March 02, 2018

KUTOKA CHINA HADI CHUO CHA TEKNOLOJIA DAR ES SALAAM (DIT)

NA KIZITO MPANGALA
DUNIANI kuna ubunifu wa namna mbalimbali unafanyika katika teknolojia ili kurahisisha shughuli mbalimbali katika maisha yetu ya kila siku. Ubunifu wa kiteknolojia umekuwa ni lulu mojawapo katika ulimwengu huu wa Sayansi na Teknolojia hasa katika umeme na elektroniksi, ingawa upo ubunifu mwimgine nje ya uga huu wa umeme.
Kiti cha magurudumu manne ni kifaa cha muhimu sana kwa wagonjwa katika hospitali mbalimbali duniani. Na ubunifu mbalimbali hufanyika ili kuboresha utendaji wa kiti hiki. Kiti hiki kwa sasa kina magurudumu manne ambapo makubwa mawili na madogo mawili na hutegemea nguvu za mgonjwa kama anaweza kukisukuma yeye mwenyewe na kama hawezi basi anasukumwa na mtu mwingine.
Tofauti na baiskeli ya magurudumu matatu, kiti hiki kina ukubwa ambao unatosha kwa mtu mmoja tu kuketi na anayesukuma hulazimika kuembea. Vilevile hakichukui nafasi kubwa. Hakiwezi kutumika kama njia mojawapo ya usafiri barabarani kama ilivyo baiskeli ya magurudumu matatu inayotumiwa na walemavu wengi duniani kote.
Kiti hiki kilianza kubuniwa nchini China mnamo karne ya tano na baadae nchini Ugiriki mnamo karne ya sita ambapo kilibuniwa kwa ajili ya kubebea watoto na wazee wasioweza kutembea na kisha kuwasukuma ili kuwafikisha sehemu waliyokusidia. Nchini China awali walikuwa wakitumia matoroli kwa ajili ya kuwabeba wazee wasioweza kutembea na pia vilema na vilevile kubebea mizigo mizito. Michoro ya kiti cha magurudumu mawili iliyochorwa nchini China ilionekana mwaka 525 B.K huko Ulaya.
Ulaya wakachangamka na wakaunda viti vya namna ile kwa wingi. Lakini baadaye ubunifu huu ulipotea ghafla na watu wakapuuzia kuutekeleza hadi kufikia mwaka 1595 kilipoonekana kiti cha namna hiyo ambacho kilitumiwa na Mfalme Philipo wa II wa Hispania. Aliyekitengeneza hakujulikana.

Wabunifu wengi waliona kwamba kiti hiki kina mapungufu fulani licha ya kuwa na sehemu ya kuegemeza miguu na sehemu ya kuegemeza mikono. Wabunifu hao walikosoa kutokuwepo kwa mfumo binafsi wa kiti hicho kujiendesha au kuendeshwa na mtu mwenyewe aliyeketi kitini hapo kwa sababu kama vilivyo viti vingi katika hospitali nyingi sasa, huhitajika mtu wa ziada kusaidia kusukuma ili kumfikisha muhusika sehemu aliyokusudia kwenda.
Mwaka 1655, Stephan Farffer, kiajana aliyekuwa na miaka 22 na fundi saa, alitengeneza kiti cha kwanza cha magurudumu manne kinachojiendesha kwa kuongozwa na mtu aliyepanda kitini hapo. Mfumo huo alioutumia ni kama ulivyo sasa katika baiskeli za walemavu ambazo wanapiga pedali kwa mikono.  Na mwaka 1760, viti vya aina hii ya Stephan Farffer vilikuwa vikiundwa kwa wingi kwa ajili ya wasiojiweza.
Mwaka 1887, katika kitongoji cha Atlantic mjini New Jersey nchini Marekani, viti hivi viliundwa kwa wingi kwa ajili ya watalii kubebea mizingo na vingine kwa ajili ya kupumzikia tu huku kikiserereka.
Mwaka 1933, Harry Jennings Mdogo (Sr), na rafiki yake Herbert Everest ambaye alikuwa kilema, wote wakiwa wahandisi wa umakanika, waliunda kiti cha kwanza ambacho ni chepesi na cha kukunjwa, yaani unaweza kukikunja na kubeba kwa urahisi. Everest alikitumia kiti hiki kutokana na kutoweza kutembea vizuri kwa kuwa alipata tatizo hilo akiwa machimboni. Jannings na Everest wakaona kwamba biashara yao hii imepokelewa vizuri na watu wengi, wakafanya maboresho zaidi.
Viti hivyo vipo vya aina mbalimbali kwa sasa kulingana na matumizi yake lakini kubwa ni kwa wasioweza kutembea. Hospitali nyingi duniani zina viti hivi kwa ajili ya wagonjwa wanaopata shida za kutembea au wanaweza kutembea lakini kutokana na matibabu hulazimika kuwa na utulivu wa mwili, hivyo hutumia viti hivi ambavyo wengi huuta baiskeli, kwa ajili ya kufika sehemu inayokusudiwa.
Leo tunaye mwanafunzi ERASTO CHISANU wa shahada ya uhandisi wa umeme katika chuo cha teknolojia jijini Dar es Salaam (DIT) ambaye ametengeneza kiti cha aina hiyo kinachotumia umeme.
Erasto alipata wazo hili kutokana na mateso aliyokuwa yakimpata bibi yake katika kutembea. Bibi yake ana shida ya miguu, hivyo hawezi kutembea kwa ufasaha sana jambo ambalo linampa maumivu ya miguu mara kwa mara anapotembea. Ndipo Erasto kwa utambuzi wake kuwa ni mhandisi anayenolewa, akaandika muswada wa ubunifu wake huu na kuuwasilisha katika idara ya kozi ya uhandisi wa umeme na kisha kuanza kazi ya kutengeneza kiti hichi mara baada ya muswada wake kupitishwa.

Erasto alilazimika kuomba ushauri wa kitaalamu kwa madakitari katika hospitali ya taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam. Alieleza wazo lake na madakitari wakamshauri kuhusu kimo cha kiti hicho. Hapo Erasto akaongeza wazo kwamba kiti kitakuwa kina uwezo wa kupanda na kushuka kinapoongozwa na mtumiaji.
Kiti hicho ambacho kukamilika kwake kimemgharimu zaidi shilingi za Tanzania milioni mbili, kinaongozwa na mfumo wa kielektroniki na kinaweza kupandishwa na kushushwa wakati mtumiajai akiwa bado kitini hapo. Kama kingekuwa na lengo la kutumika hata barabarani kwa ajili ya usafiri basi ingekuwa rahisi kwa yeyote kukitafuta na kutmia kwa sababu kiti hicho ambacho kinatumia umeme, kina betri inayohifadhi chaji inayoweza kutumika kwa umbali wa KILOMETA 30 na kisha kuchajiwa tena. Sasa kwa matumizi ya kawaida tu kwa mgonjwa aliyepo nyumbani au hospitalini, chaji hiyo inaweza kudumu kwa muda mrefu sana.

Erasto anaeleza changamoto kubwa aliyoipata ni wanafunzi wenzake wengi kumwambia kuwa hataweza kwa sababu jambo hilo lingemgharimu muda mwingi na hivyo angefanya vibaya katika masomo darasani. Lakini Erasto Chisanu hakujali maelezo hayo, aliweka wazo lake mbele na kulifanyia kazi. Mpaka sasa kiti kipo tayari, na malengo yake ni kuunda vingi zaidi ili viweze kusaidia watu wengi wenye kuhitaji viti. Pia, mwalimu mkuu wa chuo alichopo ametoauamuzi wa kumrudishia gharama ya fedha zote ambazo alitumia katika kufanikisha ufundi huu. Hii ni kutokana na kukubalika na wengi kwa kiti hicho ambacho madakitari wa hospitali ya taifa ya Muhimbili wamempongeza kwa kazi hii na kumpa hamasa ya kuunda vingi zaidi.    
© KIZITO MPANGALA (0692 555 874)

No comments:

Post a Comment

Maoni yako