November 14, 2012

SHULE ZA AWALI NYASA ZINAKABILIWA NA CHANGAMOTO LUKUKI


Na Albano Midelo, Nyasa
SERIKALI kupitia wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi iliamua kuanzisha mfumo wa elimu ya awali katika shule za msingi kwa lengo la kuwaandaa watoto wenye umri kuanzia miaka mitano.
Wizara ya elimu imedhamiria kuhakikisha kuwa watoto wenye umri wa miaka mitano hadi sita wanasoma darasa la awali kabla ya kuanza kuingia shule ya msingi wanapokuwa na umri wa miaka saba.
Uchunguzi uliofanywa katika kata za Kihagara na Liuli umebaini kuwa madarasa ya awali katika shule hizo yanakabiliwa na changamoto mbalimbali hali ambayo inaathiri utoaji wa elimu hiyo muhimu kabla ya kuanzia shule za msingi.

Wanafunzi wa Darasa la Awali wapatao 90 katika Shule ya Msingi PUULU, Kata ya LIULI, wilayani Nyasa wakiwa katika darasa ambalo halina dawati hata moja.

Mwalimu wa taaluma katika shule ya msingi Ndonga kata ya Kihagara Amos Kilongo anasema shule hiyo ina darasa la awali lenye wanafunzi 37 ambao wanasomea kwenye mti kutokana na kukosekana kwa chumba cha darasa na kwamba mwalimu anayefundisha katika darasa hilo ni aliyemaliza kidato cha nne.
“Wanafunzi wa darasa la awali hawana darasa wanasomea chini ya mti,pia darasa halina madawati wa awali wanakaa  wakati wa mvua wanafunzi hao wanasome katika kanisa katoliki ambalo tumewaomba wamiliki wa kanisa hilo wamekubali kutusaidia’’,alisisitiza.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kihagara Anet Ngindo anasema shule hiyo ina darasa la awali lenye wanafunzi 52 ambao wanasomea chumba cha shule ya msingi wakifundishwa na mwalimu ambaye hajapata mafunzo ya ualimu na sio mwajiriwa analipwa posho kupitia michango inayochangwa na wazazi.
Mwalimu mkuu katika shule ya msingi Tumbi  Evaristo Ndiwu anasema katika shule yake kuna darasa la awali lenye watoto 45 ambalo halina chumba cha kusomea ambapo mwalimu wake hana taaluma ya ualimu ni mhitimu wa kidato cha nne analipwa posho kutokana na michango ya wazazi na walezi.
Katika shule ya msingi Mango,mkuu wa shule hiyo anasema katika shule yake kuna darasa ka awali lenye wanafunzi 60 ambao hawana chumba cha kusomea na  wanafundishwa na mwalimu ambaye hajapata mafunzo ya ualimu sio mwajiriwa badala yake analipwa posho na wazazi kati ya shilingi 30,000 hadi 50,000 kwa mwezi.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ngehe Silivanus Mbeya anasema katika shule yake kuna darasa la awali lenye watoto 36 ambalo halina chumba cha kusomea na linafundishwa na mwalimu ambaye amehitimu kidato cha nne hana mafunzo ya ualimu analipwa posho na wazazi ambayo haikidhi mahitaji ya mwalimu huyo.

Uvuvi ni shughuli inayoongeza kipato na ukuaji wa uchumi kwa wakazi wa wilaya ya nyasa. hapa wavuvi wakiwa kazini.

Katika shule ya msingi Puulu  mwalimu mkuu wa shule hiyo Cathibert Maluka anasema katika shule yake kuna darasa la awali lenye wanafunzi 90 na kwamba wanafunzi hao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo na ukosefu wa madawati ambapo wanafunzi wote wanasoma kwa kukaa chini.
“Darasa la awali katika shule yetu limebahatika kuwa na walimu wawili ambao wamepata mafunzo rasmi ya kufundisha wanafunzi wa darasa la awali hali ambayo inawawezesha kutoa elimu ya awali kulingana na malengo ya wizara ya elimu licha ya wanafunzi kusomea chini’’,alisema .
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Nkali Erasmus Haule  anasema shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 210 ina darasa la awali lenye wanafunzi 45 ambao hawana darasa badala yake wanasomea kwenye banda ambalo jioni linatumika kama klabu cha pombe na kwamba mwalimu anayefundisha hajasomea.
Katika shule ya msingi Hongi  kwa mujibu wa mwalimu mkuu Simon Ndunguru shule hiyo ina darasa la awali lenye wanafunzi 52 changamoto kubwa hakuna chumba maalum cha kusomea na kwamba mwalimu anayefundisha sio mwajiriwa na wala hajasomea kufundisha darasa la awali.
Katika shule ya msingi Mwongozo yenye wanafunzi 654 inakabiliwa na changamoto ya ubovu wa darasa la awali lenye watoto 81 halina sakafu lina mwalimu mmoja ambaye hana mafunzo ya ualimu ,hajaajiriwa analipwa posho na wazazi wenye watoto hao
Baadhi ya wadau wa elimu katika kata za Kihagara na Liuli ambao ni Neema Msumba,John Ndunguru,Joel Makelele,Melikion Mapunda na Victor Komba wametoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa kila shule ya msingi inajenga darasa rasmi kwa ajili ya elimu ya awali badala ya shule nyingi kutumia vyumba vya shule ya msingi.
Wameitaka wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi kuhakikisha kuwa kila darasa la awali inapeleka walimu waliopata mafunzo rasmi ya namna ya kufundisha watoto wa awali badala ya tabia ambayo inafanywa na shule nyingi kuwatumia vijana ambao wamehitimu kidato cha nne huku wakiwa hawajapata elimu ya ualimu.
Mratibu elimu kata ya Liuli Abrahamu Challe amesema kata yake imejipanga kuhakikisha kuwa changamoto zote zinazoikabili elimu ya awali katika kata yake yenye shule saba zinatafutiwa ufumbuzi haraka ikiwemo kuwa na chumba rasmi kwa ajili ya awali,walimu na madawati.
Challe ametoa wito kwa serikali kutumia mfumo wa uboreshaji wa elimu ya awali kama ilivyokuwa kwa uboreshaji wa elimu ya msingi na sekondari kwa kujenga  vyumba viwili vya madarasa kwa kila shule na kusisitiza kuwa vifaa vyote vya ujenzi vitolewe na serikali na wananchi waachie ujenzi.
Afisa elimu msingi katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga David Mkali ambaye anahusika na wilaya ya Nyasa anasema elimu ya awali ni sera ya wizara ya elimu kuhakikisha kila shule ya msingi inakuwa na darasa la awali kwa lengo la kuinua elimu hapa nchini.
Ameahidi kushirikiana na viongozi mbalimbali wakiwemo madiwani,watendaji wa vitongoji,vijiji,kata,tarafa pamoja na wenyeviti wa vijiji kuhakikisha wanahamasisha wananchi katika maeneo yao kusimamia ujenzi wa madarasa ya awali na kutengeneza madawati ili watoto hao waweze kusoma katika mazingira bora.
“Ni ukweli madarasa ya awali yaliyo mengi yanafundishwa na walimu wasiopata elimu ni kutokana na uhaba mkubwa wa walimu uliopo katika shule nyingi nchini,lengo ni kuhakikisha tunapata walimu wa kutosha ikibidi hata kuwatumia walimu wanaostaafu kufundisha katika madarasa ya awali’’.alisisitiza.

Unaweza kuwasiliana na mwnadishi kwa anuani ifuatayo: albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

1 comment:

  1. Labda ilibidi kwanza kujenga majengo na kutafuta walimu wenye elimu na kisha kuanzisha shule...Tutafika kweli?????

    ReplyDelete

Maoni yako