October 13, 2009

BURIANI FRED NDUNGURU

"Markus! nipo Makambako naelekea Mbinga, Fred amefariki dunia!"
Napoke ujumbe huu saa kumi na mbili na dakika 27, jana jioni. Ni Yasinta rafiki yangu kipenzi, anasononeka sana, uchungu umemjaa moyoni-anasafiri kwenda kumzika kaka yake FRED AUREUS NDUNGURU.

Baada ya taarifa hiyo navuta taswira ya Fred, namkumbuka nikiwa sekondari Lundo, nakumbuka upenzi wake katika kiondoko ya Hip Hop! nakumbuka falsafa zake ambazo zilambatana na msimamo thabiti. Nakumbuka wakati ule tukitumia muda mwingi kusikiliza santuri ya DUDUBAYA ya SASA NI SAA YA KUFA KWANGU. Nakumbuka hisia za mwanamuziki huyo Godfrey Tumaini au Dudubaya. tunatumia muda kukariri mashairi yake, tunacheka kwa harara na mashmsham!

Ingawa hakuwa mpenda soka kama mimi, lakini yeye alipenda kunywa kileo kidogo lakini kwangu kileo ilikuwa mwiko na mwiko hadi sasa. Nakumbuka pamoja na hayo urafiki wetu haukuweza kuvunjika. Nakumbuka sana soga,michapo,gumzo na mambo mengi tu mazuri. Mabaya yote namwomba mungu amsamehe sana.

Nimefadhaika na kuhuzunika sana kutoweka duniani kwa FRED NDUNGURU kijana mchangamfu, msomi na mwenye msimamo mkali ambao hata baba yake alikuwa akishangaa sana. Nakumbuka pamoja na mbwembwe zake lakini alikuwa mkali katika Fizikia,Kemia na hisabati(PCM). Alijua namna ya kukabiliana na changamoto, alikubali kubeba lawama kwa maamuzi anayochukua.

Kikubwa zaidi alikuwa karibu kwa kila mmoja wetu tena kwa msimamo mkali kama humpendi naye hakupendi ndiyo sera zake. Nakumbuka mengi tukiwa Lundo sekondari huku yeye akiwa kidato cha sita pale Meta high school. Aliweza kusimamamia msiamamo wake mara nyingi tu kuhusu mwenendo wake ambao ulimkwaza hata baba yake, lakini alieleweka vema.
BURIANI FRED NDUNGURU, mungu akulaze mahali pema peponi. Malaika wake wakulinde daima kaka, ulitupenda kwa mengi sana, umetuacha tukiwa hatujakulipa upendo wako. Nawe YASINTA AUREUS NDUNGURU usilie sana, kaka amekwenda mbele za haki.
SOTE TUNAMWOMBEA MEMA. amen.

5 comments:

  1. Poleni sana wafiwa. Mungu awafariji, na amweke marehemu mahali pema Peponi. Amina.

    ReplyDelete
  2. Pole Yasinta wajina wangu, wafiwa wote, marafiki na jamaa wote. Marehemu astarehe kwa amani. Amina

    ReplyDelete
  3. pole ndugu yetu. kwa sasa tumuombe mungu akurejeshee imani, akujaze subira, akumiminie usahaulifu na akuzawadie ujasiri katika kipindi hiki cha kumpoteza rafiki wa karibu namna hii. pole.

    ReplyDelete
  4. Poleni Wafiwa!Kama kuna Mungu basi amfanyie kitu bomba!

    ReplyDelete
  5. pole kaka.

    karibu nyahbingiworrior.blogspot.com

    tukubaliane kwa kuto kubalianana.

    ReplyDelete

Maoni yako