November 07, 2013

ELIMU YETU MIKONONI MWA SHETANI


MARKUS MPANGALA (DAR ES SALAAM) NA HAPPY JOSEPH (CHANGCHUN, JILIN (CHINA).

WAKATI mwingine tunatakiwa kulalamika ka kila jambo kutokana na muktadha halisi. Tunapaswa kupiga kelele hata kama hazitakuwa na ufumbuzi, lakini angalau itakuwa inaweka rekodi sawa kwamba uamuzi uliochukuliwa hakuwa sawa. Kila mmoja anaweza kulalamika, na serikali inaweza kutuona  walalamishi zaidi, lakini kwangu mimi hili ni zaidi ya ulalamishi. Ni zaidi majuto. Ni zaidi hisia kali, kwamba tunajenga elimu ya namna gani kwa kizazi kijao. 
HAPPY JOSEPH katika pozi. Huyu ndiye nimeshirikiana naye kuandika makala hii kuhusu Elimu. Asante rafiki yangu kwa mawazo mazuri.
Kwanza tulianza kulalamikia eti kwamba mitihani ya kidato cha nne kuna watu wanapendelewa. Baadhi ya watanzania wenzetu wakapayuka mpaka kutoa povu midomoni ati mfumo wa elimu unawapendelea jamii au watu wa imani fulani. Kwangu mimi huu ulikuwa ujumbe tosha, matatizo yaliyolimbikizwa sasa yamekuwa shubiri na kusababisha kushindwa kufikiri sawasawa. 

Matatizo tuliyyalea kwa miaka mingi yamesababisha kutafuta majibu mengine ambayo hayana kichwa wala miguu. Matatizo ambayo yamelelewa kwa ustadi na kukabidhiwa mikononi mwa shetani (ujinga). Waama, elimu yetu tumeipeleka mikononi mwa shetani na hilo hakika sitachelea kusema. Akindika kwenye kitabu chake cha ‘Mwalimu Mkuu wa Watu,” Mzee wetu Pacsally Mayega, anasema, “Ndani ya kichwa mvivu ni karakana ya shetani, na mtu mvivu ni kama jiwe lililopakwa mav,”. 

Ni maneno mazito ambayo yanavuta hisia zangu kuona serikali yetu tukufu inadhani ‘Divison V’ ni moja ya ujanja mbovu kuboresha elimu yetu, badala ya kusema ukweli kwamba hilo ni daraja sifuri kwa watui waliofeli. Tabu ya nini kufika hili? 

Kwanini swerikali inajibebesha mzigo mzito kama huu? Naam, tuko mikononi mwa shetani, huku Bunge letu tukufu likiidhinisha watanzania kufikishwa kwenye pango la shetani. Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Profesa Sifuni Mchome alitutangazia madaraja mapya kwa mtazano wa serikali. 

Zamani tulikuwa na  A=80-100, B=65-79, C=50-64, D=35-49, F= 0-34 kwa upande wa kidato cha sita A=80-100, B=75-79, C=65-74, D=55-64, E=45-54, S=40-44 na F= 0-39. Naam, sasa serikali yetu sikivu imesema madaraja yatakuwa hivi; A=75-100, B+=60-74, B=50-59, C=40-49, D=30-39, E=20-29 na F=0-19, huku serikali hiyo ikisema kuwa daraja sifuri limeondolewa ili kuweka mlolongo mzuri. 

Waaooooo! Tumefika mahali kudhani mlolongo mzuri ndiyo mazingira mazuri. Tunashindwa kutibu maradhi na kuongeza ugonjwa mzito, ambao utatuchukua muda kuondokana nao. Kwamba shida yetu ilikuwa mlolongo mzuri ama tunatakiwa kupewa elimu bora?
Ni  kweli kwamba serikali imefanya vizuri kutuanzishia sekondari sisi watoto wa masikini tuliokulia ukanda wa ziwa Nyasa na wengineo kote nchi. Shule za Kata ingawa baadhi yetu hatukusoma lakini imewasaidia wale tuliowaacha nyuma kwani angalau wamepata elimu hata kama haina ubora unaotakiwa. 

Serikali ya CCM imeamua kwa dhati kabisa kutupeleka katika dimbwi la tabasamu la shetani na kudhani inaokoa kizazi hiki. Nchi yetu imeuwa ikijikita sana kwenye suala la Ilani za chama kama msingi wa maendeleo badala ya sera. 

Kilichosababisha kufutwa mitihani ya kidaoto cha nne ilikuwa Ilani ya CCM si sera ya Taifa letu. Kufutwa matokeo hakukuwa na maana kutabadilisha lolote kwani serikali yenyewe imejenga mazingira ya kila ya namna ya kuwa mchochezi namba moja kwa wananchi.
Katika hoja hii nilikumbuka maneno mazito ya rafiki yangu Happy Joseph aliyeko masomoni mjini Changchun, Jilin, nchini China akisema, “Hivi kama kocha ameona timu yake haifanyi vizuri (wachezaji wanapiga mashuti nje ya magoli), ataamua kupanua maagoli katika uwanja wa mazoezi? Je, katika mashindano na timu nyingine katika uwanja mwingine ategemee nini? 

Anaongeza kwa kusema, “Elimu ya sasa katika utandawazi huu si ya nchi Fulani, inapaswa kuwa na viwango vya kimataifa. Lazima mtu ashindane na wa mataifa mengine. Tanzania haiwezi kuwa na elimu yap eke yake, ndio maana tunapigwa change macho kwenye mikataba na mataifa mengine,”

Kama walivyo wadau wengine rafiki huyo huyu anatoa ushauri kwa serikali akisema, “Kwanza, Serikali ikae na wadau wa elimu kupitia tafiti za kielimu zilizofanywa na taasisi mbali mbali mfano Haki Elimu kuona matatizo ya elimu ni yapi, na mbinu gani zitumike kupandisha kiwango cha elimu  na si idadi ya ufaulu hewa. Pili, Serikali kuwekeza zaidi katika elimu; hakuna aisyefahamu kuwa hakuna Maabara, Maktaba, na walimu wenye nia katika shule za umma. Tatu,  Serikali itazame upya mtaala wa elimu, isiung'ang'anie, pia itazame mfumo wa elimu, kwamba ipi iwe lazima na ipi iwe ziada.

Aidha, anasema, serikali itazame maslahi ya Walimu na ubora wake.  Katika pendekezo hilo la mwisho ndiyo linanipa simanzi. Kwamba kujali maslahi ya Walimu ni suala gumu ambalo serikali imeshindwa kisheria na kiakili pia. Inaudhi kusema maneno hayo lakini hakuna namna nyingine, kwamba serikali imeshindwa kisheria japo iliagizwa hivyo na Mahakama Divisheni ya Kazi wakati ilipozuia mgomo wa Walimu kote nchini. Katika majadiliano yake na Chama cha Walimu, ilikubaliwa kuwa serikali itaongeza mishahara kwa kiwango cha asilimia 67. 

Lakini katika hali ya kustaajabisha serikali haikufikia kiwango hicho, bali ilikomea kwenye asilimia 24. Katika mkutano na waandishi wa Habari miezi kadhaa iliyopita, Rais wa Chama cha Walimu nchini, Gratian Mkoba alisema kuwa jambo hilo liliwasikitisha walimu huku serikali ikianza harakati za ‘Big Results Now’ ambayo iliitongoa huko Malaysia. 

Nia nzuri ya serikali haibezwi, lakini kinachogomba ni mtindo unaotumika kuendelea kuwategemea walewale wanaonyonywa na kudhani wanaweza kuleta mapinduzi. Walimu ndio wahanga wa unonyaji unaofanywa kwani kwa mujibu wa mazungumzo ya mezani kati yao na serikali ilikubaliwa malipo yao yafikie asilimia 67 kwa kile kilichoeelezwa kuwa nchi yetu haina fedha za kutosha. 

Labda, lakini kuomba kufika asilimia 67 kisha kushindwa kutimiza bila sababu zozote hakuna jingine zaidi ya kufikisha elimu mikononi mwa shetani. Mikono ambayo bila shaka itatuzalishia magaidi kutokana na ukosefu wa elimu wmafaka na yenye tija kwa maslahi ya taifa letu. Ni hatari kuichezea elimu kwa kiwango hiki halafu tukatarajia kukutana na wanazuoni waliokomaa. Asenteni kwa kunisoma.
Baruapepe; mwanazuoni27@gmail.com

@MAKALA HII IMECHAPISHWA GAZETI LA RAI, Novemba 7, 2013.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako