October 19, 2017

STEPHEN HAWKING: MWANAFIZIKIA MGONJWA WA MUDA MREFU.

NA KIZITO MPANGALA

STEPHEN HAWKING alizaliwa mwaka 1942 jijini Oxford nchini Uingereza kwa wazazi Frank Hawking na Isobel Hawking. Japokuwa familia yake ilikuwa na mtikisiko kifedha lakini wazazi wake walijitahidi kujiendeleza kielimu katika chuo kikuu cha Oxford. Baba yake alisoma udakitari wa dawa na mama yake alisoma Falsafa, Sayansi ya Siasa, na Uchumi katika chuo hicho.

Baba yake na mama yake walikutana kwa mara ya kwanza muda mfupi tu bada ya kuanza kwa vita ya pili ya dunia katika Taasisi ya Utafiti wa Dawa ambapo baba yake alikuwa mtafiti  na mama yake alikuwa katibu wa taasisi hiyo. Ndipo mapenzi yao yalipoanza na walibahatika kupata mtoto wa kiume ambaye ni Stephen Hawking.


Familiya ya Hawking ilisifika kwa kuwa na kiwango kizuri cha upeo wa akili tangu wazazi hadi watoto wao. Muda mwingi walipokuwa nyumbani kulikuwa na ukimya ikidhaniwa kuwa wanasafiri mara kwa mara lakini sivyo! Ukimya uliotawala ndani ya familia hiyo ulitokana na wazazi kuwazoesha watoto kujisomea vitabu jambp ambalo walilipenda na ndipo Stephen Hawking alipodhihirisha kiwango chake katika upeo wa akili. Walikuwa wakiishi kwenye nyumba kuu kuu iliyokuwa na maktaba ya familia ndani.


Stephen Hawking alianza shule katika shule ya Byron mtaa wa Highgate jijini London. Baadae alilalamikia shule hiyo kutokana na mfumo wake uliokuwa ukitumika kufundishia, jambo ambalo lilinampa ugumu katika kujifunza zaidi. Wazazi wake walipohamia katika mji wa Mt. Albans, Stephen alijiunga na shule ya upili ya wasichana ya Mt. Albans mjini hapo kwa muda mfupi na baadae akahamishiwa katika shule ya Radlett katika mji mdogo wa Hertfordshire.

Wazazi wake waliipa elimu kipaumbele kwa kiasi kikubwa na kuwahimiza wajisomee vitabu vilivyokuwepo katika maktaba ya familia ndani ya nyumba yao.  Baba yake alitamani Stephen akasome katika shule binafsi ya Westminster lakini kwa bahati mbaya siku ya kufanya mtihani wa kujiunga na shule hiyo Stephen alishikwa na homa kali lakini pia wazazi wake hawakuweza kulipa ada katika shule hiyo iliyokuwa ikitoza kiasi kikubwa cha fedha wakati huo, hivyo Stephen alibaki katika shule aliyokuwepo.


Stephen Hawking alijizolea marafiki wengi katika shule aliyokuwepo kutokana na kiwango chake cha upeo wa akili katika masomo, hivyo hata yeye mwenyewe alifurani kuwa na marafiki na kucheza nao pamoja. Wakiwa shuleni walifundishwa stadi za kazi na mambo mengine yahusuyo maisha kwa ujumla. Walijifunza kutengeneza maboti na vielelezo mbalimbali vya ndege.

Mwaka 1958 wakisaidiana na mwalimu wao wa Hisabati bwana Dikran Tahta walitengeneza kompyuta  wakitumia vifaa vya saa kubwa ya kielektroniki iliyokuwa mbovu, pia walitengeneza simu za mezani kwa kutumia vifaa vya vyombo vibovu vya kielektroniki.

Stephen Hawking alipewa jina la utani shuleni ambapo alikuwa akiitwa “Einstein”, pia alikuwa na udhaifu katika maendeleo yake kitaaluma lakini alijitathmini kwa msaada wa mwalimu wake wa Hisabati bwana Dikran Tahta na kuamua kujikita katika masomo ya sayansi, akawa anaimarika kitaaluma. Aliweka bidii zaidi katika Hisabati na alipofika chuo kikuu alisoma Hisabati zaidi.

Baba yake alimhimiza asome udakitari wa dawa (Doctor of Medicine) akimuambia kuwa kuna ajira chache sana ambazo zinahitaji wajuzi wa Hisabati, hivyo alimsihi aachane na Hisabati ili asome udakitari wa dawa. Alimsihi pia ajiunge na chuo kikuu  cha Oxford. Baada ya kujiunga ilitokea kwamba ni ngumu kusoma hisabati wakati ule kutokana na uhaba wa walimu ndipo Stephen akachagua kusoma Fizikia na Kemia. Mkuu wa chuo alimsihi Stephen avute subira hadi mwaka wa masomo utakaofuata kwamba kutakuwa na walimu wa kutosha lakini Stephen alifadhiliwa.

Alianza masomo mwezi wa kumi mwaka 1959 katika chuo kikuu cha Oxford akiwa na miaka 17. Miezi 18 tangu aanze masomo katika chuo hicho alihisi kuchanganyikiwa kitaaluma kutokana na hulka yake ya kujilinganisha na wengine kitaaluma hivyo alijiona yeye si kitu na kwamba hafai lolote kusoma chuo kikuu, lakini mwalimu wake wa Fizikia katika chuo hicho bwana Robert Berman alimtibu kisaikolojia kwa kumuambia “ninapofundisha ninataka kukuonyesha kwamba kuna kitu fulani cha pekee inabidi kifanywe, na usikifanye kwa kuangalia watu wengine walifanyaje au wanafanyaje”. Kutokana na maneno hayo, Stephen alionyesha mabadiliko makubwa kitaaluma alipoanza mwaka wa pili wa masomo na mpaka alipofika mwaka wa tatu. Kadiri ya mwalimu wake huyo alisema kwamba Stephen likuwa kijana mwerevu kati ya waerevu.

Alipenda kujisomea hadithi za kisayansi na kujihusisha na muziki. Pia alikuwa mmoja kati ya washiriki wa masindano ya kuendesha maboti katika mashindano yaliyokuwa yakifanyika chuoni hapo.

Stephen alisema kwamba katika maisha yake ya kitaaluma chuoni Oxford miaka mitatu alitumia masaa 1000 tu kujisomea katika jumla ya miaka hiyo mitatu, hivyo mtihani wa mwisho wa kumaliza mafunzo ulimpa changamoto na akaamua kujibu maswali machache tu ya kipengele kimoja cha Fizikia ya Nadharia (Theoretical Physics) akiwa na lengo la kujiendeleza na masomo ya Cosmolojia katika chuo kikuu cha Cambridge ambapo alihitajika kupata ufaulu wa daraja la kwanza. Kutokana na mfadhaiko, alilala usingizi hafifu sana siku moja kabla ya kufanya mtihani wa mwisho, hivyo akapata alama zilizopungua kidogo kupata daraja la kwanza na kulazimika kufanya mtihani wa marudio uliojulikana kama “Viva” ili kusahihisha matokeo.

Stephen Hawking alijihisi ya kwamba ni mwanafunzi mvivu na mgumu kuelewa masomo kwa ufasaha. Alipoulizwa kuhusu matokeo yake ya awali alijibu hivi “mkinipa daraja la kwanza nitakwenda Cambridge, mkinipa daraja la pili nitabaki hapa Oxford, natumaini mtanipa daraja la kwanza”. Walimu wake walitambua kipawa chake cha upeo wa akili na walikuwa wakimpa uangalizi mkubwa sana bila kumuambia yeye mwenyewe. Baadae akapewa daraja la kwanza.

Alikwenda nchini Iran na rafiki zake kwa ajili ya mapumziko baada ya kumaliza chuo huko Oxford, na aliporudi Uingereza alianza kufanya kazi zilizohusu taaluma yake katika Ukumbi wa Kisayansi wa Trinity mjini Cambridge mnamo mwaka 1962.

Alipoanza masomo ya shahada ya uzamivu alihisi kwamba amekosea njia katika taaluma. Alipata changamoto kubwa  na hivyo kukata tamaa ya kuendelea na masomo ya Cosmolojia. Pia alihisi hataweza kujiendeleza na hisabati tena kutokana na changamoto alizopata. Lakini alihimili changamoto hizo hadi mwisho wa masomo yake.

Muda mfupi baadae alipata homa na hivyo kufanyiwa upasuaji na akabainika kuwa anasumbuliwa na homa iliyoiangamiza “motor nuerone” na kumfanya apooze mwili. Dakitari alimshauri aendelee na masomo japokuwa mwili wake ulikuwa ukiendelea kupooza taratibu, hivyo hakuweza kutembea na akawa anatumia baiskeli mpaka hivi sasa, vilevile alipata ugumu wa kupangilia matamshi yake kwa usahihi kutokana na kupooza kuanzia shingoni na kuathiriwa katika matamshi wakati anapozungumza.

Alirudi masomoni katika hali hiyo na kwa mshangao mkubwa aliboreka zaidi katika taaluma na pia aliweza kuboresha matamshi yake kwa msaada wa kitabibu.

Alpoanza kuwa mkufunzi alikuta mjadala mzito uliokuwa ukijadiliwa na wakufunzi wenzake wa Cosmolojia kuhusu jinsi ulimwengu ulivyotokea. Alikuwa mkufunzi hodari licha ya kuwa maisha yake kuwa katika baiskeli muda mwingi huku shingo ikiwa imekwenda upande kama anavyonekana pichani kutokana na kupooza mwili. Mwka 1965 aliandika insha yake mashuhuri kuhusu mjadala uliokuwa ukijadiliwa kuhusu jinsi ulimwengu ulivyotokea. Aliandika akiwa bado kijana lakini akiketi kwenye baiskeli muda mwingi.

Mwaka 1966 alitunukiwa shahada ya uzamivu katika Hisabati Tumizi (Applied Mathematics) na Fizikia ya Nadharia (Theoretical Physics) na alijikita zaidi katika Cosmolojia (Cosmology). Na baadae kazi yake aliyoandika kutokana na utafiti alioufanya (licha ya kuwa na kilema kama anavyoonekana pichani) ya “Singularities and the Geometry of Space – Time” iliheshimiwa na hivyo akashinda tuzo ya Adams katika sayansi.

Mwaka 1970 aliteuliwa kuwa profesa wa hisabati katika chuo kikuu cha Cambridge. Katika maisha yake kitaaluma amejikita zaidi katika sayansi ya ulimwengu (The science of Universe). Kadiri muda ulivyosonga alizidi kudhoofika na kulazimia kupata matibabu mara kwa mara akiwa nyumbani kwake.

Mwaka 1982 alihudhuria mkutano huko Vatican kuhusu ulimwengu ndipo alipotoa msimamo wake hadharani na kusema “hakuna mwanzo, hakuna mwisho, na hakuna mipaka katika ulimwengu”, tukumbuke kuwa ulimwengu una maana pan asana kisayansi, ulimwengu ni zaidi ya ukubwa wa dunia hii au sayari yoyote kwa kuwa ulimwengu ni jumla ya sayari zote na vyote vilivyomo katika anga. Stephen Hawking ansema kwamba nadharia ya Biblia inayosema kwamba kulikuwa na mwanzo wa ulimwengu siyo ya kweli na haina mashiko, hivyo hakuna mwanzo, mwisho, wala mipaka katika ulimwengu.

Pamoja na kuwa kilema na kuwa na tatizo la kufanya mawasiliano kwa usahihi, Stephen Hawking ni mwanafizikia aliyeweka kando ukilema wake na kujikita katika taaluma yake ya Fizikia. Hali ya kuwa kilema ilimpelekea kuachana na mkewe licha ya kuwa na watoto aliopata na mkewe huyo. Alitumia muda mwingi kufikiri masuala ya sayansi na kuweza kuandika vitabu vingi kuhusu Cosmolojia ambavyo vinatumika katika vyuo mbalimbali duniani.

Stephen Hawking amesafiri kwenda sehemu mbalimbali duniani kwa shughuli binafsi na kikazi. Stephen Hawking amekuwa gwiji wa  Cosmolojia na kusikika masikioni mwa watu wengi duniani kwa umahiri wake katika fizikia na hisabati licha ya kuwa kilema kwa muda mrefu jambo ambalo lilimpelekea kuwa na baiskeli maalumu iliyounganishwa na kompyuta ambayo inamsaidia katika mazungumzo na mambo mengine katika maisha yake.

Stephen Hawking amejitokeza mara nyingi katika mijadala mingi kuhusu Cosmolojia jambo ambalo alisema ndilo la maisha yake yote. Amekuwa mtu wa kutumainiwa katika vyuo mbalimbali duniani kwa taaluma ya Cosmolojia.
Hakika kilema si ugonjwa! Leo Stephen Hawking ambaye bado anatumia pumzi ya bure aliyojaliwa na Mungu ameshinda nishani zaidi ya 10 kwa muda wote wa maisha yake aliyoyaweka katika sayansi. Hawking ansema kwamba kila mmoja anao uwezo wa kujifunza anachokipenda.

Amekuwa na afya dhaifu kwa muonekano wa kawaida mwilini lakini ana afya imara sana katika ubongo wake. Muda mwingi wakati wa mapumziko hutumia kuzungumza na binti yake Lucy Hawking na ambaye humuwakilisha katika upokeaji wa zawadi kwenye matamasha mbalimbali anayoalikwa. Bega lake la kulia ndilo lililoathirika zaidi pamoja na miguu, lakini kwa hakika Mungu ni mkubwa, ubongo wa Stephen Hawking una afya imara sana ya maarifa na mambo mbalimbali maishani. Hivi sasa vyuo vingi vinafaidi kazi zake kuhusu Cosmolojia ambapo hutumika katika mafunzo ya kupata shahada ya uzamivu katika sayansi ya anga, na maisha yake muda mwingi ni juu ya baiskeli yake maalumu kama anavyoonekana pichani. Yuko hai.

© Kizito Mpangala 
0692 555 874,   0743 369 108.  

No comments:

Post a Comment

Maoni yako