Showing posts with label tawasifu. Show all posts
Showing posts with label tawasifu. Show all posts

March 23, 2018

LAURA BASSI: PROFESA WA KWANZA MWANAMKE BARANI ULAYA.

Na Kizito Mpangala

Wanawake wanayo nafasi ya kufikia malengo ambayo wanakusudia, ni kwa juhudi na maarifa wataweza kufikia malengo hayo. Suala la kipaumbele kwa wanawake duniani kote limepitia hatua kadhaa za ushawishi na changamoto kadhaa ambazo hasa huwakabili wanawake wenyewe. Katika uga wa sayansi na teknolojia, ni wanawake wachache ambao wamefikia malengo yao ugani humo. Hata sasa uhamasishaji bado unaendelea duniani kote.

Haikuwa kazi rahisi kwa mwanafizikia Laura Caterina Bassi kufikia kiwango cha profesa wa Fizikia katika chuo kikuu cha Bologna nchini Italia.
Laura Bassi alizaliwa mwaka 1711 mjini Bologna nchini Italia ambapo baba yake alikuwa mwanasheria. Laura Bassi alifundishwa nyumbani na mwalimu aliyeajiriwa na familia yake kwa muda wa miaka saba. Alianza kufundishwa akiwa na umri wa miaka 13. Mwalimu wake, Gaetano Tacconi, alimwelekeza zaidi katika sayansi na hisabati ndipo Laura alipoingiwa na hamu ya kutaka kujua zaidi yaliyomo katika sayansi.

Kutokana na msukumo aliokuwa nao katika sayansi, Laura alivutiwa zaidi na somo la Fizikia ambapo alijifunza zaidi kuhusu Sayansi ya Newton (Newtonian Science) ingawa mwalimu wake alitarajia kwamba Laura atajikita zaodi katika hisabati, lakini haikuwa hivyo.
Laura Bassi, katika juhudi zake za masomo alilazimika kusoma pia hisabati ili kujiimarisha katika Fizikia. Hapa Laura alimuomba binamu yake, Padre Lolenzo Stegani, amfundishe hisabati. Padre Lolenzo Stegani alikuwa akijua hisabati na lugha ya kilatini. Kwa kuwa vitabu vingi viliandikwa kwa lugha ya Kilatini, Laura alipaswa kujifunza sarufi ya lugha hiyo na baadae akafundishwa hisabati kwa lugha ya Kilatini.

Baada ya kuweka juhudi zaidi katika elimu hiyo ya sayansi, mwaka 1732 Laura aliandika kazi yake ya kwanza ambayo aliitetea mbele ya hadhira katika mihadhara mbalimbali katika ukumbi wa Pazzalo. Hiyo ilikuwa dira yake ya mafanikio ya elimu aliyokuwa akiitafuta zaidi.

February 19, 2018

UHONDO WA NYASA NA VITOWEO VYAKE

February 17, 2018

WIKIENDI NJEMA WASOMAJI WETU NA PICHA ZA MAENEO YA UZAMIAJI WA SAMAKI LUNDU, NYASA

Eneo hili ni miongoni mwa yanayotumiwa na wazamiaji wengi kupata samaki. Uzamiaji wa samaki katika eneo hili hutafutwa samaki wa mapambo. Kijiji cha Lundu hutumika sana kutafuta samaki wa mapambo. Kuna samaki wazuri mno wanaotafutwa hivyo wazamiaji hutegemea kijiji hiki kujipatia samaki hao.
Watoto wakioposha samakini karibu na jiwe Stima (Liganga Stima).

SOLOMON MINTUS NORTHUP: MTUMWA ALIYEMPIGA MNYAPARA WAKE NA KUANDIKA KITABU KUELEZA MAISHA YAKE YA UTUMWA MIAKA 12.

Na KIZITO MPANGALA
Solomon Northup alizaliwa mwaka 1807 katika mji wa Essex (sasa ni New York), Marekani. Alizaliwa kwa wazazi walioachiliwa huru katika mashamba ya pamba, Louisiana. Baba yake alipokuwa mtumwa asiye huru katika mashamba ya pamba ya tajiri Henry Northup aliaminika katika kazi hiyo. Baada ya kuachiliwa huru aliamua kutumia jina la mnyapara wake, Henry Northup kama jina la pili katika kizazi chake kilichofuata. 

Hapo alimwongezea Solomon Mintus jina la NORTHUP na kuwa SOLOMON MINTUS NORTHUP. Mzee Mintus aliachiliwa huru kwa sababu alimuoa mwanamke chotara katika mji wa Minerva mjini Essex ambaye alikuwa na asili ya Afrika na Ulaya, hivyo weupe ulimzidi na kwa weupe huo alitendewa kama mtu wa kutoka Ulaya. Ndipo Solomon Mintus Northup alipozaliwa akiwa mtumwa huru pamoja na mdogo wake Joseph Mintus Northup kadiri ya sheria ya “Partus sequitur ventrem” ambayo ilirithiwa na koloni la Uingereza nchini Marekani kutoka katika Dola la Warumi (Roman Empire). Sheria hiyo humaanisha “yeyote aliyefika sehemu fulani anapaswa kufuata utaratibu (kanuni au sheria) unaofuatwa katika eneo hilo” ni kama vile kusema “ukiwa katika ardhi ya Warumi ishi kama Mrumi”

Solomon Mintus Northup alikuwa akimwelezea mama yake kuwa ni robo ya Mwafika na robo-tatu ya Mzungu anayeishi Amerika. Baba yake alifanikiwa kumiliki ardhi baada ya kuwa huru. Alijiwekea utaratibu wa kuwekea akiba ya fedha na kupata mahitaji ya lazima kwa familia yake. Pia aliwasomesha watoto wake wawili, Solomon na Joseph. 

February 16, 2018

MBUFU NI AINA YA SAMAKI KUTOKA HAPA KWETU NYASA


Upikaji wa samaki hawa hauhitaji kitunguu wala nyanya au mafuta. Wanapikwa na kulika vizuri, hawahitaji mafuta ya kupikia, nyanya wala vitunguu na vikorombwezo vingine vya mapishi. Ukitumia viungo hivyo basi utakuwa umeharibu kabisa ladha yake na kupoteza asili yake. Ni samaki watamu mno.

February 15, 2018

ABDUL-RAHMAN IBRAHIM BIN SORI: MTUMWA WA GUINEA ALIYEOKOLEWA NA SULTAN WA MOROCCO.

Na KIZITO MPANGALA

Abdu-Rahman Ibrahim bin Sori alizaliwa mwaka 1762 katika mji wa Timbo kitongoji cha Futa Djallon (sasa ni nchi ya Guinea) huko Afrika Magharibi katika jamii ya kabila la Fulani. Baba yake alikuwa mfalame wa mji wa Timbo (Guinea) na hivyo Abdul-Rahman alikuwa ni mwanamfalme (Prince)
Katika makuzi yake alipelekwa mjini Timbuktu kujifunza masuala yanayohusu dini ya Kiislamu. Akiwa mjini Timbuktu, Adul-Rahman alijifunza lugha nne za makabila ya Afrika Magharibi pamoja na lugha ya Kiarabu na aliporudi mjini timbo alijiunga na jeshi la baba yake ambaye alikuwa kiongozi wa kitongoji cha Futa Jallon mjini Timbo (sasa ni Guinea).

Abdul-Rahman alipofikisha miaka 26 alifanywa kuwa kiongozi wa jeshi hilo liliokuwa na askari 2000. Kazi yake kuu katika jeshi hilo ilikuwa kuhakikisha ulinzi wa pwani yote ya Timbo (Guinea) umeimarika na kuliweka jeshi lake tayari kwa kupambana na adui yeyote ambaye angeivamia pwani hiyo.
Kutokana na uwezo wake wa kijeshi, Abdul-Rahman aliwindwa sana na wazungu wa Uingereza ambapo mwaka 1788 wazungu hao walifanikiwa kumteka na kusafiri naye hadi katika mji wa Mississippi nchini Marekani kisha aliuzwa na kuwa mtumwa. Akiwa mjini Mississippi laitumikishwa kufanya kazi katika mashamba ya pamba ya tajiri Thomas Foster kwa zaidi ya miaka 38 kabla ya kuachiwa huru.

February 12, 2018

LEVARDIS ROBERT MARTYN BURTON JR: MSEMINARI ALIYEUVAA UAFRIKA KWENYE FILAMU YA “ROOTS” KWA JIN LA KUNTA KINTE.

Na Kizito Mpangala

Ukimtazama hata kwa picha utasema ni mzaliwa halali wa Gambia kutokana na mwonekano wake katika filamu iliyomlazimu kuwa Mgambia.
Alizaliwa mwaka 1957 nchini Ujerumani Magharibi (sasa Ujerumani) kwa wazazi Levardis Robert Martyn Burton Sr na Erma Gene. Baba yake alikuwa ni mpiga picha wa jeshi la Marekani katika kituo cha afya cha Landstuhl cha jeshi la Marekani nchini Ujerumani. Mama yake alikuwa mwelimishaji wa jamii.

Burton Jr na dada zake wawili walilelewa na mama yao katika mji wa Sacramento jijini Calofonia nchini Marekani huku baba yao akibaki Ujerumani kikazi.
Burton Jr alivutiwa na kujiunga na Seminari na hivyo akakubaliwa kuanza masomo katika Seminari ya Mtakatifu Pius X katika kitongoji cha Calt jijini Califonia kwa lengo la kuwa padre.
Alipokuwa Seminarini, alipenda kusoma vitabu vya falsafa na kufanikiwa kuwasoma wanafalsfa kadhaa Seminarini hapo. Katika falsafa hizo, alivutiwa na kuwasoma kazi za wanafalsafa Lao Tzu, Nietzsche na Kierkegaard ambazo zilimfanya awahoji walimu wake kama Ukatoliki ndiyo dhehebu pekee kweli.
Alipofikia umri wa miaka 17 alihitimu katika Seminari hiyo na kuamua kujiunga na chuo kikuu cha Califonia Kusini kwa masomo ya sanaa. Alitunumiwa shahada ya kwanza ya sanaa huku akijikita katika uigizaji.

JOSEPHINA MARGARET BAKHITA: MTAKATIFU MWAFRIKA ALIYEPONEA MIKONONI MWA MAHAKAMA YA ITALIA.

NA KIZITO MPANGALA

JOSEPHINA Margaret Bakhita alizaliwa mwaka 1869 mjini Darfur kitongoji cha Olgassa nchini Sudan katika jamii ya kabila la Daju. Baba yake aliheshimiwa sana kwa kuwa alikuwa ni kaka ya Chifu wa kabila hilo. Bakhita aliishi kwa furaha akiwa hajui mateso ya kitumwa yanakuwaje.
Alipofikia umri wa miaka minane, alitekwa na Waarabu wafanyabiashara ya utumwa ambao tayari walikwishamteka dada yake miaka miwili kabla ya kumteka Bakhita mwenyewe. Alilazimishwa kutembea mwendo wa kilometa 960 peku kutoka Darfur hadi El Obeid. Kabla ya kufika El Obeid alikuwa ameuzwa mara mbili njiani.

Bakhita alipofikia umri wa miaka 12 alikuwa ameuzwa tena mara tatu na kisha kusafirishwa mpaka Uturuki. Huko alikumbwa na mateso mengi na uchungu hali iliyompelekea kusahau jina lake la asili na hivyo alilazimika kutumia jina alilopewa na Waarabu, Bakhita likimaanisha mtu mwenye bahati. Kisha akasilimishwa.

Bakhita alinunuliwa na tajiri wa biashara ya watumwa ambaye alikwa Mwarabu na kumtumikisha kama mfanyakazi wa kuwahudumia binti zake wawili ambao waliishi nae vizuri. Alipokorofishana na mtoto wa kiume wa Mwarabu huyo alipigwa na kufikia hatua ya kushindwa kutembea kwa muda wa mwezi mmoja. 

February 03, 2018

JOHN LANGALIBALELE DUBE: MWANAFUNZI ALIYEAMINIKA KUWA NA TABIA CHAFU CHUONI MWASISI WA CHAMA CHA ANC, AFRIKA KUSINI.

Na Kizito Mpangala

John Langalibalele Dube alizaliwa mwaka 1871 kwa wazazi James Dube na Elizabeti Dube katika kitongoji cha Inanda,kwa sasa ni mkoa wa KwaZulu Natal. Jina lake la katikati yaani Langalibalele alipewa na wazazi wake likimaanisha “mwanga wa jua”. Baba yake alikuwa mchungaji katika kanisa la misheni ya Waamerika walioishi katika jamii ya Wazulu.
John Langalibalele Dube

Baba yake alikuwa kiongozi wa kabila la watu wa Qadi katika jamii ya Wazulu na jina lake lilikuwa Ngcobo Dube. Baada ya ujio wa Wamisionri alimua kujiunga na Ukristo na kisha akabatizwa kwa jina la JAMES DUBE. Huo ndio ulikuwa mwisho wa kuliongoza kabila hilo. John Langalibalele Dube alikuwa Mwalimu, Mhariri, Mpigachapa, Mshairi, Mwanafalsafa, Mwandishi wa Insha, na mwanasiasa nchini Afrika Kusini. 
 
John Langalibalele Dube alianza masomo katika kitongoji cha Inanda, na baadae akajiunga na chuo cha Adams (Adams College) kitongoji cha Amazimtoti kusini mwa mji wa Durban nchini Afrika Kusini. Akiwa chuoni hapo, walimu walipeleka lalamiko kwa wazazi wa John kwamba kijana wao ana tabia chafu chuoni hapo ambayo haiendani na sheria za chuo. Ndipo Mchungaji William Cullen Wilcox alipoteuliwa kuzungumza na kumkanya John Langalibalele Dube kwa tabia zake chafu (haikuwewa wazi ni tabia zipi hasa alizokuwa akizifanya). John alifuata nasaha alizopewa na kisha akabadili tabia.

Wamisionari wa Amerika walioondoka katika kitongoji cha Inanda, John aliambatana nao na kujiunga na chuo cha Oberline nchini Marekani. Aliambatana nao kwenda Marekani baada ya kupata ruhusa kutoka kwa baba yake Mzee James Dube ambaye alikuwa mchungaji na kiongozi katika chuo cha Adams. Wamisionari hao walikubali kwa sharti kwamba hawatamhudumia chochote kifedha, hivyo Mzee James Dube alipaswa kuingia mwnyewe mifukoni mwake.

GARETT AGUSTUS MORGAN: MJASIRIAMALI ALIYEVUMBUA TAA ZA KUONGOZEA MAGARI BARABARANI.

Na Kizito Mpangala

Garett Morgan alizaliwa mwaka 1877 katika kitongoji cha Claysville mjini Kentucky nchini Marekani akiwa na asili ya Afrika yaani. Baba yake alikuwa mtumwa aliezaliwa katika kitongoji cha Huntsville mjini Alabama. Baba yake alikuwa mtumwa kwa kurithishwa na wazazi wake waliokuwa watumwa. Miaka kadhaa baadae baba yake, John Morgan akawa Luteni Kanali wa jeshi la Marekani, Brigedia Jenerali katika jeshi la Kentucky kwa lazima. Mama yake Garett Morgan pia alikuwa mtumwa kama mume wake.

Garett Morgan alipofikia darasa la sita katika shule ya Brach Elementary mjini Claysville akiwa na umri wa miaka 16 alikwenda katika kitongoji cha Cincinnati mjini Ohio kutafuta kazi itakayompa ujira ili kupata mahitaji yake. Aliajiriwa mashambani.

Kama ilivyokuwa kawaida ya watoto wengi nchini Marekani wakati huo, Garett Morgan alilazimika kuacha shule akiwa darasa la sita na kuamua kufanya kazi katika mashamba kutwa nzima. Kutokana na bidii yake katika kazi, aliletewa mwalimu awe anamfundisha hapohapo shambani ambako ndiko yalikokuwa makazi huku akiendelea na kazi za shambani huko. 

Alifundishwa ufundi na baadae akawa fundi mahiri wa kutengeneza mashine za kushonea nguo yaani cherehani. Uzefu huo wa kutengeneza cherehani aliuheshimu na kujifunza zaidi jinsi mashine zinavyofanya kazi. Kazi yake ya kwanza kuvumbua ilikuwa ni cherehani inayotumia mkanda kama cherehani za sasa. Alivumbua cherehani hiyo tofauti na za mwanzo zilizokuwa zikizungushwa kwa mikono.

GEORGE CRUM: MPISHI MASHUHURI ALIYEVUMBUA CHIPSI YA VIAZI

NA KIZITO MPANGALA

Alizaliwa mwaka 1824 katika mji wa Saratoga, sasa ndilo jiji la New York nchini Marekani. Alijishughulisha na uwindaji na upishi katika migahawa ilikuwa katika milima ya Adirondack. Alifanya shughuli hizo kwa bidii lakini baadae alielekeza nguvu zake zaidi katika upishi. Jina lake lilikuwa ni George Speck. Kutokana na jina la uchepe kushamiri zaidi ambalo ni Crum, aliamua kujiita George Crum.

Baba yake aliitwa Abe Speck ambaye alikuwa mhamiaji kutoka Kentucky kwenda Saratoga. Akiwa Saratoga alimuoa mwanamke mwenye asili ya India ambapo baadae George alizaliwa. 

Bidii yake ilipoonekana zaidi, alichukuliwa na tajiri mmoja katika mgahawa ulioitwa Moon’s Lake House, karibu na maporomoko ya maji ya Saratoga. Mgahawa huo uliaminika kuwa ndio wenye gharama za juu za chalula. Hapo ndipo ujuzi wake wa upishi ulipofahamika na watu wengi zaidi. Licha ya kuwa na gharama za juu katika mgahawa huo watu walipenda kufika kwa wingi kutokana na umahiri wa George Crum katika upishi wake.

Bada ya kufanya kazi kwa muda mrefu katika mgahawa huo, George aliamua kumchukua dada yake ili wafanye kazi pamoja kutokana na ukata ulioikumba familia yao. Walikuwa ni wenye rangi mchanganyiko.

January 23, 2018

ZOLILE HECTOR PIETERSEN: MTOTO ALIYELAZIMU KUANZISHWA KWA KUMBUKUMBU YA MAUAJI YA KIMBARI AFRIKA KUSINI, TAREHE 16 JUNI KILA MWAKA.

Na Kizito Mpangala

Zolile Hector Pietersen akiwa amebebwa na
Mbuyisa Makhubo baada ya kupgwa risasi.
kushoto ni Antoinete Sithole, dada yake
Zolile Hector Pietersen akilia.
Zolile Hector Pietersen alizaliwa tarehe 19/08/1963 mjini Soweto nchini Afrika Kusini wakati falsafa ya ubaguzi wa rangi ikiwa imepamba moto. Falsafa ya ubaguzi wa rangi ilikuwa ikijulikana kama Apartheid, ambayo ilikuwa ikiendeshwa na makaburu waliokuwa wakitawala nchi ya Afrika Kusini.

Jina halisi la ukoo wake ambalo lilikuwa likitumika na familia yake ni Pitso, lakini fdamilia hiyo ililazimika kubadili na kuwa Pietersen ili kuendana na falsafa ya Apartheid, na kujihisi kama wao ni makaburu ilhali wakiwa ni weusi. Familia hiyo iliamaua kufanya hivyo ili kukwepa dhuruma za makaburu. Hata jina la Zolile lilifutwa kwa muda ili apate nafasi ya kusoma. 

January 21, 2018

ERATOSTHENES WA KIRENE: MWANAHISABATI ALIYEISHI AFRIKA NA KUKADIRIA MZINGO WA DUNIA KWA KIVULI CHA MWANZI.

Na Kizito Mpangala

Eratosthenes alizaliwa mwaka 276 KK (Kabla ya kuazaliwa Yesu Kristo) mjini Kirene, Libya ya sasa. Kirene ni mji mashuhuri ulioundwa na Wagiriki wa kale walioishi Afrika ya Kaskazini hasa Libya ambako ndiko ulikokuwa mji wa Kirene maeneo ya Tripolitania ( sasa ni Tripoli), na Misri maeneo ya Alexandria ilikokuwa maktaba mashuhuri iliyotumiwa na wataalamu wengi wa Ugiriki ya kale. 

Alikuwa akifanya mazoezi mbalimbali ya viungo kila siku asubuhi na jioni. Alijifunza kusoma, kuandika, na kuhesabu. Ni kama vile falsafa ya elimu ya msingi inayotumiwa nchini Tanzania yaani KKK (Kusoma, Kuandika na Kuhesabu). Pia, alijifunza uandishi wa mashairi na vilevile masuala ya muziki.