April 03, 2013

KIM POULSEN ANASTAHILI MKATABA MNONO TAIFA STARS



Hivi karibuni kocha mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen ametoa mipango mizuri kwa maendeleo ya soka. Kim ameliambia shirikisho la soka nchini kuwa anahitaji kuona kikosi cha timu ya taifa ya vijana Serengeti Boys ikishiriki michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara. 

Kocha Kim anasema, mpango wake ni kutaka kuona wachezaji hao wanakuwa wanacheza mechi za ushindani kwa kila wiki ya mwezi ili kuweza kujijenga kiushindani na kimbinu. Kwa mujibu wa kocha huyo, anasema kama wachezaji wa Serengeti Boys wataweza kucheza mechi moja kwa wiki, kisha wakafanikiwa kushiriki michuano yote ya Ligi Kuu basi hakuna shaka kabisa watakuwa kwenye ushindani mkali watakapopewa nafasi ya kuchezea timu ya wakubwa.
Kocha Kim anasema, wachezaji hao vijana wanatakiwa kuchezea timu ya taifa kwa muda kisha wakifikisha umri wa  kuvuka Serengeti Boys basi watarudishwa kwenye klabu zao ili kupisha wengine waweze kutumika katika kikosi hicho na kushiriki michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Dhumuni la kocha huyo ni lilelile kuwafanya wachezaji wengi vijana wakipata nafasi na kucheza soka la ushindani wakati wote. Pia kocha Kim anakusudia kujenga kikosi bora cha miaka ijayo hivyo hakuna wasiwasi kuwa kati ya mwaka 2015 au 2017 tanzania inaweza kabisa kushiriki michuano ya Kombe la mataifa ya Afrika pamoja na kombe la dunia mwaka 2018 nchini Russia au 2022 nchini Qatar. 

Nilipotafakari programu hiyo upesi nikakumbuka namna kocha Marcio Maximo alivyoweza kuishirikisha timu ya taifa ya vijana kwenye michuano ya kombe la taifa ambalo linashirikisha mikoa yote ya jamhuri ya muungano wa Tanzania. Moja ya faida hizo ni kumjengea uwezo mshambuliaji wa TP Mazembe, Thomas Ulinwengu ambaye alishiriki kikamilifu kwenye michuano hiyo. 

Kwa wengine sasa wanaona Thomas Ulimwengu amekuwa mshambuliaji hatari na hodari zaidi, lakini njia alizopitia zimemjengea umakini na uhodari katika soka, ambako sasa anaweza kupambana na washambuliaji hatari klabuni kwake kama Kaluyituka, Given Singuluma, na wengineo. 

Kwa mtazamo wangu uamuzi wa kocha Kim kuliagiza shirikisho la soka nchini TFF kuhakikisha Serengeti Boys inashiriki mechi za Ligi Kuu Tanzania bara kuna lengo moja tu kuhakikisha anakuwa na kikosi imara zaidi cha timu ya taifa ya wakubwa(Taifa Stars). 

Ukiangalia rekodi za kocha Kim na namna anavyoweza kujenga kikosi chake katika timu ya taifa, hakika amekuwa kocha wa kipekee sana. nasema hivi sio kwasababu ya matokeo mazuri, bali muundo wake wa utendaji kazi na namna anavyoweza kutufahamisha makosa yetu kwa hekima. 

Kim anajua kabisa tulichokosa ni misingi ya soka la vijana kwahiyo anachofanya ni kuhakikisha tunakuwa na hazina ya kutosha katika soka la vijana kupitia timu ya taifa. Wakati Kim akisema hayo wenyewe tunafahamu kuwa tuna michuano miwili muhimu sana ambayo inawajenga vijana lakini bado haionekani kuwa imara kiushindani. Mfano michuano ya Copa cocacola na michuano ya Uhai. 

Hii ni michuano inayohusisha timu za vijana ambazo kwa namna moja ama nyingine zinapata faida, lakini hakuna mwendelezo wake. Kwahiyo kocha Kim amegundua moja ya sababu za kushindwa kuwa na mwendelezo ni gharama za uendeshajiu, kwahiyo anaamua kupunguza gharama hizo kwa kuitumia timu ya taifa ili iweze kusaidia kuzalisha wachezaji imara. 

Pia anaikumbusha TFF kuwa hakuna njia ya mkato kama inataka wachezaji wazuri zaidi ya kuwekeza ikibidi shirikisho lenyewe kuwa na kituo chake. Kwa mantiki hiyo badala ya kuwkusanya vijana huko mitaani na kuwapeleka uwanja wa Karume, kocha Kim anatumia timu ya taifa kama mahali pevu ambapo pataleta hamasa kwa vijana na kuongeza ujuzi wao kipindi wakirudi kwenye klabu zao. 

Pili, hii itazisaidia timu zetu kama Yanga na Simba ambazo mara nyingi zimekuwa zikisubiri wachezaji walioko timu ya taifa ndio wawasajili. Namna gani kocha Kim ataweza kuwaendeleza wachezaji watakaofanya vema kwenye kikosi cha Serengeti Boys? Hilo litateguliwa kwa kumuongezea mkataba mpya ambao utamfanya ajikite zaidi kutengeneza timu imara za timu za taifa akishirikiana na makocha wazawa. 

Nimalize kwa kusema, hakuna jambo baya kama tutaruhusu kuondoka kwa kocha Kim Poulsen wakati huu ambapo ametuonyesha falsafa bora kabisa ya soka letu. Ni vyema TFF na serikali zinaona umuhimu wa kuongeza mkataba mnono kwa kocha huyu. Muhimu tuache blah blah katika hili.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako