November 15, 2017

NAMKUMBUSHA MBUNGE WA JIMBO LA NYASA

NA MARKUS MPANGALA
NIMEANDIKA safu hii leo baada ya kusoma Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano iliyosomwa na waziri Profesa Makame Mbarawa mjini Dodoma. Kwa mujibu Tovuti ya Mkoa wa Ruvuma inaeleza kuwa Wilaya ya Nyasa iliyopo mkoni humo, ilianzishwa rasmi mnamo Machi  2012 baada ya kumegwa kutoka wilaya ya Mbinga.

Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Mheshimiwa Stella Manyanya
Aidha, eneo la wilaya hii liko kando ya Ziwa Nyasa. Makao makuu ya wilaya yako mjini Mbamba Bay. Wakati wa sensa ya mwaka 2012, wilaya ya Nyasa ilikuwa na wakazi 146,16. Vilevile wilaya hiyo ina jumla ya Kata 16 ambazo ni Chiwanda, Kihagara, Kilosa, Kingerikiti, Liparamba, Lipingo, Lituhi, Liuli, Liwundi, Luhangarasi, Mbaha,    Mbamba Bay,Mtipwili, Ngumbo, Nindai,na Tingi.

Kwanini ninamkumbusha Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Mama Stella Manyanya? Nitaeleza sababu za msingi kwa madhumuni ya kumsaidia vipaumbele katika jimbo lake. 


Sekta ya kwanza; Babaraba;
Tunakubaliana kuwa wilaya hii inazo barabara kuu tatu; ambazo ni chanzo cha mawasiliano pamoja na ukuaji wa uchumi unaounganisha na wilaya nyingine.
Barabara ya kwanza ni Mbinga-Mbamba Bay, ya pili ni Mbinga-Lituhi (ambayo inaanzia njia panda inayounganisha wilaya tatu; Songea, Mbinga na Nyasa yenyewe) na ya tatu ni Lituhi-Mbamba Bay. Mipango ya kuinua maisha ya wakazi wa wilaya hii inatakiwa kujikita kwenye ujenzi wa barabara hizo kwa awamu ya kwanza.

Kwa mujibu wa hotuba ya bajeti ya wizara ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano kipengere cha “Sekta ya Ujenzi” kifungu cha 37 kutoka “Miradi ya Barabara na Madaraja”, serikali imesema kuwa mradi wa Barabara ya Mbinga-Mbamba Bay yenye urefu wa Kilometa 66 utaanza kujengwa. 

Taarifa nilizonazo ni kwamba ujenzi huo utaanza mwezi Juni mwaka huu. Kwangu ninaamini hii taarifa iliyochelewa na isiyo na lolote jipya, pengine inakera zaidi kuisikia kuliko kawaida. Nakumbuka wakati wa uzinduzi wa Stendi Kuu ya Mbinga na Barabara ya Peramiho-Mbinga yenye urefu wa Kilometa 78, Julai 19, mwaka 2014 na  Rais mstaafu Jakaya Kikwete alibainisha suala la ujenzi wa barabara hiyo. 

Ilielezwa kuwa ujenzi huo utafanyika kwa kutokana na ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AFDB). Benki hiyo inagharimia ujenzi wa barabara hiyo ya kiwango cha lami kati ya Mbinga na Mbamba Bay. Lengo ni kukamilisha ujenzi wa kiwango cha lami wa barabara ya ukanda wa Mtwara (Mtwara Corridor) kati ya Mtwara na Mbamba Bay yenye kiasi cha kilomita 823. 

Mradi wa Mtwara Corridor ulipangwa mwanzoni mwa mwaka 2000. Kutokana na kusuasua kwa mradi huo umesababisha hata jirani zetu Malawi watukimbie katika ushirikiano wa kibiashara na uchumi kupitia bandari ya Mbamba Bay. Mwanzoni mwa miaka hiyo Meli za abiria na mizigo za Malawi mfano Mv. Ilala ilikuwa inatia nanga bandarini Mbamba Bay, lakini kwa sasa hali ni tofauti. Bandari hiyo ingeliweza kuingiza bidhaa kutoka Msumbiji kuja Tanzania na kinyume chake. Bahati mbaya kukosekana kwa barabara rafiki kumesababisha tukimbiwe. 

Ukizitazama bajeti za toka mwaka 2012 pale wilaya (au jimbo) ilipoanza unabaki kushangaa, vipaumbele vyetu katika wilaya hii vilikuwa nini? Mathalani, kutoka mwaka 2014 kumekuwa kumekuwa na bajeti tofauti.
Utawala wa awamu ya tano uliwasilisha bajeti ya kwanza ya mwaka wa fedha 2016/2017 lakini barabara hii haijakamilika. Serikali ya awamu ya tano imewasilisha bajeti ya pili ya mwaka wa fedha 2017/2018 na kubanisha kuwa ujenzi unatarajiwa kujengwa. 

Ukijumlisha utaona tangu mwaka 2000 kumekuwa “barabara itajengwa’. Kila awamu tunajibebesha ‘excuse’ ambazo zinadhoofisha mapato ya wilaya ya Nyasa. Inadhoofisha uchumi wa wananchi wa jimbo husika. Sitegemei kuona Mbunge wa Jimbo hilo akija na ‘excuse’ ifikapo mwaka 2020 kwasababu kumekuwa na uahirishwaji usiokuwa na maelezo yanayojitosheleza. Aidha, sasa tunafahamu mfadhili husika wa mradi huu, ukicheleweshwa lawama kwa Mbunge na chama chake.

Wataalamu wa masuala ya habari tunasema ‘habari ni biashara na uchumi’. Wimbi la habari za wilaya ya Nyasa limezidi kuchanua kuliko miaka ya nyuma. Kwa sasa wananchi wa jimbo la Nyasa wanafahamu kuwa kipande cha eneo la Ndengu kwenda Nyasa hapatiki, isipokuwa wanasafiri kwasababu ya dhiki na shida walizonazo hata kuhatarisha usalama wao.  

Maisha ya wananchi wa mji wa Buruma hususani kitongoji cha Sisi kwa sisi mambo yamezidi kuwa magumu na haitashangaza siku moja kuona hawana mawasiliano na makao makuu ya wilaya au kufanya shughuli za uchumi kutoka Mbinga kwenda Mbamba bay.

Mawaziri wa awamu ya tano wamefanya ziara maeneo yanayogusa wilaya ya Nyasa. Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Muhongo alitembelea machimbo ya Makaa ya Mawe yanayofanywa na TANCOAL huko Amanimakoro, Mbinga.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na miundombinu, Edwin Ngonyani alimhakikishia mbunge wa Nyasa kuwa ujenzi wa barabara utaanza mara moja kama ambavyo Ilani ya CCM 2015-2020 inavyoelekeza. 

Naibu waziri wa Nishati na Madini, Medard Kalemani, alitembelea mji wa Liuli mnamo Februari 15 mwaka huu aliahidi kuwa nguzo za Umeme zitaanza kuwekwa mjini humo na vitongoji vyake lakini hadi hii leo hakuna chochote. Kwahiyo namkumbusha Mbunge wa Jimbo la Nyasa hayo mambo kwa moyo mkujufu kwamba yasiwe sababu ya kuanza kunyosheana vidole. 

Sisi wengine kazi zetu ni kuandika. Tutaandika barabara ya Mbinga-Lituhi ni mbovu, huku Makaa ya Mawe yakiwa bidhaa muhimu inayohitajika kuinua uchumi wa wilaya ya Nyasa. Tutaandika kuwa gati lililojengwa bandari ya Ndumbi kando ya barabara ya Lituhi-Mbamba Bay wilayani Nyasa halitakuwa na maana kama barabara hiyo inayotarajiwa kutumika itaendelea kuwa mbovu.

Aidha, ninamkumbusha Mbunge kuwa kutoka mwaka 2000 hadi leo kumekuwa mipango na Ilani vilevile lakini hakuna lililokamilishwa. Ninamkumbusha kuwa Daraja la Yungu linaounganisha miji ya Puulu na Liuli katika Barabara ya Mbamba bay-Lituhi limeharibika. 

Itaendelea …

No comments:

Post a Comment

Maoni yako