March 21, 2018

JE, JAMII IMECHOKA KUISHI KWA MAFUNDISHO YANAYOTOLEWA KWA MIFANO?

Na KIZITO MPANGALA

Mafundisho ni moja kati ya elimu ambayo haina mpinzani katika maisha yetu ya kila siku. Mafundisho hayo yapo kwa namna mbalimbali, kuna mafundisho ya jumla, kuna mfundisho ya kipekee ambayo hugusia katika uga husika kama vile mafundisho ya dini, mafundisho ya stadi za kazi, mafundisho ya maadili, mafundisho ya rika na kadhalika. Hayo yote husaidia kujenga jamii na kuiweka katika mwenendo unaokunalika na wengi na ambao una manufaa mazuri kawa jamii hiyo na pengine hata kuakisi kwa jamii nyingine mahali popote duniani.
Mafundisho ya kijinsia yana umuhimu mkubwa sana katika maisha yetu. Jinsia fulani ifundwe yale yanayopaswa kufanyika nayo ili kuendeleza maadili au jeme lipatikanalo kutoka katika mafundisho hayo. Ikiwa mtu wa jinsia tofauti ataifunda jinsia nyingine fundisho fulani, kinachotakiwa ni kufikiri kilichosemwa ili kubaini kama kina manufaa ya kurekebisha kitu fulani kwa jinsia iliyofundwa au kama kina maudhui mabaya dhidi ya jinsia iliyofundwa kishapo hukumu itolewe, iwe hukumu chanya au hukumu hasi.
Kitendo cha kutoa mafundisho kinaweza kuwa cha namna mbili. Huenda mafundisho yakatolewa kinagaubaga au kwa kutumia mifano ambayo inalenga kurekebisha jambo fulani katika jamii. Ikiwa hilo linafanyika, si vema kulalamika ghafla bila kufikiri lengo au dhamira ya mafundisho hayo. Na kwa sasa jinsi ilivyo rahisi kusambaza taarifa katika mitandao basi ndani ya dakika kadhaa dunia yote huenda ikajua kinachojiri na kisha kila aliyepata taarifa anatoa maelezo yake kadiri ya taarifa ilivyomfikia. Watasifu, watalaani, watahamasisha watu kuwa watulivu, watamshutumu mnenaji, watamtetea mnenaji na kadhalika.
Katika suala hili la kuishi katika mafundisho yanayotolewa kwa mifano, inawezekana mfundaji anakuwa na nia ya kuonya au kurekebisha jambo fulani lakini huenda akaeleweka tofauti na lengo la fundisho lake. Hii inatokea mara nyingi na pengine husababisha maandamano ambayo yanaweza kuzua madhara kwa waandamanaji wakiwa wanakemea fundisho wasilolikubali au kama limefikirirwa kuwa ni la kejeli kawa kundi fulani katika jamii.

Nchini India, profesa mmoja katika chuo cha taasisi cha Farook katika jimbo la Kerala kusini mwa nchi hiyo amekuwa katika wakati mgumu baada ya kuwakanya wasichana wa chuo hicho. Profesa Jouhar Munavvir T, aliwakanya wasichana hao kuhusu uvaaji wa mavazi ambayo huacha wazi sehemu za kifua na kusababisha mwonekano wa matiti yao huku vichwani wakiwa wavalia hijabu. Profesa Jouhar aliwaambia wanafunzi kwamba sehemu hiyo huwavutia wanaume na ndipo hutambua kuwa mnavutia vema na kisha kuwanyanyasa. Katika mafundisho yake hayo kuhusu mavazi alifananisha matiti hayo na tikitimaji huku akisema: “ni kama kipande cha tikitimaji kilichokatwa kuonyesha jinsi tunda hilo lilivyoiva vizuri,” kauli hii ambayo aliitoa kwa lengo la kuhimiza wasichana hao kujisitiri kikamilifu, imeeleweka vibaya kwa watu wengi nchini India.
Kueleweka vibaya kwa kauli hii ni kutokana na profesa Jouhar kusema kwa msisitizo huku aliwa na lengo la kuwataka wasichana hao wawe wanajisitiri vema na siyo kujisitiri kichwani tu kwa kuvalia hijabu kikamilifu huku sehemu zingine za miili yao huziacha wazi. Wanawake wengi wamemshutumu profesa Jouhar na kufanya maandamano sehemu kadhaa nchini India kwa lengo la kumkemea profesa huyo kwamba ametoa kauli ya kuwavunjia heshima wanawake kwa kufananisha matiti yao na vipande vya tikitimaji liliokatwa. Wanawake kadhaa nchini India walitumua picha zao katika mitandao ya kijamii huku wakiwa bila nguo kuanzia kiunoni kwenda juu, yaani sehemu za kifua ziliachwa wazi, wakiwa na lengo la kuiambia jamii kwamba profesa Jouhara amewadharau na hivyo wameamua kuiacha wazi sehemu hiyo watu waione na waichukulie kuwa ni ya kawaida tu. Wanawake hao walioachia sehemu hizo wazi nao walishutumiwa vikali huku wakiitwa ‘malaya’ na kwamba walikuwa wakitafuta wateja, lakini hilo halikuwarudisha nyuma.
Kwa ujumla kauli ya profesa Jouhar haikuwa ya kuvaliwa njuga kiasi hiki. Hii inaonyesha wazi kwamba jimii zetu nyingi duniani zimechoka kuishi na mafundisho yanayotolewa kwa mifano na watu mbalimbali. Na kwa upande wa wanawake uchovu huu umekuwa mkubwa sana kiasi kwamba mzigo wa kilogramu moja tu unaweza kubadili taswira ya uchovu huu duniani kote.
Wasichana na wanawake wengi sasa wanaishi mazingira kama ya wasichana wa chuo cha taasisi cha Farook na hasa huko vyuoni. Katika hali ya kawaida mwanamke fulani anaweza kuvaa mavazi ambayo yanaweka wazi sehemu fulani ua kifua chake na hivyo mgawanyika wa matiti yake ukaonekana barabara, lakini akiwa ananyonyesha ataona aibu kutoa titi moja na kumnyonyesha mtoto sehemu zenye watu wengi au sehemu za mikusnayiko mbalimbali. Sasa nani bora hapa, mtoto au fasheni?
Kauli aliyoitoa profesa Jouhar ilipaswa kutafakariwa sana na kuwa ni mafundisho kwa wasichana na wanawake wa namna hiyo lakini pia hata kwa wavulana na wanaume, utaona aibu kuchomekea vema shati lako lakini mazingira mengine unaona fahari kuvalia mlegezeo, hivyo basi, jamii inaonekana kuchoka kuishi kwa mafundisho yanayotolewa kwa mifano ili mtu arekebike. Badala yake, wanajamii wengi husukumwa na matangazo mbalimbali kuhusu mitindo ya maisha katika mitandao ya kijamii.
Rai ya profesa Jouhar si kukejeli wanawake, bali ni kurekebisha mwenendo aliouna kuwa haufai, ndiyo maana aliamua kutoa fundisho lake kwa mfano. Na mfano alioutumia ni kipande cha tikitimaji kilichokatwa kuonyesha tunda hilo lilivyoiva vizuri ili kuwavutia wateja.
© KIZITO MPANGALA

No comments:

Post a Comment

Maoni yako