April 22, 2013

UVUMILIVU WA KISIASA BUNGENI


Edgar Mwandemani, Dar es salaam
Na Edgar Mwandemani, Dar es salaam

Inaelezwa kuwa matokeo ya haya yanayoendelea hivi sasa katika siasa za Tanzania (kuzomeana, matusi na kukashfiana) ni, pamoja na mambo mengine, ukosefu wa uvumilivu wa kisiasa. Sitaki kusema tafsiri hii ni kweli ama si kweli. Pamoja na kwamba neno hili 'Uvumilivu wa Kisiasa' ni zuri linapotamkwa na wakati mwingine humwenyesha aliyelitamka ni mstaarabu, mwenye busara na asiyependa makuu.

Katika muktadha wa siasa za Kiafrika, Tanzania kwa upekee, utamaduni huu umetumika kama silaha ya kuadhibiana miongoni mwa makundi hasimu katika siasa. Kwa upande wa chama tawala kimekuwa kikiwashutumu mahasimu wake kwamba ni kutokana na uchanga wao katika siasa ndio maana wanafanya hayo wayafanyayo. Imefika hatua katika siasa za kibunge, spika wa bunge la Tanzania amewahi kusema vurumai zilizotokea mwaka jana bungeni ni matokeo ya utoto wa wabunge wa upinzani.

Kwa upande mwingine wale wa upinzani wameendelea kujitetea kwamba wanayafanya wayafanyayo katika kutekeleza ile haki ya kimsingi ya kikatiba ya 'uhuru wa maoni' na 'kusimamia maslahi ya umma'. Na kwamba juhudi zozote za kuwanyamazisha ni kuminya uhuru huo. Ili mradi kila upande unajitetea kwa namna yake!

Profesa S.S Mushi anatafsiri dhana hii kuwa ni "...harmonization of diversity or the extent to which public authorities accommodate divergent views in political governmental processes". Kwa ujumla wake ni kuvumila mawazo ya tofauti bila kujali nani ameyatoa. Lakini kuvimila mawazo/maoni tofauti si sawa na kumilia lugha chavu/matusi mbele ya jamii; kwa hivyo kwa muktadha wa yanayotokea hivi sasa hapa nyumbani, waheshimiwa hawa kwa maoni yangu hawatofautiani maoni/hoja bali tafsiri ya maneno machafu/matusi.

Aidha, Mushi anaendelea kueleza kuwa dhana hii 'uvumilivu wa kisiasa' chanzo chake ni mambo makuu mawili. Moja, ni kiwango cha mgawanyiko kilicho katika jamii yenyewe. Mgawanyiko wa makundi mfano, makabila, dini, rangi na kitaasisi unamchango mkubwa kujua kiwango cha 'uvumilivu wa kisiasa'. Jambo la pili ni, Tabia na sera za asasi za umma; kwamba ziko zile zinazowaleta pamoja raia na zingine huwagawa.

Tulipofikia jamii ya watazania imezama katika dimbwi la mgawanyiko. Hivi sasa mgawanyiko wa kidini, kimakabila, kimaeneo, makundi rika, jinsia na itikadi za vyama umeendelea kuliguguna taifa letu kiasi cha kusababisha mafarakano, magomvi na vifo katika maeneo fulani. Watu wamevaa tofauti zao kama silaha dhidi ya wenzao, hakuna tena umoja wa kitaifa. Bahati mbaya ni kuwa mambo haya yamechochewa na fikra za kipumbavu miongoni mwa makundi hayo; fikra za kujiona kila mmoja ni bora dhidi ya mwingine. Vyama siasa kwa mfano, vimedhani kwa muda mrefu, rangi zao za bendera ndio utanzania: kila chama kinataka kupuuza uwepo wa kingine!

Taasisi nazo si haba. Nyingi zake zimeendelea kuendeshwa kwa tabia na sera zinazochochea migawanyiko katika jamii. Tukichukua mfano wa Bunge letu hivi sasa; mijadala mingi inayoendeshwa humo imekuwa ikijikita katika kuonyeshana ubabe na ununda wa vyama vya siasa. Kwa upande wa chama tawala wamekuwa hawaheshimu wala kuzingatia maoni ya wale wengine kwa kisingizio cha wingi dhidi ya uchache. Upinzani nao kwakisingizio cha 'kusimamia mabadiliko' na 'uhuru wa maoni' wamekuwa wakijiona wao ndio kila kitu na kwa kuwa wamekuwa wakipuuzwa basi ni vitimbi.

Bunge limebaki kuwa mahali pa vihoja badala ya hoja; na kwa mwenye kihoja kikubwa ndio wa maana kuliko mwenzake. Katika mazingira haya itakuwa si kweli kudai kuwa siasa za Tanzania zimekosa 'uvumilivu wa kisiasa' kwani kilichopo hivi sasa ni vihoja uvumilivu utatoka wapi? Hakuna wa kuvumilia vihoja!

Kama kweli tunataka kuwepo na 'uvumilivu wa kisiasa' lazima tujitafakari juu utamaduni wa siasa zetu. Siasa ni matokeo ya utamaduni wa maisha ya kila siku katika jamii. Tusipoujenga tutarajie vurumai zaidi katika maeneo mbalimbali!

No comments:

Post a Comment

Maoni yako