March 19, 2013

GEOPOLITICS: YA RAIS AL BASHIR KUMNUSURU UHURU KENYATTA?


Markus Mpangala
IWAPO Raila Odinga wa Muungano wa CORD atashindwa kesi yake ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa Kenya, basi Uhuru Kenyatta ataapishwa kuwa Rais wa nchi hiyo. Bahati mbaya zaidi, suala linalojitokeza sasa ni namna diplomasia ya Kenya itakavyokuwa hapo baadaye.

Kuna nchi zimempongeza Uhuru Kenyatta kwa kupata ushindi; Tanzania, Zimbabwe, Afrika Kusini, Rwanda na Uganda, huku Marekani ikikwepa kutaja jina lake. Si hoja kuu kujadili uamuzi wa serikali ya Barrack Obama kukwepa kumtaja Uhuru Kenyatta.

Pamoja na hayo Uhuru Kenyatta na William Ruto wamefunguliwa mashtaka katika Mahakama Kimataifa ya Uhalifu(ICC). Hata hivyo, kesi yao itaendeshwa mjini Arusha hapa nchini baada ya serikali kukubali maombi ya ICC kuwa nchi mwenyeji. Mjadala mkubwa uliopo ni juu ya diplomasia ya Kenya  chini ya Uhuru Kenyatta na William Ruto ambao walikuwa wakiungwa mkono na Mwai Kibaki, huku Daniel Arap Moi akimuunga mkono Musalia Mudavadi.

Kote Afrika kuna mazungumzo kila kona wakihoji jinsi Uhuru Kenyatta anavyoweza kuwaumiza wananchi wa Kenya ikiwemo suala la kuwekewa vikwazo. Kwanza tunatakiwa kutambua Uhuru Kenyatta alipigiwa kura kihalali na aliingia kwenye mchakato wa kugombea urais kwa njia halali kabisa baada ya Mahakama Kuu nchini Kenya, chini ya Jaji Willy Mutunga kutupilia mbali madai ya kuzuiwa kwa wanasiasa hao kugombea urais.

Uhuru Kenyatta
Tangu wakati huo kuliibua hofu, lakini kulingana na siasa za Kenya, ukabila umeshika kasi hivyo makabila ya Kalenjin na Kikuyu yanaonekana kushinda uchaguzi huu baada ya William Ruto (mkalenjin) na Uhuru Kenyatta (mkikuyu) kushika madaraka. Hivyo hadi leo diplomasia ya Kenya inaelekea kuleta mjadala na kudhaniwa kunaweza kutokea mgogoro na nchi za kigeni hivyo kuhatarisha maisha ya wakenya.
Lakini muhimu ni kufahamu kuwa Kenyatta alipigiwa kura na wakenya, hivyo ulikuwa uamuzi wao juu ya kumchagua au kumwacha. Jambo la kuelewa hapa ni kwamba Uhuru Kenyatta anaingia kwenye nafasi ya urais (iwapo Mahakama haitabatilisha matokeo) akiwa na swahiba wake William Ruto.

UMOJA WA AFRIKA vs ICC
Umoja wa Afrika utalazimika kufikiria zaidi juu ya suala la Uhuru Kenyatta na Raila Odinga. AU inaendesha Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika (African Court on Human and People’s Right), yenye makao makuu mjini Arusha.  Mahakama hii iliidhinishwa nchini Ethiopia na kugharamiwa na serikali ya Tanzania. Dhumuni la Mahakama ya ACHPR ni kuwa na Mamlaka ya kusikiliza na kuzitolea uamuzi kesi za makosa ya Jinai sawa na Mamlaka ya Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (uhalifu wa vita na haki za binadamu) yaani ICC (International Criminal Court) yenye makao makuu The Hague, Uholanzi.  

Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika (ACHPR) inaongozwa na Jaji Gerald Niyungeko (Rais wa Majaji), Jaji Sophia Akuffo (Makamu) Jaji Elsie Nwanuri na Jaji Robert Eno (Msajili wa Mahakama hiyo).  Kwa mujibu wa AU, Mahakama ya ACHPR itakuwa na mamlaka kamili ya kutolea uamuzi wa; (i). Makosa dhidi ya Ubinadamu (Crimes against Humanity), (ii). Makosa ya kivita (War Crimes) na mamlaka yote ya kusikiliza makosa ya Jina.
Aidha, kulingana na uanzishwaji wa ICC, kuna kesi ambazo zinatolewa uamuzi The Hague, Uholanzi, lakini zinaweza kufanyiwa uamuzi na Mahakama ya Haki za Binadamu inayofanya kazi barani Afrika mjini Arusha, Tanzania. Madhumuni ya ICC ni; (i). kusikiliza makosa ya ukandamizaji (Crime of Genocide), (ii). Makosa dhidi ya Ubinadamu (Crimes against Humanity), (iii). Makosa ya Kivita (War Crimes), (iv). Makosa ya Uchokozi (Crime of Aggression), (v). Makosa ya uvunjaji wa Sheria za Kimataifa.

Mahakama ya ICC ilianzishwa rasmi mwaka 2002 baada ya makubaliano yaliyofanyika mwaka 1998 kwa kazi tulizoainisha hapo juu. Kuundwa kwa ICC ni zao la Mkataba wa Roma (Rome Statue) wa Julai 1, 2002. Kumekuwa na shutuma nyingi dhidi ya Mahakama ya ICC, lakini sasa bara la Afrika limeamua kujibu mapigo kwa kufanya kweli na kuanzisha  Mahakama yao. Mwaka 2009, Mahakama ya ICC ilianzisha mchakato wa uchunguzi wa uhalifu wa kivita katika nchi za DRC, Sudan, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Kenya, Afghanistan, Colombia, Ivory Coast, Chad na Georgia. ICC iliamua kutoa hati ya mashtaka dhidi ya Rais Omar Al Bashir kwa madai anahusika na mauaji ya yanayofanyika katika jimbo la Darfur, Sudan.
Aidha, ICC ilimhusisha Rais Bashir na wanamgambo wa Janjaweed. Kwa mujibu wa Ripoti yake, ICC ilisema Sudan siyo sehemu ya Mahakama ya Uhalifu wa Kimataifa (ICC kulingana na Mkataba uliounda Mahakama hiyo), hivyo kiongozi wake (Bashir) hawezi kukamatwa kwa mfumo wa Mahakama hiyo. Lakini ICC ikasema inachukua jukumu la kumtia mbaroni Rais Bashir kulingana na uamuzi wa Baraza la Usalama (United Nation Security Council) Namba.1593 la Machi 31, 2005, kutokana na hali ya maafa ya jimbo la Darfur. Azimio hilo linalofanya kazi chini ya Sura ya VII ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa (UN) ndilo lilitumiwa na ICC kutaka kumkamata Rais Bashir kulingana na hali mbaya ya Jimbo la Darfur.
Jean Ping, Mkuu wa zamani wa Tume ya Umoja wa Afrika
Wanachama 11 waliounga mkono azimio hilo, halafu China, Algeria na Brazil zikapinga. Hata hivyo, uamuzi wa ICC unadaiwa kuchochewa zaidi na Marekani ambayo siyo mwanachama wa Mahakama hiyo, bali ilitumia nafasi yake ya mwanachama wa kudumu wa Baraza la Usalama, na mvuto wa ICC katika hatua zake za kulinda haki za Binadamu. Hivyo kikao cha 111 cha ICC kikaidhinishwa kukamatwa kwa Rais Bashir. Lakini kwa upande wa nchi za Afrika kupitia Umoja wa Afrika zilipingana na ICC, huku zikishutumua ICC kuchukua mkondo wa nchi za kibeberu kuingilia kadhia ya Darfur.

Hati ya kukamatwa Rais Bashir ilitolewa Machi 4, 2009 haiwezi kutekelezwa kwa namna yoyote kwa mujibu wa AU hali ambayo ilileta malumbano makali. Malumbano yalichochewa zaidi baada ya serikali ya Marekani kutangaza kuunga mkono Rais wa Sudan kufikishwa The Hague. Taarifa za serikali ya Marekani zilitolewa na Robert Wood, Hilary Clinton na mwakilishi wa Marekani nchini Sudan, Jenerali Scot Gration ambao waliwakilisha maoni ya serikali yao kuhusu Hati ya kukamatwa kwa Rais Bashir. Awali  mwaka 2007, ICC ilitoa Hati ya kukamatwa kwa waziri mmoja wa zamani wa serikali ya Sudan.

UMOJA WA AFRIKA ULIVYOMTETEA RAIS BASHIR
Ripoti ya Januari 9, 2012 ilieleza waziwazi hatua ya ICC kumkamata Rais Omar al Bashir ni batili.  AU ilipinga hatua ya ICC kuzishinikiza nchi za Malawi na Chad kutoa “maelezo”  kwanini ziliruhusu Rais wa Sudan, Omar al Bashir kuzitembelea huku zikifahamu kuwa ICC imetoa Hati ya kukamatwa kwao. AU ilikosoa kwa vipengele vya sheria iliyotumika na ICC kuzishinikiza  kutoa “maelezo” kwa nchi za Chad na Malawi. Taarifa ya AU yenye Kumb. Namba. 002/2012, iliyojibu taarifa mbili za ICC;- Mosi ni taarifa yenye  Kumb. Na. CC-02/05-01/09-139, pili; yenye  Kumb. ICC-02/05-01/09-140 Desemba 12 na 13, 2011, inaeleza kwanini haikubaliani na uamuzi wa ICC.

Lakini  ICC ilieleza kuwa hatua za Malawi na Chad kumkaribisha Rais Bashir ni kukiuka Ibara ya 87(7)  ya ICC, pamoja na Baraza la nchi wanachama pamoja na Baraza la Usalama wa Umoja wa Mataifa. Aidha, ICC ilisema Malawi na Chad zilikiuka Ibara ya 27(2) na 98(1) zilizounda Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu kwa Mamlaka ya Kiongozi wa nchi kutekeleza agizo la ushirikiano na Mamlaka ya ICC.

Kwa hiyo ICC,  ilikuwa ikimshutumu marehemu Bingu wa Mutharika wa Malawi (Joyce Banda alibadilisha baadaye) na Idrissa Derby wa Chad wanadaiwa kukiuka Ibara ya 98(1) kwa kutotimiza “agizo la ushirikiano” kwa mamlaka yao mbele ya ICC. Hata hivyo, Umoja wa Afrika haukuweza ulisema Malawi na Chad ni wanachama wa AU wapo chini ya Ibara ya 23 (2) ya Sheria (Constitutive Act) ambayo inawataka nchi wanachama kuheshimu na kuzingatia Sera zinazounda Umoja wa Afrika.  
AU ikasema kulingana na Ibara ya 27(2) ambayo inaelezea taratibu maalumu za uundwaji wa ICC;- kwamba hatua zozote za kisheria zinazochukuliwa lazima zizingatie nafasi ya mhusika iwe kitaifa au kimataifa, hivyo mahakama haitakiwa kuingilia suala hilo. Ibara hiyo inajieleza kuwa ni ‘taratibu za jumla za Jinai’ lakini hatua zozote za kisheria hazichukuliwi kama kigezo cha kumkamata mhusika, vinginevyo kulingana na uhusiano baina ya ICC dhidi ya mtuhumiwa (Rais Bashir/Uhuru Kenyatta) kama inavyoelezwa kwenye Ibara ya 98(1).

Ibara hiyo inasema mamlaka ya jumla, hatuwezi kusema Mahakama za ndani hazijumuishwi, hivyo lazima ICC inatakiwa kuwa na adabu mbele ya sheria za Kimataifa (Interanational Law Helsinki Final Act) na sheria za Mahakama ya ndani. Kwa mantiki hiyo, hapa tunajikuta tukimleta Uhuru Kenyatta ambaye ni mshtakiwa wa ICC, je, atalindwa na Constitutive Act kama ilivyokuwa kwa Rais Bashir? Labda tofauti iliyopo Kenya ni mwanachama wa ICC na Sudan sio mwanachama wa mahakama hiyo. Pia Uhuru Kenyatta ameshtakiwa akiwa mwanasiasa wa kawaida sio mkuu wa nchi kama sheria za Umoja wa Afrika zinavyoagiza. Ni mtihani kwa diplomasia ya Kenya na Afrika.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako