October 11, 2017

CATALUNYA IMENIKUMBUSHA WIMBO WA TAIFA WA HISPANIA.

NA HONORIUS MPANGALA, 0628994409
 
ILIKUWA katika mechi ya kombe la dunia mwaka 2002,Korea kusini na Japan ndiko nilipohitimisha majibu ya maneno ya kusimuliwa. Kaka yangu alikuwa mtu aliyependa kunisimulia kuhusu vibweka vya kwenye soka tangu zamani na hajaacha hadi Leo. Naweza kusema ndiye aliyefanya nikawa napenda soka na kulichambua.
Wachezaji wa Hispania wakishangilia moja ya mabao waliyofunga.
Katika fainali zile pale Korea na Japan ndipo nilipoamini kweli taifa la Hispania halina maneno katika wimbo wake wa taifa. Ilikuwa katika moja ya mechi iliyokuwa na msisimko mkubwa kundi B, Hispania dhidi ya Afrika kusini. Mchezo uliopigwa katika uwanja wa Daejeon katika mji huo nchini Korea kusini.



Mechi ilimalizika kwa magoli ya 3-2 lakini ikiwa na upinzani mkali. Hapo unaizungumzia Bafana Bafana ya Lucas Radebe na Ben McCarthy. Na Hispania ya Raul Gonzalez na Gaizka Mendieta. 


Alianza Raul Gonzalez dakika ya nne, bao lake likasawazishwa na Ben McCarthy dakika ya thethini na moja. Gaizka Mendieta akafunga dakika ya arobainina tano lakini walipotoka mapumziko dakika ya hamsini na tatu Radebe akasawazisha. Bao hilo halikudumu muda mrefu dakika tatu baadae Raul tena akawainua wa Hispania.

Sasa moja ya vile vibweka kabla ya mechi ndo nikichokiona katika timu kuimba myimbo za taifa. Wakiwa katika mstari niliwasikia Vijana wa Thabo mbeki wakati huo wakiachama midomo yao huku wakiimba ule wimbo pendwa wa 'Nkosi Sikelel'i Africa' yaani Mungu ibariki Afrika uliotungwa na Mwalimu Enock Sontonga. Wimbo huo ndio uliochukuliwa ubeti wa kwanza na taifa letu la Tanzania na kuongeza maneno katika ubeti wa pili na tukautumia hadi Leo.


Zamu ya wahispania ilipofika nilishangaa kuona vinywa vya wachezaji wa Hispania havinyanyuki na kuimba chochote. Maneno ya kaka yangu nikahitimisha pale kwani aliwahi niambia juu ya hilo nilisubili kuhakikisha. Licha ya kuwa na Ala nzuri ya mziki katika wimbo wao wa taifa ambao unaoitwa 'La Marcha Real' lakini hawakuwa na neno la kutamka.

Nilipotazama nyuso za kina Fernando Morientes zilikuwa zikionyesha heshima kwa taifa kwa kusimama kwa utulivu kama ilivyo kawaida ya nyimbo za taifa lakini ndani ya sekunde 56 za 'La Marcha Real' hakukutoka neno lolote.
La Marcha Real ni wimbo uliotungwa ala yake ya muziki na mmoja wa makamanda wa jeshi la Hispania aliyeitwa Fransisco Gau Vegara. Kutokana na kushiriki katika kikundi cha muziki jeshini ndipo alipotunga wimbo ambao kutokana na mvutano ilikuja kubakishwa ala pekee bila maneno.

Hispania ni miongoni mwa mataifa manne ambayo hayana maneno katika wimbo wa taifa.Nchi kama Bosnia & Herzegovina,Kosovo na San Marino ni miongoni mwa mataifa ambayo yanatumia ala pekee bila maneno.

Ziko sababu zilizopelekea haya kuwepo katika mataifa haya kutokuwa na maneno katika wimbo wa taifa. Kwa nchi ya Hispania Tangu zama utawala wa mfalme Alfonso XIII ilishindikana kupatikana maamuzi ya lugha ya kutumia katika wimbo wa taifa.

Kutokupatikana kunatokana na mvutano uliotoka katika jamii zilizoonyesha kuwa na msimamo kwa kutaka lugha yao itumike na wengine wakikataa kutumia lugha wenzao katika wimbo huo. Licha ya kuwepo kwa lugha ya kihispania lakini jamii hizi zilionyesha kutaka kupata mamlaka katika wimbo kutumia lugha yao.

Jamii ya watu Basque ambako ndiko unakopatikana mji wa Bilbao walikuwa na msimamo wao. Na ni kati ya majimbo yanayosemekana kuwa na ubaguzi mkubwa nchini Hispania. Pia watu wa Katalunya iliko Barcelona nao walivutia ngozi kwao. 
Kocha mkuu wa Timu ya taifa ya Hispania, Julem Lopetegui
Na watu wa jamii ya Galician ambao wenyewe hujiita 'Galego' wakiwa kaskazini magharibi mwa Hispania katika mji wa Santiago de Compostela walitaka lugha yao itumike. Wale wa wanaozungumza ki-castile kutoka maneno ya Madrid na Salamanca nao walitaka kuimba kwa lugha yao.
Katika lugha nyepesi unaweza kusema Hispania kuna ubaguzi wa kila jamii kujiona bora kuliko nyingine. Na imekuwa ni mambo ambayo yametoka Tangu zama za viongozo wao kama Dikteta Fransisco Franco hadi Leo. 

'Umimi'walioupanda Tangu utawala wa viongozi hao umeendelea kuwatafuna hadi sasa.Ni rahisi kwa Ander Herrera kukubali kiwepesi kwenda kucheza katika klabu ya Athletic Bilbao na ukamshangaa akitosa kwenda Real Madrid au Bercelona. Hii yote kutokana na ubaguzi waliokua nao Tangu wangali wadogo kule Basque. 

Wakati wa kampeni za majiji kuandaa mashindano ya olimpiki mwaka 2016, Rais wa kamati ya olimpiki nchini Hispania alichagua kutumika maneno ya wimbo wa klabu ya Liverpool. 'You will never walk alone ndo maneno ambayo kamati hiyo kupitia rais wake walitaka yaweze kufasiliwa na kutambwa katika ala ya 'La Marcha Real'. 

Hali hiyo ilitokana na jamii hizo za watu wa Basque, Katalunya,Galician na mengine kuandaa maneno kwa lugha zao. Na nafasi ya kuandaa mashindano hayo ikadondokea Rio de Jeneiro nchini Brazil.

Kinachoendelea sasa katika jimbo la Katalunya waweza kusema ni mwendelezo. Mwendelezo huu ni ule uliofanya kama waHispania kushindwa kuwa na maneno katika wimbo wa taifa. Ubaguzi ni zambi inayowatafuna Tangu zamani. 

Sitashangaa kuona watu wa Basque nao siku moja wakiamua kufanya harakati za kujitenga.Siasa na masuala ya utawala yamefanya taifa hilo kuweza kuingiza ubaguzi wao hadi katika soka. Ni rahisi kwa nyota wa Bilbao akacheze nje ya Hispania kama ilivyokuwa kwa Javier Martinez kucheza Bayern munich kuliko Barcelona.

Wakati Pep Guardiola akiwa kocha wa Barcelona alimhitaji katika vipindi tofauti mchezaji yule lakini ikashindikana. Lakini ilikuwa ni biashara inayoweza kufanyika kwa Bayern Munich kuliko kwenda Katalunya.
Ligi ya Hispania ilianzishwa na klabu tatu ambazo zinatoka katika maeneo tofauti yenye mvutano wa kiitikadi ya kiutawala wa kisiasa yaani klabu ya Bilbao toka Basque, klabu ya Real Madrid toka katikati ya nchi kwa jamii ya wacastile na Barcelona kutoka kwa wakatalunya.

Katika mataifa mengi ulaya yana ubaguzi wa kikanda au kijamii kama ilivyo kwa baadhi ya nchi hapa Afrika.Lakini wamekuwa watu wenye kuuficha ukweli na mwisho hutokea aibu kama hizi za kutaka kujitenga kwenye sababu za kibaguzi.

Vuta picha eti wimbo wa taifa letu usingekuwa na na maneno ya kuimba sijui mataifa ya ulaya Wangeongeleaje hilo. Kufanikiwa kwa Wakatalunya kujitenga ni ngumu kutokana na Hispania kutotaka kuaiachia Katalunya yenye kuchangia mapato ya nchi asilimia 20.

Watu wa Ulaya wana mengi ambayo ukichunguza unabaini ni kama vile wao wanavyozisema nchi za afrika kutokuwa na umoja.Wanaongea hayo mbele ya kamera lakini moyoni wakiwa na majibu kuwa aheli wawe kama walivyo kuliko kuungana kama ilivyokuwa malengo ya Muamary Gaddafi.

Tukio la Hispania katika jimbo la katalunya litakuwa na sura ya tofuati katika kuiweka hali sawa ya ligi yao ya BBVA. Maana ni kama siasa na ubaguzi umekolezwa miongoni mwa nyoyo za mashabiki na wachezaji.Ndo maana haikushangaza kuona mlinzi wa Barcelona Gerrard Pique akiwa anapiga kura huku Sergio Ramos akashikilia bendera ya taifa lao na kuonyesha uzalendo.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako