January 11, 2013

UCHAWI: DHANA INAYOANGAMIZA JAMII YETU



Na John Chitanya, Nyasa

Mei 4, 2012 yalifanyika maandamano makubwa sana katika wilaya mpya ya Nyasa iliyogawanywa kutoka wilaya ya Mbinga. Nyasa ni wilaya ni kiserikali, lakini katika Tume ya Taifa ya Uchaguzi inafahamika kama jimbo la Mbinga Magharibi. Maandamano yaliyofanyika yalilenga kuishinikiza serikali kumruhusu Mganga wa Kienyeji apewe  kibali cha kufanya kazi yake ya kuwaumbua wachawi wilayani hapa.
Maandamano yale yalionyesha na televisheni ya TBC1  wakazi wa mji wa Kilosa nje kidogo ya mji mdogo wa Mbamba Bay, kwa hakika ilikuwa fedheha kubwa kwa wananchi wa ukanda wa ziwa Nyasa na maeneo mengine yanayounda wilaya hiyo kwa upande wa mashariki ambayo yanakaliwa na jamii ya Wamatengo.
Kwa mtazamo wangu kama kuumbuana na kushika uchawi  wameshikana sana,  sasa tunataka maendeleo sio kuimba nyimbo za wachawi kuwanyima maendeleo baadhi ya watu.  
Watu wengi wanaamini kuwa kuna kasoro pale inapotokea jambo fulani likawa baya, basi linazungumzwa kuwa linatokana na kurogwa na wachawi.
Mganga wa kienyeji
Niliwahi kushuhudia tukio moja kwa moja ya familia iliyokuwa ikiendesha kikao cha kifamilia, kwamba binti mmoja wa shule ya msingi alishindwa kusoma na kuandika hivyo walipanga kwenda kwa Mganga wa Kienyeji ‘kumfungua” kwa madai alifungwa na watu wabaya(wachawi) asiweze kujua kusoma na kuandika.
Hakika suala hilo lilileta mtafaruku kwa wale waliofanikiwa kwenda shule, wakadai kuwa hilo ni suala la mwanafunzi mwenyewe wala halina uhusiano na kufungwa kwa misingi ya uchawi. Lakini ilishikiliwa uchawi ndio umemfunga binti yule. Hadi naandika makala hii juhudi za kumfikisha mwanafunzi yule kwa Mganga wa kienyeji zilikuwa zimesimishwa ila sina shaka zitaendelea kwani nia yao ipo na wanaonekana kuamiani sana uchawi umetumika kwa binti yule.
Matukio ya uchawi yamekuwa yakitangazwa sana hata wakati uchaguzi unapofanyika, kwani wagombea mbalimbali wanadaiwa kuwategemea waganga wa kienyeji, wapiga ramli na kuamua hatima ya harakati zao. Kwenye michezo ya mpira wa miguu na mingine suala la uchawi limekuwa likichukua nafasi kubwa bila kutegemea sayansi ya kuleta mafanikio.
Hatua za vigogo kuhangaika na kuwategemea waganga wa kienyeji inaleta ujumbe kuwa jamii yetu inakabiliwa sana na janga la uchawi na kutoamini nguvu zilizomo kwenye akili na miili yetu.
Leo hii ni vigumu kufanya jambo la maajabu kwa kutohusisha uchawi. Hapa ndipo mimi siku zote huamini mapinduzi ya maendeleo ya wilaya ya Nyasa na yale yenye kasumba za kutegemea wachawi yanapaswa kuanzia katika fikra zetu. Tuna mambo mengi ya kuyafanyia maandamano katika nchi hii, mfano umeme, bandari, barabara isiyoisha na mengine mengi, lakini wananchi wameshikilia na kuamini kuwa uchawi umesababisha wawe na maisha duni.
Hata hivyo tukio la mji wa Kilosa, waliohamasishwa mapema mwezi Mei, ili Mganga wa kienyeji kutoka Tanga walikamatwa na mamlaka zinazohusika. Mganga huyo alihamasisha vijana wa Mbamba Bay wafanye fujo kushinikiza apewe kibali ili atoe uchawi kwenye nyumba za watu, basi wale vijana wakavunja ofisi za serikali na kuchoma moto, huku  wakalazimisha kila familia kuchangia shilingi 5000.
Mamlaka zinazohusika zilifanikiwa kuzima jaribio hilo, na kuwakamata baadhi ya vijana waliohusika. Baadhi ya vijana yao ni mabinti watatu waliokamatwa kwa kosa la kuandamana bila kibali na kufanya vurugu, walishikiliwa mjini Kilosa, Mbamba Bay. Tukio hilo linaturejesha kwenye mjadala hivi masuala ya uchawi yanachukuliwaje kama turufu ya kufanya uhalifu au uvunjifu wa amani? Uchawi umekuwa ukizungumziwa sana katika jamii zetu.
Wafanyabiashara wanategemea uchawi, watu wa kawaida wanategemea uchawi, ina maana hata masuala yenye kuhitaji utaalamu yamepewa dhana ya uchawi. Jamii yetu imeshikilia dhana ya uchawi kama nyenzo ya kupata mafanikio. Wengi hushikilia sana kupiga ramli, wamekuwa wakishindwa kujielemisha na kupata ufumbuzi wa matatizo ya familia na jamii huku wakiamini matukio hayo yanatokana na uchawi. 
Idadi ya wapiga ramli nayo inaongezeka kila kukicha. Ulimwengu unatuacha nyuma, na kila mwenye mafanikio maishani anaweza kutazamwa kwa namna mbili; mosi aliiba mahli na pili amefanya uchawi. Hakuna watu wanaoamini kuwa juhudi hizo zimefanywa na mhusika. Kuna masimulizi mengi sana kwa wana jamii ya wilaya ya Nyasa kuhusiana na uchawi. Magari yakipinduka husemwa uchawi, hakuna anayesema kuwa barabara ni mbovu, wote husikilia uchawi.
Kuna mambo mengi yanatisha na bila juhudi za serikali kusambaza elimu kila jambo lingeonekana kwua uchawi. Na serikali yetu haiamini uchawi hivyo ni kosa la mtu kufanya fujo kama vijana wale kwa kisingizio cha uchawi. Sio hapa tu, hata Afrika Kusini, aliyekuwa kocha wa timu ya taifa ya nchi hiyo, Pits Mosimame aliwahi kukaririwa na vyombo vya habari akijibu swali kwanini Bafana Bafana haijashinda mechi nyingi tangu achukue madaraka.
Naye  alijibu kwa urahisi kuwa shirikisho la soka la Afrika Kusini halijamlipa Sangoma (mganga wa kienyeji) tangu michuano ya kombe la dunia. Hali hiyo inaonyesha namna gani jamii imetawaliwa na uchawi. Kila kitu tunachofanya kinaonekana kimetokana na uchawi. Wachawi wamekuwa vikwazo kwenye mafanikio ya jamii yetu.
Dhana hii ya uchawi itaendelea kutuangamiza ikiwa juhudi za makusudi hazitachukuliwa. Kwa mtazamo wangu, naona uchawi ni sumu kali sana, lakini kama uchawi wa kisayansi basi nitasema kila nchi inao uchawi.
Nasema kila nchi inao uchawi kwa maana ya kisayansi kutokana na mila na desturi za nchi hiyo. Ujerumani walileta utabiri wa Pweza Paul, akatabiri ushindi kwa wahispania. Nao ni uchawi kama wapiga ramli za kisayansi sio mazingaombwe. Zipo nchi zinatumia uchawi wa kisayansi kwa njia ya maneno hususani katika dini,  “kuapishwa” au “kusimikwa”, kinachotendeka ni uchawi, ni mila na desturi za nchi husika na tamaduni zao. Mikoa ya kanda ya ziwa inakabiliwa na dhana hii ya uchawi imesababisha hofu kwa ndugu zetu albino, na wazee wenye macho mekundu. Wazee hao huuawa kwa kisingizio eti wachawi. Nionavyo uchawi uliosababisha watu wa mji wa Kilosa waandamane mapema mwezi Mei mwaka huu ni sumu kali sana, na kawaida sumu haiwezi kutibu ugonjwa mwingine, kwani huua.

John Chitanya ni mwandishi na mwalimu wa Miracle Center, mjini Songea. Niandikie: 0718 005557

No comments:

Post a Comment

Maoni yako