September 25, 2017

UCHAMBUZI WA KITABU; BUSARA ZA MZEE


KITABU: BUSARA ZA MZEE
MWANDISHI: TITUS AMIGU
MCHAMBUZI: KIZITO MPANGALA

BUSARA ZA MZEE ni kitabu chenye mkusanyiko wa aya mbalimbali ambazo zimekusanywa katika nyakati tofauti na kuwekwa kitabuni. Ni kiatabu ambacho kimechapishwa na Moccony Printing Press jijini Dar es salaam, Tanzania na kupata namba ya usajili ISBN 978 9987 9639 7 3 ambapo kimechapishwa katika kurasa 281.

Mwandishi anasema busara hizi amezikusanya na kuzieleza, na zile zinazoeleweka moja kwa moja basi ameziandika bila maelezo. Buasara hizi amezipata sehemu mbalimbali; amezipata kwa kuwasikia watu wakizungumza mara kwa mara, zingine amezipata kwenye magari alipokuwa akisafiri katika safari mbalimbali akiwasikia abiria wenzake wakipeana michapo, zingine amezipata vilabuni, zingine amezipata kwenye nguo kama vile kanga, zingine amezipata kwenye mabango ya pikipiki na bajaji na kadhalika. Zote ni busara.

Mwandishi amenuia kusema busara mbalimbali kwa watu wote kwa ujumla katika ulimwengu huu ili waweze kupata mafundisho ambayo hawatajutia kuyapata. Ni mafunzo yenye nia njema na yenye kujaa tafakari mbalimbali kulingana na ujumbe unaopatikana katika busara husika. Kwanza mwandishi anawaasa watu wote kumkalibia muumba wa mbingu na dunia hii ili wajazwe furaha na amani zaidi katika maisha yao.

Mwandishi ameandika busara nyingi, ni ngumu kuzieleza zote kila moja kwa nafasi yake. Lakini tutapata baadhi tu. Mwandishi anasema kama mtu anafanya jambo fulani lenye manufaa katika maisha yake basi alifanye kwa morali zaidi ili afaidi matunda yatokanayo na jambo hili kwa furaha na amani.





Kama ni mwanajeshi uwe mwanajeshi kweli, kama ni mfanyabiashara uwe mfanyabiashara kweli, kama ni mwalimu uwe mwalimu kweli, kama ni polisi uwe polisi kweli, kama ni karani uwe karani kweli, kama ni mpishi uwe mpishi kweli, kama ni bwana mifugo uwe bwana mifugo kweli, kama ni mwanafunzi uwe mwanafunzi kweli na kadhalika. Usimuwekee mtu masharti magumu katika jambo ambalo faida inaegemea upande wako tuu. Haupaswi kutegea kufanya kazi yoyote iwe kuosha vyombo, kuchota maji, kulima, kupalilia na kadhalika. 

Mambo yakikuendea kombo usiogope kiasi cha kukata tama, yawezekana kwenda kombo kwa mambo yako ni kipimo cha kuhimili matatizo mbalimbali ili ukomae zaidi. Jiweke katika hali ya kuweza kutatua matatizo mbalimbali. Ikiwa una njaa usipende au usijiweka katika hali ya kupokea kila neno, mengine yanakuwa ni ujwongo ili kukuteka vizuri kwa kukuhadaa ya kwamba utaondolewa njaa. Mwandishi anasema, siyo jambo la kiungwana kuwaharibiwa wenzako CV zao kwa kuiongezea thamani CV yako ionekane katika ubora wakati huna weledi. 


Utajiri si haramu na wala si dhambi, unaweza kuutafuta lakini uutafutapo utafuta katika njia halali isiyo na mawaa kwa jamii. Siku nyingine ishi kwa kula chakula cha kiakili kama vile kujisomea vitabu na kuhudhuria semina mbalimbali. 


Ni ruksa kuiga lakini usiige kila kitu. Wapo wanaovaa vimini unaiga. Wapo wanaovaa nguo nyespesi hadharani zina matundu kama chekecheke unaiga. Watu hawataki kuchapa kazi unaiga. Basi jiweke kando na ukweli huu. Jiapishe kwanza mwenyewe kwa kuonyesha juhudi na morali ya kazi ndipo uapishwe. Majina makubwa hayakupi mafanikio ya namna yoyote ile ispokuwa utapata ari, morali, uzoefu na mafunzo zaidi. Soma vitabu vingi upate kujua mengi. Mambo mengi watu wamekishayaandika tayari. Ukiwasoma mawazo yao, yawe mazuri au mabaya akili yako itagongana nayo na hivyo utalazimika kuyachuja na kuyapambanua. Usiwe mtumwa mkubwa wa kutazama picha za runinga, unalaza ubongo. Afadhali maandishi kuliko picha. Maisha yetu yana changamoto za aina mbalimbali, hivyo basi mawandishi wa Busara za Mzee ameonyesha namna watu wanavyoweza kukabiliana na changamoto hizo. Nidhamu na bidii.

Watoto ni tarajio la watu wengi katika maisha yetu ya kila siku. Busara kwa watoto zinahitajika ili kuwaweka katika mazingira yenye makuzi mazuri na yenye nidhamu bora. Ni vibaya kuwazoesha watoto kila wanachokitaka, wakati mwingine mzazi au mlezi atalazimika kuwa hata fisadi au mwizi ilimradi atomize hitaji la mtoto. Mtoto anaongozwa na mzazi au mlezi lakini sio mzazi alu mlezi aongozwe na mtoto kwa kutekeleza kila anachoamriwa na mtoto huyo. Basi watoto kuweni utulivu mnapolelewa. Kusema vitu vingi upewe wewe mara kwa mara haipendezi, kwa mfano mtoto anaweza kusema “siendi shuleni hadi uninunulie pipi”, “mimi nataka babulishi”. 

Maagizo haya ya kila mara halafu mzazi au mlezi unatekeleza ni malezi mabaya kwa mtoto kwani asiyefunzwa na mamaye hufunzwa na ulimwengu. Basi, wazazi na walezi kuweni katika misimamo thabiti ya malezi kwa watoto na kuwahimiza mambo yenye manufaa zaidi kwa wakati waliopo na wa baadae katika maisha yao.

Wavulana na mambo ya ujana wanapaswa kusaidiwa ili wajengwe katika makuzi mazuri. Wavlana wapambane na tama za miili yao ili wajiongezee katika kujiamni na kluheshimu watu kwa muktadha murua. Wavulana wajifunze kazi kwa bidii ili ziwasaidie katika maisha yao. Ubabe ba jeuri havina manufaa yoyote kwa wavualana wala kwa yeyote katika maisha. 

Wasichana msiwaache wavualana wafanye majaribio yao katika miili yenu kama majaribio ya mabomu ya atomiki au mabomu ya nyuklia. Msidanganyike kwa bembelezo wala kwa zawadi nono. Ijalini miili yenu msidanganywe na wavualana wala wanaume watu wazima kwamba wanataka kukuoeni, kama wanataka kukuoeni kwa nini wahangaike kuila embe ambayo itakuwa yao daima? Tamaaa ya pesa na mambo mengine yanayohusiana itakufanyeni mtupiwe chambo kwenye ndoana nyingi sana na hivyo kuchanganyikiwa na ndoana hizi zenye chambo nyingi nono. 

Mwanafunzi uwapo shuleni au chuoni makinika na taaluma uiendeayo. Kufanya maandamano au migomo na kuzilazila ovyo si uungwana kitaaluma. Wakati mwingine unafanya mgomo eti kudai wali, pilau, tambi, chai ya maziwa, eboo! Makinika na kisomo ili upate muongozo wa kutatua matatizo mbalimbali, na ujiwekee malengo ya muda mrefu. Usiitwe jina lisiloendana na ufanyalo. Ukiwa mwanafunzi vumilia mengi. Mwanafunzi usiwe na urafiki na mwalimu anayekupa mwanya wa kukwepa masomo katika baadhi ya mada eti kwa kuwa ni ngumu au haziulizwi katika mitihani. Fahamu kuwa elimu ni zaidi ya mitihani iulizwayo makaratasini. Elimu ni kujua mengi kwa morali na utulivu. Makinika na ukweli huu.

Mwanamke umeumbwa kuwa mpole na amani na kuwa mvumilivu katika malezi, hivyo basi, usiwe na kiburi chochote kwa kigezo chochote ili kukwepa sifa hizi. Mwanamke unayo hekima nzuri ya kutuliza na kuleta amani, unazo busara za aina nyingi, basi makinika na hayo ili ubaki na asili hii bila kuathiriwa na mambo mengine. Wewe ni mama na mlezi makini zaidi. Makinika na jambo hilo. 

Mwanaume unalo jukumu la kuleta fuaraha na kuchukulia mambo kwa wepesi. Mwanaume uache ubabe usio wa lazima, makinika na hayo ili ujenge familia bora na yenye kufuata misingi huysika bila kukwazana na mwanamke yeyote. Mwanaume hujenga dunia si fitina. Basi usimakinike na fitina, jenga dunia.
Yeyote anayetafuta mafanikio ya aina yoyote basi ajiozeze katika nidhamu ya njia anazopitia ili aweze kupata anachokikusudia. Ajihusishe na watu sahihi. 

Fungua ubunifu wa kuzaliwa nao. Jisomee maandiko mbalimbali ili kijiboresha katika fikra na kuongeza utaalamu. Fanya kile unachokipenda jweli. Usiruhusu kushindwa kuwe chaguo lako sahihi. Uwe mtu wa maamuzi kamili.
Wazee ni watu bora sana katika kumkuza kijamna maishani mwake. Wazee wasiwe na matusi. Wazee wasionekane na hatia yoyote ile mbele ya vijana. Basi wazee wamakinike na hekima zaidi.

Kuelimika ni uwezo wa kuyaweka pamoja mambo na kisha kuyapambanua kwa ufasaha. Uvivu usitukwamishe bali tufanye kazi kwa bidii zaidi ili tuwe na maendeleo tunayohitaji. Katika Afrika kuna mambo mengine yanachochewa kwa makusudi ili ukosekane utulivu wa kufikiri, basi mwafrika wewe makinika na amani na utulivu wa kufikiri na pia jiondolee hofu zisizo za lazima na imani ambazo zinatia hofu tu. Wengi kuwategemea wachache ni falsafa ambayo mwafrika anapaswa kuikwepa daima. Mwafrika makinika na bidii ya mambo. Imarisha mifumo ya elimu ili elimu hiyo isitolewe kiholela. 

Kiongozi yeyote wa Arika awe makini na akumbuke kuwa ughaibuni wakitaka kujaribu ubora au udhaifu wa kitu fulani wanakuja Afrika. Majaribio ya chanjo, majaribia ya mifumo fulani ya kisiasa, majaribio ya dawa za magonjwa mbalimbali na kadhalika. Hivyo basi ni vema kumakinika na tahadhari hii na kujinasua. Si vema kubaki kubaki kupeperushwa. Mwandishi anasema kiongozi unapaswa kumakinika na mazingira yako na kuacha kupeperushwa. 

Kwa mafano, matoleo ya televisheni yakibadilika, matoleo ya ndege yakibadilika, matoleo ya redio, simu, basikeli, pikipiki, magari na kadhalika yakibadilika basi watu wa kiongozi wa Afrika wanalazimika kubadilisha vile walivyokuwa wanatumia ili kununua matoleo mapya kwa mlango wa mbele au mlango wa nyuma. Himiza bidii ya kazi kwa manufaa ya wengi katika nchi yako.,
Busara hizi za mzee ziwamakinishe wengi ili waweze kupata mafundisho mengi yaliyomo katika busara hizo na kuweka wazo dhamira zao. Shukrani kwa mzee kwa ktupatia busara hizi.

Kizito Mpangala
Nishani Media
0692 555 874

No comments:

Post a Comment

Maoni yako