October 27, 2017

KWANINI WILAYA YA NYASA IMESHIKA MKIA KATIKA MATOKEO YA DARASA LA SABA?



RAYMOND NDOMBA, SONGEA
WILAYA ya Nyasa iliyopo mkoa wa Ruvuma imekuwa ya mwisho katika matokeo ya darasa la saba mwaka huu 2017 kimkoa. Swali la kujiuliza ni kwanini hali hiyo imetokea. 


Mawazo yangu ni haya; Pamoja na sababu nyingi zilizosababisha matokeo hayo ya aibu kubwa. Wazazi wanapaswa kubeba lawama kubwa. Wengi wao hawafuatilii maendeleo ya watoto wao, pia makuzi na malezi mabaya.

Miaka ya hivi karibuni (kuanzia mwaka 2000), Wazazi wengi katika wilaya ya Nyasa hawajali elimu, hawajigusi katika ufuatiliaji wa watoto wao kielimu na hata kitabia (Angalia matokeo ya mitihani ya Taifa ya shule za msingi na sekondari kunzia miaka hiyo ya 2000 kwa shule kongwe ndani ya wilaya). 


Wazazi wanapenda tu kuona mtoto anakwenda shule ila sio kufuatilia ili afahamu mtoto huyo anafanya nini huko shuleni. Hawajigusi hata kujua kama mtoto kalala ndani au yuko wapi nyakati za usiku (saa 1 adi 6 usiku). Binafsi katika janga hili, asilimia 75 za lawama zangu nazielekeza kwa wazazi. 

Mwezi wa 8 na 9, 2017 nimekaa sana Nyasa. Nimetembelea Tingi, Chimate, Kwambe, Likwilu/Kilosa, Mango, hadi Lituhi; katika maeneyo yote niliyopita wazee kwa vijana wako sambamba na wanzuki (Mabobo). Muda wote na siku zote za wiki wao ni mitungi tu. 


Sehemu kama Kwambe, Matenje, Mtipwili, Ruhekei, Kilosa, Maporomoko Liuli, Lundu, Mbaha, Lituhi nk; nimeshuhudia wazee kwa vijana wakiwa wanakunywa komoni/wazuki (Mabobo) kuanzia saa 2 asubuhi. Wazazi wengi wamejiweka mbali kabisa na mambo yanayo husu taaluma. 

Kwao kazi ya malezi, makuzi na maendeleo ya watoto wao kitaaluma ni jukumu la mwalimu. Kitu ambacho si sahihi. Kila mwana Nyasa aliangalie tatizo hili kwa jicho la pekee. Tukawaelimishe wazazi wetu, ndugu zetu na watoto wetu juu ya umuhimu wa ufuatiliaji wa karibu wa maendeleo ya kitaaluma na kitabia ya watoto wetu waliopo shuleni.

Katika hili, binafsi napingana na wale wanaoelekeza lawama zao kwa Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Stella Manyanya. Tatizo hapa lipo kwetu wenyewe (wana Nyasa). Ili tuitatua changamoto hii, yatupasa tuanze kuangalia upya makuzi na malezi ya vijana wetu kuanzia ngazi ya familia pamoja na kufuatilia mienendo yao kitabia wakiwa nyumbani na hata shuleni. 

Hatuwezi pata matokeo chanya kwa watoto wenye tabia hasi, hatuwezi pata vijana wenye mitizamo ya kimaendeleo toka kwa familia isiyo fuatilia malezi, makuzi na mienendo ya mtoto wao kitabia na kitaaluma na hatuwezi pata matokeo chanya toka kwa viongozi wa elimu wenye uwezo mdogo kitaaluma. 

Baadhi ya wakuu wa shule na maafisa walishindwa kwenda kujiendeleza kitaaluma kwa nia ya kulinda vyeo vyao. Na baadhi yao walichangia sana kushuka kwa kiwango cha elimu kwa vile walikuwa wanashindwa kusimamia majukumu yako ipasavyo na wengine kushindwa kuwawajibisha walimu wengine walio wazidi kitaaluma.
Baadhi ya Majengo ya Mbamba Bay High School yakiendelea kujengwa.
Tukiacha kubadilika na kuchukua hatua mapema hata hiyo “Mbamba Bay High School” ambayo inajengwa kwa kasi na majengo ya kisasa, itakuwa ni jiko la kuwapika vijana toka nje ya wilaya ya Nyasa.
Mwaka 2016 vijana wa kidato cha nne Lundo Sekondari waligoma kufanya mitihani ya muhula kwa madai eti itawapotezea muda wa kujisomea kwa ajili ya maandalizi ya mtihani wa Taifa. Nini chanzo cha tabia kama hii na wanafunzi wale walitoa wapi ujasiri wa kuwagomea walimu wao? TABIA TABIA TABIA.

Mwandishi wa makala haya ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Askofu James cha Mtakatifu Agustino-Songea, Ruvuma

No comments:

Post a Comment

Maoni yako