April 04, 2013

KIKUNDI CHA HABARI CHAKUTANA KUWEKA MIKAKATI


Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam

NAIBU Waziri wa Sheria na Katiba, Angellah Kairuki amewataka wanachama wa kikundi cha waandishi wa habari cha kujikomboa kiuchumi (Habari Group) kupendana na kuaminiana ili kukifikisha kikundi hicho mbali.


Kairuki ambaye pia ni mlezi wa Habari Group, alikitaka kikundi hicho kutokuwa wachoyo wa kusaidia waandishi wa habari wengine wenye nia ya kuungana na kufanikiwa kimaisha.

Akizungumza na kikundi hicho Dar es Salaam juzi, alisema ili mtu afanikiwe ni lazima awe mwenye upendo na kusaidia wengine pale penye mwanya wa kufanya hivyo na kuwataka wanachama wote kuwa na moyo wa kujitolea kwa ajili ya kikundi.  "Sitopenda kusikia kikundi hiki kimekufa kwa sababu ya mifarakano na chuki miongoni mwenu kwani kwa kufanya hivyo hamtofikia malengo mliyokusudia," alisema Kairuki.


 Aliongeza kuwa wakati anaingia madarakani aliweka vipaumbele kwa wafanyakazi wa majumbani, madereva wa aina zote, wafanyakazi wa mashambani, wahudumu wa baa na nyumba za wageni, walinzi na waandishi wa habari.  Na kwamba ameanza kushughulikia haki mbalimbali za makundi hayo, ambapo kwa sasa wapo kwenye mchakato wa kuishinikiza serikali kusaini mkataba wa kuridhia haki za wasichana wa majumbani.

Aliwapongeza waandishi wa habari kwamba pamoja na changamoto nyingi wanazokutana nazo, lakini hawakati tamaa na wamekuwa wakifanya kazi yao kwa moyo mmoja na kwa bidii. 

Kama mkakati wake wa kuwasaidia waandishi wa habari, alisema atasimamia Habari Group ili wawe mabalozi wazuri kwenye mambo mbalimbali kwa jamii, ikiwemo kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali, kuwapa elimu ya umuhimu wa cheti cha kuzaliwa, sambamba na kushirikiana nao bega kwa bega kwenye mambo muhimu ya kijamii.

"Kuwasidia kwenu ni miongoni mwa malengo yangu niliyojiwekea ya kupigania haki ya baadhi ya makundi ambyo nimeona haki zao kama wafanyakazi hazitekelezwi,"aliongeza.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako