December 29, 2012

AZIMIO LA ZANZIBAR LILISAHAU B.E.E


Na Markus Mpangala 



Azimio la Zanzibar linafahamika kuwa nyenzo iliyotumika kuua lile la Arusha.
Ingawaje viongozi wetu hawasemi walichokubaliana kule Zanzibar, lakini hali haijifichi na inaonekana tunazidi kusonga mbele.
Kuna mtikisiko wa kijamii unaendelea kwa sasa, kutoka kwenye mitazamo na maisha ya ujamaa hadi kwenye kiwango cha chini cha ubepari. Bahati nzuri ni kwamba ujamaa upo mioyoni mwetu yaani ndio maisha ya watanzania.
Ni kwa sababu hii ndiyo maana Mwalimu Nyerere aliuita ujamaa wa kiafrika. Sasa basi, katika azimio la Zanzibar viongozi wetu bila shaka walikusudia kufanya mabadiliko katika uchumi. Bahati mbaya mabadiliko hayo yalikuwa yanafanyika kwa kudanganywa na Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Dunia.
Walichodanganywa viongozi wetu ni sera za asasi hizo kuwa mwongozo wa uchumi wetu. Halafu hali ikiwa mbaya wanachofanya ni kulaumu kuwa nchi imeshindwa. Sera za IMF na WB hazijali mazingira ya mwanadamu wa kitanzania.
Maeneo mengi imetokea hali hiyo na hivyo kuongeza kiwango cha ufukara kwa wananchi katika nchi husika. Ufukara huo unachochewa zaidi na jinsi sera inavyopuuza hali halisi ya mazingira ya nchi na utamaduni wa watu.
Sera za IMF na WB zinatokana na uzoefu wa nchi za Ulaya na Amerika. Kule wataimba nyimbo kuwa ruzuku ni muhimu kwa mkulima na wanakwenda nchi zetu za Afrika na kusema kama, ‘utampatia ruzuku mkulima basi unampunguzia uwezo wa kuwa mbunifu.’
Lakini hatujiulizi kwanini wakulima wa Ulaya wanapewa ruzuku na kadhalika. Sera za IMF na WB ndizo zilisababisha azimio la Zanzibar kuonekana kituko mbele wa wajuzi wa mambo.
Azimio hilo lililo katika kibarua cha Azimio la Arusha halikuja na mbinu mbadala ya kuweka msingi wa kukuza uchumi. Badala yake likaja na mageuzi ya uchumi katika mkondo wa sera za IMF na WB.
Kimsingi hilo lilikuwa kosa na dosari kiuchumi. Serikali yetu haikumwandaa au haikuhodhi moja kwa moja uchumi. Bali ikadanganywa na IMF na WB kuwa jambo muhimu ni kufungua milango ya mageuzi ya uchumi.
Milango iliyofunguliwa sio ile ambayo ilifunguliwa na chama cha siasa cha ANC cha Afrika Kusini. Chama cha ANC kilifungua milango ya mageuzi ya uchumi kwa sera yake, misingi yake na baadaye kikawa kinapokea ushauri tu.
Sera kubwa ambayo iliing’arisha ANC ni B.E.E. ( Balack Economic Empowerment). ANC ilikuwa wazi kabisa, hata kama sera hiyo iliwalenga watu weusi wa Afrika Kusini, na kuwatenga wazungu ambao ni raia halali wa nchi hiyo, lakini kilichofanyika ni kuziba pamba masikioni.
ANC ikasema inatambua kuwa B.E.E inaonekana kama inabagua lakini ni wajibu wao kutimiza uwezeshaji wa watu weusi katika mitaji ya kiuchumi. Mazao ya ANC ndio Tokyo Saxwalle, au familia ya kina Khoza.
Mfanyabiashara Tokyo Saxwalle anafahamika kuwa miongoni mwa matajiri wakubwa na wawekezaji wa kiwango cha juu kutoka jamii za waafrika. Ni kutokana na sera hiyo iliwezesha kuibua wafanyabishara, wawekezaji na wajasiriamali wengine ambao walifanya kila jitihada kwa kutumia sera ya B.E.E kufanikiwa.
ANC ikasema lazima watu weusi wawezeshwe. Tafsiri sahihi hapa ni kuwawezesha wazawa. Hali hiyo ilitokana na miaka mingi ya utawala wa kaburu kuwanyonya na kuwakandamiza watu weusi. ANC ilipania, ikathubutu, ikatimiza dhamira yake.
Ni sababu hiyo tunaona baadhi  wawekezaji wakubwa waafrika kutoka Afrika Kusini, vinginevyo ubaguzi ulioanzishwa na makaburu ungeendelea kuwafanya waafrika wabaki hohehahe.
Mfano wa pili ni Chujusong, Korea Kaskazini. Tangu mwaka 1925 Korea Kaskazini chini ya chama cha kikomunisti ilifanya jitihada kubwa ya kujenga uchumi huku ikitanganza kuwa ni Jamhuri ya Kisoshalisti.
Chujusong ni mpango wa kujitegemea kiuchumi. Msingi mkuu ulikuwa kuhakikisha mitaji ya kiuchumi inakuwa huru ili kuondokana na utegemezi kutoka nje. Sera hiyo ilichukua ngumu na kuhodhi mwenendo wa nchi hiyo kujenga uchumi wake.
Polepole mabadiliko makubwa yakajitokeza hadi Korea Kaskazini tunayoiona leo. Hapa kwetu sera ya wazawa tu ilitushinda, na kwakuwa tulikuwa tumekosa uelewa wa kutosha tukadhani sera hiyo inabagua.
Laiti tungelikuwa na msimamo na uelewa wa kutosha kuwa huo siyo ubaguzi sababu hata wageni walioingia nchini mwetu waliwabagua wenyeji. Kwahiyo ili kukabaliana na pengo lililokuwepo zama za ukoloni, ilipaswa serikali ya awamu ya pili ilipofungua milango kuruhusu mageuzi ya kichumi, itunge sera za B.E.E.
Mpango wa kuwawezesha waafrika sio dhambi. Mpango wa kuwawezesha wazawa sio dhambi. Wazawa hao maana yake tuwe na wawekezaji sampuli ya Reginald Mengi.
Watu wa aina yake tuwe nao wengi ili kuimarisha mitaji ya serikali na uchumi wetu. Tusipokuwa na misingi inayoakisi ustawi wa taifa kiuchumi, itawezesha fedha nyingi za Tanzania kuishia mikononi mwa wadokozi. 
Na wadokozi wengine tulipowajua wakati wa miaka ya 1990 ntumejikuta sasa nchi inabomolewa benki yake. Sasa baada ya kuipoteza misingi hii tumejikuta tunahamasisha ujasiriamali.
Tunahangaika na ujasiriamali sababu wakati wa kufungua milango ya mageuzi ya uchumi hatukujua mageuzi hayo yanafanyikaje na uchumi utakuwaje.
Milango iliyofunguliwa ikawa ni kuruhusu wachuuzi ambao walidhaniwa wawekezaji, wakawa wanachuma mali za watanzania. Sasa, akili inapoibuka kipindi hiki tunajikuta kumbe wakati tunazika azimio la Arusha tulipaswa kutamka kwakuwa lazima tuwezeshe wazawa. Lazima watu weusi wawezeshwe kwenye mitaji. Na iwe sera sio huruma. Kwa sasa tumejikuta tunao wawekezaji wengi kutoka nje, halafu wawekezaji wa ndani bado uwezo wao  sio mkubwa sababu hawakuwa sehemu ya mageuzi ya uchumi yaliyofunguliwa wakati ule.
 Nionavyo, tunatakiwa kuwa na sera za kuondokana na uchuuzi wa kijasiriamali. Lazima tujenge uwezo kwa wazawa. Lazima tuwaige ANC kwa sera ya Black Economic Empowerment. Tujiulize, hivi kuna ofisi ngapi za Benki ya Dunia na IMF katika nchi za Kiarabu? Jibu hakuna ofisi hizo kwakuwa hazihitajiki. Tafakari. Nahitaji changamoto. 

No comments:

Post a Comment

Maoni yako