June 20, 2013

JAMES ZOTTO; TUNATENGENEZA BOMU KWENYE ELIMU


Na Markus Mpangala, Dar es salaam

Wanafunzi ambao walianza Darasa la kwanza mwaka 2002, walipoanza shule ada ikafutwa, na walipofika Darasa la 4 mitihani ikafutwa na hatimaye wakaibuki kidato cha kwanza mwaka 2009. Walipofika kidato cha pili mitihani ikafutwa mwaka 2010, pia matokeo yao ya mtihani wa kidato cha nne mwaka 2012 yakafutwa baada ya kufeli sana. 

SWALI: Ndugu Zotto, hii ni mara ya pili tunafanya mazungumzo kuhusu sekta ya elimu. Unachukuliaje matokeo mapya ya kidato cha nne baada ya kufutwa yale ya awali?

ZOTTO: Ningepata hata Daraja la Tatu wakati ule nikiwa sekondari, hakika leo ningejivunia sana kuliko hizi  madaraja ya kwanza ya matokeo haya.
Kipindi tunasoma Sekondari ya Ilboru, tulitaka kugomea mtihani wa Mock ya Mkoa baada ya kusikia tetesi kuwa imevuja. Tuliposikia mtihani wa Taifa, nayo imevuja na hivyo maswali yamekuja kwa fax, nakumbuka nilimwambia mwenzangu Frank Mirindo afadhali tukalale kuliko kuona maswali hayo. Leo hii serikali imewafanyia wanafunzi NECTA. Sitashangaa hata wakifanyiwa wanafunzi wa kidato cha sita.

SWALI; Tukichambua matokeo ya haya ya pili unadhani ni suluhisho kwa uamuzi uliochukuliwa na serikali?

ZOTTO; Hapa naona imekuwa kama suluhu ya mchezo wa mpira hapa nchini, ambapo timu zilikuwa zinapewa ushindi wa mezani, lakini hawa wadogo zetu wameiumbua serikali kwa kuiambia mazingira ya elimu ni mabovu. Hata hivyo, si unajua serikali yenu ni sikivu? Haya liwalo na liwe!

SWALI; Inaelekea hujaridhishwa na matokeo  mapya. Huoni kuwa kuna sababu za msingi kufutwa matokeo?

ZOTTO; Sioni sababu mpya hata kidogo hapo, maana siku hizi visingizio vingi;- Walimu hawafundishi, Walimu hawana sifa, hakuna Maabara, hakuna Maktaba, kuna twisheni, shule fulani wanafundisha vizuri, serikali isaidie kufaulisha. Ndugu yangu ninajua fika mwisho wa hayo matokeo na visingizio, ila wenyewe walioamua kufuata, watakuwa ndio wanaondoka madarakani, lakini ukweli utabaki ukweli kwamba elimu yetu ni bomu.

SWALI; Unaamini kuna siku vyuoni wanafunzi wataandamana kupinga matokeo, na mtakuwa tayari kuyafuta? 

ZOTTO; Mimi naeleweka kwa msimamo wangu, haitatokea huo upuuzi kwangu. Kuna chuo waliniletea mizengwe kisa niliwaambia sina marks (alama) za mezani. Ila walijua uwezo wangu na wanalitambua hilo. Niliwaambia, mimi nitabaki kusimamia taaluma na sipendi fedheha. Hawa wanafunzi wakiwa chuoni wanataka wapite tu hata kama hawastahili, lakini wakimaliza wanajua mwalimu gani mbabaishaji. Katika taaluma, tuna evaluation za aina mbili, formative na summative evaluations.

SWALI; Takwimu zipo wapi na zinazonyesha mabadiliko ya matokeo. Je, unadhani takwimu zitasaidia kuboresha ufaulu wa wanafunzi wetu?

ZOTTO; Mimi si muumini wa takwimu japo nilifaulu vizuri. Udhaifu wa takwimu ni kukosa maelezo na hivyo watu kufikiri namba ni ukweli. Ina maana gani ufaulu umeongezeka kwa desimali, maelezo yapoje? 

 Shule zimepata daraja la kwanza wanafunzi 6, darja la tatu ndo lukuki na la nne. Kipimo cha ufaulu ni daraja la 4 ambao hawastahili kwenda vyuoni na tumefuta vyuo vya ufundi? Kwa sababu hiyo, naamini kuwa wanafunzi wamefeli na matokeo ni hovyo. Ingekuwa zama zetu ambapo vyuo ni viduchu, hawa watu wengi wasingeenda vyuo vikuu. Hata hivyo, wengi hawastahili kwenda vyuo vikuu. 

Hizi division one zimekuwa adimu kwa nini? Mwaka wetu kati ya wanafunzi 100, zaidi ya sitini ilikuwa division one. Sasa tunajipongeza ufaulu wa desimali na daraja la tatu na la nne? Tumeua Polytechnics, sasa hawa daraja la nne wataenda wapi? 

Kwanini sisi tunawaza kuwa maana ya elimu ni kufika chuo kikuu tu? Plato alikuwa sahihi kutoa mgawanyiko wa elimu japo watu wamesema kuwa ni matabaka, akatoa makundi yao Golden Boys, Silver boys na Iron boys.Tusio na uwezo wa kuingia chuoni basi twendeni sehemu zinazostahili. Lakini je, hivyo vyuo vipo? Hatma ya hawa laki mbili walofeli ipoje, hii itasaidia kuleta mapinduzi.

SWALI: Kuna vyuo vingi vimeanzishwa hapa nchini. Karibu kila mwaka utasikia chuo kikuu kimeanzishwa. Una mtazamo gani katika suala hili? 

ZOTTO: Hapana hapata shida, najiuliza mengi. Hivi vyuo vyetu vilivyoota kama uyoga vinakidhi mahitaji ya elimu tunayoyahitaji? Kila chuo kipya hasa binafsi vinatoa shahada ya elimu hata kama kuna upuuzi mkubwa! Mmeamua kufanya elimu kuwa biashara. Hawa walimu wakitosha, hivi vyuo vitatoa shahada gani? Na je tuko washindani kuuza wahitimi wetu nje ya nchi? Na hizi kozi zetu zina tija? Mitaala yetu haina mashiko.

SWALI; Kuna tofauti gani ya elimu ya zamani ambayo ilikuwa inafundishwa na walimu wa UPE na waliopo sasa baadhi yao ni zao la mafunzo ya muda mfupi. Unadhani nini hasa kinasababisha kuwa na tofauti yoyote kuzalisha wanafunzi bora kutoka makundi haya mawili ya Walimu?

ZOTTO; Ni kweli kuna kipindi tuliambiwa kulikuwa na walimu wa UPE na wasio na adabu wakawaita walimu weupe, hebu angalia waliopo madarakani nani hakufundishwa na hao walimu? Leo hii hali ikoje? Sitaki turudi nyuma, lakini tujifunze kwanini wale walifundisha na tukaandika mwandiko mzuri lakini leo hii wanafunzi wanaingia kidato cha kwanza hawajui kuandika majina yao.

SWALI: Katika mahojiano yetu ya kwanza ulisema wanafunzi ni wazembe kupindukia. Ni kwanini una mtazamo huo?

ZOTTO: Wanafunzi wanapenda sana mteremko hasa huku vyuoni na haya ni matokeo ya kubomoka ngazi za chini, wakiambiwa wakafanye citation, wao wanataka kuandika essay kama barua iendayo kwa wapenzi wao. Yaani ile morali ya kazi haipo tena, unaweza kuona wanafunzi wanasoma kozi fulani na wanaiona ngumu bila sababu yoyote.

SWALI:  Je wanafunzi wetu wanajibidisha kupanua uelewa na ushindani katika soko la ajira ndani na nje ya nchi pamoja na sifa zinazostahili?

ZOTTO: Lazima tuwe na maswali ya msingi tupate muongozo. Mitaala yetu ya elimu inatoa fursa kwa wahitimu kuajiriwa nje ya nchi? Wanafunzi wetu wanaandaliwa kwa masoko ya nje na wanajiamini ipasavyo?Ukimchukua mhitimu wa chuo X atalinganishwa na mhitimu wa chuo Y ambao wote wamesoma masomo hayohayo? Napata wasiwasi napoona baadhi ya wahitimu wa vyuo vikuu hawawezi kuandika CV. 

Kwenye elimu tumekoroma maana huwezi ukajieleza kwenye usaili kwa kuwa eti CV sio muhimu. Kitu cha kwanza kwenye usaili watahitaji kujua wewe ni nani, kwahiyo CV mbovu itakuwezeshaje usaili. Huanzi kuomba kazi kwa usaili bali kwa CV. Watu wanatumia vyeti vya marehemu, wengine vya walioenda high school wakaenda kusomea ualimu.
Tukianza kufuatilia cheti cha kila mtu makazini humu jamani sijui wangapi watapona.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako