October 12, 2012

UELEWE MRADI WA FRESH FARM(T) NA KILIMO CHA MITI. HAPA NI MAELEZO KAMILI JINSI YA KUFANIKISHA MRADI HUO


ALBERT SANGA; NATAKA KUOKOA MAZINGIRA NA KUWATAJIRISHA WATANZANIA

Albert Sanga(katikati) akiwa na mgeni wake kutoka Chuo Kikuu cha Moshi alipotembelea Mradi wa kampuni ya Fresh Farms(T) katika mashamba yake yaliyoko eneo la Mapanda, huko mufindi mkoa wa Iringa.
 SWALI: Habari za kazi ndugu Sanga. Watanzania wangependa kufahamu zaidi, nini hasa uanchomaanisha kuokoa mazingira na kutatajirisha watanzania?

SANGA: Nashukuru ndugu yangu, kazi zinakwenda vizuri na hakika hii ya kuokoa mazingira imenipa wasaa wa kujadiliana na wadau mbalimbali nchini. Lakini dhumuni langu ni kuwatajirisha watanzania.

SWALI: Bado hujatoa jibu, ni kwa vipi unaweza kuokoa mazingira na kuwatajirisha watanzania kwa wakati mmoja?

SANGA: Kwa muda mrefu sana nimekuwa nikinuia kuzikomboa fikra za watu kutoka kuitazama serikali kwa kila kitu kuja katika kutekeleza wajibu wao ipasavyo. Nalenga hasa kuanzia uhaba wa kifedha kwenda katika utele wa kifedha na kuwa na mfumo chanya wa kufikiria.

SWALI: Ni hilo tu ndio linakusukuma uokoe mazingira, ama njia nyingine ya kutunza mazingira kwa kuhimiza utajiri?

SANGA: Ndio maana nimesema kukomboa fikra za wengi. Mkondo huu ni kuingia katika utekelezaji/matumizi ya fikra chanya. kwahiyo kuna mradi wa kibiashara ambao napenda watanzania washiriki kujitajirisha katika biashara ya miti. Nitakueleza kila kitu ikiwemo, hali ya biashara hiyo kwa sasa na miaka ijayo, gharama na hatua za kuanzisha biashara hiyo, usimamizi wa biashara hii, nadhani miti itaokoa mazingira pia.

SWALI: umezungumzia biashara ya miti ambayo ndio msingi wa kuwatajirisha watanzania, halafu unasema unaokoa mazingira. Je unaweza kueleza namna ya biashara ya miti ilivyo na jinsi ya kuokoa mazingira?

SANGA: Lazima nikiri kilimo cha miti kimepata umaarufu kwa miaka ya karibuni kutokana na ongezeko la mahitaji ya mazao ya miti na changamoto ya mazingira.

Hapa Iringa tunaongoza kwa misitu mikubwa ya kupandwa. Sasa hii, miti inatumika kwa mbao, nguzo za umeme, nguzo za kujengea pamoja na utengenezeaji wa karatasi.

Hapa najua wengi tumezoea kuona mashirika ya kimazingira kutoka Ulaya yananunua hewa ukaa.

Kwa maana hiyo unaweza kupanda shamba la miti halafu ukawa unakusanya dola kwa kuuza hewa ukaa wakati ukisubiri miti ikomae uvune mbao, nguzo ama miti ghafi ya kutengenezea karatasi. Utakuwa umeokoa mazingira pia.

Albert Sanga akiwa na mgeni wake Emmanuel Lulandala kutoka Chuo Kikuu cha Biashara na Ushirika cha Moshi
SWALI: Umeeleza kuwa kuna mashirika kutoka nchi za Ulaya yananunua hewa ya Ukaa, kisha unazungumzia pia biashara ya miti, hivi unatenganisha vipi haya mambo matatu?

SANGA: Binafsi niliichangamkia biashara hii miaka minne iliyopita. Nimejiwekea lengo la kupanda miti ekari ishirini kila mwaka.

Kilimo hiki cha miti ni uwekezaji wa muda wa kati na mrefu. Unajua tena, Watanzania wengi huwa hawavutiwi na uwekezaji wa muda mrefu.  

Lakini kama una mpango kuimarika kiuchumi usikwepe kufikiria uwekezaji wa muda mrefu. Waingereza husema “Information is power”.

Wengi hawajachangamkia fursa hii kwa kukosa taarifa tu. Ndio maana nasema wenzetu Ulaya na Amerika wananunua hewa ya Ukaa, sisi tusizubae kwa hilo. Kilimo cha miti ndio suluhisho.

SWALI: Sawa, kwahiyo unataka kusema kuna ekari ambazo zinauzwa kwa wateja ama watanzania wanaotaka kuanzisha kilimo cha Miti hapa Iringa na gharama zake zipoje kwa manufaa yao?

SANGA: ndiyo, zipo ekari zinauzwa, kwa utaratibu rasmi na kwa mujibu wa sheria ya ardhi. Kwa mfano ekari moja ya shamba inachukua wastani wa miti mia sita (600).

Wastani wa chini wa mti mmoja kwa sasa uliokomaa ni shilingi elfu ishirini (20,000). Ina maana katika ekari moja ukiwa na miti iliyokomaa unakusanya jumla ya shilingi milioni kumi na mbili (12,000,000).

Hiyo fedha ni kadirio la chini sana, utaipata ikiwa unaamua kuuza kwa bei ya jumla miti ikiwa shambani.

Lakini kama ukiamua kupasua mbao mwenyewe unaweza kuvuna mbao hadi za milioni ishirini na tano (25,000,000) kwa ekari moja.

                 
maeneo ya Mufindi yanafaa pia wka kilimo cha Chai. Ni mji wenye uoto wa asili na udongo unafaa kwa Kilimo cha Miti na Chai
SWALI: Hivyo kilimo hicho cha miti kinalenga kupasua mbao na kuziuza. Huoni kuwa hilo la miaka minne na gharama za upasuaji mbao zipo juu, unadhani mteja atamudu namna gani kwa hilo?

SANGA: Hapana, hakuna gharama za moja kwa moja hapa, kumbuka Iringa ni mkoa wenye miundombinu nafuu. Kwa mfano gharama za kununua shamba tupu ni shilingi laki mbili hadi milioni moja, kutegemea na maeneo unayotaka.

Gharama za kuandaa shamba, kununua miche na kupanda ni kati ya shilingi laki nne hadi laki sita. Hii ina maana unaweza kumiliki ekari moja ya msitu wa miti kwa shilingi laki sita tu!

SWALI: Je,suala la ulinzi na usalama wa miti hiyo linakuwa mikononi mwa mteja au muuzaji, na kuna utaratibu gani katika suala hilo?

SANGA: Kwanza elewa kilimo cha miti ni rahisi sana kwa sababu ukishapanda hakihitaji uangalizi mkubwa na wala huhitajiki kuwa karibu na shamba/mradi muda wote.

Kuna kazi chache ambazo zinahitajika ukishapanda shamba lako. Mvua inyeshe ama isinyeshe mti wa mbao, nguzo ama karatasi ukishachipua huwa haufi kwani huendelea kutumia unyevu wa ardhini.

Kazi namba moja unapokuwa umeshakamilisha upandaji wa miti kwenye shamba; ni kutengeneza njia za kuzuia moto walau mara moja kwa mwaka, kazi ya pili ni kufyekea miti inapokua walau kwa mwaka mara moja (prooning). Gharama zote hazizidi laki mbili kwa mwaka mzima.

SWALI: Kwahiyo unataka kusema kilimo hicho kina muda wake kama kingine. Na, je miti hiyo inachukua muda gani hadi kukomaa kisha mteja akavuna faida?

SANGA: Ndio maana nasema nataka kuwatajirisha watanzania. Hii miti hukomaa kuanzia miaka sita hadi kumi, lakini inategemea na utunzaji wako.

Kwa mfano ukichukua shilingi laki mbili kugharimia shamba kila mwaka ukazidisha mara sita unapata shilingi milioni moja na laki mbili (1,200,000/=) na ukizidisha mara kumi unapata shilingi milioni mbili (2,000,000/=).

Gharama za kuhudumia shamba la miti ekari moja kutoka kupandwa hadi kuvunwa ni kati  ya shilingi milioni moja na laki mbili na milioni mbili.
Ukichanganya na gharama ya kupata ardhi na kupanda miti yenyewe unapata kuwa gharama nzima hadi unavuna ni kati ya shilingi milioni milioni mbili (2,000,000/=) kwa kadirio la chini sana.

SWALI: Suala hilo la kilimo cha miti bila shaka inakusudia kuwa biashara yenye tija kwa mmiliki. Lakini wewe umesema mwanzoni kuwa unakusudia kutunza mazingira. Je utafanya hivyo kwa namna gani?

SANGA: Nadhani unafahamu kuwa ardhi ni rasilimali inayopanda thamani kila siku. Vile vile tunatambua kuwa suala la mazingira ni tete kwa sasa na katika karne zijazo kama wataalamu wanavyosema.

Kwahiyo sisi Fresh Farm(T) ukiwa na shamba la miti leo; thamani ya ardhi hiyo inazidi kupanda kila siku na miti uliyopanda inazidi kupanda thamani kila kukicha.

Jambo la uhakika ni kuwa hata kama bei ya miti, mbao, nguzo itayumba hutaweza kupoteza mtaji uliotumia na wala hutakosa kuzalisha faida kwa shamba utakalokuwa umemiliki, iwe ni ekari moja, kumi, mia ama elfu moja.

Mbali na hivyo unaweza kudhani  miaka sita hadi kumi ni mingi mno; bado una nafasi ya kupata faida hata ndani ya mwaka mmoja, miwili n.k.

Ukishapanda shamba la miti ekari moja kisha baada ya mwaka mmoja ukaamua uuze utauza si chini ya milioni mbili hadi nne.

Kukusanya milioni nne kwa mtaji wa laki sita, pasipo kutumia muda mwingi ama usumbufu wa kusimamia; hakika ni faida nono. Na utakuwa umechangia kutunza mazingiara, hiyo ndio maana yangu ndugu.

SWALI: Sanga, watu wengine wanaishi Moshi (Kilimanjaro), Musoma (Mara) au Ilemela (Mwanza), wangependa wawe wakulima wa miti. Lakini hawapafahamu Iringa na hata kama wanafahamu wataanzia wapi kupata hayo maeneo, wengine wako mbali hawawezi kuhudumia shamba lao Iringa, watafanyaje?

SANGA: Ni kweli kwa wengine imekuwa changamoto. Lakini majibu hayakosekani.  Kiukweli msimu wa kutafuta na kuandaa mashamba sisi Fresh Farm (T) tunaanza Agosti na Oktoba na upandaji ni Novemba, Desemba na Januari.

Katika kuwasaidia wengine ili wawekeze katika biashara hii ya mashamba ya miti mimi na wewe tuungane na serikali na dunia nzima katika kupambana na mabadiliko ya tabia nchi kwa kupanda miti mingi.

SWALI: umekuwa ukitaja suala la Fresh Farm (T). Ni nini hicho ambacho kinaweza kuwaelewesha watanzania?

SANGA: ndugu yangu, siku zote napenda kuendeleza wafanyabiashara na wawekezaji wapya, kupitia mfumo wa biashara zetu. Hivyo tumeanzisha kitengo maalumu cha Fresh Farms (T).

Kazi yetu kupitia kitengo hiki itakuwa ni kutoa ushauri wa kibiashara, kutafuta maeneo ya kilimo cha miti hapa Iringa, na kiasi cha ekari anazohitaji mteja.

Kazi nyingine ni kuandaa hayo mashamba, kupanda miti na kusimamia utunzaji wa shamba katika hatua za awali.

SWALI: Ndugu Sanga, kwa kumalizia naona bado hujafafanua suala la umilikaji ardhi, yaani ekari zinazonunuliwa na mteja. Kuna utaratibu gani?

SANGA: sisi Fresh Farm (T) tunatumia sheria ya ardhi ya mwaka 1999, pia taratibu na tamaduni zote za wenyeji zinazohusiana na umilikaji ardhi. Tuna uhakika wa kutunza mazingira na kuwatajirisha watanzania. Nawakaribisha sana hapa Mufindi.

2 comments:

  1. nawatakieni kila la kheri pia mafanikio mema na kazi iende ikiwa imenyooka.

    ReplyDelete
  2. Nashukuru kwa maelezo yako mazuri sana.Ningependa kufahamu kama kuna mbolea yoyote inayohitajika wakati wote wa kutunza miti tya mbao.Kama ipo ni aina gani?

    ReplyDelete

Maoni yako