NA
EZEKIEL KAMWAGA
JANA,
ripoti kuhusu utafiti wa kimataifa ulioonyesha kwamba nchi yetu ina hali mbaya
kwenye kigezo cha furaha kwa watu wake ilizua mjadala wa aina yake. Kuna
walioupinga utafiti huo moja kwa moja kwa hoja kwamba ziko nchi zina vita
wakati huu na haiwezekani wananchi wake wakawa na furaha kuliko sisi. Wengine
wakapinga tu kwa sababu huwa wanapinga. Wengine wakaunga mkono kwa sababu za
kisiasa tu.
Kitu
kikubwa ambacho nilikiona jana ni kwamba wengi wetu tulitoa maoni kabla hata ya
kuisoma ripoti yenyewe. Na hili ndilo tatizo kubwa ambalo wengi wetu tunalo.
Tunapenda kutoa maoni katika mambo ambayo ufahamu wetu ni mdogo sana. Nafurahi
kwamba nilijipa muda kuisoma ile ripoti jana. Hapa chini ni mawazo yangu baada
ya kuisoma. Nimeyagawa mawazo yangu katika pande mbili tofauti; kabla ya
kuisoma ripoti hiyo na baada ya kuisoma.
KABLA
YA KUISOMA
Mimi
ni muumini wa dhana kwamba furaha ni jambo gumu sana kulipima kwa mwanadamu.
Nimewahi kuandika humu mitandaoni kwamba kuwa na furaha si jambo unaloweza
kulipima kwa sababu ya wingi wa mali au marafiki.








