wa sehemu nyingine wanahitaji maono mbadala, uongozi mbadala, sera mbadala na mwelekeo mbadala wa kitaifa ambao utaangalia mahitaji yao, utazingatia raslimali zilizopo na utaunganisha utendaji wa sekta mbalimbali katika kutengeneza mfumo wa kiutawala na kiuchumi ambao utaliinua taifa zima.
Ni kwa sababu hiyo naamini chama changu ni jibu sahihi kwa matamanio na kiu ya wananchi wa Mtwara na sehemu nyingine nchini. Ikumbukwe kuwa katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya 2010 tulielewa haja ya kuangalia mikoa hii ya Kusini kwa namna ya pekee na kuipa mwelekeo wa kipekee katika sera.  Bado tuna makusudio hayo tunapoelekea 2015 na tukishika Dola wananchi wa Mtwara na sehemu nyingine zote zilizoachwa pembezoni mwa mafanikio wajue kuwa wamepata rafiki na mshirika wa karibu wa kushirikiana nao kuleta maendeleo.
Siyo katika suala la gesi tu bali katika nishati, maji, elimu, miundombinu, kilimo, ufugaji, uvuvi, utalii. Mtwara kama ilivyo mikoa mingine ina raslimali za kutosha kuweza kuwainua wananchi wake kimaisha, na zaidi ya yote kutoa mchango mkubwa wa kiuchumi. Hili ambalo ni kweli kwa Mtwara ni kweli kwa mikoa mingine kama Kigoma, Manyara, Katavi, Lindi n.k.
NB: ZITTO KABWE ni mbunge wa Kigoma Kaskazini kupitia Chadema.