January 15, 2018

ELIMU BURE INAVYOTESA WATOTO WA WANANCHI WA HALI YA CHINI

NA HONORIUS MPANGALA
KITAALUMA na hisia zangu zimenifanya niwe mtu tofauti kabisa kuhusiana na matumizi ya baadhi ya maneno hapa nchini. Mengi hutumiwa na viongozi wa ngazi za juu kuwaona wale waliopo chini au wasio na vyeo kama wao kuwa  wenye kiwango fulani cha dhiki kinachostahili kuitwa cha chini. Ni hapo ndipo nakuwa na hisia tofauti sana juu ya kutumia maneno fulani dhidi ya kundi jingine hasa lile ninaloongoza au viongozi wanaloliongoza. 
Japokuwa nimekuwa mtu nisiyependezwa na na hili neno “Wananchi wa hali ya chini”' lakini najiuliza hao wa hali ya juu ni akina nani, wanafanya nini kutokuwa na hali ya chini na njia zao zikoje ili tuwaambie wa hali ya chini wajifunze kwenda huko juu? 
Suala elimu katika nchi yoyote ni muhimu na linatakiwa kupewa kipaumbele sana. Kiuhalisia mazingira ya wanafunzi kwa shule nyingi zinazomilikiwa na serikali zimekuwa na changamoto kubwa na kupelekea hata matokeo mabaya kwa shule hizo. Lakini unakuta baada ya kutazama wapi walipojikwaa wao wanakawaida ya kulaumu mwendo Wa aliyedondoka kuwa hatazami vyema au hatembei vyema.

Tangu iliposemwa elimu bure maisha ya wanafunzi yamekuwa na changamoto zake na wazazi waliipokea katika mitazamo yao hii hoja. Kutokana na kuzoea kupewa pewa tangu zama za wakaloni, waafrika wengi wamekuwa wavivu wa kujitafutia wao na kutatua changamoto wao huku wakitegemea tusaidiwa kama ilivyokuwa katika maisha ya ukoloni au kwa wale waliokuwa wanaishi karibu na Taasisi za kidini zilivyokuwa zikitoa misaada.

Maisha yamebadilika wananchi kama wangetambua kuwa maendeleo ya kila mahali yanategemea nguvu zao wakisaidiwa na serikali na wakaishi hivyo basi changamoto nyingi zingetatuliwa na wao wenyewe.

Baada ya tamko la elimu bure wazazi nao wameacha kila kitu ,unakuta mzazi anashindwa hata kumrekebishia mwanae sare ikiyochanika au kufumuka akielekezwa anajibu elimu bure. Wako wanaofikiria elimu bure hata vitendea kazi vya mwanafunzi navyo hutoka kwa serikali.

Kwa upande wa serikali nao wanawajibika katika kuhakikisha kuwa watendaji wao wanafanya kazi ya kutatua changamoto, zinazojitokeza katika taasisi zao. Kata ina diwani lakini diwani hana hata idadi ya upungufu wa watumishi anaohitaji kuwa nao katika kata yake. Sasa unajiuliza huu uwakilishi wake uko kwa namna ipi.

Shule hazina madawati, wanafunzi wanakaa chini tena sekondari kitu ambacho kinashangaza sana. Zamani ilikuwa wanafunzi wanaripoti na dawati na ilisaidia wanafunzi wote kukaa kwenye madawati, leo hii wanakaa chini ajabu sana.

Hii elimu bure wananchi wanatakiwa kuitathimini wenyewe vyema. Miaka ya nyuma tulikuwa tunaona wananchi wakijitolea kufyatua tofali na kujenga nyumba za watumishi lakini leo hakuna mwananchi anayetaka kushiriki katika shughuli za kimaendeleo katika jamii husika.

Tusingeona upungufu wa madarasa, nyumba za waganga, walimu na hata nyumba za watendaji wa vijiji kama serikali ingekuwa iko wazi kwa wananchi juu ya miradi ya maendeleo. Tatizo kila jambo hulifanya kwa kuegemea katika masuaka ya kisiasa na kuacha uhalisia wa kiutendaji ndiyo maana wananchi hawana muda wa kushiriki katika miradi ya serikali kwa kujitolea badala yake hushiriki inapokuwa kwa malipo peke yake.

Tujitafakari kama hii nchi inajengwa na wananchi au kila mwananchi anajenga familia yake. Na kuiacha nchi ikijengwa na serikali? Tukitafakari kwa undani unagundua hili ni tatizo la kutojiweka wazi kwa wananchi juu ya mipango wanayoifanya kwani inakuwa a chembe ya kisiasa.

No comments:

Post a Comment

Maoni yako