Showing posts with label siasa.. Show all posts
Showing posts with label siasa.. Show all posts

February 12, 2018

ANA KWA ANA NA MBUNGE WA VITI MAALUMU CHADEMA, NDUGU UPENDO PENEZA


Sisi katika blogu yetu tunakutana na wanasiasa mbalimbali bila kujali itikadi zao. Au pia viongozi wa kila kada tunazungumza nao bila kujali fani zao. 
Madhali wengi wao ni marafiki zetu maana ni watanzania wenzetu basi huwa tunazungumza nao mambo yahusuyo  ustawi wa jamii yetu kwa ujumla wake. Tunazungumzia maendeleo ya elimu, uchumi, siasa, utamaduni, afya na kadhalika.
Madhumuni yetu ni kuendelea kuzungumzia maendeleo ya wananchi pamoja na furaha ya jamii. Tunajikita katika maslahi ya taifa letu. Tanzania ni nchi yetu na hatuna kwingine. Tutailinda na kuikosoa ikibidi.
Pichani; kutoka kushoto ni Gabriel Mushi (mwandishi wa gazeti la RAI), mhariri wa Blogu hii Markus Mpangala (katikati) na Mbunge wa Viti maalumu ndugu Upendo Peneza.

January 04, 2018

ITIKADI HAIELEWEKI, SIASA YA UTAIFA HAIPENDWI

NA MARKUS MPANGALA
KATIBA ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaruhusu wananchi wake kuwa wanachama wa chama cha siasa. Ni suala la uhuru wa kuchagua. Utashi wa mwanadamu pia unamfanya awe mwanachama, mfuasi au mtu yeyote mwenye kuamini kuwa ili awe mkamilifu lazima ajiunge na chama cha siasa.
Vyama vya siasa vimevuna wanachama kwa mtindi mwingi, ikiwemo mikutano, wanasiasa, familia,pamoja na ununuzi wa wanasiasa kutoka upande wowote.
Katika eneo hili wanachama na wanasiasa wote hupendelea sana kushabikia itikadi ya chama chao. Labda niseme kwanza maana ya Itikadi katika vyama vya siasa (hoja hii haitajikita kwenye upande mwingine wa itikadi). Wataalamu wa masuala ya sayansi ya siasa wanatuambia kuwa Itikadi ni mkusanyiko wa imani unaoshikiliwa au kuaminiwa na kikundi cha watu fulani. Kwahiyo Itikadi ni imani au mawazo fulani ambayo ni misingi ya nadharia za mfumo wa kisiasa au kiuchumi.

November 15, 2017

HALI YA ZIMBABWE MCHANA HUU



1.Waziri wa Fedha wa Zimbabwe Ignatius Chombo amekamatwa na Jeshi la Zimbabwe. Pia wanajeshi wameua walinzi watatu wa waziri huyo. (Chanzo: PaZimbabwe).
2. Jeshi hilo pia lilitembelea nyumbani kwa Profesa Jonathan Moyo ambaye ni waziri wa elimu ya juu, amekamatwa (Chanzo: NewsDay)
3.Baadhi ya mawaziri wameripotiwa kutoroka, wakiwemo Saviour Kasukuwere  na Makamu wa rais Phelekezela Mphoko anayedaiwa kukimbilia Afrika kusini.

October 30, 2017

TAARIFA YA KUNG’ATUKA LAZARO NYALANDU, MBUNGE WA SINGIDA KASKAZINI



NIMEAMUA kujiuzulu NAFASI yangu ya Ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, pamoja na nafasi zote za Uongozi ndani ya Chama kuanzia leo, Oktoba 30, 2017.

October 16, 2017

“RAIS ANA MIAKA 31”


Sebastian Kurz
JUMAMOSI nilikuwa nasoma makala ya James Masters kwenye tovuti ya CNN. Sentesi yake ya kwanza ilinivutia sana, “Ulikuwa unafanya nini ulipokuwa na umri wa miaka 31? Ingawa aliendelea na mengine lakini staili pekee haikuwa kivutio bali mtu aliyekuwa akizungumzwa alivutia zaidi.
James Masters alikuwa anamzungumzia Sebastian Kurz ambaye amewahi kuwa waziri wa  Ushirikiano wa Kimataigfa tangu mwaka 2013 akiwa na miaka 27.  Sebastian  Kurz ambaye amekuwa Kansela wa Austria mwenye umri mdogo zaidi kwani sasa hivi ana miaka 31 tu. 

Ni mwenyekiti wa chama cha  OVP. Sebastian kuanzia jana jumapili aanaongoza serikali ya Austria ( kama vile Rais hapa kwetu) baada ya chama chake kushinda viti vingi vya bunge. 

September 27, 2017

HOJA 10 ZA WABUNGE WA CHAMA CHA NRM


KAMPALA, UGANDA

1. Acha "Mamlaka ya Raia" iamue. Kuweka ukomo wa umri ni kuwanyang'anya ni kuwanyima mamlaka yao ya Kikatiba.
2. Uhuru wa Raia kuchagua wampendae uheshimiwe. Kama hawampendi kura zitaamua.

April 03, 2013

STRAIN THEOTY/CRIMENOLOGY VS UDINI NA DINI=CUHUMI?



Wataalamu kama Robert Merton waliwahi kusistiza umuhimu wa uhalifu katika jamii. Lakini kwa wataalamu hao hao wanasema, ikiwa njia za kujipatia pato zikibanwa au zikibinywa uhalifu ni kitu kinachochukua nafasi ambapo watu hutafuta pato kupitia njia zozote zile ikiwemo uhalfu. 
 
Wakasema kuwa kuna umuhimu wa uhalifu sababu unaileta jamii pamoja. Jamii inakuwa kwenye kutafuta njia mwafaka kumaliza uhalifu, lakini lazima jamii hiyo ijitolesheleze ndipo tunaweza kuufanya uhalifu kumalizika. .......

Naam kama nchi yenu haiongelei suala la ukuzaji uchumi, itaongelea nini? Kama tumeshuhudia watu kule Mwanza wanauana kisa HAKI YA KUCHINJA na kuvaa mavazi ya DINI kisha kumwaga damu, nini tafsiri yako? Je, umewaona wanaoshiriki zoezi la kuuana ni watu wa namna gani? ....je wale wanawezaje kuachwa katika faili la UCHUMI? Hatuna uchumi imara lakini hatutakiwi kuacha kutafuta UCHUMI imara.   

@Nakupenda sana nchi yangu TANZANIA. 

Hatutendi haki hata kidogo kutoandika 'aya' za uchumi wetu ambayo ndio msingi wa taifa letu na kumwachia Rais wetu Kikwete akihutubia mambo machache. Labda afadhali hayo machache kuliko kukosa kabisa. Kama tunataka kujenga utamaduni wa kutomwambia basi tunajenga taifa la watu wasioweza kufikiri au taifa la watu wanaopendelea mambo mepesi. 

Hatukatai kuona kuwa hotuba ya rais wetu haiwezi kuwaridhisha watu wote, lakini mimi naona kuna haja pia kuwakumbusha wale wote wanaohusika kuwa, wajaribu na waweze kufanya kitu ambacho kinaakisi jamii yao. Kama tunakubaliana kwamba uhalifu ni kitu kinacholeta jamii pamoja, na kwamba lazima jamii ijitosheleze basi yatupasa kujiuliza itajitosheleza katika lipi na kwanini? 

Lazima tumfanye rais wetu awe 'mgumu' kwa maana mtu 'mzito' kwa hoja nzito. Kwahiyo tusitegemee kuwa Rais anaweza kufanya hilo pekee bali lazima tusaidie, lazima kumfanya awe bora sababu ni mali yetu na tunajivunia yeye. Lakini kama kuna watu wanadhani kukosoa hotuba ya Rais ni dhambi ati sio saizi yetu hatuba budi kusema labda akina sisi tunaokosoa tumechanganyikiwa na tunakaribia kuchojoa nguo. 

Ni jambo baya sana tunapoona kila mtu anadhani waandishi wa hotuba ya Rais wanajua kila kitu. Lakini wanayo fursa ya kupata tafiti za kisasa za uchumi, makabrasha na kadhalika ili kuweza kuelezea jambo la msingi kuhusu hali ya maisha ya watu wetu. 

Ni vigumu sana kuamini kuwa Rais wetu anaandikiwa hotuba nusu, labda wenzetu walisahau, ila nakumbusha kama huijui jamii yako basi unaelekea kuchanganyikiwa. Turuhusu waandishi wa hotuba ya rais wawe hodari kwa kuwajengea hoja zenye maana sio kuwatusi. Tuwape nafasi ya kujisahihisha sababu wao sio miungu hata kidogo..

January 28, 2013

JE WAJUA ZANZIBAR ILIFANIKIWA KUWA MWANACHAMA WA UMOJA WA MATAIFA?


Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Siku kama ya Jana (Tarehe 16 Mwezi wa 12) miaka 49 iliyopita (mwaka 1963) Bendera ya lililokuwa Taifa la Zanzibar (sasa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania) na Bendera ya Jamhuri ya Kenya zilipandishwa Hewani katika Viwanja vya Umoja wa Mataifa huko New York, Marekani ikiwa ni ishara ya kutambulika Rasmi kwa Mataifa hayo kama Wanachama wapya wa Umoja wa Mataifa.

Zanzibar ilipata Uhuru wake Disemba 10, mwaka 1963 chini ya Utawala wa Sultan kama Mkuu wa Nchi na Uongozi wa Shughuli za Serikali wa Waziri Mkuu Sheikh Mohammed Hamad Shamte wa Ushirikiano wa Vyama vya Zanzibar & Pemba Peoples Party (ZPPP) na Zanzibar Natiolist Party (ZNP) au "Hizbu" cha aliyekuwa Waziri wa Kwanza Mambo ya Nje wa Zanzibar Sheikh Ali Muhsin Barwany.
Balozi Hilal Mohammed Hilal Al-barwan aliteuliwa kuwa Balozi wa Kwanza wa Zanzibar katika Umoja wa Mataifa ambapo Disemba 16, 1993 Waziri Mkuu Mohammed Hamad Shamte alilihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika Hotuba yake ya kuitambulisha Zanzibar kama Mwanachama Mpya wa Umoja wa Mataifa.

Tarehe 17 Disemba, 1963 Balozi Hilal Mohammed Hilal Al-Barwan aliwasilisha Hati zake za Utambulisho kama Balozi wa Kudumu wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana U Thant.

Serikali husika (iliyokabidhiwa Uhuru) ilidumu kukaa Madarakani kwa muda Mchache tu kabla ya kufanyika Mapinduzi yaliyoongozwa na Makomredi wa ASP na wale wa Chama cha Ummah Party kwa Msaada Mkubwa wa Serikali ya Chama cha Tanu ya iliyokuwa Nchi ya Tanganyika (sasa Tanzania Bara, ikiwa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania).

Mapinduzi hayo yalimleta Madarakani Sheikh Abedi Amani Karume kama Rais Mpya wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika Serikali iliyoundwa kwa ubia wa Wanachama wa Chama cha ASP na wale wa Ummah Party cha Komredi Abdulrahman Mohammed Babu.

MCHAKATO ULIPOANZIA.

Mchakato wa Zanzibar kuwa Mwanachama wa Umoja wa Mataifa ulianza Mwaka 1960 ambapo aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Dag Hamaskold aliitembelea Zanzibar Tarehe 6, Januari, mwaka 1960 wakati akielekea katika Ziara yake Maalum ya Kikazi Nchini Zaire (Sasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo).

Pichani ni Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Dag Hamaskold akiwa pamoja na Viongozi Mbalimbali pamoja na Wajumbe wa Baraza la kutunga Sheria la Zanzibar (Legco) katika Viwanja vya Bustani ya Victoria huko Zanzibar wakati wa Ziara yake hiyo, ambapo Picha hii hutajwa kama Picha ya Mwisho ya Bwana Darg na jopo lake kabla ya Ndege yake kuanguka huko Rhodesia ya Kusini (sasa Zambia) wakati akielekea Zaire.

Wengine kwenye Picha waliosimama kutoka kushoto kwenda kulia ni Sheikh Dahman (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia chama cha ZNP), Sheikh Ali Sharif (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia Chama cha ASP), Bwana N.V.Patel (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia ASP), Bwana Master (Mjumbe katika Msafara wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Sheikh Rashid Al-Ghaithy (Mjumbe Baraza la kutunga sheria, LEGCO kupitia ZNP) na Sheikh Juma S. Al-Mugheiry (Karani wa Baraza la kutunga sheria, LEGCO).

Waliokaa kutoka Kushoto kwenda kulia ni Sheikh Juma Aley (Waziri kupitia Chama cha ZNP), Sheikh Abeid Amani Karume (Waziri kupitia ASP) Bwana Dag Hamaskold (Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa), Bwana Smithson (Waziri katika Serikali ya Uingereza), Bwana Kirk Madan (Katibu Mkuu Kiongozi), Bwana Hilal Mohammed Hilal Al-Barwani (Waziri, ZNP na Pia Balozi wa Kwanza wa Zanzibar Umoja wa Mataifa) na Sheikh Ameir Tajo (Waziri, ASP).

ZANZIBAR NA TANGANYIKA ZAPOTEZA UANACHAMA WAKE KATIKA UMOJA WA MATAIFA.

Tanganyika imekuwa Mwanachama wa Umoja wa Mataifa tokea Disemba 14, mwaka 1961 mara baada ya kupata Uhuru wake tarehe 9 Disemba, mwaka 1961 kutoka kwa Wakoloni wa Kiingereza ambapo Dr. Vedastus Kyaruzi alikuwa Balozi wa Kwanza wa Tanganyika katika Umoja wa Mataifa akifuatiwa na Balozi A. Z. Nsilo Swai na kisha Chifu Erasto A. M. Mang'enya kuwa Balozi wa Mwisho wa Tanganyika katika Umoja wa Mataifa. 
Mara baada ya Muungano wa Nchi za Tanganyika na Zanzibar Mwaka 1964 na kuundwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Nchi ya Zanzibar pamoja na Nchi ya Tanganyika zilipoteza Viti vyake katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambapo kilitengwa kiti kipya kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kiti ambacho kimeendelea kuwepo mpaka leo kikiiwakilisha Tanzania huko Umoja wa Mataifa. 
Tarehe 19 Mwezi Novemba Mwaka 1964 Bwana John Samuel Cigwensisi Malecela aliteuliwa Kuwa Balozi wa kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Tanzania. Mabalozi wengine waliowahi kuiwakilisha Tanzania katika Umoja wa Mataifa ni Balozi Akil B.C. Daniel, Balozi Salim Ahmed Salim, Balozi Paul M. Rupia, Balozi Mohamed Ali Foum, Balozi Dr.Wilbert K. Chagula, Balozi Anthony B. Nyaki, Balozi Daudi N. Mwakawago, Balozi Dr.Augustine P. Mahiga, Balozi Ombeni Y. Sefue na huyu Mpya Balozi Tuvako Manongi.

CHANGAMOTO ZA MUUNGANO.

Miongoni mwa mambo ambaye yamekuwa yakiibuliwa kama moja ya malalamiko ya baadhi ya Wazanibari juu ya kero za Muungano ni ukweli kuwa Ushirikiano wa Kimataifa halikuwa katika moja ya Mambo yaliyokubalianwa katika Mkataba wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar (Kimsingi Mambo ya Nje ndio moja ya yaliyokubalianwa katika Mkataba wa Muungano).
Hivyo basi kuingizwa kwa Ushirikiano wa Kimataifa katika Mambo ya Muungano kinyume na Makubaliano ya Muungano huonekana kama ni batili na sehemu ya kuiminya Zanzibar katika Muundo wa Muungano (ukitolewa Mfano kuwa katika Mabalozi wote waliowahi kuiwakilisha Tanzania katika Umoja wa Mataifa tokea Muungano Wawili tu ndo Wazanzibari na waliobaki wote ni Watanganyika).
Kwa kiasi flani hali hii (ya kuingizwa kinyemela kwa Ushirikiano wa Kimataifa kwenye Mambo ya Muungano na kutokuwepo kwa uwiano wa kuridhisha wa Uteuzi wa Mabalozi wa Kudumu katika Chombo hiki kikuu cha Ushirikiano wa Kimataifa Duniani) inatumika kama moja ya sababu kuu za Msingi za wanaodai Zanzibar huru na kuvunja Muungano, lakini pia imekuwa Moja ya madai makuu ya wanaotaka kuendelea kwa Mashirikiano na Muungano wenye Utu na Heshima kati ya Tanganyika na Zanzibar kwa Kuboresha Muundo na kuondoa zile ambazo zinaonekana kuwa ni kero za Muungano. 
Jambo hili ni zito na lina Mantiki makubwa katika mustakabali wetu kama Nchi, Kwa nafasi yetu kila mmoja ana wajibu wa kulitafakari hili na kuja na majibu ya msingi kulingana na uelewa wake, mifano kuntu na uzoefu juu ya hali hii kutoka katika Mataifa mbalimbali yenye Mashirikiano kama yetu.

Naamini Tutafanikiwa, Mungu Ibariki Tanzania.

Picha ni kwa Hisani kubwa ya Bwana Shafiq Sanya na Maelezo ni Kwa Hisani Kubwa ya Seif Abalhassan wa Watanzania Mashuhuri.

November 14, 2012

SHULE ZA AWALI NYASA ZINAKABILIWA NA CHANGAMOTO LUKUKI


Na Albano Midelo, Nyasa
SERIKALI kupitia wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi iliamua kuanzisha mfumo wa elimu ya awali katika shule za msingi kwa lengo la kuwaandaa watoto wenye umri kuanzia miaka mitano.
Wizara ya elimu imedhamiria kuhakikisha kuwa watoto wenye umri wa miaka mitano hadi sita wanasoma darasa la awali kabla ya kuanza kuingia shule ya msingi wanapokuwa na umri wa miaka saba.
Uchunguzi uliofanywa katika kata za Kihagara na Liuli umebaini kuwa madarasa ya awali katika shule hizo yanakabiliwa na changamoto mbalimbali hali ambayo inaathiri utoaji wa elimu hiyo muhimu kabla ya kuanzia shule za msingi.

Wanafunzi wa Darasa la Awali wapatao 90 katika Shule ya Msingi PUULU, Kata ya LIULI, wilayani Nyasa wakiwa katika darasa ambalo halina dawati hata moja.

Mwalimu wa taaluma katika shule ya msingi Ndonga kata ya Kihagara Amos Kilongo anasema shule hiyo ina darasa la awali lenye wanafunzi 37 ambao wanasomea kwenye mti kutokana na kukosekana kwa chumba cha darasa na kwamba mwalimu anayefundisha katika darasa hilo ni aliyemaliza kidato cha nne.
“Wanafunzi wa darasa la awali hawana darasa wanasomea chini ya mti,pia darasa halina madawati wa awali wanakaa  wakati wa mvua wanafunzi hao wanasome katika kanisa katoliki ambalo tumewaomba wamiliki wa kanisa hilo wamekubali kutusaidia’’,alisisitiza.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kihagara Anet Ngindo anasema shule hiyo ina darasa la awali lenye wanafunzi 52 ambao wanasomea chumba cha shule ya msingi wakifundishwa na mwalimu ambaye hajapata mafunzo ya ualimu na sio mwajiriwa analipwa posho kupitia michango inayochangwa na wazazi.
Mwalimu mkuu katika shule ya msingi Tumbi  Evaristo Ndiwu anasema katika shule yake kuna darasa la awali lenye watoto 45 ambalo halina chumba cha kusomea ambapo mwalimu wake hana taaluma ya ualimu ni mhitimu wa kidato cha nne analipwa posho kutokana na michango ya wazazi na walezi.
Katika shule ya msingi Mango,mkuu wa shule hiyo anasema katika shule yake kuna darasa ka awali lenye wanafunzi 60 ambao hawana chumba cha kusomea na  wanafundishwa na mwalimu ambaye hajapata mafunzo ya ualimu sio mwajiriwa badala yake analipwa posho na wazazi kati ya shilingi 30,000 hadi 50,000 kwa mwezi.
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ngehe Silivanus Mbeya anasema katika shule yake kuna darasa la awali lenye watoto 36 ambalo halina chumba cha kusomea na linafundishwa na mwalimu ambaye amehitimu kidato cha nne hana mafunzo ya ualimu analipwa posho na wazazi ambayo haikidhi mahitaji ya mwalimu huyo.

Uvuvi ni shughuli inayoongeza kipato na ukuaji wa uchumi kwa wakazi wa wilaya ya nyasa. hapa wavuvi wakiwa kazini.

Katika shule ya msingi Puulu  mwalimu mkuu wa shule hiyo Cathibert Maluka anasema katika shule yake kuna darasa la awali lenye wanafunzi 90 na kwamba wanafunzi hao wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo na ukosefu wa madawati ambapo wanafunzi wote wanasoma kwa kukaa chini.
“Darasa la awali katika shule yetu limebahatika kuwa na walimu wawili ambao wamepata mafunzo rasmi ya kufundisha wanafunzi wa darasa la awali hali ambayo inawawezesha kutoa elimu ya awali kulingana na malengo ya wizara ya elimu licha ya wanafunzi kusomea chini’’,alisema .
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Nkali Erasmus Haule  anasema shule hiyo yenye jumla ya wanafunzi 210 ina darasa la awali lenye wanafunzi 45 ambao hawana darasa badala yake wanasomea kwenye banda ambalo jioni linatumika kama klabu cha pombe na kwamba mwalimu anayefundisha hajasomea.
Katika shule ya msingi Hongi  kwa mujibu wa mwalimu mkuu Simon Ndunguru shule hiyo ina darasa la awali lenye wanafunzi 52 changamoto kubwa hakuna chumba maalum cha kusomea na kwamba mwalimu anayefundisha sio mwajiriwa na wala hajasomea kufundisha darasa la awali.
Katika shule ya msingi Mwongozo yenye wanafunzi 654 inakabiliwa na changamoto ya ubovu wa darasa la awali lenye watoto 81 halina sakafu lina mwalimu mmoja ambaye hana mafunzo ya ualimu ,hajaajiriwa analipwa posho na wazazi wenye watoto hao
Baadhi ya wadau wa elimu katika kata za Kihagara na Liuli ambao ni Neema Msumba,John Ndunguru,Joel Makelele,Melikion Mapunda na Victor Komba wametoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa kila shule ya msingi inajenga darasa rasmi kwa ajili ya elimu ya awali badala ya shule nyingi kutumia vyumba vya shule ya msingi.
Wameitaka wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi kuhakikisha kuwa kila darasa la awali inapeleka walimu waliopata mafunzo rasmi ya namna ya kufundisha watoto wa awali badala ya tabia ambayo inafanywa na shule nyingi kuwatumia vijana ambao wamehitimu kidato cha nne huku wakiwa hawajapata elimu ya ualimu.
Mratibu elimu kata ya Liuli Abrahamu Challe amesema kata yake imejipanga kuhakikisha kuwa changamoto zote zinazoikabili elimu ya awali katika kata yake yenye shule saba zinatafutiwa ufumbuzi haraka ikiwemo kuwa na chumba rasmi kwa ajili ya awali,walimu na madawati.
Challe ametoa wito kwa serikali kutumia mfumo wa uboreshaji wa elimu ya awali kama ilivyokuwa kwa uboreshaji wa elimu ya msingi na sekondari kwa kujenga  vyumba viwili vya madarasa kwa kila shule na kusisitiza kuwa vifaa vyote vya ujenzi vitolewe na serikali na wananchi waachie ujenzi.
Afisa elimu msingi katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga David Mkali ambaye anahusika na wilaya ya Nyasa anasema elimu ya awali ni sera ya wizara ya elimu kuhakikisha kila shule ya msingi inakuwa na darasa la awali kwa lengo la kuinua elimu hapa nchini.
Ameahidi kushirikiana na viongozi mbalimbali wakiwemo madiwani,watendaji wa vitongoji,vijiji,kata,tarafa pamoja na wenyeviti wa vijiji kuhakikisha wanahamasisha wananchi katika maeneo yao kusimamia ujenzi wa madarasa ya awali na kutengeneza madawati ili watoto hao waweze kusoma katika mazingira bora.
“Ni ukweli madarasa ya awali yaliyo mengi yanafundishwa na walimu wasiopata elimu ni kutokana na uhaba mkubwa wa walimu uliopo katika shule nyingi nchini,lengo ni kuhakikisha tunapata walimu wa kutosha ikibidi hata kuwatumia walimu wanaostaafu kufundisha katika madarasa ya awali’’.alisisitiza.

Unaweza kuwasiliana na mwnadishi kwa anuani ifuatayo: albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

November 01, 2012

JAMES ZOTTO ALIPOZUNGUMZIA MGOGORO WA ZIWA NYASA, KABLA YA KUWASILISHA UTAFITI WAKE KWENYE UMOJA WA AFRIKA NCHINI ETHIOPIA

Mgogoro wa mpaka Malawi na Tanzania: siasa na ukweli

Na James Zotto, University of Dar es Salaam
Ndugu zangu watanzania, naamini mnafuatilia vizuri tatizo la mpaka wetu wa ziwa Nyasa na Malawi! Na pia mmefanikiwa kusikia au kusoma hotuba ya Waziri wa Mambo ya nje, Benard Membe. Nilishtushwa kidogo na hotuba hiyo. Niharakishe kusema, mimi napenda utaifa wangu na uzalendo wangu. Lakini napenda sana kutetea mambo yangu kwa kukubali ukweli, kujua hali halisi, kukubali hata zile zinazonipinga, ili nami nijipange kujenga joja. Niongeze tu kuwa, eneo hili nafanyia study yangu ya PhD. Sidhani kama nipo sahihi zaidi na lengo langu si kusema nani anamiliki nini!  
James Zotto akiwa pembezoni mwa ziwa Nyasa.
Ukweli ninaofahamu, tatizo si kubwa sana kama tunavyolifikiri, na pengine tutachukua muda kupitia nyaraka zote muhimu. 
Kwanza, tunahitaji kwenda Idara ya Kumbukumbu ya Uingereza(Public Records Office). Pili tunapaswa kufuatilia Colonial Archives Potsdam, Ujerumani. 
Aidha, tufuatilie pia Malawi National Archives, Tanzania National Archives, Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es salaam(UDSM) na Chancellor College Malawi. Ninaamini ubishi utaisha kwa kuwa nyaraka zote zipo.
Naomba nianze kujadili kwa kuweka angalizo katika suala hili ili ikilazimika, Malawi wasalimu amri kwa njia yoyote tutakayoamua, nitasema hapo baadaye. 
Angalizo lenyewe: ziwa Nyasa liligawanywa na mabeberu wa Kiingereza, Kijerumani na Kireno. mkataba wa mwaka 1890 uitwao Anglo-German Agreement, unasema mpaka wa uliokuwa miliki ya Ujerumani au kwa kiingereza German East Africa (Tanzania Bara ya leo) na Nyasaland (Malawi ya leo) unapita kando kando ya ziwa Nyasa kutoka mto Ruvuma(mkoani Ruvuma) mpaka mto Songwe(mkoani Mbeya).
Mkataba huo upo katika nyaraka nyingi sana. Mathalani katika Sheria za Kimataifa (International Law) wanafahamu jambo hilo na sina shaka ndugu zetu wanasheria wa kimataifa (International Lawyers) wanaelewa nini nazungumza! 
Sehemu nyingine ilikuwa ya mkataba ilikuwa mwaka 1891 kati ya Ujerumani na Ureno. Kulingana na mkataba huo, walikubaliana kuwa mipaka ilianzia mto Ruvuma kuelekea Portuguese East Africa (Msumbiji ya leo).
Mkataba mwingine ulikuwa ni kati ya Ureno ambayo ikawekeana mipaka na British Nyasaland (Malawi), kwahiyo, kipindi cha Ujerumani, mipaka inasomeka 'it passes along the shore of the lake (Nyasa).”
Hata hivyo kuliwahi kutokea mabadiliko ya mipaka hiyo. Mabadiliko ya mipaka yalianza kipindi cha ukoloni, kabla ya Ujerumani kuondoka.
                    
                             Kikwete na Banda
Marekebisho ya mipaka yalifanyika kati ya Ujerumani na Ureno kwa kusogeza mipaka mbele na kutamka, “0.5 KM from the original tripartite point” na vijisiwa vya mto Ruvuma vikagawanywa. Mipaka hiyo ipo hivyo hadi leo. 
Na eneo lingine ni kati ya Uingereza na Ureno, ambapo, kisiwa kilichopo eneo la Malawi kinamilikiwa na Msumbiji mpaka leo na eneo la ardhi lililopo Msumbiji linakaliwa na Malawi. 
Huo ulikuwa mkataba wa marekebisho na ipo hivyo mpaka leo. Kwahiyo, tulivyorithi mipaka, tumerithi na mabadiliko haya na hivyo hatuwezi kugombana na Msumbiji wala Msumbiji hawawezi kugombana na Malawi. 
Mpaka wetu na Malawi haukurekebishwa popote pale mpaka Ujerumani ilipoondoka nchini. Nafikiri viongozi wajiandae pia kwa hili ili tuweze kuwashinda ndugu zetu wa Malawi.
Marekebisho ya mipaka kipindi cha Uingereza:- sote tunajua German East Africa, ni sisi(Tanzania) pamoja na Rwanda na Burundi tuligawanywa katika sehemu kuu mbili.
Mosi, tulipokuwa chini ya League of Nations tukiangaliwa na Uingereza. Kuna mambo nahitaji tuweke sawa ili kuongeza hoja kwa mheshimiwa waziri wa mambo ya nje, Bernad Membe. 
Tulipokuwa chini ya League of Nations, tukaitwa ‘Mandated Territory’, na Uingereza ikawa ni ‘Mandatory Power’. Turudi katika Kamusi tutofautishe “a an annexed colony and a mandate.” 
Mpaka ukawekwa kati ya Ubelgiji na Uingereza, uliitwa The Milner-Orts Agreement of 1922! Naam, katika mkataba huu, mto Kagera ulikatwa katikati , hivyo  hadi naandika makala hii mipaka hiyo tumerithi hivyo. 
Hapakuna mahali popote pale ambapo eneo la ziwa Nyasa kama palirekebishwa kwa njia ya mkataba baina ya Nyasaland State na Tanganyika State.
Isipokuwa tofauti na Mandates zote, Tanganyika pekee, ilikuwa na tofauti ndogo, ambapo mpaka wake wa ziwa Nyasa ukapewa wanachoita 'Wording'. Na hivyo, ramani ya Tanganyika na Official Records zikaonyesha kuwa mpaka umepita katikati ya ziwa Nyasa! 
Hapa ndipo tatizo linapoanza na sisi tumeshindwa kusogea mbele kidogo. Ninachokisema hapa kipo pale National Archives Secretariat Files, Accession Numbere AB 8 na AB 30!

                 
James Zotto akiwasilisha utafiti wake kuhusu mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa.
Nafikiri hotuba yote ya mhehimiwa Waziri Membe imetokana na Files hizo, ndizo walizopelekewa. Ndugu zangu watanzania, ni muhimu kujadili zaidi ya hapo.
Twende mbele kidogo, ni kweli kama mheshimiwa alivyosema katika hotuba yake, ramani nyingi kuanzia mwaka 1922 hadi mwaka 1939 zinaonyesha mpaka upo katikati ya ziwa Nyasa! 
Je, ukweli huu utatutosha pekee mbeleni tukifikishana mbali? Hapana, tuendelee kusaidiana kwa hili, nafikiri ujumbe utawafikia tu.
Waziri Membe hakusema kuwa ramani zingine, japo chache muda huu na Official Reports hazionyeshi mpaka au zinaonyesha mpaka upo chini. Lakini ni chache! Kwanini hili?
Bado natafuta majibu, lakini kwa haraka, tunaweza kusema kuwa Uingereza ilitamani Tanganyika iwe koloni lake na si Mandate! Na pia ilishinikizwa na wawekezaji na hata jeshi ilisema afadhari waiteke ili liwe koloni na waachane na Mandate
Nahitaji tuelewe maana ya mandate. Hii yote ilitokea baada ya gavana Donald Cameroon, wa Tanganyika kusema kuwa “Tanganyika is a part of the British empire and it will remain so”.
Hii ni siasa na si ukweli kama unaelewa maana ya kuwa wao hawakuwa wamepewa koloni kama mali yao, bali kuliangalia hadi wananchi wapate 'akili' ili wapewe uhuru! 
Kwa hiyo na kimsingi, kwa maana ya sheria ya kimataifa, Tanganyika haikuwa Part ya British Empire kama yalivyo makoloni yaliyotekwa moja kwa moja na Uingereza yenyewe! 
Hapa pakatokea mvutano mkubwa sana katika House of Lords na House of Commons! Na hivyo basi, mtafaruku huu wa mipaka ulianzia hapo, hivyo hata waingereza wenyewe walivutana kuhusu mipaka. 
Kwa mfano, mwaka 1926, wajumbe wa mabaraza waliibana serikali iseme mipaka ya Tanganyika na ule wa ziwa Nyasa! Mabishano, kama haya yetu leo yalikuwa makubwa, ila si kwa kutishiana kwa kuwa walikuwa wenyewe na walitaka kuwekana sawa!     
                              
Rais Kikwete na Joyce Banda walipokutana katika kikao cha SADC mjini Maputo, Msumbiji.
Naam, ndipo Secretary of state for colonies alibanwa na mjadala ulikuwa wa kisheria zaidi ukihoji Status of the Mandate, British Empire n.k, na kama waingereza wana mamlaka ya kujipangia kuhusu koloni walilokabidhiwa kuliangalia(nieleweke na sio kulimiliki koloni).
Mwishowe wenye dhamana(Waingereza) walisema kwamba, hata wao wanashindwa kuelewa, 'What exactly is the sovereignty of  Tanganyika lying', jamani mnamwelewa huyu mtu wa kiingereza? 
Kwamaana hiyo, haelewi vizuri mipaka yetu, ambayo wenyewe ndo wameirekebisha au kuipa 'Wording'! hivyo, tatizo linaanzia hapa na si muda mwingine wowote!
Jambo kubwa ambalo Waziri Membe hakusema ni hili: kuanzia mwaka 1939, mambo yalibadilika na hawa hawa watu(Wakoloni) tunaochukua ushahidi kutoka kwao, wakafanya madudu! 
Na ilipoisha vita ya pili ya dunia, jamani oneni haya, hawa waingereza katika ramani zao, tena nyingi mno, tuangalie East Africana Section ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam, katika sehemu ya Thesis, kuna Cabins 3 zimejaa ramani na bado ni mpya sana kutokana na kutunzwa na pia kutotumika sana.
Zinaonyesha, bila shaka yoyote, kuwa mpaka wa Tanganyika na Nyasaland unapita pembeni mwa ziwa na sio katikati! Nieleweke naonyesha tu mambo yalivyo ili tuweze kuchukua hatua zaidi. 
Hotuba ya Waziri Membe, iliishia nyaraka za mwaka 1939! Kumbe hawa jamaa walichora tena ramani zote zikionyesha mpaka upo pembeni mwa ziwa! Kwanini hili? Natafuta majibu.
Lakini kwa haraka naweza nikakisia mambo mawili. Mosi, karibu na vita vya pili vya dunia, ilisikika tetesi kule duniani(ughaibuni) kuwa, Ujerumani inarudi na inakuja kuchukua makoloni yake. 
Tukitaka kuhakikisha jambo hili, tusome National Archives of Tanzania, Secretariat Files zote zenye kichwa cha habari, 'The future of Tanganyika in British Empire'
Kwa hiyo, waingereza walihofia kutimuliwa na kurudi kwa wajerumani, na hivyo, wakarudisha ule mpaka wa awali wa mwaka 1890 unaotumiwa tena na Malawi kwa sasa! 
Na pia, katika kipindi hicho, baada ya kumalizika vita hivyo, Tanganyika ikawa chini ya Umoja wa Mataifa(United Nation Organisation), ambapo ilipewa Trusteeship Status!
                            
                                      RAMANI YA ZIWA NYASA.
Maana ya hii ni rahisi kuliko Mandate! Kwanini? Hii ilimaanisha ‘to be granted immediate independence’! maana ya neno ‘immediate’ hapa ni kwamba, kwa tafsiri yangu, waingereza walifahamu wanatimka mapema mno kwani mkataba unasema hivyo.
Nafikiri, wakarudisha ramani zikionyesha mpaka upo pembeni mwa ziwa na kitabu cha ‘Nyasaland’ cha mwaka 1958, kinaonyesha mipaka ya Nyasaland na ziwa lote likiwa kwao! 
SASA TUFANYE NINI WATANZANIA?
Tukitaka kuwashinda watu wa serikali ya Malawi, lazima tukisome vizuri kipindi hiki na tuelewe ukweli, hoja zipi zinawapa kiburi. Na hoja zipi sisi tuzitumie kupambana nao, tunaweza! 
Kwahiyo hatima ya nchi yetu haikujulikani itakuwaje. Kipindi hiki, pamoja na mipaka yake pia, tujiulize, kwa maana ya Mandate, waingereza walikuwa na ‘Legal Authority  'kurekebisha' mpaka wa ziwa nyasa? 
Na je makosa waliyofanya waingereza, ndio Legal backing yetu sisi Watanzania?  Hebu tuzame tena tutafute ukweli zaidi ili tuwashinde hawa jamaa wa Malawi!
Tulishindwana na Uingereza kurekebisha mipaka. Mwalimu Nyerere, alisubiri hadi Malawi ipate uhuru, ndipo akatoa miaka mitatu tu na asingetambua mipaka ya kikoloni(Soma Hansard, 1962). 
Malawi walipopata uhuru, kukawa na matatizo ambayo Waziri Membe aliweza kuyaeleza. Nampongeza kwa hilo, ni dhahiri mwaka 1964 wakati wa mgogoro wa baraza la mawaziri la Malawi, na baadhi ya mawaziri kutorokea nchini kwetu kupitia ziwa Nyasa, Rais Kamuzu Banda akaona ziwa ni infiltration route
                                
                             WAZIRI MEMBE akinawa maji ya ziwa Nyasa mjini Mbamba Bay.
Sera zetu za mambo ya nje za Tanzania zilikuwa tofauti na Malawi. Tanzania ilikuwa nchi iliyoongoza ukombozi wa nchi za kusini mwa Afrika, wakati wenzetu Malawi wakaunga mkono Makaburu na Wareno na wakawa na balozi sehemu hizo
Rais Banda akagombana na Mwalimu Nyerere, na matukio ya kutishiana kijeshi yalijitokeza kati ya miaka ya 1967-8; matusi na kejeli zikatawala kati yetu na wao.
Tunakumbuka tuliimba, .....kipara cha Kamuzu Banda kina magamba”, tuliimba tukiwa jeshini hayo. Mwalimu Nyerere  akasema suala mipaka ni hadi Malawi itakapota Sensible Leader akitokea Malawi ndipo tutajadili tena, sio utawala ule wa Kamuzu Banda! 
Kipindi chote hicho tulikuwa kimya, na kuanzia mwaka 1975, hatukuwa na tatizo, lakini sio kusema kuwa tulitatua tatizo la mipaka yetu na Malawi! 
Tulikaa kimya! Mipaka haina tatizo isipokuwa ni time bomb ambapo ikitokea rais mwendawazi akamwaga petroli tu, basi ni vurugu kubwa! 
Tuliirithi kupitia Article III ya Azimio la Umoja wa Afrika la mwaka 1964(OAU Charter, 1964), baadaya ya majadiliano makubwa na wengi wakaridhia “uti possidetis, ita possidetis principle” (so as you exist, so may you exist).
Kama kawaida yetu tulinakili kanuni za mipaka za kibeberu za Westphalia(Westphalia border inviolability)! Hatukupata muda mwingi wa kutafakari na kuangalia kila mpaka na matatizo yake....tulirithi na matatizo na yanatutatiza leo!!!
UTATUZI WA MGOGORO: Tusonge mbele! Nakiri tuna namna tatu ya kulimaliza;- moja ni kwa majadiliano ya kawaida(Diplomacy) kama Waziri Membe alivyosema katika hotuba yake. 
Pili ni kupigana vita (war is another means of diplomacy). Ndugu zangu watanzania nadhani mnataka kuniona kichaa kutamka hilo! Huo ndo ukweli, atakayeshindwa atasalimu kama ilivyokuwa kwa Uganda na sisi watanzania. 
                        
                     WAZIRI WA MAMBO YA NJE, BERNARD MEMBE.
Tatu; ni Mahakama ya Kimataifa(International Court of Justice) hapa nina wasiwasi. Kama nyaraka zenyewe ni zile za Waziri Membe tu, sijui kama tutafanikiwa kushinda kesi.
Tutulie, tuite wataalamu wetu wajikite ndani sana. Ni kweli kama alivyosema Waziri Membe kwenye hotuba yake kwa kunukuu kesi nyingi na zilizoshinda, na kwa kusema kuwa, tukienda mahakama ile sisi ndo tutashinda. 
Nina shaka, tumejipa favour  ya verdict, kabla ya kesi. Sijui, ila nina shaka kubwa, kuna kushinda, kushindwa au suluhu! Ninashaka tena na tena!
Mimi ni mzalendo, nataka ukweli kwa njia ya mahojiano na kuumiza kichwa, tutetee mali zetu tukijua tunawashinda kwa hoja.
WASIWASI: Inasemekana kuna mafuta ziwani,  kwahiyo tujue Marekani na washirika wake hawako mbali! Kampuni ya Surestream ya Uingereza ndio ilipewa leseni ya kutafiti mafuta na utawalawa Bingu wa Mutharika.
Lakini, tujue operesheni ya majeshi ya kibeberu na huyu mama Joyce Banda, ambaye ni mpwa wa Kamuzu Banda, anapata wapi hiki kiburi? Nyuma yake kuna nini na nani? Tuangalie haya pia. 
HITIMISHO: Tusiwe na hoja moja tu mkononi kama ndio water-tight evidence yetu kwa serikali na wananchi kwa ujumla. Tujaribu kuzibishanisha hoja zetu. Na hoja nzuri ni zile zinazopingana nasi na tusizozipenda, tukizielewa na kuzikubali ndipo tutajipanga namna ya kuzigalagaza. Tumwelewe vizuri adui yetu. Mungu ibaraki Tanzania, ziwa Nyasa, wanyasa, na watanzania! Tusing'ang'anie tu Reparian Law.
James Zotto ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam(UDSM).